HABAKUKI
(Habakuki) [Kumbatio Changamfu].
Nabii Mwebrania kutoka Yuda na mwandikaji wa kitabu cha Biblia chenye jina lake. (Hab 1:1; 3:1) Kutokana na maneno ya umalizio ya kitabu hicho (“Kwa kiongozi; kwa kutumia vinanda vyangu”) na wimbo wa maombolezo kwenye sura ya 3, inasemekana kwamba huenda Habakuki alikuwa mwimbaji wa hekalu wa kabila la Lawi. Lakini maneno katika Habakuki 3:19 hayathibitishi jambo hilo, na nyimbo za maombolezo hazikuimbwa na Walawi tu, ziliimbwa na watu wengine pia. (2Sa 1:17, 18) Ingawa kuna mapokeo yanayotofautiana kumhusu Habakuki, mapokeo hayo hayategemeki, na Maandiko yenyewe hayafunui habari zozote kuhusu wazazi wake, kabila lake, hali zake maishani, au kifo chake. Uthibitisho unaopatikana kwenye kitabu cha Habakuki unaonekana kuonyesha kwamba alikuwa nabii katika miaka ya mwanzoni mwa utawala wa Yehoyakimu, huenda kabla ya Nebukadneza kushinda majeshi ya Misri huko Karkemishi mwaka wa 625 K.W.K.