MFUKO WA CHAKULA
Mfuko ambao kwa kawaida ulitengenezwa kwa ngozi, uliobebwa juu ya mabega na wasafiri, wachungaji, wakulima, na watu wengine. Ulitumiwa kuweka chakula, nguo, na mahitaji mengine, hata hivyo haukuwa sawa na mkoba wa pesa uliofungwa kwenye mshipi, uliotumiwa kuweka dhahabu, fedha, na sarafu za shaba. (Mt 10:9; Mk 6:8) Ni wazi kwamba ‘mfuko wa mchungaji’ wa Daudi ulikuwa mfuko wa chakula. (1Sa 17:40) Yesu Kristo, alipowatuma mitume wake 12 kwanza na baadaye wanafunzi 70 ili wakahubiri katika Israeli, aliwaambia wasibebe mifuko ya chakula. (Mt 10:5, 9, 10; Lu 9:3; 10:1, 4) Yehova angewapa mahitaji yao kupitia Waisraeli wenzao, waliokuwa na desturi ya kuonyesha ukarimu. Kabla ya kifo chake, Yesu alionyesha kwamba hali zingebadilika kwa sababu ya kuanza kwa upinzani, hivyo aliwaambia wanafunzi wake wabebe mkoba wa pesa na mfuko wa chakula. Hata hivyo, walipaswa kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu badala ya kuhangaikia mahitaji ya kimwili; kufanya hivyo kungethibitisha kwamba walimtegemea Yehova Mungu awatunze wanapoendelea na huduma.—Lu 22:35, 36; Mt 6:25-34.