Je! Wewe Unafundisha Watoto Wako?
“Maneno haya ninayokuamuru . . . uwafundishe watoto wako kwa bidii.”—Kum. 6:6, 7.
1. Kwa sababu gani ni muhimu sana kwamba wazazi wawafundishe watoto wao?
JE! WEWE unapendezwa kwa unyofu kuona watoto wako wakikua wawe waaminifu, watu wanyofu wampendao Mungu na mwanadamu mwenzao? Bila shaka hii ni mojawapo ya tamaa zako kubwa. Lakini je! unajua kwamba kama tamaa hii inatimilizwa au sivyo inategemea sana juu ya namna unavyowafundisha? Hii ni kweli. Na zaidi ndivyo ilivyo sasa wakati ambapo kuna mikazo mingi sana juu ya vijana kugeukia ufisadi, kutumia dawa za kulevya kwa njia mbaya na namna nyingine za uasi. Ndiyo sababu kufundisha watoto wenu ni mojawapo ya kazi za muhimu zaidi mtakazozifanya ninyi wazazi katika maisha. Je! unaliona jambo hili kama lenye muhimu huu? Je! unajua linaloweza kutukia, na linalotukia kweli katika jamaa ambapo wazazi wameshindwa kuendelea kwa kawaida kupashana habari kwa hiari na watoto wao?
2, 3. Ni jambo gani lililotokea kweli linaloonyesha kinachoweza kutukia wakati kupashana habari kati ya wazazi na mtoto kunapokoma?
2 Majuzi gazeti lijulikanalo sana lilisimulia juu ya jamaa moja katika Long Island, New York, ambamo mlikuwa hamna kupashana habari. Mvulana huyu alikuza vipindi vya chuki, kimya na kufanya vita. Mwishowe alianza kutumia dawa za kulevya. Wazazi wakagundua, lakini wasiweze kweli kulizungumza jambo hili naye. Mahali pake, kulikuwako mabishano yenye hasira tu, naye mvulana huyu akayadharau maagizo ya wazazi wake kuacha kutumia dawa za kulevya. Katika jamaa nyingine nyingi katika mzingo wa wazazi wa marafiki, watoto vile vile walikuwa watumiaji wa dawa za kulevya. Kwa kweli, mwanasheria mmoja wa wilaya alikadiri kwamba robo tatu za vijana nchini walikuwa wamekwisha kujaribu bangi na dawa nyingine za kulevya!
3 Katika jamaa hii, hali ziliharibika hata baba akawa anampigia mwanawe kelele, naye mwanawe akawa akimpigia kelele vile vile na kuwatisha wazazi wake. Mwishowe, Jumapili alasiri, Februari 27, 1972, akiwa chini ya maongozi ya dawa za kulevya, mvulana huyu alimjia baba yake na kisu cha mezani. Baba akachomoa bunduki aliyokuwa amebeba ajilinde naye akaifyatua hata moyoni mwa mwanawe. Alipoulizwa nyumaye sababu gani alikusudia kuua, baba alisema: “Niliyoweza kufikiria tu ni kwamba kama ningemjeruhi tu mvulana huyo, angerudi na kumwua Carol [mama yake] na mimi. Kulikuwako vitisho vingi sana.” Lo! msiba huo!—Life, Mei 5, 1972.
4. (a) Kama inavyoonyeshwa na 2 Timotheo 3:14, 15, imempasa mtu aanze kuwafundisha watoto wake wakati gani? (b) Njia za kupashana habari zawezaje kuendelezwa kuwa wazi watoto wanapokua?
4 Ni wazi kwamba kuna uhitaji mkubwa kwa wazazi kuwa na kupendezwa na kuwafundisha watoto wao na kuziweka njia za kupashana habari kwa hiari wazi sikuzote! Biblia yaonyesha kwamba wakati wa kuanza kujitahidia hili ni wakati ambapo watoto ni wachanga sana. (2 Tim. 3:14, 15) Kisha zapaswa jitihada ziendelezwe kila siku, kila mwaka, tangu utoto uchanga hata kupita ujana. Hakuwezi kuwako kuchoka katika mpango wa kufundisha. Ikiwa watoto wataupokea uongozi wanaouhitaji sana, lazima wazazi waendelee kujitahidi kushika ujamaa utakaowatia watoto wao moyo wa kuzungumza nao kwa hiari na kuwatumaini.
UONGOZI WA KIMUNGU WANAOUHITAJI WATOTO
5, 6. (a) Hata ingawa wazazi wengine wanajaribu kuwalea watoto wao ipaswavyo, kwa sababu gani wanapata matokeo yenye msiba? (b) Ni maagizo gani bora ambayo Mungu aliwapa watu wake Israeli juu ya kulea watoto?
5 Lakini, hata wazazi wengine wanaojitahidi kweli kweli kuwalea watoto wao ifaavyo wanapata matokeo yenye msiba, kama inavyoshuhudiwa katika kisa cha jamaa iliyotajwa juu. Kwa mfano, baba alikuwa akijaribu kumsaidia mwanawe kwa kuchukua vitabu vya wanyama na uangalizi wao katika maktaba, jambo lililompendeza mwana. Nao wazazi wote wawili walimtia mvulana huyu moyo apendezwe na michezo. Lakini, zijapokuwa jitihada zao, kwa wazi kilikosekana kitu fulani, kama ilivyo katika nyumba nyingi sana leo. Nacho ni kitu gani kinachokosekana? Wazazi wanakosa kuyatii sana maagizo YA MUNGU juu ya kulea watoto. Zamani za kale Yehova Mungu aliwapa watu wake Israeli shauri juu ya namna ya kuwalea watoto wao. Na linalofurahisha ni kwamba uongozi huu umehifadhiwa katika neno lake Biblia kusudi kwamba wazazi leo waweze kufaidika kutokana nao.
6 Yehova Mungu alimtumia mnenaji wake Musa kutoa maagizo haya kwa watu wake: “Na hii ndiyo sheria, na amri, na hukumu, alizoziamuru [Yehova], Mungu wenu, mfundishwe . . . Sikiza, Ee Israeli; [Yehova], Mungu wetu, [Yehova] ndiye mmoja. Nawe mpende [Yehova], Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa nguvu zako zote. Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako. Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.”—Kum. 6:1, 4-9.
7. (a) Katika maagizo haya ya Mungu, ni jambo gani la kwanza lililo muhimu linalotajwa kwa kulea watoto kwa matokeo mema? (b) Kwa sababu gani ni muhimu kutumia wakati pamoja na watoto hata ingawa huenda ikahitaji marekebisho katika mipango?
7 Kuliko kulipita shauri hili la kimungu kwa haraka, ebu na tulifikirie kwa makini. Linakazia nini kwa wazazi? Kwanza, je! halionyeshi umuhimu wa wazazi kutumia wakati wakiwa pamoja na watoto wao? Angalia kwamba linazungumza juu ya mzazi na mtoto wakiwa pamoja ‘wanapoketi katika nyumba, na watembeapo njiani, na walalapo, na waondokapo.’ Umuhimu wa kutumia wakati pamoja na watoto wako hauwezi kutiliwa mkazo kupita kadiri. Hii ni kwa sababu watoto ambao wazazi wao hawana wakati mwingi wa kutumia nao mara kwa mara wanajitia katika mabaya. Kweli, huenda kupanga kuwa na watoto wako muda mwingi zaidi kukahitaji kufanya shauri, pengine hata kukuhitaji ujinyime raha fulani za kipekee na utendaji mwingine. Lakini thawabu ya kuwakuza watoto wako wawe wanaume na wanawake wenye kutii sheria na wenye heshima bila shaka inastahili jitihada hii.
8. (a) Nini kingine anachosema Mungu yawapasa wazazi wafanye, na je! watu wazee kwa ujumla leo wana bidii juu ya kufanya hivi? (b) Ikiwa mtu ana kazi nyingi kweli kweli wakati watoto wanapotaka kuzungumza, anaweza kufanya nini? Kwa sababu gani?
8 Lakini, kuwa pamoja tu na watoto wako siyo yote yanayohitajiwa. Angalia kwamba maagizo ya Mungu yanasema ‘tunene’ na watoto vile vile. Haiwapasi wazazi waudharau umuhimu wa kusema na watoto wao wakati wo wote. Na msisahau, sehemu ya muhimu ya mazungumzo ya watu wawili ni kusikiliza. “Manung’uniko ya msingi ya Waamerika vijana,” alisema mwandikaji mmoja maarufu, ni “kwamba wao hawawezi kuzungumza na watu wazima. . . . Jitihada zao za kupashana habari na sisi ni sawasawa sikuzote nazo ni za dharau kabisa.” Kwa bahati mbaya, mara nyingi hii ni kweli. Mara kwa mara wazazi wanamsukumia mbali mtoto wao mwenye kuuliza ulizo kwa sauti kali: “Ondoka; huoni nina kazi nyingi?” Usiruhusu hili litukie nyumbani mwako wakati wo wote! Ikiwa ni kweli una kazi nyingi sababu gani usimwambie mtoto wako utalizungumza jambo hilo nyumaye pamoja naye, halafu ufanye hivyo? Kwa njia hii mtoto wako ataona kwamba unapendezwa naye kweli na atakutumaini wewe kwa hiari zaidi. Kwa hiyo ulitii shauri la Biblia la kimungu! Sema na watoto wako, nawe ufanye hivyo kwa kawaida, kama Mungu asemavyo: “Uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”
“MANENO HAYA” LAZIMA UYAFUNDISHE
9. (a) Ni maulizo gani yanayotokezwa juu ya “maneno haya” ambayo Mungu anasema wamepaswa watoto wafundishwe? (b) Ni mafundisho ya namna gani, yajapokuwa ya muhimu, yameonekana kutokutosha?
9 Lakini kutumia wakati ukiwa na watoto wako na kuzungumza nao hakutoshi bado. Ukiyatazama maagizo ya Mungu tena, utaona kwamba Yeye anaeleza mambo ambayo yawapasa wazazi wayazungumze na watoto wao. Yeye anasema: “Maneno haya . . . lazima uyasisitize katika mwana wako na kuyazungumza (NW).” “Maneno haya” ni nini? Je! ni juu ya mafundisho ya kawaida, kuwafundisha watoto wako kuona ubora wa muziki mzuri, vitabu vizuri, maajabu ya maisha na mambo mengine mazuri sana yanayotuzunguka? Je! ni juu ya adabu njema na tabia zifaazo, kama vile kuwa malidadi, mwenye utaratibu, kufika mahali wakati unaotakiwa, na mengineyo? Bila shaka haya ni mambo mema kufundisha watoto. Lakini je! si kweli kwamba wazazi wengi waliowafundisha watoto wao mambo kama hayo wameshtuka kugundua kwamba watoto wao wamejitia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya, au tendo jingine la uhalifu, au kwamba binti zao wamepata mimba kama matokeo ya ngono isiyoruhusiwa? Kwa wazi kuna jambo fulani lililo bora hata zaidi ambalo imewapasa wazazi wawafundishe watoto wao.
10. (a) Zaidi, “maneno haya” ambayo yawapasa wazazi wawafundishe watoto wao ni nini? (b) Neno “kusisitiza” lina maana gani, na kwa hiyo, kwa kweli Mungu anaambia wazazi nini?
10 Uchunguzi wa makini zaidi wa maagizo ya Mungu wafunua kwamba Mungu anazungumza juu ya kuwatolea watoto mambo ya kiroho. Wazazi wanaambiwa, “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” “Nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na nafsi yako yote na nguvu zako zote. Na maneno haya . . . lazima uyasisitize katika mwana wako (NW).” Ndiyo, wanalopaswa wazazi kuwafundisha watoto wao kwanza ni juu ya Yehova Mungu—kwamba yeye ndiye Muumba aliye wa pekee na Mpaji wa Uzima—na kwamba anaustahili upendo wetu wa nafsi yote na ibada. Nawe angalia kwamba Mungu hasemi kwamba mambo haya yamepaswa yasemwe tu kwa watoto, lakini anasema: “Lazima uyasisitize katika mwana wako.” Kulingana na Webster’s Third New International Dictionary, neno la Kiingereza kwa “kusisitiza” linamaanisha “kufundisha na kukazia kwa kurudia-rudia au kuonya mara kwa mara: kusihi sana au kukazia akilini.”a Yaani, hapa Mungu anawatia wazazi moyo waanzishe mpango uliofanyiwa shauri wa mafundisho ya Biblia ulio na kusudi la wazi la kukazia akilini mwa watoto wao mambo ya kiroho.
11. Ni mambo gani mengine yanayotiwa ndani ya “maneno haya” ambayo imewapasa wazazi wayasisitize katika watoto wao, na twajuaje?
11 Lakini “maneno haya” yanayopaswa kusisitizwa katika watoto yanatia ndani na kanuni za Mungu za adili au matakwa vile vile. Hii inaonyeshwa na maneno yanayozunguka habari ambamo maagizo haya kwa taifa la Israeli yanapatikana. Nabii Musa alikuwa ametoka tu kuzirudia amri zilizo kubwa za sheria ya Mungu kwa Israeli, yaani, kutokutoa ushuhuda wa uongo, kutokuiba, kutokuua, kutokufanya uzinzi, na nyinginezo. (Kum. 5:6-21) Na kwa kuwa muda mfupi nyuma ya hapo Musa aliendelea kusema, “Na maneno haya . . . lazima uyasisitize katika mwana wako,” ni wazi kwamba wazazi walikuwa wanakaziwa umuhimu wa kutoa ubora wa adili kwa watoto wao. Ni mafundisho ya namna ile ile wanayopaswa wazazi wa Kikristo kuwapa watoto wao leo ikiwa watawahakikishia kuwa na wakati ujao wenye usalama na furaha.—Mt. 22:37-40; 1 Kor. 6:9, 10; Ufu. 21:8.
12, 13. (a) Ni akina nani walio na daraka kubwa la kufundisha watoto? (b) Maana yake nini kuwalea watoto katika “rekebisho la moyoni la Yehova”?
12 Kwamba baba na mama vile vile wana pendeleo na daraka la kushiriki katika kutoa mafundisho haya inaonyeshwa na amri ya Biblia kwa watoto: “Mwanangu, shika maagizo ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Mit. 6:20) Lakini, likionyesha ni nani anayechukua daraka kubwa la kuwafundisha watoto, Neno la Mungu linasema: “Ninyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika adabu na rekebisho la moyoni la Yehova.” (Efe. 6:4, NW) Ndiyo, zaidi ni akina baba wa Kikristo wanaokabidhiwa daraka la kuwafundisha watoto wao.
13 Lakini, maana yake nini kwa akina baba kuwalea watoto wao katika “rekebisho la moyoni la Yehova”? “Rekebisho la moyoni,” katika Kigiriki cha kwanza, lina maana ya “kutia nia katika.” Na kwa hiyo baba za Kikristo hapa wanasihiwa watie nia ya Yehova Mungu katika watoto wao. Nao huu utakuwa ulinzi kama nini kwa watoto wao! Kwa maana ikiwa watoto wamesisitiza akilini mwao mawazo ya Mungu, njia yake ya kufikiri, huu utakuwa ulinzi wa ajabu juu ya kujitia kwao katika kutenda mabaya.
KUITIA NIA YA MUNGU KATIKA WATOTO WAKO
14. Nini kingine kinachohitajiwa kwa kawaida ili kuitia nia ya Mungu katika watoto mbali na kuwaambia tu sheria za Mungu?
14 Lakini inakubaliwa si vyepesi kuwalea watoto katika rekebisho la moyoni la Yehova. Kuwaambia tu nia ya Mungu juu ya mambo mara nyingi hakutoshi kuwafanya wayakubali ayasemayo Mungu. Hivyo huenda mzazi akamsomea mwanawe au bintiye kutoka katika Biblia juu ya sheria za Mungu zinazokataza uasherati, hata akafanya hivyo mara nyingi sana. (Gal. 5:19, 21; Efe. 5:5) Kurudia-rudia huko huenda kukazie juu ya watoto sheria ya Mungu ni nini. Lakini, mara nyingi kutia nia ya Mungu ndani yao kunahitaji mengi zaidi. Wamepaswa watoto wasaidiwe kufikiri juu ya ubora wa sheria ya Mungu kusudi kwamba wasadiki kwamba ni ya haki na ni njema, na ni kwa ajili ya faida yao. Unapofikiri pamoja nao juu ya usawa wa Maandiko, watakuja kupatana kabisa na maoni ya Mungu. Ndipo, kwa njia hiyo, iwezapo kusemwa kwamba umeitia nia ya Mungu ndani yao.
15. (a) Ni vema kujua nini ili kuitia nia ya Mungu katika watoto, na awezaje mzazi kugundua hili? (b) Mzazi aweza kutenda namna gani mtoto wake akitoa maoni yenye makosa?
15 Ukiwa umesadiki kwamba imekupasa ujaribu kuitia nia ya Mungu katika mtoto wako, waweza kuchukua hatua ya kwanza ya muhimu katika kufanya hivyo kwa kuchunguza anayoyafikiri mtoto wako. Mara nyingi maulizo yanayofaa yatavuta mawazo yake ya ndani yenyewe. Kwa mfano, katika kuzungumza naye juu ya sheria ya Mungu inayokataza uasherati, waweza kuuliza: “Je! wafikiri kwamba twafaidika kutokana na utiifu kwa sheria hii ya Mungu, au inatuondolea furaha yetu?” Au ungeweza kuuliza: “Kuna tofauti gani kama tunaishi kwa kulingana na sheria ya Mungu au sivyo?” Nyuma ya kuuliza ulizo kama hilo, yakaribishe maoni ya mtoto wako. Ukimkemea au kumlaumu vikali ambapo maoni anayoyatoa ni yenye makosa, huenda hii ikagandamiza kupashana habari kutakakofuata. Bali, sababu gani usimshukuru kwa kuwa mnyofu katika kutoa mawazo yake, na kumtia moyo awe akizungumza nawe kwa hiari sikuzote? Umetimiliza mambo mengi ikiwa mtoto wako anakueleza mawazo yake ya ndani yenyewe. Inakuweka wewe katika hali bora ya kuzungumza naye.
16. Mzazi anaweza kumsaidia mtoto wake aufahamu usawa wa sheria ya Mungu inayokataza uasherati kwa njia gani?
16 Ukigundua kwamba maoni ya mtoto wako ni yenye makosa, basi uwe tayari kufikiri pamoja naye juu ya jambo lenyewe. Kwa mfano, waweza kukazia fikira kwenye utaratibu wa mwujiza sana wa uzazi ambamo chembe moja iliyotiwa mimba inagawanyikana na kuongezeka kulingana na mpango uliowekwa mapema ikawe kitoto cha kibinadamu, halafu uulize: “Je! hufikiri kwamba Yeye aliyekusudia utaratibu huu wa ajabu wa uzazi ajua mengi zaidi sana juu ya namna iwapasavyo wanadamu kuutumia uwezo wao waliopewa na Mungu wa uzazi?” (Zab. 139:13-17) Au ungeweza kuuliza: “Je! wafikiri kwamba Muumba wetu mwenye upendo angeweza kufanyiza sheria kusudi atuondolee furaha yetu ya maisha? Au wafikiri sheria zake zilifanyizwa ziiongeze furaha yetu?” (Zab. 145:16) Maulizo kama hayo yanaweza kumfanya mtoto wako aanze kulifikiri jambo hilo. Halafu labda waweza kukazia fikira zake kwenye mifano ya namna ufisadi ulivyoelekeza kwenye kukata tamaa, magonjwa ya kisonono na kaswende na msiba. (2 Sam. 13:1-33) Kwa njia hii mtoto anasaidiwa kuiona busara na usawa wa sheria ya Mungu. Kama matokeo, huenda akaja kuyakubali maoni ya Mungu, nawe kwa njia hiyo utakuwa umeitia nia ya Mungu ndani yake.
17. Sala inaweza kusaidiaje katika kulea watoto katika “rekebisho la moyoni la Yehova”?
17 Katika njia ile ile, utataka kuitia nia ya Mungu ndani ya watoto wako juu ya mambo mengine mengi, kwa mfano, ukisisitizia ndani yao sheria za Mungu juu ya kusema kweli, kuwa mwenye fadhili, mwenye amani, mwenye upendo, na nyinginezo. Lakini ikiwa una magumu katika kuwafundisha watoto wako, je! ufanyeje? Manoa, baba yake Samsoni, alimwomba Yehova uongozi katika kumlea mvulana wake. (Amu. 13:8-14) Sababu gani usiufuate mfano wake? Sala kwa Yehova yaweza kutimiliza mengi sana. Baba mmoja alieleza kwamba nyakati nyingi mwanawe alipokuwa mwenye huzuni na kusema machache, yeye alikuwa akienda kwenye chumba chake usiku na, akiisha kubisha hodi, kuingia na kusema: “Mwanangu, hakuna jambo jingine ambalo ningaliweza kufanya lakini naona kwamba huonekani kuwa katika hali yako ya kawaida siku chache hizi zilizopita. Je! una jambo fulani akilini mwako, jambo tuwezalo kulizungumza?” Kwa kawaida waliweza kuzungumza, naye baba alikuwa anashauri kuuomba msaada wa Yehova, akisema: “Itakuudhi nikifanya hivyo kwa ajili yetu?” Sala ilipokwisha, na walipoisha kulizungumza jambo lenyewe, kwa kawaida mwana alifaidika sana. Magumu yanapotokea, kusali pamoja na watoto wako, kuuomba uongozi wa Yehova, kutakuwa msaada katika kuwalea katika “rekebisho la moyoni la Yehova.”
18. Ni nini mbali na uwezo wa kufundisha kinachohitajiwa kulea watoto katika “rekebisho la moyoni la Yehova”?
18 Kwa kweli mengi yanatiwa ndani katika kutia nia ya Mungu ndani ya watoto wako, pamoja na wakati mwingi sana, jitihada na uwezo wa kufundisha. Na hali si shauri la kukamilisha njia fulani za kufundishia, bali, ni upendo wako kwa watoto wako, unaoshuhudiwa na kuwafundisha kwa bidii, kusadikisha na shauku, utakaokuwa na matokeo sana katika kuwalea katika “rekebisho la moyoni la Yehova.” (Mit. 3:1-7) Vile vile, watoto wako watasaidiwa ukiwaeleza kwamba wewe, vile vile, u chini ya wajibu wa kuzitii sheria za Mungu, na kwamba unashukuru kwa ajili ya sheria hizi kwa maana zimekusaidia kufurahia maisha bora. Je! wewe una mpango wa kawaida wa kuwafundisha watoto wako, ukianza kufanya hivyo wakati ni wachanga sana, hata kutokea wanapokuwa wadogo sana?
MSAADA BORA KATIKA KUFUNDISHA WATOTO
19. (a) Ni msaada gani uliotolewa na Watch Tower Society wa kuwasaidia wazazi wawafundishe watoto wao? (b) Mengine ya masomo yanayofundishwa katika msaada huu ni nini?
19 Kwa maana Watch Tower Society ilifahamu namna ilivyo kazi ngumu kwa wazazi kulea watoto katika hii taratibu mbovu ya mambo, ilipanga kwamba msaada utolewe kwa wazazi katika kufundisha watoto wao. Kuanzia na toleo la Machi 1, 1971 la Mnara wa Mlinzi, ulichapwa mfululizo wa makala ‘zilizokusudiwa hasa kwa wazazi wazisome pamoja na watoto wao.’ Makala hizi zilionekana karibu katika kila gazeti kufikia toleo la Mei 1, 1973. Halafu katika mwaka wa 1971 kitabu kidogo Listening to the Great Teacher kikatolewa kienezwe. Hakina makala hizi zilizofanywa nyepesi kufahamika za Mnara wa Mlinzi tu, lakini hata na habari nyingine. Kila habari imekusudiwa kukazia akilini mwa mtoto kanuni fulani au fundisho la Neno la Mungu. Kwa jumla, kuna habari 46 zenye msingi wa mifano, mafundisho, miujiza na mambo yaliyompata Mwalimu Mkuu maishani, Yesu Kristo. Kwa mfano, ile inayoitwa “Jirani Mwema” inakazia shauri la kwamba imetupasa tuwe wenye fadhili kwa kila mtu; “Mwenye Ukoma Mmoja Alimtukuza Mungu” inaonyesha kwamba haitupasi tusahau kusema ‘Asante’; “Mtumwa Asiyesamehe” inakazia umuhimu wa kuwa wenye kusamehe; “Wenye Furaha Ni Wenye Amani” inaeleza sababu gani haitupasi tujitie katika mapigano; “Watu Wawili Ambao Hawakusema Kweli” inafundisha kwamba imetupasa tuseme kweli sikuzote, na kuna masomo mengi bora yaliyofundishwa.
20, 21. Ni faida gani zilizopatikana kwa kutumia msaada huu wa kufundishia?
20 Wakati habari hii ilipoanza kuchapwa, barua nyingi zilianza kupokewa zikionyesha shukrani kwa msaada huu wa kufundishia. Mzazi mmoja aliandika: “Matokeo yamekuwa ya kustaajabisha. Si kwamba binti yetu si mwasi tena tu, lakini hawezi kungoja mpaka Mnara wa Mlinzi ufike ndipo azisome makala hizi.” Mama mmoja alieleza: “Nilikuwa na wakati wenye shida nyingi kuwafanya watoto wangu wajifunze Biblia pamoja nami. Walijaribu kila walichoweza wajiepushe na funzo. Sasa, kwa sababu ya shauku wanayoionyesha, mume wangu, aliyekuwa asiyeamini, ameanza kujifunza Biblia.” Baba mmoja aliandika: “Nimekuwa na ugumu kuwapasha watoto wangu kweli kutoka kwa Yehova kwa maana lazima mtu azieleze kwa njia fulani anayoweza kufahamu mtoto. Makala hizi zimenisaidia mimi kuzungumza nao katika njia ya kupendeza na ya kufurahisha zaidi. Tumalizapo kuzisoma makala watoto wote watano wanasema pamoja, ‘Ati sasa tu tumemaliza?’”
21 Hata watu wasio mashahidi wa Yehova wameuona huu kuwa msaada bora katika kufundisha watoto. Mwalimu wa shule aliyekuwa amepewa kitabu Listening to the Great Teacher alisema: “Nashukuru sana. Hiki ndicho kitu kile kile ambacho nimekuwa nikitafuta. Wengi wa watoto hawa hawazoezwi sana nyumbani kwa hiyo lazima tuwafunze mambo mengi ya msingi kama vile kutokusema uongo, kutokuiba, na mengineyo. Leo niliwasomea sura ya kwanza kwa maana lazima wajue Mwalimu Mkuu ni nani.” Mtoto mwenye umri wa miaka saba katika shule moja ya Indiana alijitolea alisomee darasa lake kitabu hiki. Kufikia Machi 1972 alikuwa amekwisha kuwasomea sura 30, na wengi shuleni wakajipatia vitabu.
22. Nini iliyo zawadi nzuri kupita zote ambayo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao?
22 Je! wewe unautumia msaada huu bora kufundisha watoto wako? Bila shaka unahitaji kila msaada uwezao kupokea usisitizie katika watoto wako mashauri ya kiroho na ubora wa adili ambavyo Mungu ameamuru kwamba watoto wafundishwe. Wazazi wengi wameona kuwa kitabu Listening to the Great Teacher ndicho kitu kile kile walichohitaji ili kufanya hivi. Kwa hiyo usikose kukitumia kwa kawaida. Kwa kweli, hakuna zawadi bora uwezayo kuwapa watoto wako kuliko kuwapa mafundisho ya kiroho yanayotia ndani yao nia ya Mungu!
—Kutoka The Watchtower, Sept. 15, 1973.
[Maelezo ya Chini]
a Hii, vile vile, ndiyo maana ya neno la asili la Kiebrania, namna yenye mkazo ya sha·nanʹ, inayomaanisha “kurudia,” “kusema tena na tena,” “kukazia sana.”