Mtafute Mungu Maadamu Anapatikana
“[Mungu] akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone.”—Matendo 17:26, 27.
1. Ilikuwaje Paulo akawa mtu asiyejulikana katika mji usiojulikana, ikiongoza kwenye matokeo gani?
MTU huyu hakujulikana mjini, na wakati wa kufika kwake hakuujua mji. Akitazama kumzunguka, aliona madhabahu iliyowekwa wakf “KWA MUNGU ASIYEJULIKANA.” Je! wewe ungependa kuwamo katika kuabudu Mungu uliyemwona kama asiyejulikana? Ilikuwa hali isiyofaa hata kidogo, na bila shaka ndivyo alivyoona mtume Paulo alipofika Athene katika safari yake ya pili ya umisionari, karibu na mwaka wa 50 C.E. Ilitukia kwamba ndugu za Paulo za Kikristo walikuwa wamemleta kutoka Beroya mpaka Athene, nao wakawa wamemwacha huko, kulingana na maagizo yake. Ni nyuma ya kupokea agizo la kimbinguni tu kwamba majuzi Paulo alikuwa ametembelea Makedonia, kaskazini mwa Athene, na kwa wazi hakuwa amefika Athene mbele ya hapo. Yaelekea alijua palikuwa mahali pakuu pa masomo, vile vile pa dini. Aliudhiwa na jambo hili la pili, “na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu, roho yake ilichukizwa sana ndani yake.” Je! Paulo alitendaje katika hali hii? Je! kama wewe ulikuwa Myahudi Mkristo, ungalitendaje?—Matendo 16:9, 10; 17:15, 16, 23.
2. Ni kwa njia gani kile ‘kisichojulikana’ kinavyoweza kuwa chenye kudhuru, naye Paulo alijaribuje kuzuia hili?
2 Kitu ‘kisichojulikana’ hakina mipaka iliyoonyeshwa wazi. Uhakika huu waweza kuleta madhara mengi, ukiongoza kwenye msiba kwa wepesi. Kwa hiyo, ikiwezekana, imetupasa tuizuie hali hii. Paulo aliizuia. Alianza kujijulisha mwenyewe na kazi yake, na, wakati ule ule, kujifahamisha mwenyewe zaidi na Waathene na njia zao za kufikiri. “Basi katika sinagogi akahojiana na Wayahudi na waliomcha Mungu, na wale waliokutana naye sokoni kila siku.” (Matendo 17:17) Pengine maono yake kwa Wayahudi huko Athene hayakuwa tofauti sana na yaliyotukia katika miji mingine. Lakini aliwafikia wengi sokoni waliojisifia kupendezwa kwao katika masomo na filosofia. Kwa maana “Waathene [wote] na wageni waliokaa huko walikuwa hawana nafasi kwa neno lo lote ila kutoa habari na kusikiliza habari za jambo jipya,” je! ingeweza kusemwa wao walikuwa wakimtafuta Mungu ndani ya mipaka yenye kujulikana ya kidini? Hata. Ebu na tuwatazame kidogo hawa waliosongamana sokoni.—Matendo 17:21.
3. Waepikureo na Wastoiko walijulikana kwa mambo gani, na hali inayofanana inaonekanaje leo?
3 Waepikureo wanatajwa. Waliamini kwamba kupata anasa nyingi zaidi bila ya matokeo mabaya yenye kupita kadiri ndilo lililokuwa kusudi kubwa katika maisha. Paulo alikuwa “akihubiri habari za Yesu na ufufuo,” zilizotofautiana na maoni ya “na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.” (Matendo 17:18; 1 Kor. 15:32) Mpaka mmoja ambao wao walijaribu kutouruka ulikuwa jambo lo lote lililotaka kuwanyima kutafuta kwao anasa na kuipata. Hapana, wao hawakuwa wakimtafuta Mungu wa kweli ndani ya mipaka aliyoiweka Yeye. Wastoiko vile vile wanatajwa. Wao hawakuamini katika Mungu mwenye utu, bali, walifikiria mungu asiye na utu, ambaye kwake nafsi ya kibinadamu ilitoka. Kwao, maisha ya wema yalimaanisha ‘kufuata maumbile,’ kwa maana waliamini kwamba kitu cho chote kilichoko na nguvu ndiyo mambo ya asili. Waliamini kwamba bahati ndiyo iliyoongoza mambo ya kibinadamu. Wao, vile vile, wakiwa si watafuta kweli kabisa, hawakuwa waelekevu kuukubali ujumbe wa Paulo uliotolewa na Mungu. Kwa ufupi, si vigumu kuona mfano unaolingana kati ya mafundisho ya vikundi hivyo na mafundisho ya wengi leo, pamoja na hali zao za kutafuta mambo ya kimwili na kupenda anasa. Kwao, bila ya kujali kama wanasema hivyo au hapana, “Mungu amekufa,” walau kwa kadiri ambavyo kupendezwa kwao katika kumtafuta yeye kwa unyofu, au hata kumtafuta kwa kupapasa-papasa kunapaswa.
4. Kwa sababu gani Paulo alipelekwa kwenye Areopago, naye angelionaje jambo hili?
4 Nia ya wengi kuelekea Paulo ilikuwa isiyofaa. ‘Walihojiana naye kwa ubishi,’ nao wakamwita “mpayukaji” na “mhubiri wa miungu ya kigeni.” Wakampeleka kwenye Areopago, yawezekana ili wamjaribu. Paulo angependezwa kwa nafasi hii atoe ushuhuda mwema, nasi twafurahi kwamba hotuba yake wakati huo iliandikwa kwa ajili ya faida yetu. Tutapendezwa kuona namna alivyouanza ugumu wa “asiyejulikana” na ulizo linalolingana la mipaka. Wazia kwamba sisi tuko pale tukimsikiliza yeye.—Matendo 17:18-22, NW.
MIPAKA YA KITHEOKRASI
5. (a) Kitu gani kinachostahili kuangaliwa katika maneno ya kuanzia ya Paulo? (b) Je! yeye anauanzaje ugumu wa “asiyejulikana”?
5 “Enyi watu wa Athene, katika mambo yote naona ya kuwa ninyi ni watu wa kutafakari sana mambo ya dini. Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.” (Matendo 17:22, 23) Lo! ni maneno ya kuanzia yenye busara kama nini! Hakuna linalosemwa kuwapinga wasikilizaji ama kuwafanya wajione kuhitilafiana naye. Yeye anachagua mojawapo la “mambo ya ibada” yao wenyewe, na, kana kwamba ilikuwa, anaungana nao katika kufikiri habari za madhabahu hii yenyewe. Bila ya kutua aulize ni namna ya mungu gani ambaye huenda waabudu wanafikiria, yeye anaanza kukuza habari yenye busara na ya kuvuta, akiweka jambo moja la kweli lenye nguvu juu ya jingine. Kwanza, anaondoka kwa “asiyejulikana.” Hasemi ni kosa waziwazi, lakini anasema tu kwamba yeye atakihubiri, au kukisimulia, kitu kilicho cha pekee kifaacho cha ibada ya kimungu. Ebu angalia anavyofanya hivyo.
6. Paulo anaimarisha ukweli gani juu ya kusudi la Mungu kwa mwanadamu na makao yake?
6 Yeye anaeleza kwamba Mungu, Muumba wa vitu vyote na Mpaji wa uzima na pumzi, hakai katika mahekalu yaliyojengwa kwa mikono, wala hana haja ya kutumikiwa kwa mikono ya kibinadamu. Ikiwa hii huenda ilete maoni ya kwamba Mungu alikuwa mbali asipoweza kufikiwa na mwanadamu, maneno yake yafuatayo yanatoa ufahamu wa kweli. “Naye [Mungu] alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:24-27) Sayansi na Biblia vile vile yashuhudia uhakika wa kwamba jamaa yote ya kibinadamu yaweza kufuatisha chanzo chake kwa mtu mmoja; mtu huyu, naye, alipokea uzima wake na pumzi kutoka kwa Mungu, Muumba wake. Basi jambo linalopendeza linatokezwa kwamba mpaka mpana wa makao ya mwanadamu ni “uso wa nchi yote.” Hii, bila shaka, haipatani na usemi wenye kujikuza kwamba mbingu ndio mpaka. Huenda mwanadamu asafiri kupita anga na hata achunguze mpaka mwezini, lakini hawezi kukaa humo sikuzote. Yampasa aridhike kuishi ndani ya mpaka wake uliotolewa na Mungu.
7. Wakati Mungu anapotoa amri au cho chote kingine kinacholingana, kitu gani kinachofanywa sikuzote?
7 Je! Paulo anamaanisha nini anapoendelea kusema kwamba Mungu ‘aliziamuru nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa [‘kuwekwa kwa mipaka,’ kwa halisi] ya makazi ya wanadamu, ili wamtafute Mungu’? Angalia neno hilo ‘aliziamuru.’ Wakati Mungu Bwana Mwenye Enzi Yote, atoapo amri au cho chote kingine kinacholingana, kama vile sheria, basi mpaka wa kitheokrasi, mpaka usiogeuka, unawekwa mara moja. Huu lazima uwe hivyo sikuzote, kwa maana kuwekwa kwake kunaamuru matakwa fulani na masharti ambayo lazima yashikwe. Utii unahitaji kwamba ukae ndani ya mipaka yake. Kutokutii kwamaanisha kwamba unaruka au kuivunja mipaka hiyo, kwa njia hiyo ukiwa nje ya mipaka, kama tusemavyo, na pengine mwenye hatia ya kuingilia haki za wengine. Uchunguzi zaidi wa hili kwa msaada wa Maandiko utatusaidia kumtafuta Mungu, lakini kwanza twataka kujua juu ya “nyakati zilizowekwa” na “mipaka iliyowekwa ya makazi ya wanadamu,” (NW).
8. Ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu ilifunuaje mipaka fulani?
8 Akiongozwa na Neno la Mungu na roho, Paulo anatafuta matukio yaliyofuata kuumba kusudi aonyeshe namna ambavyo Mungu aliye mmoja wa kweli alikuwa ameweka mipaka fulani, katika wakati na vile vile mahali. Ni gani hiyo? Ingawa ahadi ya kwanza na unabii vilitolewa Edeni, ni wakati ambapo Mungu alifanya agano lenye kiapo na Ibrahimu tunapopata kiungo kinachotakiwa, hatua ya kwanza. Yehova alimalizia agano kwa maneno haya: “Na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwa. 22:18) Hii bila shaka yaonyesha kwamba Ibrahimu hakuwa ‘akitoa ibada ya kimungu bila kujua kwa Mungu Asiyejulikana.’ Ni vingine kabisa! Hii vile vile yamaanisha kwamba mataifa yasingeweza kujaribu kujibariki yenyewe kwa ujinga kulingana na maoni yao wenyewe kwa matokeo mazuri. Wanadamu wanaweza kumpata Mungu na kupata baraka yake kwa njia ya Mungu iliyowekwa peke yake. Kama vile Isaya alivyosema: “Mtafuteni [Yehova], maadamu anapatikana.” Vile vile inakupasa utafute mahali ambapo aweza kupatikana, “maadamu yu karibu.” (Isa. 55:6) Je! wewe, kama Ibrahimu, u tayari kuisikiliza sauti ya Mungu kwa kuitikia?
9. Ahadi hiyo ilimalizikaje, ikitia ndani wakati na mahali vile vile?
9 Sasa angalia namna ahadi ya Mungu ilivyomalizika, ikiwa na mipaka katika wakati na mahali vile vile. Juu ya uzao wa Ibrahimu, Mungu alisema: “Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake . . . muda wa miaka mia nne. . . . Na kizazi cha nne kitarudi hapa.” Yehova aliendelea kuahidi: “Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa Misri mpaka huo mto mkubwa, mto Frati.” Katika wakati ufaao, nyuma ya hicho kipindi cha miaka 400, wakati Waisraeli, wazao wa Ibrahimu, walipokuwa wakipokea Torati penye Mlima wa Sinai, Yehova aliahidi waziwazi: “Nami nitakuwekea mpaka wako tangu Bahari ya Shamu hata bahari ya Wafilisti, tena tangu jangwani hata huo Mto.” Kwa upande mwingine, walipokuwa wakisafiri jangwani, Waisraeli walionywa wasije wakaharibu mipaka ya mataifa mengine, kama vile Moabu na Amoni. Hii inatuongoza kufahamu namna yalivyokuwa ya kufaa maneno ya wimbo wa Musa katika Kumbukumbu la Torati 32:8: “Yeye Aliye Juu alipowapa mataifa urithi wao, . . . aliweka mipaka ya watu kwa kadiri ya hesabu ya wana wa Israeli.”—Mwa. 15:13-21; Kut. 23:31; Kum. 2:4, 5, 18, 19.
10. (a) Ni kwa kusudi gani Mungu aliamuru “nyakati zilizowekwa” na “mipaka iliyowekwa”? (b) Juu ya hili, ni maneno gani zaidi na onyo yaliyofuata kutolewa?
10 Sasa twaweza kufahamu kwa njia bora aliyoyamaanisha Paulo juu ya “nyakati zilizowekwa” na “mipaka iliyowekwa ya makazi ya wanadamu.” Ni kwa kusudi gani Mungu aliviamuru hivyo? Mara nyingi, wanadamu wanaweka mipaka, kama vile ukuta mrefu, kuwazuia wale wasiojulikana na wasiotakiwa. Lakini katika mfano huu tunayo tofauti ya kupendeza. Paulo anasema kwamba kusudi lake ni kutenda kama viongozi kwa wanadamu “ili wamtafute Mungu . . . wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.” Hii inategemezwa na ukumbusho wa kwamba mwanadamu anamtegemea Mungu kwa uzima na mwendo, “kama vile watunga mashairi wengine wenu walivyosema, ‘Kwa maana sisi vile vile tu wazao wake.’ “Kisha Paulo anatoa onyo juu ya kutoongozwa vibaya na ibada ya sanamu, namna ya ibada ambayo msingi wake ni ujinga: “Kwa hiyo, kwa maana sisi tu wazao wa Mungu, haitupasi kudhani kwamba Aliyeko wa Kimungu ni . . . kama kitu kilichochongwa kwa ustadi na akili ya mwanadamu.” Tunaposikiliza, twataka kujua tunayohitajiwa kuyafanya juu ya jambo hili. Bila ya kukawia, twaambiwa: “Kweli, Mungu amezisahau nyakati za ujinga huo, hali sasa awaambia wanadamu kwamba imewapasa wote kila mahali watubu.”—Matendo 17:27-30, NW.
11. Nini uliokuwa upeo wa maneno ya Paulo, ikitia ndani mipaka gani ya kitheokrasi?
11 Kwa haraka mtume anaufikia upeo wa maneno yake, walau kwa kadiri ambavyo anaruhusiwa kuendelea. Kwa maneno machache, amefika nyuma kabisa kwenye mwanzo wa kuumba, sasa anaonyesha mambo ambayo Mungu anawaambia wanadamu wafanye, kisha anatoa sababu yake kwa kuufikia wakati ujao. Kwa sababu gani mwito wa kutubu? “Kwa maana [Mungu] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.” (Matendo 17:31) Je! waiona mipaka ya kitheokrasi, “siku” iliyowekwa na “mtu” aliyewekwa anayeahidiwa na Mungu kutoa hukumu ya haki, ifaayo kwa wale wanaomtafuta kwa unyofu? Mipaka hii iliyowekwa inazungumza mambo makuu kuliko “mipaka iliyowekwa ya makazi ya wanadamu” kama ilivyotajwa mapema katika Matendo 17:26 (NW). Kwa kuwa twatamani hukumu ifaayo, sisi leo twapaswa kupata maoni safi ya mpaka kati ya utii na kutokutii kuelekea Mungu, kati ya yaliyo haki na makosa. Usijiamulie mpaka huu mwenyewe. Kama tutakavyoona, inahitaji uangalifu zaidi kuliko unavyofahamika kwa kawaida, ikitia ndani moyo na akili vile vile.
12, 13. (a) Kutajwa kwa ufufuo kulileta matokeo gani kwa watu wengi, isipokuwa kwa watu gani? (b) Ni kwa njia gani tunavyoweza kutazamia kufaidika kwa kutazama nyuma?
12 Mtajo wa Paulo wa ufufuo kutoka kwa wafu uliwalemea walio wengi wa wasikilizaji. “Wengine wakaanza kufanya mzaha, hali wengine wakisema: ‘Tutakusikiliza juu ya hili hata wakati mwingine.’” Lakini, ushuhuda mwema alioutoa Paulo haukuwa bila matokeo kabisa. “Watu wengine wakajiunga naye nao wakawa waamini, miongoni mwao akiwamo Dionisio vile vile, hakimu wa baraza ya Areopago, na mwanamke mmoja jina lake Damari, na wengine pamoja nao.” Twafurahi kujua kwamba wengine walisikiliza kwa kuitikia nao wakawa watiifu.—Matendo 17:32-34, NW.
13 Ilimlazimu Paulo aseme machache wakati huo. Lakini kwetu sisi, tukiwa hatuko chini ya mkazo huo wa ghafula leo, tutaona inatufaa kutazama nyuma na kuona namna gani na sababu gani haja ilitokea ya kumtafuta Mungu mbele ya siku za Paulo, namna ambavyo haja hiyo imetimizwa, na masharti yaliyoko juu yetu.
NAMNA GANI NA SABABU GANI KUTAFUTA KULIANZA
14. (a) Uhakika wa kwamba ilimpasa Yehova kumtafuta mwanadamu ulionyesha nini? (b) Adamu alionyeshaje wazi dhamiri yenye kusumbuka, lakini je! ulikuwapo ushuhuda wo wote wa toba la kweli?
14 Katika Biblia inashangaza kuona kwamba mtajo wa kwanza wa kutafuta si kutafuta kwa upande wa mwanadamu akimtafuta Mungu, lakini tofauti yake. Twasoma katika Mwanzo 3:9: “[Yehova] Mungu akamwita Adamu, akamwambia [kwa kurudia-rudia], Uko wapi?” Lo! hali ya kustaajabisha namna gani! Je! kulikuwa kumetendeka kosa? Ndiyo, tendo baya lilikuwa limetukia, ambalo kama matokeo yake, Adamu na mkewe ‘walipoisikia sauti ya Yehova Mungu, akitembea bustanini... wakajificha kati ya miti ya bustani, Yehova Mungu asiwaone.’ Tunapojaribu kujificha uso wa mtu, mara nyingi ni kwa sababu ya dhamiri inayosumbuka, ikileta woga na aibu. Wewe unayajua maoni. Ndivyo Adamu alivyojisikia alipomjibu Mungu: “Nalisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi; nikajificha.” Kujisikia mwenye woga na kutaka kujificha ni jambo moja, lakini kujisikia mwenye kutubu na kujaribu kurudisha ukamatano mwema ni jambo jingine kabisa. Haikuwako dalili ya hili jambo la pili kwa upande wa Adamu ama mkewe wakati wo wote. Bila shaka, waliyasikitikia matokeo ya tendo lao kwa majonzi, lakini haukuwapo wonyesho wa masikitiko wala aibu kwa sababu ya tendo lenyewe. Nini lililokuwa tendo lao baya?—Mwa. 3:8, 10.
15. Agizo la Mungu katika Mwanzo 2:16, 17 liliwekaje mpaka, kwa halisi na kwa adili?
15 Adamu na mkewe vile vile walikuwa wameruka mipaka fulani ya kitheokrasi, kwa halisi na kwa usemi wa mfano, au kwa adili. Vile vile walikuwa na hatia ya kuingilia haki za wengine. Mungu alipomweka Adamu katika Edeni kwanza, si kwamba alimkaribisha tu Adamu ale kwa uhuru katika kila mti isipokuwa mmoja. Bali, twasoma kwamba Mungu “akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” Mara mbili nyumaye Mungu alilisema kama agizo. (Mwa. 2:16, 17; 3:11, 17) Kwa kupendeza, wakati Shetani, kupitia kwa nyoka, alipomhoji Hawa juu ya agizo hili, hapana ye yote kati yao aliyelisema kama agizo, bali kama jambo tu alilokuwa amelisema Mungu. (Mwa. 3:1, 3) Lakini, kama ilivyotajwa mapema, agizo sikuzote linaweka mpaka mmoja au mingi zaidi. Katika habari hii, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” ulikuwa nje ya mipaka ya Adamu na Hawa kabisa. Haikuwapasa wale tunda lake wala kuligusa. Lakini haukuwa usioweza kufikika; kwa hiyo, ulitokezwa mpaka wenye maana zaidi ya yote wa adili. Agizo la Mungu lililazimisha jaribu la utii wao.
16. Juu ya Hawa, nini kilichosababisha kuvunja mpaka wa adili, ikiongoza kwenye kosa gani zaidi?
16 Kumsikiliza nyoka kwa kuitikia kuliongoza kwenye uvunjaji wa mpaka wa adili. “Mwanamke akaona kwamba ule mti . . . ulikuwa wa kutamanika, naam, ule mti ulikuwa wa kupendeza macho.” Tamaa na hamu zinatoka moyoni. Ingawa alikuwa amelirudia agizo la Mungu wakati huo tu, mwanamke aliacha habari ya uongo iingizwe moyoni mwake kupitia akilini mwake. Alidanganywa kufikiri kwamba yeye mwenyewe angeweza kujiamulia mpaka, ‘akijijulisha mema na mabaya’ mwenyewe. Je! sivyo wafanyavyo watu wengi katika maisha, wakijiwekea kanuni zao wenyewe za yaliyo haki na makosa, au wakizikubali kanuni za wengine? Je! labda ndivyo wewe umefanya, ukitiwa moyo na wengine mbali na Mungu, ukiamini kwamba unyofu ni uongozi wa kutosha?—Mwa. 3:5, 6, NW.
17. Hii ilifuatwaje na kuvunjwa kwa mpaka wa halisi, vile vile kuingiliwa kwa haki za wengine?
17 Nyuma ya Hawa kuuvunja mpaka wa adili kwa kutamani isivyofaa na kuamua kula tunda lililokatazwa, kulifuata upesi kuvunjwa kwa mpaka wa halisi. Yeye “alitwaa katika matunda yake akala, akampa na mumewe, naye akala.” (Mwa. 3:6) Kuruka mpaka mara nyingi kunamaanisha kuingilia haki za wengine. Katika kisa hiki, Hawa kwanza aliingilia haki za mumewe juu ya ukichwa, akiiweka hiari mikononi mwake mwenyewe. La maana zaidi, wote wawili waliingilia haki za Yehova Mungu kwa kujiamulia mwendo wao wenyewe katika tendo na roho ya kutokutii. Kwa makusudi wakaruka mpaka. Yaani, kwa makusudi waliupuza mpaka wa Mungu kati ya lililofaa na lisilofaa, nao wakajiwekea wao wenyewe. Kwa matokeo gani?
18. (a) Mungu alizilindaje haki zake? (b) Ni kwa kadiri gani wanadamu wamepaswa na kutokutii kwa Adamu, ikitokeza maulizo gani?
18 Nyuma ya hukumu ya Mungu kutangazwa, Adamu na mkewe walifukuzwa katika makao yao ya bustani. Kuyarudia kulifanywa kusiwezekane. Yehova “akamfukuza huyo mtu, akaweka Makerubi, upande wa mashariki wa bustani ya Edeni, na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.” (Mwa. 3:24) Hii ilikuwa alama ya mpaka yenye kukataza; kizuizi kisichopenyeka kwao. Lililo baya zaidi, walifukuziwa mbali watoke machoni pa Yehova. Kama watoto wa Adamu, sote, ‘tukiwa tumefanywa kutoka kwa mtu mmoja,’ tunapaswa kwa njia kubwa. Kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa na kutokamilika, pasipo kutaja ‘zamani za ujinga’ tunamoishi, sisi tumefarikishwa na Mungu. (Matendo 17:26, 30) Hata hivyo, kuna dini nyingi zinazozoewa kati ya watu waliofarikishwa na Mungu. Kuna dini nyingi, na watu wengi wanaridhishwa na dini yao yenyewe. Wanajiamulia wenyewe kati ya mema na mabaya katika mambo ya dini au ambapo pana ulizo la adili la kuangaliwa. Je! wewe wafanya hivyo? Na je! hii maana yake hakuna tumaini? Je! kumtafuta Mungu wa kweli na dini ya kweli ni kazi bure? Je! kutafuta huku kwaweza kumalizwa kwa ajili yetu kwa matokeo mazuri? Angalia lililotukia mwanadamu alipofukuzwa katika Edeni, na faraja iwezayo kupatikana katika hili.
NAMNA AMBAVYO KUTAFUTA KWAWEZA KUMALIZWA
19. Ni tofauti gani inayoonekana kati ya wana wawili wa kwanza wa Adamu, nao mwendo wa Kaini ulikuwaje?
19 Wana wawili wa kwanza wa Adamu, kwa njia ya kulinganisha, wanatoa mengi yatakayotusaidia katika kutafuta kwetu. Kila mmoja wao alimletea Yehova sadaka, lakini, kama matukio yalivyoonyesha, kila mmoja wao akiwa na nia tofauti. Labda sadaka ya Kaini ya “mazao ya ardhi” ilikuwa desturi tu, asije akashindwa na nduguye mdogo, Habili, aliyeleta sadaka bora ya “wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama.” Kwa njia fulani isiyoonyeshwa wazi, Yehova alimpendelea Habili na sadaka yake, lakini “Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake.” Kwa hiyo, Kaini “akaghadhibika sana.” Kisha Yehova akamwonya kwa upole: “Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.” Hii yafunua kwamba Kaini alikuwa amekuwa akitenda kwa njia mbaya, kwa wazi akitafuta “kibali” kwa roho ya kichoyo, ya ushupavu. Kwa njia yenye hatari alikaribia kuuruka mpaka wa kujiweza. Aliuruka, naye akawa mwuaji wa kwanza. Yeye “akatoka mbele za uso wa [Yehova], akakaa katika nchi ya Nodi,” nchi ya kuikimbia haki.—Mwa. 4:3-16.
20. Ni kwa njia gani Habili angeweza kukuza imani yenye nguvu, ikiambatana na sifa gani nzuri nyingine?
20 Tunapomtazama Habili, lo! mfano tofauti wenye furaha namna gani! Kwa njia fulani Mungu alimpendelea. Habili alijua hili kabisa. Paulo analitilia mkazo, akisema kwamba “kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo, ijapokuwa amekufa, angali akinena.” (Ebr. 11:4) Imani ya Habili ilikuwa na msingi mzuri. Bila shaka alikuwa ameelezwa habari zote za mipango mingi ya Yehova iliyofurahiwa katika Bustani ya Edeni. Bila shaka alijua namna Yehova alivyokuwa amesema na Adamu kama vile baba akisema na mwanawe. Aliijua ahadi ya Edeni na unabii wa Yehova Mungu juu ya kupondwa kwa kichwa cha nyoka, naye alikuwa na tumaini hakika la utimizo wake, ingawa bila ya kujua wakati barabara ama kwa njia gani. Mbali na imani na tumaini, yeye alikuwa na ile sifa nyingine iliyo nzuri zaidi. Yeye alisitawisha upendo wa kweli kwa Yehova, ukiambatana na maono yenye nguvu ya uaminifu na shukrani, yenye nguvu za kutosha kuyashinda maongozi mabaya na mfano wa wazazi wake na nduguye mkubwa.—Mwa. 3:15; 1 Kor. 13:13.
21. Ni faraja gani tuwezayo kupata kutokana na kumwangalia Habili?
21 Kwa Habili, ukiwapo ushuhuda wa baraka ya Yehova juu yake, kumtafuta Mungu wa kweli kulimalizwa. Yeye hakuwa na haja ya kumtafuta Mungu, isipokuwa katika maana ya kujaribu sikuzote kushika kibali chake Yeye kwa mwenendo ufaao katika roho ya utii wa kweli wa kupenda. Kilichowezekana kwa Habili chawezekana kwako. Tutatazamia kulichunguza Neno la Mungu kwa matumaini kwa uongozi zaidi na faraja. Kumbuka namna Yehova alivyomsaidia Habili, na, twaweza kusema, hata akamtolea Kaini msaada.
[Picha katika ukurasa wa 35]
Mtume Paulo, akisema na Waathene juu ya Areopago aliwatia moyo wamtafute Mungu wa kweli
[Picha katika ukurasa wa 37]
Mungu alipowaumba Adamu na Hawa, Yeye aliwapa wanadamu “uso wa nchi yote” uwe makazi yao
[Picha katika ukurasa wa 40]
Hawa aliuvunja mpaka uliowekwa kwa kimungu kwa kulila tunda lililokatazwa