SOMO LA 18
Kichaka Kinachowaka Moto
Musa aliishi Midiani kwa miaka 40. Alioa na kupata watoto. Siku moja alipokuwa akichunga kondoo karibu na Mlima Sinai, aliona kitu chenye kustaajabisha. Kichaka kilikuwa kikiwaka moto lakini hakikuteketea! Alipokikaribia ili aone kwa nini hakikuwa kikiteketea, alisikia sauti kutoka kwenye kichaka hicho ikisema: ‘Musa! Usikaribie zaidi. Vua viatu vyako kwa sababu mahali ambapo umesimama ni ardhi takatifu.’ Yehova ndiye aliyekuwa akizungumza kupitia malaika.
Musa aliogopa, kwa hiyo akauficha uso wake. Sauti hiyo ilisema hivi: ‘Nimeyaona mateso ya Waisraeli. Nitawakomboa kutoka kwa Wamisri na kuwapeleka kwenye nchi nzuri. Wewe ndiye utakayewaongoza watu wangu kutoka Misri.’ Je, unafikiri jambo hilo lilimshangaza Musa?
Musa akauliza hivi: ‘Watu wakiniuliza ni nani aliyenituma, niwaambie nini?’ Mungu akamjibu hivi: ‘Waambie kwamba Yehova, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo amekutuma.’ Kisha Musa akasema hivi: ‘Vipi ikiwa watu hao hawatanisikiliza?’ Yehova alimpa Musa uthibitisho kwamba atamsaidia. Alimwambia Musa atupe fimbo yake chini, nayo ikawa nyoka! Musa alipomkamata nyoka huyo kwenye mkia, akageuka kuwa fimbo. Yehova akasema hivi: ‘Ukiwafanyia muujiza huu, utathibitisha kwamba nimekutuma.’
Musa akasema: ‘Mimi si msemaji mzuri.’ Yehova akamwahidi hivi: ‘Nitakufundisha mambo unayopaswa kusema, nami nitamtuma Haruni, ndugu yako, ili akusaidie.’ Akiwa na uhakika kwamba Yehova alikuwa pamoja naye, Musa akamchukua mke na watoto wake, na kurudi Misri.
“Msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo.”—Mathayo 10:19