SURA YA KUMI TANO
Jinsi ya Kumwabudu Mungu kwa Njia Inayofaa
1. Ni nani anayepaswa kutufundisha jinsi ya kumwabudu Mungu?
DINI nyingi zinadai kwamba zinafundisha ukweli kumhusu Mungu. Hata hivyo, si kweli, kwa sababu dini hizo zinafundisha mambo yanayotofautiana kabisa kumhusu Mungu na jinsi tunavyopaswa kumwabudu. Tunawezaje kujua njia inayofaa ya kumwabudu Mungu? Yehova peke yake ndiye anayeweza kutufundisha jinsi tunavyopaswa kumwabudu.
2. Unawezaje kujifunza jinsi ya kumwabudu Mungu kwa njia inayofaa?
2 Yehova ametupatia Biblia ili tujifunze jinsi ya kumwabudu kwa njia inayofaa. Kwa hiyo, jifunze Biblia, unapofanya hivyo Yehova atakusaidia ufaidike na mafundisho yake kwa sababu anakupenda sana.—Isaya 48:17.
3. Mungu anataka tufanye nini?
3 Baadhi ya watu husema kwamba Mungu hukubali dini zote, hata hivyo Yesu hakutufundisha hivyo. Alisema hivi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu.” Kwa hiyo, ni muhimu sana tujifunze na kuyafanya mapenzi ya Mungu. Hilo ni jambo zito kwa kuwa Yesu aliwalinganisha watu wasiomtii Mungu na wahalifu ‘wanaotenda uasi sheria.’—Mathayo 7:21-23.
4. Yesu alisema nini kuhusu kufanya mapenzi ya Mungu?
4 Yesu alisema kwamba tukiamua kufanya mapenzi ya Mungu, tutakabili upinzani. Alisema hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba, kwa sababu lango ni pana, na barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa, na ni wengi wanaoipitia; lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na ni wachache wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Barabara nyembamba, au njia inayofaa ya kumwabudu Mungu, inaongoza kwenye uzima wa milele. Barabara pana au njia isiyofaa ya kumwabudu Mungu inaongoza kwenye uharibifu. Hata hivyo, Yehova hataki mtu yeyote aangamizwe. Anampa kila mtu fursa ya kujifunza kumhusu yeye.—2 Petro 3:9.
JINSI YA KUMWABUDU MUNGU KWA NJIA INAYOFAA
5. Unawezaje kuwatambua wale wanaomwabudu Mungu kwa njia inayofaa?
5 Yesu alisema kwamba tunaweza kuwatambua wale wanaomwabudu Mungu kwa njia inayofaa. Tunaweza kufanya hivyo kwa kuchunguza mambo wanayoamini na kutenda. Alisema hivi: “Kwa matunda yao mtawatambua.” Kisha akaongeza: “Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri.” (Mathayo 7:16, 17) Hilo halimaanishi kwamba wale wanaomwabudu Mungu ni wakamilifu. Hata hivyo, watumishi wa Mungu wanajitahidi kufanya yaliyo sawa. Sasa tutachunguza mambo yatakayotusaidia kuwatambua wale wanaomwabudu Mungu kwa njia inayofaa.
6, 7. Kwa nini ibada ya kweli inategemea Biblia? Mfano wa Yesu unatufundisha nini?
6 Ibada yetu inapaswa kutegemea Biblia. Biblia inasema: “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo hivi: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali si kama neno la wanadamu, bali kama lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Ibada ya kweli inategemea Biblia Neno la Mungu. Haitegemei mawazo ya wanadamu, utamaduni, au jambo lingine lolote.
7 Mambo yote ambayo Yesu alifundisha yalitegemea Neno la Mungu. (Soma Yohana 17:17.) Mara nyingi alinukuu Maandiko. (Mathayo 4:4, 7, 10) Waabudu wa kweli wa Mungu wanafuata mfano wa Yesu na kila jambo wanalofundisha linategemea Biblia.
8. Yesu alitufundisha nini kuhusu kumwabudu Yehova?
8 Tunapaswa kumwabudu Yehova peke yake. Zaburi 83:18 inasema hivi: “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Yesu alitaka watu wamjue Mungu wa kweli, naye aliwafundisha jina la Mungu. (Soma Yohana 17:6.) Yesu alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Hivyo, tukiwa watumishi wa Mungu tunafuata mfano wa Yesu. Tunamwabudu Yehova peke yake, tunatumia jina lake, na tunawafundisha wengine jina la Mungu na mambo atakayotufanyia wakati ujao.
9, 10. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunawapenda wengine?
9 Tunapaswa kuwapenda watu. Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wapendane. (Soma Yohana 13:35.) Tunapendana hata ingawa tunatoka katika nchi na tamaduni mbalimbali au iwe sisi ni matajiri au maskini. Upendo unapaswa kutuunganisha kuwa ndugu na dada. (Wakolosai 3:14) Kwa sababu hiyo hatushiriki vita wala kuua watu. Biblia inasema: “Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni wazi kwa jambo hili: Yeyote ambaye haendelei kufanya uadilifu hatokani na Mungu, wala yule ambaye hampendi ndugu yake.” Pia inaongezea hivi: “Tunapaswa kupendana; si kama Kaini, aliyetokana na yule mwovu akamuua ndugu yake.”—1 Yohana 3:10-12; 4:20, 21.
10 Tunatumia wakati, nguvu, na mali zetu ili kusaidiana na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) ‘Tunawatendea wote mema.’—Wagalatia 6:10.
11. Kwa nini tunaamini kwamba Yesu ndiye njia inayotuongoza kwa Mungu?
11 Tunapaswa kumtii Yesu kwa kuwa yeye ndiye njia inayotuongoza kwa Mungu. Biblia inasema: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote, kwa maana hakuna jina lingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu ambalo kupitia hilo tunaweza kuokolewa.” (Matendo 4:12) Katika sura ya 5 ya kitabu hiki, tulijifunza kwamba Yehova alimtuma Yesu aje atoe uhai wake ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu watiifu. (Mathayo 20:28) Yehova amemchagua Yesu atawale akiwa Mfalme wa dunia. Ndiyo sababu Biblia hutuambia kwamba ni lazima tumtii Yesu ikiwa tunataka kuishi milele.—Soma Yohana 3:36.
12. Kwa nini hatujihusishi na siasa?
12 Hatupaswi kujihusisha na siasa. Yesu hakujihusisha na siasa. Kesi yake ilipokuwa ikisikilizwa, alimwambia hivi Pilato, mtawala Mroma: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Soma Yohana 18:36.) Kama Yesu, tunashikamana na Ufalme wa Mungu, hivyo hatujihusishi na siasa. Hata hivyo, Biblia inatuamuru tutii “mamlaka zilizo kubwa,” yaani, serikali. (Waroma 13:1) Tunatii sheria za nchi. Hata hivyo, sheria za wanadamu zinapopingana na sheria za Mungu, tunaiga mfano wa mitume, ambao walisema hivi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”—Matendo 5:29; Marko 12:17.
13. Tunahubiri ujumbe gani kuhusu Ufalme wa Mungu?
13 Tunaamini kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la matatizo ya ulimwengu. Yesu alisema kwamba, “habari njema ya ufalme” itahubiriwa katika dunia yote. (Soma Mathayo 24:14.) Hakuna serikali ya wanadamu inayoweza kufanya mambo ambayo Ufalme wa Mungu utafanya. (Zaburi 146:3) Yesu alitufundisha tusali kuhusu Ufalme wa Mungu aliposema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Biblia inatueleza kwamba Ufalme wa Mungu utaziharibu serikali zote za wanadamu, “nao pekee utasimama milele.”—Danieli 2:44.
14. Ni nani wanaomwabudu Mungu kwa njia inayofaa?
14 Baada ya kujifunza mambo hayo, jiulize: ‘Ni nani ambao mafundisho yao yanategemea Biblia? Ni nani wanaowafundisha wengine jina la Mungu? Ni nani ambao wana upendo wa kweli na wanaamini kwamba Mungu alimtuma Yesu ili atukomboe? Ni nani ambao hawajihusishi na siasa? Ni nani wanaohubiri kwamba Ufalme wa Mungu pekee ndio unaoweza kuondoa matatizo yetu?’ Ni Mashahidi wa Yehova peke yao.—Isaya 43:10-12.
UNAHITAJI KUFANYA NINI?
15. Ni lazima tufanye nini ikiwa tunataka Mungu akubali ibada yetu?
15 Haitoshi tu kuamini kwamba kuna Mungu. Hata roho waovu wanaamini kwamba kuna Mungu, lakini hawamtii. (Yakobo 2:19) Ikiwa tunataka Mungu akubali ibada yetu, hatupaswi tu kuamini kwamba yupo, bali tunapaswa kufanya mapenzi yake.
16. Kwa nini tunapaswa kuacha kushirikiana na dini za uwongo?
16 Ili Mungu akubali ibada yetu, lazima tuache kushirikiana na dini za uwongo. Nabii Isaya aliandika hivi: “Tokeni kati yake, iweni safi.” (Isaya 52:11; 2 Wakorintho 6:17) Hiyo ndiyo sababu tunahitaji kukataa kila kitu kinachohusiana na ibada ya uwongo.
17, 18. “Babiloni Mkubwa” ni nini, na kwa nini ni muhimu utoke kwake?
17 Dini za uwongo ni zipi? Ni dini zote zinazofundisha kinyume na Neno Mungu. Biblia inaziita dini zote za uwongo “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:5) Kwa nini? Baada ya Gharika ya siku za Noa, mafundisho mengi ya dini za uwongo yalianzia katika jiji la Babiloni. Mafundisho hayo ya uwongo yalienea katika dunia yote. Kwa mfano, watu wa Babiloni waliabudu kikundi cha miungu watatu. Leo, dini nyingi zinafundisha kwamba Mungu ni Utatu. Lakini Biblia inafundisha wazi kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli, Yehova, na kwamba Yesu ni Mwana wake. (Yohana 17:3) Pia, Wababiloni waliamini kwamba kitu fulani huendelea kuishi baada ya mwili kufa na kwamba kinaweza kuteseka katika moto wa mateso. Fundisho hilo ni la uwongo.—Soma Maelezo ya Ziada 14, 17, na 18.
18 Mungu ametabiri kwamba hivi karibuni dini zote za uwongo zitaharibiwa. (Ufunuo 18:8) Je, unaelewa kwa nini ni muhimu utoke haraka katika dini za uwongo? Yehova Mungu anataka ufanye hivyo kabla hujachelewa mno.—Ufunuo 18:4.
Unapomtumikia Yehova pamoja na watu wake, utajiunga na familia ya ulimwenguni pote
19. Yehova atafanya nini ukiamua kumtumikia?
19 Unapoamua kuacha dini za uwongo na kuanza kumtumikia Yehova, huenda baadhi ya rafiki au watu wa familia wasikubaliane na uamuzi wako na hata wanaweza kukupinga. Hata hivyo, Yehova hatakuacha. Utajiunga na familia kubwa yenye upendo wa kweli ya mamilioni ya watu ulimwenguni pote, pia utakuwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Marko 10:28-30) Baadaye, huenda baadhi ya rafiki na watu wa familia ambao wanapinga uamuzi wako wa kumtumikia Yehova wakaamua kujifunza Biblia.
20. Kwa nini ni muhimu kumwabudu Mungu kwa njia inayofaa?
20 Hivi karibuni, Mungu atawaharibu watu waovu na Ufalme wake utatawala dunia. (2 Petro 3:9, 13) Huo utakuwa wakati mzuri sana! Sote tutamwabudu Yehova kwa njia anayokubali. Kwa hiyo, ni muhimu sana uamue sasa kumwabudu Mungu kwa njia inayofaa.