Kumfurahia Yehova Yajapokuwa Magumu ya Har–Magedoni
“Ujapokuwa mtini wenyewe usichanue, na kusiwe na mazao katika mizabibu; . . . hata hivyo, kwangu mimi, mimi nitamfurahia Yehova mwenyewe; mimi nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.”—Hab. 3:17, 18, NW.
1. Har–Magedoni nini, na ni akina nani wanaoonekana wakikusanywa hapo na kwa njia gani?
MATAIFA yote ya wanadamu yanakaribia kwa kasi hali ya kupigana kati ya Mungu na wanadamu inayoitwa Har–Magedoni. Mwandikaji aliyeongozwa na roho ya Mungu wa kitabu cha mwisho cha Biblia Takatifu anasema kwamba kuna “roho za mashetani” na kwamba ‘zatoka na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi. . . . Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.’—Ufu. 16:14-16.
2, 3. N’nani walioliweka neno Har–Magedoni katika orodha yao ya maneno, nalo latumiwaje hadharani?
2 Kulingana na masimulizi haya mafupi, vita ya Har–Magedoni yamaanisha mpambano kati ya wanadamu wenye uadui na Mungu Mwenye Nguvu Zote. Tangu mwisho wa Vita ya Pili ya Ulimwengu katika mwaka wa 1945, wakuu na waandishi wameliweka jina Har–Magedoni katika orodha yao ya maneno na kufanya matumizi ya kisasa juu yake. Mwandishi mmoja katika The Spectator la Canada, chini ya tarehe ya Desemba 8, 1971, na chini ya kichwa kikubwa “Umoja wa Mataifa na Vita,” alisema maneno haya: “Wajapokuwa viongozi wa mataifa wanajua kabisa kwamba hali kama ile ya mgogoro wa Mashariki ya Kati na vita kati ya Wahindi na Wapakistani zingeweza kuleta kwa vyepesi matumizi ya silaha za atomiki, wengine wanaona ni afadhali wajihatirishe na Har–Magedoni kuliko kuachilia mamlaka yo yote kwa jeshi la mataifa yote, hata liwe linawakilisha wingi wa wanadamu.” (Fungu la tano)
3 Muda mfupi nyumaye, chini ya tarehe ya Januari 1, 1972, katika gazeti The Philadelphia Inquirer, mwandishi aliipa makala yake kichwa “Twakaribisha Mwaka Mpya Har–Magedoni Ikiwa Ingali Imezuiwa,” naye akaimalizia makala na fungu hili: “Lakini, usiku wa manane uliopita, ingeweza kusemwa kwamba wanadamu wameweza kupita katika siku nyingine 365 bila ya kujifutilia mbali, nalo taifa limekaa miezi mingine kumi na miwili bila ya maasi yenye umwagaji wa damu. Na iwapo katika mwaka wa 1972 Har–Magedoni yaweza kuzuiwa tena, itafaa kwa mara nyingine.”
4. (a) Vita ya Har–Magedoni itakuwa kati ya nani hasa? (b) Vita hii itawaletea wanadamu wote nini, na, kwa sababu hiyo, ni maulizo gani yanayotokea juu ya namna ambavyo mtu atatenda?
4 Katika maneno hayo yaliyochapwa twaona kwamba Har–Magedoni yadhaniwa kuwa vita kati ya wanadamu tu duniani. Waandikaji walikosa kuyachukua maoni ya Biblia kwamba Har–Magedoni itakuwa vita kati ya wanadamu duniani na Mungu Mwenye Nguvu Zote Muumba wa mwanadamu na dunia. Vita vyote vimewaletea watu ugumu na mataifa yaliyokuwamo, lakini “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni itawaletea ugumu wanadamu wote katika dunia nzima. Itakuwa ndiyo vita iliyo kubwa kupita zote iliyopata kuonekana na wanadamu. Kwa lazima hivyo, kwa maana itakuwa vita ya watawala wote wa kisiasa wa dunia yote inayokaliwa na watu juu ya Shujaa wa Vita aliye mkuu kupita wote waliopata kuwa hai, Mungu Mwenye Nguvu Zote. Haya, basi, kwa kuwa ugumu mwingi lazima utawapata wanadamu wote, je! itawezekana kwa ye yote duniani kufurahi penye Har–Magedoni? Basi kungeweza kuwako sababu gani kwa ye yote kati ya wanadamu kufurahi? Kutakuwa na msaada na faida gani kwa ye yote kufurahi penye Har–Magedoni? Kitabu kitakatifu ambacho ndicho chanzo cha jina Har–Magedoni kinatoa majibu ya pekee kwa maulizo haya.
5. (a) Ni nabii gani wa karne ya saba B.C.E. ambaye vile vile alipata njozi ya vita hiyo, nalo jina lake lina maana gani? (b) Habakuki 3:1 aonyeshaje kwamba yeye alipendezwa na muziki mtakatifu?
5 Karne saba mbele ya mtume wa Kikristo Yohana kutoa jina la uwanja wa vita ijayo ya ulimwengu wote, Har–Magedoni, kulikuwako nabii wa Kiebrania aliyetoa masimulizi ya vita iyo hiyo. Jina lake la Kiebrania lilikuwa Habakuki, ambalo maana yake ni “Kumbatio (la upendo),” au, “Kumbatio Lenye Shauku.” Yeye alimaliza kuuandika unabii wake wenye kusisimua karibu mwaka wa 628 mbele ya Wakati wetu wa Kawaida. Yeye alipendezwa na muziki mtakatifu. Hii yaonyeshwa katika sura ya tatu ambayo ndiyo ya mwisho ya kitabu cha unabii wake, ambacho namna yake ni mashairi ya kinubi. Mstari wa kwanza wa sura hii waonyesha sauti za maombolezo za muziki, kama zile za majonzi, ukisema: “Sala ya Habakuki nabii katika majonzi” (NW); au, kama vile isemavyo The Jerusalem Bible: “sauti kama ya majonzi.” Tafsiri nyingine za Biblia zinalionyesha neno la Kiebrania hapa la “majonzi,” nazo zasema hivi: “Juu ya Shigionoth,” au, “kulingana na nyimbo, au, sauti za nyimbo” au, kulingana na maandishi ya pembeni ya Biblia ya Authorized Version: “kulingana na nyimbo zenye kugeuka, au, sauti za nyimbo.” (Jewish Publication Society; An American Transiation; Authorized Version) The New American Bible yasema: “Kwa sauti yenye huzuni.”
6. (a) Mwisho wa Habakuki 3:19 wazidi kutoa maoni gani juu ya nabii? (b) Bila shaka yeye alilifikiria jengo gani, na kwa nini?
6 Sura hiyo yamalizia na mtajo mwingine wa muziki, ikisema: “Kwa msimamizi wa vyombo vyangu vya muziki.” (Hab. 3:19; Byington; AT) Tafsiri nyingine zinalitafsiri neno la Kiebrania kwa “msimamizi” kama “mstadi wa waimbaji” na “Kiongozi.” (Revised Standard Version; Je; JP) Tafsiri ya Moffat inasema hivi: “Kutoka kwa mkusanyo wa Mstadi wa Waimbaji.” Mitajo hii ya muziki imewapa wengine maoni ya kwamba Habakuki alikuwa mshiriki wa waimbaji wa hekalu katika Yerusalemu na kwa hiyo alikuwa Mlawi. Walau, alipoimaliza sala yake ya huzuni, nabii Habakuki alimpa hiyo msimamizi wa muziki katika hekalu aitungie wimbo ufaao. Bila shaka nabii Habakuki alilifikiria hekalu, kwa maana, mara tu mbele ya sala yake ya huzuni, anasema: “Lakini [Yehova] yumo ndani ya hekalu lake takatifu; dunia yote na inyamaze kimya mbele zake.”—Hab. 2:20.
7. Ni hekalu lipi lililomaanishwa katika Habakuki 2:20?
7 Yaelekea kuwa hekalu alilokuwa akilifikiria Habakuki lilikuwa la Yerusalemu, lakini mtajo wenyewe ni kwa hekalu la kiroho la kimbinguni la Yehova, ambalo Yeye alijenga, wala siyo Mfalme Sulemani wa Yerusalemu. Ni ndani ya Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu hili la kiroho alimoingia Yesu Masihi nyuma ya ufufuo wake kwa wafu na kupaa kwake mbinguni mwaka wa 33 wa Wakati wetu wa Kawaida.—Ebr. 8:2; 9:23, 24.
8, 9. Maandiko Matakatifu yanauweka utimizo wa sala ya unabii ya Habakuki mahali gani, na namna gani hivyo?
8 Tunapojifunza sala ya huzuni ya Habakuki, twaweza kufahamu kwa nini alitaka iwe na sauti za nyimbo zenye huzuni au za majonzi. Yeye hakuishi akaione sala yake ya unabii ikijibiwa. Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki yanautaja unabii wa Habakuki na kuuweka utimizo wake wa mwisho katika wakati ujao, katika kizazi chetu wenyewe. Ndiyo sababu twapendezwa nao. Imani yetu katika kuongozwa kwa unabii huu na roho ya Mungu na uhakika wake yatuongoza kuutafuta utimizo wake katika kizazi chetu. Kitabu cha Waebrania, walichoandikiwa Waebrania waliofanywa Wakristo karibu mwaka wa 61 wa Wakati wetu wa Kawaida, kinautaja unabii wa Habakuki, sura ya pili, mstari wa tatu na wa nne, na kusema:
9 “Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi. Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, yeye ajaye atakuja, wala hatakawia. Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; naye akisita-sita, [nafsi] yangu haina furaha naye. Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa [nafsi] zetu.”—Ebr. 10:36-39.
“SALA” KWA AJILI YA NANI, KWA AJILI YA NINI?
10. (a) Ajapokuwa alijisema mwenyewe, Habakuki alikuwa akisema kwa njia gani? (b) Hivyo sala ingewezaje kujibiwa kwa ajili ya yeye aliyeombewa?
10 Katika sala yake ya unabii, Habakuki anajisema mwenyewe. Kwa kweli, hata hivyo, anasema kama mwakilishi. Analiwakilisha taifa la watu wake, watu wa ufalme wa Yuda Yerusalemu ukiwa ndio mji wake mkuu. Hii ni wazi kutokana na sura ya tatu, mstari wa kumi na tatu mpaka wa kumi na sita, ambapo twasoma: “Ukatokea kwa ajili ya wokovu wa watu wako, kwa ajili ya wokovu wa [mtiwa mafuta] wako; . . . Ukakichoma kichwa cha mashujaa wake kwa fimbo zao wenyewe; [walipokuja] kama kisulisuli ili kunitawanya; . . . nikatetemeka katika mahali pangu; ili nipate kuingoja ile siku ya dhiki.” Kwa hiyo yeye aliyepaswa kutawanywa na jeshi la mashujaa wa vita wakiwa chini ya kiongozi wa kijeshi alikuwa, si Habakuki mwenyewe, bali taifa ambalo nabii Habakuki alikuwa mshiriki wake. Kwa hiyo jibu kwa sala ya Habakuki lingeweza kuja yeye mwenyewe akiisha kufa, na hali lingekuja juu ya taifa lenye kungoja kwa unyamavu ambalo alisali kwa ajili yake.
11. Twaweza kusema nini juu ya kama sala ya Habakuki ilitimizwa juu ya Waisraeli mwaka wa 607 B.C.E., au mwaka wa 539 B.C.E., au mwaka wa 70 C.E., na mwaka wa 1967 C.E.?
11 Katika mwaka wa 607 mbele ya Wakati wetu wa Kawaida mji wa Yerusalemu na hekalu lake viliharibiwa na majeshi ya Babeli, lakini wakati huo sala ya Habakuki haikujibiwa. Wala haikujibiwa mwaka wa 539 B.C.E., wakati ambapo mji wenye kuta zenye nguvu wa Babeli katika Mto Frati ulianguka mikononi mwa majeshi yenye ushindi ya Wamedi na Waajemi yakiwa chini ya mfalme wa Kiajemi, Koreshi Mkuu. Mji wa Yerusalemu uliojengwa upya nyumaye, tangu mwaka wa 537 B.C.E. na kuendelea, ulipatwa na uharibifu pamoja na hekalu lake lililojengwa upya. Hilo lilitendwa mwaka wa 70 wa Wakati wetu wa Kawaida, na vikosi vya Rumi vikiwa chini ya Jemadari Tito. Na hali wakati huo sala ya unabii ya Habakuki haikujibiwa. Katika mahali ulipokuwa mji ulioharibiwa wa Yerusalemu mji mpya ulijengwa na Warumi. Hata Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilipotokea mwaka wa 1914 mji huo uliendelea kuwa chini ya usimamizi wa watawala wasio wa Kiyahudi au wa Mataifa. Kutekwa kwa mji wenye kuta za zamani wa Yerusalemu na Waisraeli katika vita ya siku sita ya Juni 5-10, 1967, hakukuwa jibu kwa sala ya Habakuki. Hakuna kitu kilichotukia kwa Waisraeli wakati huo au tangu wakati huo kama kile kinachosimuliwa katika sura ya tatu ya Habakuki.
12, 13. (a) Kwa hiyo ni juu ya nani sala ya Habakuki itatimia kwa wakati wake? (b) Mwebrania aliyefanywa Mkristo Paulo anawaita hawa nini?
12 Kwa msaada wa mambo ya hakika ni wazi kwamba sala ya unabii ya Habakuki haitakuwa na utimizo juu ya Jamhuri ya Israeli ya kisiasa wala “Zionist movement” wala Waisraeli wa asili ambao ni raia za nchi mbalimbali za Mataifa katika dunia nzima. Kuna sababu yake. Ilifunuliwa kwa Waebrania waliofanywa Wakristo wa karne ya kwanza C.E. kwamba lazima unabii wa Habakuki upate utimizo wake kwa kuwapendelea wafuasi waaminifu wa Yesu Masihi. Wanafunzi hawa wake wa kweli walitiwa mafuta na roho takatifu ya Yehova Mungu mwaka wa 33 C.E. na nyuma ya hapo, na kwa hiyo hawa wanafanyiza Israeli wa Mungu wa kiroho. Wao ni Waisraeli wa kiroho, Wayahudi wa kiroho. (Rum. 2:28, 29) Akimtaja Israeli huyu wa kiroho, Mwebrania aliyefanywa Mkristo, mtume Paulo, aliwaandikia Wakristo katika jimbo la Galatia:
13 “Isitukie kamwe kwamba mimi nijisifu, isipokuwa katika mti wa mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kupitia kwake ulimwengu umetundikwa mtini kwangu mimi na mimi kwa ulimwengu. Kwa maana kutahiriwa si kitu wala kutotahiriwa, lakini kiumbe kipya ni kitu. Na wote wale watakaotembea kwa utaratibu kwa kanuni hii ya mwenendo, amani na rehema na viwe juu yao, hata juu ya Israeli wa Mungu.”—Gal. 6:14-16; Moffatt, The Jerusalem Bible, Revised Standard Version.
14. (a) Twaweza kusema nini juu ya kama Kristendomu ndiye “Israeli wa Mungu”? (b) Waisraeli wa kiroho wa karne ya kwanza na wale wa leo wanalinganaje kwa habari ya maono yao?
14 Siku ambazo mtume Paulo aliyaandika maneno hayo, Kristendomu hakuwapo, na kwa hiyo Paulo hakuwa akimwita Kristendomu “Israeli wa Mungu.” Ni karne tatu za kwanza nyumaye Kristendomu alipotokea, siku za Mfalme wa Kirumi Konstantino Mkuu, Askofu Mkuu, na hata sasa Kristendomu hajajionyesha mwenyewe kuwa Israeli wa Mungu wa kiroho, aliyebarikiwa na “amani na rehema.” Vita ya Kwanza ya Ulimwengu na Vita ya Pili ya Ulimwengu vilitukia vyote viwili katika Kristendomu, na mataifa ambayo hayakuonyeshana rehema zaidi yalikuwa mataifa ya Kristendomu. Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza ambao mtume Paulo aliwaita “Israeli wa Mungu” waliteswa na Milki ya Kirumi. Kwa kulingana, mabaki yenye kuokoka ya huyo Israeli wa Mungu waliokuwa hai wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu na ya Pili waliteswa na mataifa yenye kupigana ya Kristendomu. Kwa nini? Kwa maana Waisraeli hao wa kiroho, waliotiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu, walijaribu ‘kutembea kwa utaratibu kwa kanuni hii ya mwenendo,’ bila ya kuwa na ushirika wo wote wa bidii katika kumwaga damu pamoja na mataifa ya Kristendomu.
15. Ni akina nani wanaofanyiza mabaki haya ya Israeli wa kiroho tangu mwaka wa 1914 C.E., nao walipaswa kujulikanaje?
15 N’nani waliofanyiza mabaki hayo ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta kwa roho takatifu ya Yehova Mungu? Mambo ya hakika ya historia yaonyesha ni akina nani. Wao ndio wale ambao Yesu Kristo alisema hivi juu yao katika unabii wake juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo”: “Ndipo watu watakapowatoa ninyi mpate dhiki nao watawaua, nanyi mtakuwa vyombo vya chuki ya mataifa yote kwa ajili ya jina langu.” (Mt. 24:9, NW) Wakristo hao waliotiwa mafuta ambao juu yao maneno hayo ya unabii yalitimia tangu mwaka wa 1914 C.E. walikuwa ndio wanafunzi wa Biblia wajulikanao kama mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Hali yao ya mfano wa Kristo ya kutokuwamo kuelekea siasa za kitaifa, maasi na vita vya mataifa yote inajulikana sana ulimwenguni pote, nayo imeelekeza kwao chuki na mateso ya Kristendomu na vile vile ya mataifa yasiyo sehemu ya Kristendomu. Hata hivyo, wao wanapendwa na Yehova Mungu wao. Kana kwamba ilikuwa, wao wamo katika ‘kumbatio lake la upendo,’ jambo linaloonyeshwa katika jina la nabii, Habakuki.
16, 17. (a) Kwa sababu gani ni muhimu sana kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kusali kama Habakuki? (b) Kwa nini ilifaa Habakuki amwagize “msimamizi” aifanye sala iwe ya sauti za majonzi?
16 Waisraeli hao wa kiroho leo wanasali sala ya unabii ya Habakuki kama yao wenyewe, nao wanautazamia utimizo wake juu yao wenyewe kama jibu kutoka kwa Yehova, ambaye mashahidi hawa waliotiwa mafuta ni wake. Hii ni sababu ya muhimu sana kwao kutoa sala hiyo kwa Mungu. Kulingana na unabii mbalimbali wa Biblia na hali inayositawi duniani mwote, wao wanatazamia kwamba karibuni, mnamo kizazi hiki, “dhiki kubwa” itampata Kristendomu na sehemu nyingine yote ya hii taratibu ya mambo nayo itaufikia upeo wake katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni. Wao wanajua kwamba hii itamaanisha ugumu mwingi kwao na kwa wote wale wanaosimama upande wa mabaki yaliyotiwa mafuta na kuwa wenzi wao waaminifu katika taabu. Tayari kuna “mkutano mkubwa” wa wenzi hao wenye kumcha Mungu, ambao ni kama wageni ndani ya malango ya Israeli wa kiroho. (Ufu. 7:9, 10, 14; Kut. 20:10; Mt. 24:21, 22) Kwa hiyo ilifaa sana kwamba nabii Habakuki akamshauri “msimamizi” wa muziki wa hekalu katika Yerusalemu azitunge sauti za majonzia kwa maneno haya ya kwanza:
17 “Ee Yehova, mimi nimezisikia habari juu yako wewe. Nimeuogopa utendaji wako Ee Yehova.”—Hab. 3:2, NW.
‘KUOGOPA’ KWA SIKUZOTE KWA SABABU YA “UTENDAJI” WA NGUVU ZIPITAZO ZILE ZA MWANADAMU
18. Habakuki alizisikiaje “habari” juu ya Yehova, nao mabaki ya Israeli wa kiroho wanazisikiaje “habari”?
18 Kama nabii Mwisraeli Habakuki, mabaki yaliyotiwa mafuta ya Waisraeli wa kiroho leo wamezisikia habari juu ya Mungu huyu wa Biblia Takatifu, ambaye jina lake ni Yehova. Wakati wa unabii wa Habakuki, sehemu iliyo kubwa zaidi ya Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na roho ya Mungu ilikuwa imekwisha andikwa, na kupitia kwa kurasa zake yeye alikuwa amekwisha ‘kuzisikia habari’ juu ya Yehova. Leo mabaki ya Waisraeli wa kiroho wanayo Maandiko ya Kiebrania yote yaliyoongozwa na roho ya Mungu, na, zaidi ya hayo, vitabu vyote 27 vya Maandiko ya Kigiriki yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Kwa kujifunza kwa bidii. Maandiko Matakatifu haya mabaki waliotiwa mafuta na roho ‘wamezisikia habari,’ habari za kweli kabisa, juu ya Mungu wake Habakuki, Yehova. Ni habari zenye kuogofya juu ya yaliyotukia hasa kwa sababu ya Yehova Mungu.
19, 20. (a) Mabaki yaliyotiwa mafuta, kama Habakuki, wanauonaje utendaji wa kale wa Yehova? (b) ‘Habari” za utendaji huo wa kimungu zapaswa kuwa na matokeo gani juu ya mabaki yaliyotiwa mafuta?
19 Kupitia kwa “habari” za Maandiko nabii Habakuki alimwona Mungu wake Yehova akitenda. Vivyo hivyo, mabaki yaliyotiwa mafuta ya leo, kwa kuwa na maono ya “utendaji” wa Yehova kama unavyosimuliwa katika “habari” za Maandiko, nao vile vile wamemwona Yeye akitenda. Kama wao wenyewe wangalikuwako katika mahali hapo huko nyuma wawe washuhudiaji wa utendaji wa Yehova, ‘wangaliogopa,’ kama vile Habakuki alivyosema aliogopa kwa kuzisikia habari peke yake. Ebu uwazie utendaji wa Yehova mwaka wa 1513 B.C.E., alipowakomboa babu zake Habakuki katika Misri kisha akayaharibu magari ya vita na wapanda farasi wa Farao wa Misri walipokuwa wakiwafuatia Waisraeli wenye kutoroka kwa kiruu kupita bonde kavu la Bahari ya Shamu.
20 Wazia, vile vile, onyesho la kuogofya ambalo Yehova alionyesha penye Mlima Sinai katika Arabuni wakati alipowatangazia Amri Kumi Waisraeli waliopiga kambi. Tena, wazia utendaji aliouonyesha kwa mwujiza kwa ajili ya watu wake wateule mnamo wakati wa kutanga-tanga kwao kwa miaka 40 katika jangwa la hatari na namna ambavyo, mwishoni mwa miaka hiyo 40, aliwapitisha watu hawa wenye kuhama katika Mto Yordani uliokuwa umefurika na kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi, mwaka wa 1473 B.C.E. Wazia tena utendaji wa Yehova mnamo karne zilizofuata alipowainua waamuzi watende kama wakombozi wa watu wake walioonewa. Ndiyo, wazia wakati ambapo, si muda mrefu mno mbele ya wakati wa Habakuki, Yehova alipomtumia malaika wake wa kimbinguni kufutilia mbali Waashuru maadui katika usiku mmoja na kuukomboa Yerusalemu usitekwe na mfalme wa Kiashuru Senakeribu mwenye kumdharau Mungu. Tukijaribu kuuwazia utendaji huu wote kwa upande wa Mungu Mwenye Nguvu Zote Yehova, hauwi na matokeo mengine ila kutuogofya. Habakuki alikubali kwamba aliogopa.
21, 22. (a) Kwa sababu gani kulikuwako haja ya kuzikumbuka “habari” hizo zenye kuogofya, kwa habari ya Habakuki na mabaki yaliyotiwa mafuta vile vile? (b) Kwa hiyo ni sala gani ya juhudi ambayo sasa ndio wakati wa mabaki kuisema?
21 Hata hivyo, kwa nini mtu ajiogopeshe? Kwa nini azifikirie “habari” hizo zenye kuogofya? Kulikuwako haja ya kufanya hivyo kwa maana Habakuki alitazama mbele kwa unabii kwenye wakati ujao naye akatangulia kuona shambulio la mataifa yote juu ya waabudu wa kweli wa Yehova. Kuna haja ya kufanya lilo hilo leo kwa mabaki yaliyotiwa mafuta, kwa maana sasa mabaki haya wanajua kwamba wanaukaribia wakati wa shambulio hilo la mataifa yote litakalofanywa na maadui wa Yehova. Sasa ni wakati wa kuamini na kutumaini kwamba Mungu huyu wa “utendaji” huo wa kale si mfu! Kwa ajili ya mabaki yaliyotiwa mafuta na wenzi wao waaminifu yampasa kuwa hai na mwenye kutenda kama alivyokuwa huko nyuma. Kwa hiyo huu ndio wakati wao wa kuichukua sala ya juhudi ya Habakuki na kusema:
22 “Katikati ya miaka Ee na uufufue! Katikati ya miaka na uujulishe. Wakati wa ghadhabu na ukumbuke kuonyesha rehema.”—Hab. 3:2, NW.
23, 24. (a) Hivyo Habakuki alikuwa akisali juu ya nini ambacho kingefufuliwa katikati ya miaka? (b) “Ghadhabu” hapa ilikuwa ya nani na juu ya nani, nako kuonyesha rehema kungekumbukwaje?
23 Habakuki alikuwa akisali juu ya nini hapa alipokuwa akizungumza kwa unabii kwa ajili ya mabaki yaliyotiwa mafuta ya leo? Ilikuwa ili Yehova Mungu aurudie utendaji wake, aufufue, katika miaka ya nyumaye, wakati wa hatari mnamo miaka hiyo. Naye arudie tena kuujulisha utendaji wake kwa ajili ya waabudu wake waliohatirishwa. Ikiwa ghadhabu yake i juu ya mabaki yaliyotiwa mafuta na “mkutano mkubwa” wa wenzi waaminifu kwa sababu ya makosa yo yote kwa upande wao, Yeye na akumbuke kuonyesha rehema kwa neema kwa ajili ya jina lake takatifu. Lakini ikiwa ghadhabu yake i juu ya watesi na washambuliaji wa waabudu wake, basi, mnamo wakati wa tendo ambalo ghadhabu yake inamsukuma kulitenda juu ya maadui hawa wenye kiburi, na akumbuke kuonyesha rehema kwa mabaki na “mkutano mkubwa” wa wenzi wao katika taabu yao. Yeye asiiache “dhiki kubwa” iwafishe. Na autimize unabii wa Mwanawe Yesu Kristo juu ya “dhiki kubwa”:
24 “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.” (Mt. 24:21, 22) “Kwa kweli, kama Yehova asingalizifupiza siku hizo, hapana mwili ambao ungeokolewa. Lakini kwa ajili ya wateule ambao yeye amewateua amezifupiza siku hizo.”—Marko 13:20, NW; The Christian’s Bible—New Testament, ya George N. LeFevre (1928), ambayo vile vile yatumia jina la Yehova hapa.
MUNGU KATIKA MWENDO!
25, 26. (a) Ni kutoka sehemu gani mbili za historia ambako Habakuki sasa anamsimulia Mungu katika mwendo wake? (b) Sura za sehemu hizo mbili zilikuwaje?
25 Nabii Habakuki anapokwisha kusali kwa Yehova aufufue tena utendaji wake wa kale katika miaka ijayo, namna ya utendaji ambayo kwa ajili yake Habakuki anasali sasa anatoa masimulizi, akisema: “Mungu alikuja kutoka Temani, Yeye aliye mtakatifu kutoka Mlima Parani. Utukufu wake ukazifunika mbingu, nayo dunia ikajaa sifa yake. Mwangaza wake ulikuwa kama nuru; alikuwa na mishale ya nuru ubavuni pake; ndipo ulipofichwa uweza wake. Mbele zake ilikwenda tauni, na makaa ya moto yakatoka miguuni pake.”—Hab. 3:3-5.
26 Hapa Habakuki anataja sehemu mbili za historia katika Mashariki ya Kati, yaani, Temani na Mlima Parani. Temani ilishirikishwa na nchi ya Edomu. Edomu (ikimaanisha “Nyekundu”) ndilo jina la kupangwa alilopewa mjukuu wa Ibrahimu Esau alipokwisha kuiuza haki yake ya uzaliwa ya ukoo wa Ibrahimu kwa ndugu yake pacha Yakobo kwa ajili ya mchuzi mwekundu wa mboga ili aitosheleze njaa yake yenye kuwaka. (Mwa. 25:27-34) Parani lilikuwa jimbo la jangwa lenye milima lililokuwa kaskazini ya Mlima Sinai. Katika jimbo hili la jangwa taifa lenye kuhama la Israeli lilitanga-tanga karibu miaka 38 mbele ya kuishambulia Nchi ya Ahadi. (Hes. 10:11, 12; Kum. 2:14) Nchi ya Edomu ilikuwa mashariki ya kaskazini yake, kati ya Hori ya Akaba na Bahari ya Chumvi. “Njia kuu ya mfalme” ilipita katika Edomu. Na kwa habari ya Temani (maana yake “-a kusini”), kulikuwako mzao wa Edomu (Esau) aliyeitwa Temani, napo mahali palipoitwa kwa jina la Temani huenda palikuwa mji wa Kiedomu. Lakini wakuu wa Kiyahudi wanasema palikuwa katika mashariki ya kaskazini ya Edomu. Lakini ni kutoka Temani kwamba “Mungu alikuja” alipokuwa akiwaelekeza watu wake wateule kwenye Nchi ya Ahadi.
27, 28. (a) Waisraeli wenye kuhama waliendeleaje kusonga mbele bila ya kujali maadui na watu wasio na urafiki? (b) Mitajo ya Musa ilipatanaje na ile ya Habakuki kwa habari ya mahali ambapo Waisraeli walianzia mwendo?
27 Kwa sababu ya katazo na upinzani wa Waedomu, taifa lenye kuhama la Israeli halikupita katika njia kuu ya mfalme katika nchi ya Edomu, lakini yaelekea lilipita kuelekea kaskazini karibu na mpaka wa mashariki wa Edomu na kuzunguka Moabu kuielekea Bahari ya Chumvi. (Hes. 20:14-21) Hivyo, maadui na watu wasio na urafiki katika njia ya safari hawakuwazuia Waisraeli walipokuwa wakisafiri kutoka jimbo lenye milima la Parani kupita Temani na kuelekea kwenye Nchi ya Ahadi. Nabii Musa alikuwa ndiye kiongozi anayeonekana wa taifa lenye kusafiri, nayo masimulizi yake yanapatana na yale ya Habakuki kwa habari ya safari ya kusini ya kuondoka kwa Waisraeli wenye kusonga mbele. Mnamo miezi miwili tu mbele ya Waisraeli kuvuka Mto Yordani” kuingia katika Nchi ya Ahadi, alianza kuwabariki Israeli kwa kusema:
28 “[Yehova] alitoka Sinai, akawaondokea kutoka Seiri [iliyokaliwa na Waedomu]; aliangaza katika kilima cha Parani, akaja Meriba-kadeshi. Upande wa mkono wake wa kuume palikuwa na sheria ya moto-moto kwao. Hakika awapenda hayo makabila ya watu; watakatifu wake wote wamo mkononi mwako.”—Kum. 33:1-3.
29. Yehova alikwendaje mbele ya watu wake wenye kusonga mbele, na ni kumbukumbu la namna gani alilojifanyia?
29 Bila shaka, Yehova hakutokea kwa kuonekana mbele ya safu za Waisraeli wenye kusonga mbele. Walakini, ajapokuwa hakuonekana kwa jicho la kibinadamu, yeye alijifanyia kumbukumbu linalostahili sifa kama Kiongozi wao asiyeonekana. Vile vile, mfano wake Yeye wenye kuonekana, yaani, nguzo ya wingu wakati wa mchana na nguzo ya moto wakati wa usiku, uliwatangulia.—Kut. 13:21, 22; Hes. 14:14; Kum. 31:15.
30. Yalipokwisha makumi ya miaka wakiwa gizani, Waisraeli walitokezwaje tena nuruni?
30 Katika mwaka wa 1474 B.C.E., wakati ambapo mwishowe Yehova aliwaondoa watu wake wasio na makao watoke katika jimbo lenye milima la Parani awapeleke kwenye Nchi ya Ahadi, mataifa yasiyo ya Kiyahudi yaligundua hili. Ilikuwa kana kwamba ni nuru yenye kuangaza iliyowafunulia mambo wazi. Ulikuwa ushuhuda wa kwamba Mungu mwenyewe akiwa mwenye fahari alikuwa katika mwendo. Kwa makumi ya miaka watu wake walikuwa wamekuwa katika giza katika jangwa la Mkono wa Nchi wa Sinai, na sasa walitokezwa nuruni. Ulikuwa ni ‘mkono’ wa Yehova wenye nguvu uliokuwa ukionekana ukitenda. Ilikuwa kana kwamba miali maradufu ya nuru ilikuwa ikitoka “mkononi” mwake, ikitoa nuru pande zote. Nguvu zimefichwa mkononi mwa Yehova. Nuru itokayo humo ni nuru yenye nguvu. Mataifa maadui hayawezi yakaizimisha au kushindwa kuuona utukufu wake.—Hab. 3:4.
31, 32. (a) Habakuki 3:5 itatimiaje juu ya ugonjwa wa kipuku na homa kali? (b) Katika nyanda za Moabu, Yehova aliuonyeshaje uwezo wake wa kufanya hivi?
31 Juu ya “wakati wa mwisho,” ambao historia yahakikisha ulianza mwaka wa 1914 C.E. kama ilivyoonyeshwa na Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, Yesu alitabiri kwamba, kusingekuwa na vita ya mataifa yote tu, bali vile vile kungekuwako matetemeko ya ardhi, njaa kubwa na magonjwa ya kipuku. (Mt. 24:3, 7, 8; Luka 21:10, 11; Dan. 12:4, NW) Magonjwa hayo ya kipuku yalisababishwa na hali chafu za wanadamu wafisadi na walioumizwa na vita. Lakini, wakati ambapo Yehova ataelekea kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni katika wakati ujao ulio karibu, ataleta kifo juu ya maadui wake kwa njia isiyo na jeuri na ya unyamavu, ugonjwa wa kipuku.
32 Wakati huo itakuwa hatari, jambo la kufisha, kufunga njia ya Yehova ya kuelekea kwenye ushindi, kwa maana mbele yake atapeleka ugonjwa wake wa kipuku na nyuma yake atawaacha mateka yaliyoteswa na homa kali sana yenye kufisha. Ni kama vile Habakuki 3:5 (NW) alivyosema juu ya siku inayokuja ya Yehova: “Mbele zake ugonjwa wa kipuku ukazidi kwenda, na homa kali sana ilikuwa ikitokea miguuni pake.” Yeye aliuonyesha uwezo wake wa kufanya hivi wakati wa siku za mwisho za Musa, wakati ambapo Yehova aliwalaza mautini Waisraeli wafisadi 24,000 katika nyanda za Moabu ng’ambo nyingine ya mto kutoka Nchi ya Ahadi, kwa sababu walizivunja amri zake na wakafanya uasherati na wanawake wapagani na kugeuka na kumwabudu mungu wa uongo, Baali wa Peori.—Hes. 25:1-9.
MATAIFA YATASHTUSHWA
33. Mbele ya kusonga mbele na kuyashambulia majeshi ya adui penye Har–Magedoni, Yehova atafanya nini, kama inavyoonyeshwa na Habakuki 3:6?
33 Kulingana na namna ambavyo Yehova ametenda kale chini ya hali fulani, yeye atauchunguza uwanja wa vita ya Har–Magedoni na kuziangalia safu za maadui. Kwa hiyo sala ya mfano wa majonzi ya Habakuki yaendelea kusema: “Akasimama, akaitetemesha dunia; akatazama, akawasitusha mataifa; na milima ya zamani ikatawanyika; vilima vya kale vikainama; miendo yake ilikuwa kama siku za kale. Naliziona hema za Kushani katika taabu; mapazia ya nchi ya Midiani yakatetemeka.”—Hab. 3:6, 7.
34. (a) Dunia itatetemeshwaje na kusimama zizima kwa Yehova? (b) Mataifa yatarukaje wakati Yehova ‘atakapoona’?
34 Yehova hafanyi fujo haraka haraka bila ya kutunga shauri la jambo lo lote. Yeye anakaa mahali pake na kupafikiria mahali panapohitaji kuchukuliwa hatua, aone kwamba maadui wake wako mahali pale pale anapowataka wawe, wakionyesha wazi makusudi yao. Kusimama kwake zizima, akiwa tayari kutenda, kwaleta msukosuko katika “dunia” ya mfano iliyoko chini yake; kwaleta, kana kwamba ilikuwa, tetemeko la ardhi katika tengenezo la kidunia la adui. Inapokuwa wazi kwamba kweli ni Yehova aliyekaribia naye asimama mbele yao, tengenezo la kidunia lote latikisika sana mbele ya kuangukia uharibifu. Wakati ambapo mwishowe mataifa yanagundua kwamba Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote ‘anawaona’ na kwamba anawaangalia wao, wanashtuka kweli kweli. Sasa wakiamka wayaone mambo hasa yalivyo, wanaruka, siyo kwa furaha, lakini kwa kishindo, kwa mshindo wa fadhaa. Watakuwa kama waendesha magari na askari wapanda farasi Wamisri, ambao, walipotopezwa katikati ya Bahari ya Shamu, waliiona sababu yenyewe ya taabu yao nao wakaanza kupiga kelele: “Na tukimbie mbele ya Israeli; kwa kuwa [Yehova] anawapigania, kinyume cha Wamisri.”—Kut. 14:25.
35. (a) Nini kitakachotukia kwa matengenezo, kama milima na vilima, yatakayokuwa katika njia ya Yehova? (b) Ni kwa njia gani “miendo ya siku za kale” itakavyokuwa ile ya Yehova wakati huo?
35 Hakuna tengenezo la kidunia, hata liwe lenye fahari ajabu kama mlima, litakaloruhusiwa kuuzuia mwendo wa Yehova kwenye ushindi. Matengenezo hayo yote yenye mfano wa mlima, yajapokuwa yanaonekana kama yenye kuendelea milele, yatapondwa. Matengenezo mengine ya kidunia yasiyotokeza sana, ambayo uwezo wayo wa kukaa ulielekea kuwa wenye kudumu milele, kama ule wa vilima, itayapasa kuinama yameshindwa, yakimwacha Yehova aendelee kusonga mbele, akiwakanyaga-kanyaga kwa nyayo zake. Miendo yake itakuwa kama ‘miendo yake ya siku za kale,’ isipokuwa itakuwa ya kadiri kubwa sana. Alivyofanya Yeye wakati wa kale aweza kufanya na leo. Yeye ataufufua utendaji wake wa kale.
36. (a) Nini kinachofananishwa na kutaabika kwa hema za Kushani na kutetemeka kwa mapazia ya hema za Midiani? (b) Watu hao hawamo kati ya watu gani wenye kufurahi?
36 Yale anayoyafanya Mungu wa Habakuki anaposonga mbele bila ya kuzuiliwa yanatia hofu kuu ndani ya wote wale wanaozisikia habari zake, hawa wakiwa wasio na urafiki kwa Yehova na watu wake wateule. Kama mfano wa hawa, Habakuki anawatumia wakaaji wa hema wa Kushani na wa nchi ya Midiani, maeneo yaliyokaribiana. Ijapokuwa nchi ya Midiani ilikuwa mashariki ya Hori ya Akaba na haikulingana kabisa na njia waliyopita Waisraeli wakielekea kwenye Nchi ya Ahadi, hata hivyo Wamidiani walitetemeka kana kwamba ilikuwa hata mapazia ya hema yakitetemeka kama wakaaji waliomo. Nabii Habakuki aliona “taabu” juu ya hema za Kushani. Wenye kupiga hema waliona kwamba kupita kwa Yehova karibu pamoja na watu wake waliokombolewa hakukumaanisha mema kwa wale waliokuwa Kushani. Maono ya huzuni na wasiwasi yaliyowatesa yaliwaumiza, yakawasumbua, yakawaweka mashakani. Bila shaka haitakuwa vema kuwamo kati ya wale watakaoteswa na maono yenye maumivu na fadhaa kwa sababu ya habari za miendo ya kusonga mbele ya Yehova penye Har–Magedoni. Wao hawamo kati ya wale wanaomfurahia Yehova wakiwa chini ya hali hizo, yajapokuwa magumu yatiwa ndani.
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha maandiko ya chini ya Habakuki 3:19 na maandiko ya juu ya Zaburi 4 na 54.
[Ramani katika ukurasa wa 278]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
PARAN
EDOM
RED SEA
Mt. Sinai
Gulf of Aqabah
Teman
Dead Sea
[Picha katika ukurasa wa 274]
“Utendaji” wa Yehova uliyaharibu majeshi ya Farao yalipokuwa yakiwafuatia Waisraeli kupita Bahari ya Shamu
[Picha katika ukurasa wa 276]
“Habari” za Biblia zaonyesha kwamba Yehova aliwapitisha Waisraeli katika Mto Yordani ulipokuwa umefurika na kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi