Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/1 kur. 550-552
  • Yehova Aleta ‘Kutiwa Muhuri’ kwa Wateule Wake Kwenye Kikomo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Aleta ‘Kutiwa Muhuri’ kwa Wateule Wake Kwenye Kikomo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘KUTIWA MUHURI’ KWA MWISHO
  • KUJICHUNGUZA MWENYEWE
  • MFANO
  • MAMBO AMBAYO YATAFANYWA NA WALIOTIWA MAFUTA KWA KWELI
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Ni Nani Ambao Kwa Kweli Wana Mwito wa Mbinguni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • “Tutakwenda Pamoja Nanyi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/1 kur. 550-552

Yehova Aleta ‘Kutiwa Muhuri’ kwa Wateule Wake Kwenye Kikomo

MTUME Paulo aliwaandikia ndugu zake waliozaliwa kwa roho hivi: “Roho yenyewe hushuhudia pamoja na roho yetu kwamba sisi tu watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi tu watoto, sisi tu warithi pia: warithi kweli wa Mungu, lakini warithi washirika pamoja na Kristo, tukiteswa pamoja ili tupate kutukuzwa pia pamoja.”​—Rum. 8:16, 17, NW.

‘Kushuhudia’ huku kwafanywaje? “Roho yetu,” yaani, nia kuu ya Wakristo hawa waliozaliwa kwa roho, yageuzwa na roho takatifu ya Mungu hata wanakuja kuujua ujamaa walio nao na Mungu. Lakini hili halifanywi kwa njia ya fumbo. Neno la Mungu, kushughulika kwake na kundi la Kikristo, “chakula kwa wakati wake” kupitia kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” elimu ambayo ndugu zetu wanatusaidia kuipata na maoni mazuri ya makusudi ya Mungu pamoja na utimizo wa unabii, vyote vyaungana na utendaji wa roho takatifu ya Mungu, katika ‘kushuhudia’ huku.

‘KUTIWA MUHURI’ KWA MWISHO

Mahali pamoja pa Biblia panapoonyesha utendaji wa Mungu kwa watiwa mafuta wake duniani wakati huu ni Ufunuo 7:l-8. Humo, malaika wenye kuzizuilia pepo zenye kuharibu za “dhiki kubwa” wanaambiwa wasiziachilie mpaka Waisraeli wa kiroho 144,000 ‘wametiwa muhuri’ katika vipaji vya nyuso zao. (Mt. 24:21) Huku ‘kutiwa muhuri’ ni nini? Wengine wamekuelewa kumaanisha kwamba, mnamo “mavuno” ya kiroho, ambayo ndiyo “mwisho wa taratibu ya mambo,” uteuzi wa ndugu za kiroho za Masihi Yesu utaendelea mpaka mwaka wa mwisho, siku, saa na dakika mbele ya “pepo nne” kuanza kuvuma duniani. Je! huu ndio ufahamu ufaao? Sivyo. Kwa sababu gani sivyo?​—Mt. 13:39, 40, NW.

Basi, ‘kutiwa muhuri’ kunakotajwa hapa hakumaanishi mwanzo wa kutiwa muhuri kwa 144,000, kana kwamba wote hawa, zaidi wote wale ambao wangali duniani, hawakuwa wametiwa muhuri. Mtume Paulo anaonyesha kwamba kutiwa muhuri huku kwa kwanza kunatukia wakati wa uteuzi wa mtu kwa ajili ya urithi wa kimbinguni. Anawaambia ndugu zake wa kiroho hivi: “Kwa njia ya [Kristo] pia, baada ya mlipoamini, mlitiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa.”​—Efe. 1:13, NW.

Kwa hiyo, wengine wa ‘mabaki’ walitiwa muhuri katika maana hii ya kwanza mbele ya malaika kutumwa akiwa na “muhuri ya Mungu aliye hai.” Kutia muhuri ambako malaika anafanya ni kutia muhuri kwa mwisho, uamuzi wa kudumu kwa kutiwa muhuri kwa kwanza, kusudi kwamba “Israeli wote [wa kiroho]” waokolewe, hesabu kamili ya 144,000 ikiuhakikisha mwito wao na uteuzi. (Rum. 11:26; 2 Pet. 1:10) Karibu wote hawa, ikiwa si wote, walikuwa wamekwisha tiwa muhuri miaka mingi iliyopita kwa muhuri ya kwanza. Ijapokuwa ni kweli kwamba wengine, mbele ya muhuri kuwa ya kudumu, huenda wakawa wasio waaminifu na kwa hiyo ikawa lazima kwa wengine kutiwa muhuri, hakuna mkusanyo mkuu wa wanafunzi wanaotiwa muhuri kwa mara ya kwanza katika wakati huu unaokaribia mwisho. Ikiwa Waisraeli hao wa kiroho watakuwa waaminifu kwa kusudi la Mungu kwao, haielekei kwamba Mungu angetia muhuri wengine wapya kwa mara ya kwanza wa kundi hili la warithi wa kimbinguni katika ‘dakika ya mwisho.’

KUJICHUNGUZA MWENYEWE

Je! wawezaje kujichunguza mwenyewe ikiwa jambo hili lakutatiza akilini mwako?

Kwanza, yakupasa uyachunguze maoni yako ya kinachomaanishwa na kutiwa muhuri kwa ajili ya urithi wa kimbinguni. Je! wewe unaona kuwa mmoja wa Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta wa Mungu kama kunakotoa cheo cha pekee katika kundi la Kikristo, kukikustahilisha heshima kuu zaidi kuliko ambavyo ingekuwa kama ungekuwa mmoja wa “mkutano mkubwa” wa wale wanaotazamia urithi wa kidunia? Je! waona kutakupa ujuzi zaidi? Je! wadhani utapokea ufunuo wa pekee au ufahamu wa unabii mbalimbali, na mambo kama hayo? Huenda ukaona shauku ya kuyafurahia mambo hayo. Pengine u mwenye matokeo mazuri katika kuangusha vitabu vya Biblia, katika kuongoza mafunzo ya Biblia, katika kujibu maulizo ya Biblia, katika kutoa hotuba za Biblia. Huenda ukawa mwenye bidii nyingi sana, ukifanya maendeleo ya kiasi, ukiishi maisha bora ya kitheokrasi. Pengine haya yote ndivyo yalivyo. Lakini haya yasingekuwa ndiyo mambo ambayo juu yake mtu atasitawisha maoni ya kwamba anastahili mgawo wa Ufalme wa kimbinguni. Kwa nini sivyo? Kwa maana Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta na “kondoo wengine” vile vile wanacho kibali cha Mungu, na lazima wote waishi maisha zinazopatana na mapenzi ya Mungu.

Samsoni na watu wengine wengi katika siku zilizoitangulia Pentekoste walikuwa wenye bidii nyingi sana na ufahamu. Roho ya Mungu ilikuwa juu yao na, kama matokeo, waliweza kutimiza matendo makuu yasiyowezekana kwa uwezo wa kibinadamu. Na hali hakuna hata mmoja wa hilo “wingu kubwa” la waaminifu aliyekuwa wa jamii ya kimbinguni.​—Amu. 14:6, 19; 15:14; linganisha Kutoka 35:30, 31; 1 Samweli 10:6; 16:13; Ezekieli 2:2; Waebrania 11:32-38; 12:1.

Halafu waweza kurudia kuiangalia hali yako ya kwanza na tabia. Je! wewe unaliona shauri hili kwa njia ya kusisimka? Mtu aliyekuwa katika dini ya uongo iliyoonyesha kwenda mbinguni kama tumaini la pekee​—zaidi mojawapo ya dini zenye maoni zaidi ya kwamba ndizo zilizokuwa za kwanza​—huenda akavutwa na msisimko na maoni yaliyopita. Mbele ya kuja kwenye ujuzi wa kweli, je! umepata kutumia dawa za kutia usingizi na za kutulizia akili? Je! umepata kutibiwa kwa sababu ya masumbufu ya akilini na moyoni? Yajapokuwa mambo haya yasingezuia kwa lazima kupokea mwito wa kimbinguni, kwa habari ya mwanafunzi aliyetubu, akaongolewa na kubatizwa, ni mambo yanayopaswa kufikiriwa kwa uzito.

Wengine wamesema kwamba wanapatwa na masumbufu ya ndani, wachache hata wakisema kwamba kupokea kwao tumaini la kimbinguni kulitokeza ndani yao ‘mkazo kweli kweli.’ Wengine wamesema kwamba kwanza walishindana nalo. Wengine, kwamba kwa kitambo walikata tumaini kabisa​—kwamba Mungu alikuwa ameliondosha tumaini lao la kwanza la kidunia kwa kitambo kisha mwishowe akawapa tumaini la kimbinguni. Utaratibu huo ungekuwa tofauti na njia ya Mungu ya kutenda, kwa maana mtu hawezi akamtumikia Mungu kwa kumpendeza bila ya kuwa na tumaini la thawabu. (Ebr. 11:6) Hakuna mashaka juu yake. Imani si yenye mashaka, bali yenye matumaini, iliyosadikishwa.

MFANO

Mfano mwepesi waweza kusaidia: Wachunguzi wa uhai na asili yake (biologists) wanasema kwamba kinachoamua kama mtoto atakuwa wa kiume au wa kike ni ile tofauti ndogo mno ya mojawapo ya zile chromosome 46 katika yai lililotiwa mimba. Yai hili, lililotiwa mimba na chembe ya shahawa ya mwanamume, lina jozi 23 za chromosome. Jozi moja inaamua kama mtoto atakuwa wa kiume au wa kike. Jozi hii yaweza kuwa na “chromosome” mbili za “x” au “chromosome” moja ya “x” na nyingine ya “y” (“chromosome” ya “y” ikiwa fupi zaidi). Ikiwa chembe ina “chromosome” mbili za “x,” mtoto ni msichana; ikiwa ina “chromosome” ya “x” na ya “y,” mtoto ni mvulana. Tofauti hii ndogo sana ndiyo inayoanzisha, katika ukuzi wa mtoto, tofauti zote kubwa zinazotokea kati ya mwanamume na mwanamke.

Sasa, twajua kwamba hakuna anayepaswa kumwambia mtu aliye timamu kama yeye ni mwanamume au mwanamke. Tofauti hii, iliyofanyizwa na kupangwa na Yehova na inayokuwa ndogo sana hapo kwanza, inatokeza tofauti kubwa sana katika umbo la mwanamume na mwanamke. Moyo wa mwanamume na akili vinaelekea mambo ya wanaume, kama vile ufundi wa mashine, ujenzi, na mambo kama hayo; naye mwanamke anapenda mambo ya wanawake, kama vile nyumba, mavazi, mapambo na mambo kama hayo. Wala mwanamume wala mwanamke hawezi kumweleza mwenzake kufikiri kwake hasa, kuwaza na kuona mambo. Ni mpango wa Mungu.

Ndivyo ilivyo na kwa “kundi dogo” lililozaliwa kwa roho na kwa “kondoo wengine.” Mtume Petro anawaambia ndugu zake waliozaliwa kwa roho: “Mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele.” (1 Pet. 1:23) Ikiwa Mungu anaweza kutokeza njia tofauti sana ya kufikiri na kutamani kwa tofauti ya chromosome moja iliyo ndogo sana, bila shaka anaweza kutoa tumaini la kimbinguni, njia ya kufikiri, tamaa na mradi au maelekeo kwa wale anaowateua kulingana na mapenzi yake. Kwa roho yake na Neno anaweza kuipanda ile “mbegu” inayomfanya mtu “kiumbe kipya,” pamoja na matumaini yanayolingana ya kimbinguni. (2 Kor. 5:17) Hata katika mwili wa kibinadamu Mungu anaviweka viungo kulingana na anavyoona mwili unahitaji.​—1 Kor. 12:18.

Kwa hiyo, wale ambao ni warithi waliotiwa mafuta wa Ufalme ni wenye furaha kwamba wameteuliwa kwa utumishi mkubwa namna hiyo na thawabu, sawa na mwanamume aliye timamu anavyofurahi kwamba yeye ni mwanamume na kama vile mwanamke anavyofurahi kwamba yeye ni mwanamke. Kila mtu yu kama alivyofanywa na Mungu. Mwanamume au mwanamke hana haja ya kutiwa moyo ‘atafute mahali pake’ kati ya wanaume na wanawake. Iliamriwa hivyo na Mungu na haiwezi kugeuzwa, wala mtu hana haja ya kuamuliwa na mwingine yeye ni wa namna gani.​—Rum. 9:16.

Kwa hiyo, si lazima, au vema, tunapojifunza au kuzungumza na watu wapya katika ujuzi wa kweli ya Biblia, kushauri wajaribu kujiamulia kama wao ni wapokeaji wa ‘mwito’ wa kimbinguni au kama wanalo tumaini la kidunia. Ikiwa hawakuitwa kwenye mwito wa kimbinguni, kwa wazi wao ni wa jamii ya kidunia. Ikiwa wakati wo wote kutakuwako mageuzi yo yote, hili na aachiwe Mungu aamue na kuwajulisha katika wakati wake.

Wakati huu lengo kuu la ujumbe wa Mungu si watu wapate kuwa washirika wa “Bibi-arusi” wa kimbinguni wa Kristo. Bali, Biblia yasema: “Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo!” Mwaliko huu sasa ni mwito kwa watu wa mataifa, waishi katika paradiso ya kidunia ambayo kwayo “maji ya uzima” yatatiririka bila ya kizuizi, yakitokeza miti yenye kuzaa matunda na majani “ya kuwaponya mataifa.”​—Ufu. 22:1, 2, 17.

MAMBO AMBAYO YATAFANYWA NA WALIOTIWA MAFUTA KWA KWELI

Sasa wale ambao kwa kweli ni Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta watakuwa wakifanya nini? Watajipanga kwa juhudi waziangalie faida za Ufalme, wakiwahudumia “kondoo wengine.” Isingekuwa kuziangalia faida zilizopo za Ufalme kama wale wa jamii ya watiwa mafuta wakijitenga wenyewe wawe na vipindi vya kawaida vya ‘kuzungumza juu ya tumaini lao la kimbinguni.’ Mambo wanayoyazungumza yamepaswa yawe mambo yanayositawisha na kuweka amani na umoja katika kundi lote. Hii itawasaidia “kondoo wengine” na kuwasaidia watiwa mafuta wenyewe namna ile ile. Hivyo jamii zote mbili zitaunda “kundi moja.” (Yohana 10:16) ‘Chakula cha kiroho kwa wakati wake’ ndicho kinachopaswa kuliwa na wote sawasawa. Chakula hiki kitalisitawisha tumaini la ndani la watiwa mafuta waliotiwa muhuri na “kondoo wengine” vile vile.​—Mt. 24:45-47.

Shauri hili juu ya kujitenga latajwa kwa sababu, nyakati fulani, watu wenye kujidai kuwa wametiwa mafuta juzijuzi wameelekea kujitenga wenyewe, au kuunda kikundi kilicho peke yake. Hii inafanyiza mtengano na kwa kweli imeleta mgawanyiko katika kundi katika visa fulani.​—Mit. 18:1.

Wanapoulizwa, wale walioitiwa urithi wa kimbinguni pamoja na Yesu Kristo wanakubali kwamba kwa kweli wao ni wapokeaji wa mwito huu. Penye mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni kila mwaka wanaonyesha kwamba wanalo tumaini hili la kimbinguni kwa kuila mifano inayopitishwa. Lakini wao hawautangazi uhakika huu sikuzote. Wao hawaukazii fikira kwa majivuno ili kila mtu kundini awe akijua hivyo. Wao hawatazamii watendewe kwa kupendelewa. Bali, ni wenye shughuli kwa njia iliyosimuliwa na mtume Yohana: “Kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu.”​—1 Yohana 3:3.

Katika 2 Petro 1:5-11, mtume huyu anaonyesha namna ambavyo ndugu za kiroho za Kristo watakuwa wenye shughuli, wakijitahidi kuyatokeza matunda ya roho “kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu.” Hii inahitaji “unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa [roho] katika kifungo cha amani.”​—Efe. 4:1-3.

Kwa habari ya wazee na washiriki wengine wa kundi, haiwapasi kujaribu kuamua hali ya mtu aliyebatizwa juzijuzi anayefikiri ni mwenye mwito wa kimbinguni. Si juu yao kumlaumu huyo kwa sababu ya tumaini analodai kuwa nalo. Si jambo la kufanyia ubishi. Matakwa yaliyowekwa juu ya mtiwa mafuta yanaweza yakazungumzwa kumsaidia mtu yule apate ufahamu mzuri kama iwezekanavyo wa Maandiko. Naye anayejidai kuwa wa jamii ya watiwa mafuta amepaswa kuona ubora wa majaribio ya kumsaidia yeye. Lakini, yote yanapokwisha kusemwa na kufanywa, ni Mungu anayeteua na ni kati ya mtu yule na Mungu kwa habari ya anaposimama. Watu hao watendewe sawa na wengine wote katika kundi wanavyopaswa kutendewa, kwa upendo, ufahamu na ushirikiano wote ‘wakifanya kazi pamoja na Mungu na Kristo.’​—Kol. 3:12-17; 2 Kor. 6:1, NW.

Katika wakati huu unaokaribia mwisho katika kutimilika kwa makusudi ya Yehova kwa kundi la Kikristo, ni wazi kwamba mkazo hauko juu ya mwito mkuu wa wanafunzi kwenye urithi wa kimbinguni. Jambo la msingi sasa ni kumtumikia Mungu kwa nafsi yote, tukikaza fikira kwenye ukamilifu wetu wa Kikristo na kazi ya kuwakusanya “kondoo wengine.” Hakuna anayepaswa kuacha maoni yake juu ya hali yake mwenyewe au ile ya mwingine itokeze shindano katika kundi. Ni lazima katika huu “wakati wa mwisho” wa kujitahidi wote waunganishwe katika upendo, ambao “ndio kifungo cha ukamilifu.”​—Kol. 3:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki