SOMO LA 4
Hasira Yasababisha Mauaji
Baada ya Adamu na Hawa kufukuzwa katika bustani ya Edeni, walizaa watoto wengi. Mtoto wa kwanza aliitwa Kaini, naye alikuwa mkulima, na mtoto wa pili, Abeli, alikuwa mchungaji wa wanyama.
Siku moja Kaini na Abeli walimtolea Yehova dhabihu. Je, unajua dhabihu ni nini? Ni zawadi ya pekee. Yehova alifurahishwa na dhabihu ya Abeli, lakini alichukizwa na dhabihu ya Kaini. Jambo hilo lilimkasirisha sana Kaini. Yehova alimwonya Kaini kwamba hasira ingeweza kusababisha afanye jambo baya. Hata hivyo, Kaini hakusikiliza.
Badala yake Kaini alimwambia Abeli hivi: ‘Twende shambani.’ Walipokuwa peke yao shambani, Kaini alimshambulia ndugu yake na kumuua. Yehova angefanya nini kuhusu jambo hilo? Yehova alimwadhibu Kaini kwa kumfukuza aende mbali na familia yao. Kaini hakuruhusiwa kurudi tena nyumbani.
Tunajifunza nini? Tunajifunza kwamba tunaweza kukasirika mambo yanapoenda kinyume na matarajio yetu. Tunapoona kwamba tumeanza kukasirika—au tunapoonywa na wengine kuhusu hasira—tunapaswa kukubali kurekebishwa na kujitahidi kudhibiti hisia hizo kabla hazijaanza kututawala.
Kwa sababu Abeli alimpenda Yehova na alifanya mambo mema, sikuzote Yehova atamkumbuka. Mungu atamfufua Abeli wakati atakapoifanya dunia kuwa paradiso.
“Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.”—Mathayo 5:24