Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 1/1 kur. 3-4
  • Wewe Unajua Kuvumilia Huzuni Nyingi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Unajua Kuvumilia Huzuni Nyingi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Habari Zinazolingana
  • Kukabiliana na Huzuni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
  • Hali Unazoweza Kutazamia
    Amkeni!—2018
  • Katika Toleo Hili: Kukabiliana na Huzuni ya Kufiwa
    Amkeni!—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 1/1 kur. 3-4

Wewe Unajua Kuvumilia Huzuni Nyingi?

WAKATI kifo kinapopata jamaa ya mtu na kumpokonya mwenzi wake wa ndoa au mpendwa mwingine, ule mshtuko wa kuachwa na mpendwa wake unaweza kuwa ndilo pigo kali zaidi la moyoni la maisha yake yote. Watu wengi wameona ni vigumu sana kuvumilia huzuni nyingi hata wakawa wakishindwa kupata usingizi siku nyingi, wakawa wakikaa siku nyingi bila matumaini wala kujisikia hawajui wataendesha maisha namna gani, hasa ikiwa aliyekufa alikuwa mwenzi wa ndoa. Wakati huo kunakuwa na uhitaji mkubwa wa kujua namna ya kuvumilia huzuni nyingi.

Si lazima kufungia huzuni nyingi ndani ya moyo, kuificha kwa kujikaza na kujifanya hakuna huzuni nyingi na kumbe kwa ndani mtu anajisikia sana akiwa nayo. Kuifungia kwa njia hiyo kunaweza kuukaza sana moyo hata tatizo la kuivumilia liongezeke. Hakuna ubaya wa kuonyesha huzuni na masikitiko ya kupoteza mpendwa. Mtu akijiruhusu aonyeshe anavyojisikia moyoni kwa njia ya asili, lakini si kwa kushindwa kujiweza, kwa ukawaida anajisikia vizuri zaidi.

Wakati Abrahamu mzee wa ukoo anayetajwa na Biblia alipofiwa na Sara mkewe mpendwa hakufungia huzuni yake kuu ndani ya moyo wake kwa kujikaza isionekane. Aliifungulia huzuni hiyo ikatoka nje kwa kulia machozi. (Mwa. 23:2) Mfalme Daudi Mwisraeli alifanya ivyo hivyo wakati Absalomu mwana wake alipouawa kwa upanga. Maandishi ya Biblia yanasema: “Naye mfalme akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Sam. 18:33) Hapo ni baba aliyekuwa na huzuni nyingi sana kwa kufiwa na mwana mpendwa.

Daudi hakuendelea kuhuzunika sana kwa wakati usio na kikomo. Yeye alijua kwamba walio hai hawawezi kuwarudisha wafu waishi tena, kwa hiyo lazima warekebishe maisha yao ili waweze kuendelea kuishi pasipo kuwa na wapendwa wao waliokufa. Ingawa Daudi alimkumbuka mwanawe kwa kumthamini sana, huzuni yake nyingi ingalikuwa jambo gumu zaidi kuvumilia kama angalianza kujifikiria yeye mwenyewe tu bila kujali ni mambo gani mengine yaliyokuwa yakifanyika huko nje, akijaribu sana kuishi maisha ya kumfikiria-fikiria mwanawe saa zote bila kuwajali watu wengine.

Watu wengi wamekuja kujua kwamba wanakiendeleza kidonda kilichowapata moyoni wakijaribu kukumbuka-kumbuka mambo ya watu wao waliokufa. Watu fulani wanafanya hivyo kwa kuifanya nyumba kwa miaka mingi ionekane ikiwa na hali zile zile ilizokuwa nazo wakati mpendwa wao alipokuwa hai. Wale wanaorefusha huzuni yao nyingi kwa njia hiyo wanajaribu bure tu kufanya maisha yawe kama yalivyokuwa zamani, badala ya kutambua kwamba wanaweza kupata furaha nyingi wakiishi kwa ajili ya wakati ujao. Kama angalikuwa hai, mpendwa ambaye mtu huyo amefiwa naye angalitaka aliyebaki afanye marekebisho yanayohitajiwa sana ili awe na maisha yenye furaha na matokeo mazuri. Ni jambo la hekima kufanya marekebisho hayo.

Kwa uhakika mtu aliyefiwa atajisikia akiwa na pengo lililoachwa na mpendwa aliyekufa, lakini maumivu ya kufiwa yanaweza kupunguzwa kwa kujaribu kulijaza pengo hilo na utendaji mbalimbali wenye kujenga. Kufanyia wengine wenye kutaabika moyoni mambo yenye msaada bila uchoyo kumewasaidia watu wengi ambao wamefiwa na wenzi wao wa ndoa. Kumewasaidia waache kujifikiria-fikiria wao wenyewe. Labda kizuizi kilicho kikubwa zaidi cha kuvumilia huzuni nyingi ni maelekeo ya mtu kuzidi kuweka akili yake juu ya hasara ya kibinafsi aliyopata kwa kufiwa na mpendwa wake. Kwa kuwa anafikiria jinsi alivyo mpweke sasa na mambo ambayo lazima sasa ajifanyie aliyokuwa akifanyiwa na mpendwa wake, huzuni yake inakuwa nyingi mpaka inakuwa vigumu kuivumilia. Lakini, akiacha kujifikiria mwenyewe na kuweka akili yake juu ya mambo anayoweza kufanyia wengine, ataona kwamba kidonda alichopata moyoni kinaweza kupona na pengo lililo katika maisha yake linaweza kujazika polepole. Mtu anaweza kufanya mambo mengi afanye maisha yake yafae ikiwa atawafikiria wengine, awapende kama vile yeye angependa wampende.

Kweli za Neno la Mungu lililoandikwa zinasaidia sana kumletea faraja mtu aliyefiwa, zikimpa kusudi la kuishi. Zinaweza kuondoa wasiwasi anaoweza kuwa nao kwa sababu ya kutokujua ni jambo gani limempata mpendwa wake. Kupitia Biblia Muumba wa uhai anamwambia mtu huyo jambo linalompata mtu anayekufa na ana tumaini gani la kupata uhai tena.

Kwa sababu ya tumaini hilo lililo zuri ajabu, Mkristo hahitaji kuwa na masikitiko yale yenye uchungu mwingi wanayokuwa nayo watu wasiojua Mpaji-uzima aliye mkuu amesema nini juu ya wafu au wale wanaokosa kumwamini kwa maana hawana imani. Mambo hayo aliyosema yenye kutegemeka yanasaidia sana kupunguza maumivu ya huzuni nyingi. “Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini.” (1 The. 4:13) Kama mtume Paulo, yeye anaweza kumtumaini “Mungu, awafufuaye wafu.”—2 Kor. 1:9.

Wale ambao wamepata maarifa ya mambo ambayo Yehova Mungu ameweka katika Neno lake lililoandikwa, Biblia Takatifu, kwa faida na faraja ya wanadamu wanaweza kuwasaidia sana wengine wavumilie huzuni nyingi wakiwafundisha Neno la Mungu bila uchoyo. Utendaji huo mzuri wa kiroho, wa kufundisha, unaweza kulijaza pengo ambalo kifo kimeacha katika maisha zao. Utafanya akili zao ziendelee kufikiria utendaji usio wa kichoyo na wenye kujenga. Utawapa sababu nzito ya kusonga mbele.

Wale wanaohuzunika sana wanaweza kupata nguvu katika Mungu kwa kumgeukia katika sala. Hata mtu aseme nini, Mungu hapaswi kulaumiwa kwa kifo cha mpendwa. Kwa kujifunza kutokana na Maandiko sababu ya kifo na tumaini lililopo kwa wafu la kuishi tena, mtu aliyefiwa ana sababu ya kumpigia Mungu asante. Kujua hivyo kunamwondolea hali ya kuogopa sana na kushuka moyo ya kufikiri hakuna tumaini. (Zab. 46:1) Kujua hivyo kunasaidia sana sana katika kuvumilia huzuni nyingi.

Akiwa na tumaini linalotolewa na Neno la Mungu, mtu aliyefiwa anaweza kurekebisha maisha yake kwa wepesi zaidi aweze kusonga mbele bila ya kuwa na mpendwa wake. Mtu huyo atakuwa mwenye shukrani kwamba mpendwa wake alionja maisha naye akaweza kushiriki kumpa furaha ya maisha. Atapiga asante kwamba Mungu amepanga kwa upendo kuwe na ufufuo wa wafu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki