MAJUMA SABINI
Ni kipindi cha wakati wa kinabii kinachorejelewa kwenye Danieli 9:24-27 ambacho katika hicho Yerusalemu lingejengwa upya na Masihi angetokea kisha akatiliwe mbali; baada ya kipindi hicho jiji hilo na vileveile patakatifu pangefanywa ukiwa.
Katika mwaka wa kwanza wa Dario “mwana wa Ahasuero wa uzao wa Wamedi,” nabii Danieli alifahamu kutokana na unabii wa Yeremia kwamba wakati wa kuachiliwa kwa Wayahudi kutoka Babiloni na kurudi kwao Yerusalemu ulikuwa karibu. Kisha Danieli akamtafuta Yehova kwa bidii katika sala, kupatana na maneno ya Yeremia: “‘Na hakika mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza. Nanyi kwa kweli mtanitafuta na kunipata, kwa maana mtanitafuta kwa moyo wenu wote. Nami nitajiacha mnipate,’ asema Yehova. . . . ‘Nami nitawarudisha katika mahali ambapo kutoka hapo niliwapeleka uhamishoni.’”—Yer 29:10-14; Da 9:1-4.
Danieli alipokuwa akisali, Yehova alimtuma Gabrieli malaika wake akiwa na unabii ambao karibu waelezaji wote wa Biblia hukubali ni wa Kimasihi, ijapokuwa uelewaji wao kuuhusu hutofautiana. Gabrieli alisema hivi:
“Kuna majuma 70 ambayo yameamuliwa juu ya watu wako na juu ya jiji lako takatifu, ili kukomesha makosa, na kumaliza kabisa dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya kosa, na kuleta uadilifu mpaka wakati usio na kipimo, na kupiga muhuri juu ya maono na nabii, na kupatia mafuta Patakatifu pa Patakatifu. Nawe ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62. Atarudi na kujengwa hakika, pamoja na kiwanja cha watu wote na handaki, lakini katika dhiki ya nyakati. Na baada ya yale majuma 62 Masihi atakatiliwa mbali, bila kuwa na chochote kwa ajili yake. Na watu wa kiongozi anayekuja wataharibu jiji na mahali patakatifu. Na mwisho wake utakuwa kwa mafuriko. Na mpaka ule mwisho kutakuwa na vita; kilichoamuliwa ni ukiwa. Naye ataendelea kulitendesha agano kwa ajili ya wengi kwa juma moja; na katika nusu ya juma hilo atakomesha dhabihu na toleo la zawadi. Na juu ya bawa la machukizo kutakuwa na yule anayesababisha ukiwa; na mpaka maangamizi, kitu kile kilichoamuliwa kitamwagika pia juu ya yule anayekaa ukiwa.”—Da 9:24-27.
Unabii wa Kimasihi. Ni wazi kabisa kwamba unabii huu ni “johari” kuhusiana na suala la kumtambulisha Masihi. Ni wenye umuhimu mkubwa kabisa katika kuamua wakati wa kuanza kwa yale majuma 70, na vilevile urefu wayo. Kama haya yangelikuwa ni majuma halisi ya siku saba kila moja, ama unabii huo ulikosa kutimizwa, nalo hilo ni jambo lisilowezekana (Isa 55:10, 11; Ebr 6:18), au la sivyo Masihi alikuja karne zaidi ya 24 zilizopita, katika siku za Milki ya Uajemi, na hakutambuliwa. Kama ni hivyo, basi, sifa zile nyingine chungu nzima za kutambulisha zinazotajwa kihususa katika Biblia kuhusu Masihi hazikutimizwa. Kwa hiyo, ni wazi kwamba yale majuma 70 yalikuwa ya kufananisha muda mrefu zaidi. Kwa hakika matukio yanayoelezwa katika unabii huo asili yake ilikuwa kwamba hayangeweza kutukia katika majuma 70 halisi, au muda unaozidi kidogo mwaka mmoja na miezi minne. Walio wengi kati ya wasomi wa Biblia hukubali kwamba “majuma” ya unabii huo ni majuma ya miaka. Baadhi ya tafsiri husema “majuma sabini ya miaka” (AT, Mo, RS), “miaka saba mara sabini” (BHN); Tanakh, ambayo ni tafsiri mpya ya Biblia iliyotangazwa mwaka 1985 na Chama cha Utangazaji cha Kiyahudi, inatia pia tafsiri hiyo katika kielezi-chini.—Ona Da 9:24, klz-chn.
Hayo “majuma sabini” ya kinabii yalianza lini hasa?
Kwa habari ya mwanzo wa majuma 70, Nehemia alipewa ruhusa na Mfalme Artashasta wa Uajemi, katika mwaka wa 20 wa utawala wake, katika mwezi wa Nisani, ili ajenge upya ukuta na jiji la Yerusalemu. (Ne 2:1, 5, 7, 8) Katika kupiga hesabu zake kuhusiana na utawala wa Artashasta, ni wazi Nehemia alitumia kalenda ya mwaka ambayo ilianza na mwezi Tishri (Septemba-Oktoba), kama ilivyo kalenda ya kijamii ya kisasa ya Wayahudi, na kumalizia na mwezi Eluli (Agosti-Septemba) kama mwezi wa 12. Haijulikani kama hiyo ndiyo iliyokuwa njia yake ya kufanya hesabu au ndiyo iliyokuwa njia ya kufanya hesabu iliyotumiwa kwa ajili ya makusudi fulani katika Uajemi.
Huenda wengine wakakataa taarifa hiyo inayotangulia na huenda wakaelekeza kwenye Nehemia 7:73, ambapo Nehemia anazungumza juu ya Israeli wakikusanywa katika majiji yao katika mwezi wa saba—hapa utaratibu wa miezi ukiwa unategemea mwaka wa Nisani-hadi-Nisani. Lakini hapa Nehemia alikuwa akinakili kutoka katika “kitabu cha uandikishaji wa kiukoo cha wale waliokuja pale mwanzoni” pamoja na Zerubabeli, mwaka 537 K.W.K. (Ne 7:5) Tena, Nehemia anaeleza juu ya sherehe ya Sikukuu ya Vibanda ya wakati wake kuwa ilifanyika katika mwezi wa saba. (Ne 8:9, 13-18) Jambo hilo lilifaa hasa kwa sababu masimulizi yanasema kwamba waligundua yale aliyoamuru Yehova yakiwa ‘yameandikwa katika sheria,’ na katika sheria hiyo, kwenye Mambo ya Walawi 23:39-43, inasema kwamba Sikukuu ya Vibanda ilipasa kuwa katika “mwezi wa saba” (yaani, mwezi wa kalenda takatifu, iliyoanza Nisani hadi Nisani).
Hata hivyo, ukiwa uthibitisho kwamba huenda Nehemia alitumia mwaka wa kuanzia vuli-hadi-vuli kurejelea matukio fulani, tunaweza kulinganisha Nehemia 1:1-3 na 2:1-8. Katika kifungu cha kwanza anaeleza juu ya kupokea habari mbaya kuhusu hali ya Yerusalemu, katika Kislewi (mwezi wa tatu katika kalenda ya kijamii na wa tisa katika kalenda takatifu) katika mwaka wa 20 wa Artashasta. Katika kile cha pili, anatoa ombi lake kwa mfalme kwamba aruhusiwe aende kujenga upya Yerusalemu, naye anapewa ruhusa katika mwezi Nisani (wa saba katika kalenda ya kijamii na wa kwanza katika ile takatifu), lakini bado ikiwa ni katika mwaka wa 20 wa Artashasta. Kwa hiyo ni wazi Nehemia hakuwa akiihesabu miaka ya utawala wa Artashasta kwa msingi wa Nisani-hadi-Nisani.
Ili kujua wakati wa ule mwaka wa 20 wa Artashasta, tunarudi nyuma hadi mwisho wa utawala wa baba na mtangulizi wake Shasta, ambaye alikufa katika sehemu ya mwisho ya mwaka 475 K.W.K. Kwa hiyo mwaka wa Artashasta kupanda cheoni ulianza katika 475 K.W.K., na mwaka wake wa kwanza wa utawala ungehesabiwa kuanzia 474 K.W.K., kama inavyoonyeshwa na uthibitisho mwingine wa kihistoria. Basi, mwaka wa 20 wa utawala wa Artashasta ungekuwa ni 455 K.W.K.—Ona PERSIA, PERSIANS (The Reigns of Xerxes and of Artaxerxes).
“Kutolewa kwa Lile Neno.” Unabii huo unasema kungekuwa na majuma 69 ya miaka “tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi.” (Da 9:25) Historia ya kilimwengu, pamoja na Biblia, hutoa uthibitisho kwamba Yesu alimjia Yohana, akabatizwa, hivyo akawa Mtiwa-Mafuta, Masihi Kiongozi, mapema vuli ya mwaka 29 W.K. (Ona JESUS CHRIST [Time of Birth, Length of Ministry].) Hesabu ikipigwa kurudi nyuma kwa msingi huo wa kihistoria, twaweza kujua kwamba yale majuma 69 ya miaka yalianza mwaka 455 K.W.K. Huo ndio uliokuwa mwaka hatua muhimu ilichukuliwa ya “kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi.”
Katika Nisani (Machi-Aprili) ya mwaka wa 20 wa utawala wa Artashasta (455 K.W.K), Nehemia alimsihi mfalme hivi: “Ikiwa mtumishi wako anaonekana mwema mbele yako, unitume Yuda, kwenye jiji la makaburi ya mababu zangu, nipate kulijenga upya.” (Ne 2:1, 5) Mfalme huyo alitoa ruhusa, naye Nehemia akafunga safari hiyo ndefu kutoka Shushani hadi Yerusalemu. Karibu na tarehe nne ya Abi (Julai-Agosti), baada ya kufanya ukaguzi wa kuta hizo usiku, Nehemia akawapa Wayahudi amri hii: “Njooni tujenge upya ukuta wa Yerusalemu, ili tusiendelee kuwa kitu cha aibu tena.” (Ne 2:11-18) Kwa njia hiyo, “kutolewa kwa lile neno” la kujenga upya Yerusalemu, kama ilivyoidhinishwa na Artashasta, kulitekelezwa na Nehemia katika Yerusalemu mwaka huohuo. Kwa wazi hilo linathibitisha 455 K.W.K kuwa mwaka ambao yale majuma 70 ya miaka yangeanza kuhesabiwa.
Kazi ya kukarabati kuta ilikamilishwa katika siku ya 25 ya Eluli (Agosti-Septemba), muda wa siku 52 tu. (Ne 6:15) Baada ya kujengwa upya kwa kuta hizo, ukarabati wa sehemu nyinginezo za Yerusalemu uliendelea. Kwa habari ya yale “majuma” saba ya kwanza (miaka 49), Nehemia, akisaidiwa na Ezra na, baadaye, wengine ambao huenda walifuata nyuma yao, walifanya kazi, “katika dhiki ya nyakati,” kukiwa na magumu ya kutoka ndani, miongoni mwa Wayahudi wenyewe, na ya kutoka nje, upande wa Wasamaria na wengineo. (Da 9:25) Kitabu cha Malaki, ambacho kiliandikwa baada ya 443 K.W.K, kinasikitikia hali mbaya ambayo ukuhani wa Kiyahudi ulikuwa umeangukia kufikia wakati huo. Inafikiriwa kurudi kwa Nehemia katika Yerusalemu baada ya kufanya ziara kwa Artashasta (linganisha Ne 5:14; 13:6, 7) kulitokea baada ya jambo hilo. Biblia haifunui yeye binafsi aliendeleza jitihada zake za kujenga Yerusalemu muda mrefu kadiri gani baada ya 455 K.W.K . Hata hivyo, ni wazi kazi hiyo ilikamilika katika muda wa miaka 49 (majuma saba ya miaka) kufikia kiwango kilichohitajiwa, na Yerusalemu na hekalu lake likadumu kwa ajili ya kuja kwa Masihi.—Ona MALACHI, BOOK OF (Time of Composition).
Kuwasili kwa Masihi Baada ya ‘Majuma 69.’ Kwa habari ya “majuma 62” yanayofuata (Da 9:25), na hayo, yakiwa ni sehemu ya yale 70 nayo yakiwa yametajwa ya pili katika utaratibu huo, yangeendelea kuanzia umalizio wa yale “majuma 7.” Kwa hiyo, ule wakati wa “tangu kutolewa kwa lile neno” la kujenga upya Yerusalemu hadi “Masihi aliye Kiongozi” ungekuwa “majuma” 7 kuongezea 62, au “majuma” 69—miaka 483—kuanzia mwaka 455 K.W.K hadi 29 W.K. Kama ilivyotangulia kutajwa, katika vuli ya mwaka huo, 29 W.K., Yesu alibatizwa katika maji, akatiwa mafuta kwa roho takatifu, na kuanza huduma yake akiwa “Masihi aliye Kiongozi.”—Lu 3:1, 2, 21, 22.
Kwa hiyo, karne nyingi mapema unabii wa Danieli ulielekeza hususa kwenye mwaka barabara wa kuwasili kwa Masihi. Pengine Wayahudi katika karne ya kwanza W.K. walikuwa wamefanya hesabu kwa msingi wa unabii wa Danieli na kwa hiyo walikuwa chonjo kuona Masihi akitokea. Biblia inaripoti hivi: “Basi kwa kuwa watu walikuwa wakitarajia na wote walikuwa wakiwaza mioyoni mwao juu ya Yohana: ‘Je, labda yeye ndiye Kristo?’” (Lu 3:15) Ijapokuwa walikuwa wanamtazamia Masihi, ni wazi hawangeweza kutaja mwezi, juma, au siku barabara ya kuwasili kwake. Kwa hiyo, walitaka kujua kama Yohana alikuwa ndiye Kristo, hata ingawa kwa wazi Yohana alianza huduma yake katika masika ya 29 W.K., karibu miezi sita kabla ya Yesu kujitokeza mwenyewe abatizwe.
“Atakatiliwa mbali” katika nusu ya juma hilo. Gabrieli aliendelea kumwambia Danieli hivi: “Baada ya yale majuma 62 Masihi atakatiliwa mbali, bila kuwa na chochote kwa ajili yake.” (Da 9:26) Ilikuwa muda fulani baada ya mwisho wa ‘majuma 7 kuongezea 62,’ kwa kweli karibu miaka mitatu na nusu baadaye, ndipo Kristo alipokatiliwa mbali katika kifo juu ya mti wa mateso, akatoa kila kitu alichokuwa nacho, awe fidia kwa ajili ya jamii ya wanadamu. (Isa 53:8) Uthibitisho waonyesha kwamba nusu ya kwanza ya “juma” hilo ilitumiwa na Yesu katika huduma. Katika pindi moja, yawezekana ni katika vuli ya 32 W.K., alitoa mfano, kwa wazi akiongea juu ya taifa la Kiyahudi kana kwamba ni mtini (linganisha Mt 17:15-20; 21:18, 19, 43) ambao haukuzaa matunda yoyote kwa “miaka mitatu.” Mtunza-mizabibu akamwambia mwenye shamba la mizabibu: “Bwana, uache mwaka huu pia, mpaka niupalilie na kuweka mbolea; na ndipo ukizaa matunda wakati ujao, basi ni vema; lakini ikiwa sivyo, utaukata.” (Lu 13:6-9) Huenda hapa yeye alirejelea kipindi cha huduma yake mwenyewe katika taifa hilo lisiloitikia, huduma ambayo kufikia hatua hiyo ilikuwa imeendelea kwa karibu miaka mitatu nayo ingeendelea iingie katika mwaka wa nne.
Agano kutendeshwa “kwa juma moja.” Danieli 9:27 lasema hivi: “Naye ataendelea kulitendesha agano kwa ajili ya wengi kwa juma moja [au miaka saba]; na katika nusu ya juma hilo atakomesha dhabihu na toleo la zawadi.” Haingewezekana “agano” liwe lilikuwa ni lile agano la Sheria, kwa maana miaka mitatu na nusu baada ya kuanza lile “juma” la 70, dhabihu ya Kristo ilisababisha hilo liondolewe na Mungu: “Yeye ameiondoa [ile Sheria] njiani kwa kuipigilia misumari juu ya mti wa mateso.” (Kol 2:14) Pia, “Kristo kwa kutununua alituachilia huru kutoka katika laana ya Sheria . . . Kusudi lilikuwa kwamba baraka ya Abrahamu ije kupitia Yesu Kristo kwa ajili ya mataifa.” (Gal 3:13, 14) Mungu, kupitia Kristo, alipanua baraka za agano la Abrahamu zifikie uzao wa asili wa Abrahamu, bila kutia ndani Watu wa Mataifa hadi Injili ilipopelekwa kwao kupitia mahubiri ya Petro kwa Kornelio Mwitalia. (Mdo 3:25, 26; 10:1-48) Kugeuzwa imani huku kwa Kornelio na nyumba yake kulitokea baada ya kugeuzwa imani kwa Sauli wa Tarso, ambako kijumla hufikiriwa kulitokea karibu na mwaka 34 W.K.; baada ya hilo kutaniko lilifurahia kipindi cha amani, likiwa linajengwa. (Mdo 9:1-16, 31) Basi, inaonekana kwamba kuingizwa kwa Kornelio ndani ya kutaniko la Kikristo kulitokea karibu na vuli ya mwaka 36 W.K., ambao ungekuwa ndio mwisho wa lile “juma” la 70, ikiwa ni miaka 490 tangu 455 K.W.K
Dhabihu na matoleo ‘yakomeshwa.’ Usemi ‘kukomeshwa,’ unaotumiwa kurejelea dhabihu na toleo la zawadi, wamaanisha, kihalisi, “kusababisha au kufanya sabato, kupumzika, kuacha kufanya kazi.” Zile “dhabihu na toleo la zawadi” ambazo ‘zinakomeshwa,’ kulingana na Danieli 9:27, hazingeweza kuwa ni fidia ya dhabihu ya Yesu, wala kwa kufikiri vizuri hazingeweza kuwa ni dhabihu yoyote ya kiroho yenye kutolewa na wafuasi wa nyayo zake. Lazima ziwe zinarejelea dhabihu na matoleo ya zawadi yaliyotolewa na Wayahudi kwenye hekalu katika Yerusalemu kulingana na Sheria ya Musa.
“Nusu ya juma hilo” ingekuwa katikati ya miaka saba, au baada ya miaka mitatu na nusu ndani ya hilo “juma” la miaka. Kwa kuwa “juma” la 70 lilianzia karibu vuli ya mwaka 29 W.K. wakati wa ubatizo wa Yesu na kutiwa mafuta awe Kristo, nusu ya juma hilo (miaka mitatu na nusu) ingeendelea hadi masika ya 33 W.K., au wakati wa Pasaka (Nisani 14) ya mwaka huo. Inaonekana siku hiyo ilikuwa ni Aprili 1, 33 W.K., kulingana na kalenda ya Gregory. (Ona LORD’S EVENING MEAL [Time of Its Institution].) Mtume Paulo anatuambia kwamba Yesu alikuja ‘kufanya mapenzi ya Mungu,’ mapenzi ambayo yalikuwa ni ‘kuondolea mbali lile la kwanza [dhabihu na matoleo kulingana na ile Sheria] ili asimamishe lile la pili.’ Alifanya jambo hilo kwa kutoa mwili wake mwenyewe kuwa dhabihu.—Ebr 10:1-10.
Ijapokuwa makuhani wa Kiyahudi waliendelea kutoa dhabihu kwenye hekalu katika Yerusalemu hadi lilipoangamizwa katika 70 W.K., kwa Mungu dhabihu hizo kwa ajili ya dhambi ziliacha kuwa zenye kukubalika na kuwa halali. Kabla tu ya kifo chake, Yesu aliliambia Yerusalemu hivi: “Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt 23:38) Kristo “alitoa dhabihu moja kwa ajili ya dhambi daima . . . Kwa maana ni kwa toleo moja la dhabihu kwamba yeye amewafanya wale wanaotakaswa wawe wakamilifu daima.” “Sasa mahali palipo na msamaha [wa dhambi na vitendo vya ukosefu wa sheria] wa mambo hayo, hapana tena toleo kwa ajili ya dhambi.” (Ebr 10:12-14, 18) Mtume Paulo anataja kwamba unabii wa Yeremia ulisema juu ya agano jipya, kwa hivyo, lile agano lililotangulia (agano la Sheria) likiwa halitendi tena na kuchakaa, lilikuwa “karibu kutoweka.”—Ebr 8:7-13.
Makosa na dhambi zakomeshwa. Kukatiliwa mbali kwa Yesu katika kifo, ufufuo wake, na kuonekana kwake mbinguni kulitokeza ‘ukomeshaji wa makosa, na kumaliza kabisa dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya kosa.’ (Da 9:24) Agano la Sheria lilikuwa limewafunua Wayahudi kuwa watenda-dhambi, likawahukumu kuwa hivyo, na kuleta juu yao laana ya kuwa wavunja-agano. Lakini mahali ambapo dhambi ‘ilizidi’ ikiwa imefunuliwa au kudhihirishwa na Sheria ya Musa, rehema na kibali cha Mungu vilizidi zaidi kupitia Masihi. (Ro 5:20) Kupitia dhabihu ya Masihi, makosa na dhambi ya watenda-dhambi wenye kutubu yanaweza kufutiliwa mbali na adhabu yake kuondolewa.
Uadilifu wa milele waingizwa. Thamani ya kifo cha Kristo juu ya mti iliandaa upatanisho kwa ajili ya waamini wenye kutubu. Kifuniko chenye kupatanisha kilifunikizwa juu ya dhambi zao, na njia ikafunguliwa ili ‘watangazwe kuwa waadilifu’ na Mungu. Uadilifu huo utakuwa wa milele nao utawaletea uzima wa milele wale wanaotangazwa kuwa waadilifu.—Ro 3:21-25.
Kutia Mafuta Patakatifu pa Patakatifu. Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu wakati wa ubatizo, roho takatifu ikimshukia kwa njia yenye kuonekana ikiwakilishwa na umbo la njiwa. Lakini kutia mafuta “Patakatifu pa Patakatifu” kwarejelea mengi zaidi ya kumtia mafuta Masihi, kwa sababu usemi huo haurejelei mtu binafsi. “Patakatifu pa Patakatifu” au “Patakatifu Zaidi” ndio usemi unaotumiwa kurejelea hema la kweli la Yehova Mungu. (Da 9:24; Kut 26:33, 34; 1Fa 6:16; 7:50) Kwa hiyo, ni lazima kutia mafuta “Patakatifu pa Patakatifu” kunakotajwa katika kitabu cha Danieli kuhusiane na “hema kubwa zaidi na kamilifu zaidi ambalo halikufanywa kwa mikono,” ambamo ndani yake Yesu Kristo akiwa Kuhani Mkuu zaidi aliingia “kwa damu yake mwenyewe.” (Ebr 9:11, 12) Yesu alipomkabidhi Baba yake ile thamani ya dhabihu yake ya kibinadamu, mbingu zenyewe zilipata sura ya uhalisi wa kiroho uliowakilishwa na Patakatifu Zaidi pa lile hema na hekalu la baadaye. Kwa hiyo, makao ya kimbingu ya Mungu hakika yalikuwa yametiwa mafuta, au kutengwa, kwa kuwa “Patakatifu pa Patakafitu” katika mpango wa hekalu kuu la kiroho palianzishwa wakati Yesu alipotiwa mafuta kwa roho takatifu mwaka 29 W.K.—Mt 3:16; Lu 4:18-21; Mdo 10:37, 38; Ebr 9:24.
‘Kutia muhuri juu ya njozi na nabii.’ Kazi yote hii iliyotimizwa na Masihi—dhabihu yake, ufufuo wake, kuonekana kwake akiwa na thamani ya dhabihu yake mbele za Baba wa mbinguni, na mambo yale mengine yenye kutokea wakati wa lile juma la 70—‘hutia muhuri juu ya njozi na nabii,’ kuonyesha mambo hayo ni ya kweli na kutoka kwa Mungu. Inayatia muhuri wa tegemezo la kimungu, kwamba yametoka kwa chanzo kimoja cha kimungu wala si kutoka kwa mwanadamu mwenye kukosea. Inatia muhuri njozi hiyo kuwa ilimhusu Masihi peke yake kwa sababu inatimizwa katika yeye na kazi ya Mungu kupitia yeye. (Ufu 19:10) Kufasiriwa kwayo kumo ndani yake, nasi hatuwezi kumtazamia mwingine yeyote ipate kutimia. Hapana kingine chochote kitakachofungua muhuri wa maana ambayo hiyo inahusisha.—Da 9:24.
Maangamizi kwenye jiji hilo na mahali patakatifu. Iilikuwa baada ya “majuma” 70, lakini likiwa tokeo la moja kwa moja la Wayahudi kumkataa Kristo wakati wa lile “juma” la 70, matukio ya sehemu za mwisho za Danieli 9:26 na 27 yalitimizwa. Maandishi ya historia yanaonyesha kwamba Tito mwana wa Maliki Vepasiani wa Roma alikuwa ndiye kiongozi wa vikosi vya Roma vilivyokuja dhidi ya Yerusalemu. Kwa kweli majeshi hayo yaliingia ndani ya Yerusalemu na hekalu lenyewe, kama mafuriko, na kuliangamiza jiji hilo na hekalu lake. Kusimama huku kwa majeshi ya kipagani katika mahali patakatifu kuliyafanya yawe “chukizo.” (Mt 24:15) Jitihada zote zilizofanywa kabla ya mwisho wa Yerusalemu ili kunyamazisha hali hiyo zilishindwa kwa sababu amri ya Mungu ilikuwa ni hii: “Kilichoamuliwa ni ukiwa,” na “mpaka maangamizi, kitu kile kilichoamuliwa kitamwagika pia juu ya yule anayekaa ukiwa.”
Maoni ya Kiyahudi. Maandishi-matini ya Masora, yenye mfumo wake wa nukta za irabu, yalitayarishwa katika sehemu ya mwisho ya nusu ya milenia ya kwanza W.K. Ni wazi kwa sababu ya kumkataa Yesu Kristo kuwa Masihi, Wamasora walitia alama ya mkazo kwenye maandishi-matini ya Kiebrania kwenye Daniel 9:25 wakiweka ʼath·nach′, au “kituo cha kikomo,” baada ya “majuma saba,” kwa jambo hilo wakagawanya hilo na yale “majuma 62”; katika njia hiyo yale majuma 62 ya unabii, yaani, miaka 434, yanaonekana kuhusu wakati wa kujenga upya Yerusalemu la kale. Tafsiri ya Isaac Leeser inasema hivi: “Basi ujue na kuelewa, kwamba tangu kutoka kwa neno la kurudisha na kujenga Yerusalemu hadi mtiwa-mafuta aliye mkuu kutakuwa majuma saba: [kituo cha kikomo hapa kinawakilishwa na nukta mbili] na wakati wa majuma sitini na mawili ndipo litakapojengwa tena likiwa na barabara na mahandaki (kulizunguka), naam katika mikazo ya nyakati hizo.” Tafsiri ya Chama cha Uchapishaji cha Kiyahudi cha Marekani yasema vivyo hivyo: “kutakuwa majuma saba; na kwa majuma makumi sita na mawili, litajengwa tena.” Katika tafsiri hizi mbili (katika Kiingereza) maneno “wakati” na “kwa,” yanaonekana katika tafsiri ya Kiingereza, bila shaka ili yaunge mkono fasiri ya watafsiri hao.
Profesa E. B. Pusey, katika kielezi-chini kimoja katika mojawapo mihadhara yake iliyotolewa kwenye Chuo Kikuu cha Oxford, anatoa maelezo haya juu ya utiaji alama za mkazo za Wamasora: “Wayahudi walitia kituo kikuu cha mstari huo chini ya שׁבעה [saba], wakikusudia kutenganisha hizo namba mbili, 7 na 62. Lazima wawe walifanya hivyo kwa udanganyifu, למען המינים (kama Rashi [Rabi maarufu wa Kiyahudi wa karne ya 11 na ya 12 W.K.] anavyosema katika kukataa mafafanuzi halisi yaliyowafaa Wakristo) ‘kwa sababu ya wazushi,’ yaani, Wakristo. Kwa kishazi hicho cha mwisho, kugawanywa hivyo, ingeweza kumaanisha tu, ‘na wakati wa majuma makumi sita na mawili barabara na ukuta vitarudishwa na kujengwa,’ yaani, kwamba Yerusalemu lingechukua miaka 434 kujengwa upya, jambo ambalo lingekuwa ni upuuzi.”—Daniel the Prophet, 1885, ukur. 190.
Kwa habari ya Danieli 9:26 (Le), ambalo lasema hivi, kwa sehemu, “Na baada ya yale majuma-sitini na mwili ndipo mtiwa-mafuta atakapokatiliwa mbali bila kuwa na mwandamizi mwenye kumfuata,” Wafafanuzi wa Kiyahudi hutumia hayo majuma 62 kufikia kipindi cha enzi za Wamakabayo, na usemi “mtiwa-mafuta” kumhusu Mfalme Agripa wa 2, aliyeishi wakati wa kuangamizwa kwa Yerusalemu, 70 W.K. Au wengine husema huyo alikuwa kuhani mkuu, Oniasi, aliyepinduliwa na Antioko Epifane katika 175 K.W.K Matumizi yao ya unabii huo kuhusu mojawapo kati ya wanaume hao yangekuwa yenye kuukosesha umuhimu au maana yoyote iliyo halisi, na tofauti hiyo katika kukadiria tarehe ingefanya yale majuma 62 yawe unabii usio na wakati ulio sahihi hata kidogo.—Ona Soncino Books of the Bible (ufafanuzi juu ya Da 9:25, 26), kilichofanyiwa uhariri na A. Cohen, London, 1951.
Katika jitihada ya kutetea maoni yao, wasomi hao wa Kiyahudi husema kwamba yale “majuma saba” si 7 mara 7, au miaka 49, bali ni miaka 70; na huku wanahesabu yale majuma 62 kuwa 7 mara miaka 62. Wanadai hilo lilirejelea kile kipindi cha uhamisho wa Babiloni. Wanamfanya Koreshi au Zerubabeli au Kuhani Mkuu Yeshua awe “mtiwa-mafuta” katika mstari huu (Da 9:25), na huku yule “mtiwa-mafuta” katika Danieli 9:26 akiwa mtu mwingine.
Inaweza kuangaliwa, kuhusiana na hilo, kwamba tafsiri ya Septuajinti, iliyofanywa na wasomi wa Kiyahudi katika karne tatu za kwanza K.W.K, yasema hivi, kwenye Danieli 9:25, “Tangu kutolewa kwa amri ya kujibu na kujengwa kwa Yerusalemu hadi Kristo aliye mkuu kutakuwa majuma saba, na majuma sitini na mawili: kisha ule wakati utarudi, na barabara itajengwa, na ukuta.” (LXX, Bagster) Kwa sehemu, Septuagint ya Thompson inasema hivi: “majuma saba, na majuma sitini na mawili. Hakika wao watarudi na barabara itajengwa na ukuta.”
Tafsiri zilizo nyingi za Kiingereza hapa hazifuati alama za maandishi za Wamasora. Ama zina alama ya mkato baada ya usemi “majuma saba” au katika matumizi ya maneno zinaonyesha kwamba yale majuma 62 yanafuata yale 7 yakiwa sehemu ya yale 70, nazo hazionyeshi kwamba yale majuma 62 yanahusu kile kipindi cha kujenga upya Yerusalemu. (Linganisha Da 9:25 katika UV, AT, Dy, NW, Ro, Yg.) Taarifa ya mhariri ya James Strong katika Commentary on the Holy Scriptures cha Lange (Da 9:25, klz-chn, ukur. 198) yasema hivi: “Hoja pekee ya tafsiri hii, ambayo inatenganisha vile vipindi viwili vya majuma saba na majuma sitini na mawili, ikionyesha hayo ya kwanza kuwa ndio wakati wa kuwasili kwa Mkuu aliye Mtiwa-Mafuta, na hayo ya mwisho kuwa ndio upeo wa wakati wa kujenga upya, ni alama za maandishi za Wamasora, ambazo zinatia ile alama ya nukta katikati yake. . . . na tafsiri inayohusika inatia ndani muundo usiofaa wa sehemu ya pili, bila kihusishi. Kwa hiyo, ni afadhali zaidi, na ni sahili zaidi, kushikilia chapa ya Authorized Version, inayofuata tafsiri nyinginezo zote za kale.”—Kimetafsiriwa na kufanyiwa uhariri (Kiingereza) na P. Schaff, 1976.
Maoni mengine mengi, mengine yakiwa ni ya Kimasihi na mengine yasiyokuwa ya Kimasihi, yametolewa kuhusu ni nini maana ya unabii huo. Mengine hujaribu kubadili utaratibu wa vipindi hivyo vya wakati wa unabii huo, huku mengine yakiyafanya yaende sambamba au kukanusha kwamba yana wakati halisi wa utimizo. Pia, kumekuwa na jitihada nyingi za kufanya matukio hayo yaliyotajwa yafae kipindi cha Wamakabayo au hata wakati wa kumalizia wa mwisho. Lakini wale wanaotokeza maoni hayo wanajiingiza katika utata mkubwa, na jitihada zao za kujinasua huwaingiza katika upumbavu au ukanushaji wa moja kwa moja kwamba unabii huo umeongozwa kwa roho au ni wa kweli. Kuhusu maoni hayo ya mwisho hasa, ambayo hutokeza matatizo mengi zaidi kuliko yale ambayo husuluhishwa nayo, msomi huyo aliyetangulia kutajwa, E. B. Pusey, anaeleza hivi: “Hayo ndiyo yaliyokuwa matatizo yasiyowezekana kusuluhishwa na ukosaji imani; ilibidi huo ujifanyie suluhisho, jambo ambalo, kufikia hapa, ndilo lililokuwa rahisi zaidi; kwa maana hapana lisilowezekana kuaminiwa na ukosefu wa imani, isipokuwa yale anayofunua Mungu.”—Ukur. 206.