ALFA NA OMEGA
Ni herufi ya kwanza na herufi ya mwisho katika alfabeti za Kigiriki; maneno hayo yanatumiwa pamoja mara tatu katika kitabu cha Ufunuo kama cheo. Maneno hayo yaliongezwa kwenye tafsiri ya Zaire Swahili Bible katika Ufunuo 1:11, hata hivyo, hayaungwi mkono na baadhi ya hati za kale za Kigiriki, kutia ndani Kodeksi ya Alexandria, Sinai, na Efraimu rescriptus. Hivyo, tafsiri nyingi za kisasa zimeyaondoa.
Ingawa wasomi wengi hutumia cheo hicho kwa Mungu na Kristo, uchunguzi wa kina wa matumizi hayo unaonyesha kwamba majina hayo yanamhusu Yehova Mungu peke yake. Mstari wa kwanza wa Ufunuo unaonyesha kwamba ufunuo ulitoka kwa Mungu kupitia Yesu Kristo, hivyo, wakati mwingine yule aliyekuwa akizungumza (akitumia malaika kuwa mwakilishi wake) ni Mungu mwenyewe na wakati mwingine ni Kristo Yesu. (Ufu 22:8) Kwa hiyo, Ufunuo 1:8 (UV) inasema: “‘Mimi ni Alfa na Omega,’ mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu [“Yehova Mungu,” NWT], aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi.” Ingawa mstari uliotangulia unazungumza kuhusu Kristo Yesu, ni wazi kwamba katika mstari wa 8 cheo kinachotajwa ni cha “Mwenyezi” Mungu. Kuhusiana na hilo, kitabu Barnes’ Notes on the New Testament (1974) kinasema hivi: “Haiwezi kusemwa kwa hakika kwamba katika mstari huo mwandishi alikusudia kihususa kumrejelea Bwana Yesu . . . Pia, haitakuwa kosa kusema kwamba mwandishi alikusudia kumrejelea Mungu.”
Cheo hicho kinatajwa tena katika Ufunuo 21:6, na mstari unaofuata unamtambulisha anayezungumza kwa kusema: “Yeyote anayeshinda atarithi vitu hivi, nami nitakuwa Mungu wake naye atakuwa mwanangu.” Kwa kuwa Yesu anawaita wale watakaotawala pamoja naye katika Ufalme wake kuwa “ndugu,” na si “wana,” lazima yule anayezungumza katika mstari huo ni Baba wa Mbinguni wa Yesu, Yehova Mungu.—Mt 25:40; linganisha na Ebr 2:10-12.
Cheo hicho kinatajwa kwa mara ya mwisho katika andiko la Ufunuo 22:13, linalosema: “Mimi ndiye Alfa na Omega, wa kwanza na wa mwisho, mwanzo na mwisho.” Ni wazi kwamba watu kadhaa wanaonyeshwa wakizungumza katika sura hiyo ya kitabu cha Ufunuo; mstari wa 8 na 9 unasema kwamba malaika alizungumza na Yohana, ni dhahiri kwamba mstari wa16 unamhusu Yesu, sehemu ya kwanza yamstari wa 17 unataja kuhusu “roho na bibi harusi,” na bila shaka anayezungumza katika sehemu ya mwisho ya mstari wa 20 ni Yohana mwenyewe. Hivyo, maneno “Alfa na Omega” katikamstari wa 12-15, yanaweza kwa kufaa kuwa yanamrejelea yule aliyetajwa mara mbili akiwa na cheo hicho: Yehova Mungu. Maneno, “Tazama! Ninakuja upesi,” katika mstari wa12, hayamaanishi kwamba mistari iliyotangulia kutajwa inamhusu Yesu, kwa kuwa Mungu anasema kwamba ‘atakuja’ kutekeleza hukumu. (Linganisha Isa 26:21 26:21.) Malaki 3:1-6 inataja kuhusu kuja kwa Yehova akiwa pamoja na “mjumbe wa agano” ili kutekeleza hukumu.
Maneno “Alfa na Omega” yanabeba wazo sawa na “wa kwanza na wa mwisho” na “mwanzo na mwisho” yanapotumiwa kumrejelea Yehova. Kabla yake hakukuwa na Mungu Mweza-Yote na baada yake hakutakuwa na yeyote. Atamaliza suala linalohusu ni nani aliye Mungu wa kweli, na kwa umilele wote yeye peke yake atathibitika kuwa Mungu Mweza-Yote.—Linganisha Isa 44:6.