Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 7/1 kur. 294-303
  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “NENO LA IMANI TUNALOLITANGAZA”
  • MANENO BILA MATENDO YANA FAIDA GANI?
  • JE! IMANI YAKO IMEKUFA AU I HAI?
  • USHUHUDA WA IMANI ILIYO HAI
  • RIPOTI YA ULIMWENGUNI POTE
  • Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Je, Kweli Una Imani Katika Habari Njema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • “Tupe Imani Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Zoea Imani Yenye Msingi Wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 7/1 kur. 294-303

“Imani Iliyotenganishwa na Matendo Imekufa Kama Mzoga”

“Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! ile imani yaweza kumwokoa?”​—Yak. 2:14.

1. Eleza maana ya imani, nayo maelezo hayo yanachukua maoni gani mengine?

WAKATI tunapozungumza, juu ya imani twaifikiria imani ya mtu katika Mungu. Mtume Paulo alisema hivi alipokuwa akieleza imani kwa Wakristo Waebrania: “Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.” (Ebr. 11:1) Taraja lililohakikishwa lina kitu kinacholitegemeza. Kinachukua maoni ya kwamba taraja hili limehakikishwa kabisa, kwamba wakati ujao litamilikiwa. Wengine wanatoa maoni ya kwamba imani ni kama hati ya kuthibitisha uenyeji wa mambo yanayotumainiwa. Imani vile vile yaweza kutia ndani uaminifu kwa ahadi za mtu au utii kwa wajibu. Mtu aliye na imani katika Yehova Mungu na katika Mwanawe, Kristo Yesu, atataka kuonyesha uaminifu, akitenda kwa kupatana kabisa na njia za Yehova na kuzitetea kwa wengine.​—Zab. 145:10, 11.

2, 3. (a) N’nini kinachofanyiza imani ya kweli ya Kikristo? (b) Ni kwa kadiri gani ambavyo wanafunzi wa Yesu waliieneza imani hiyo ya kweli? (c) Mtume Paulo alishirikije katika kuieneza imani hiyo ya kweli?

2 Mambo ambayo Yesu Kristo aliwafundisha wanafunzi wake na yaliyopitishwa kwa Wakristo wote katika karne zote kwa njia ya Neno la Mungu yanafanyiza imani ya kweli ya Kikristo. (Efe. 1:15-17; 4:5) Wanafunzi wa Yesu walipoyazungumza mambo ambayo Yesu alikuwa amewafundisha siku za kwanza za Ukristo, wengi waliamini nao wakamwamini Kristo Yesu na mafundisho yake. Wanafunzi waliitanguliza kazi hii ya kuhubiri na kufundisha mbele ya mambo mengine. “Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.” (Matendo 6:7) Habari njema hizi zilizohubiriwa na wanafunzi bila shaka zilienea, nayo imani yao wenyewe katika habari njema hizo ikajulikana sana; kwa hiyo, Paulo angeweza kusema hivi kwa kweli, alipokuwa akiwaandikia Warumi: “Kwanza namshukuru Mungu wangu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu nyote, kwa kuwa imani yenu inahubiriwa katika dunia nzima.”​—Rum. 1:8.

3 Paulo alikuwa mtangazaji wa injili kweli kweli, mtangazaji wa habari njema. Yeye alijifunza juu ya Yesu Kristo, ambaye kwa kufa kwake juu ya mti wa mateso alitoa njia ya kuondolea dhambi ya ulimwengu, naye Paulo alijifunza juu ya ufufuo wa Yesu kutoka kwa wafu. Paulo aliufahamu sana ubora wa mambo haya hata akaona kila mtu amepaswa ayajue. Kwa hiyo alisafiri maelfu ya maili, zaidi sana kwa miguu, akihubiri na kufundisha. Alianzisha eneo jipya kama ambavyo mmisionari angefanya, na kuletea watu wengi wa mataifa mengi ujumbe ambao ungewapa msingi wa imani.

“NENO LA IMANI TUNALOLITANGAZA”

4. N’nini lililokuwa “neno la imani” ambalo Paulo alilitangaza, naye alishirikije katika kulitangaza?

4 Paulo aliwaambia watu kama vile alivyowaandikia Warumi: “‘Neno li karibu nanyi: li midomoni penu na moyoni mwenu.’ Hii maana yake neno la imani tunalolitangaza. Ikiwa midomoni penu pana ungamo, ‘Yesu ni Bwana’, na moyoni mwenu imani ya kwamba Mungu alimfufua yeye kutoka kwa wafu, basi mtapata wokovu. Kwa maana imani iongozayo kwenye haki imo moyoni, nalo ungamo liongozalo kwenye wokovu lipo midomoni.” (Rum. 10:8-10, The New English Bible) Paulo alizungumza katika masinagogi, kando kando ya mito, shuleni, gerezani, katika nyumba za faragha, kwa watu wa namna zote, Wayahudi na Wagiriki, na kwa makundi madogo na makubwa. Paulo alipozungumza, “neno” lilikaribishwa kwao, karibu sana hata wangeweza kulirudia kwa midomo yao wenyewe na kulihifadhi katika mioyo yao wenyewe. Wengine waliamini na kujizoeza imani hiyo mioyoni mwao.

5. Ili wonyesho wa imani utokeze msimamo wenye haki mbele za Mungu, lazima utie na imani katika nani?

5 Kwa habari ya “imani iongozayo kwenye haki,” Paulo aliwaandikia Warumi hivi: “Tuseme nini, basi? Ya kwamba watu wa Mataifa, wasioifuata haki, walipata haki; lakini ni ile haki iliyo ya imani; bali Israeli wakiifuata sheria ya haki hawakuifikilia ile sheria.” (Rum. 9:30, 31) Ni wazi sana kwamba kwa sababu ya kutangaza injili kwa Paulo watu wengi wasio Wayahudi walisaidiwa kuifikia haki. Vile vile, wanafunzi wengine kwa kufundisha kwao katika miji mingi walileta maelfu ya watu wasio Wayahudi kwenye ujuzi wa Kristo Yesu, nao hawa waliifikia haki, haki inayotokana na imani katika Mwana wa Mungu. Kutokana na ambayo Paulo aliwaonyesha Wayahudi waliofanya jitihada kubwa wapate kuishika sheria ya Musa, hawakuweza wakati wo wote kuifikia haki. “Kwa sababu gani ikawa hivyo? Kwa maana msingi wa jitihada zao haukuwa imani, bali (kama walivyodhani) matendo. Waliliangukia ‘jiwe’ linalotajwa katika Andiko: ‘Hapa naweka katika Sayuni jiwe la kuangukia, mwamba wa kujikwaa; lakini yeye aliye na imani katika yeye hataaibishwa.’”​—Rum. 9:32, 33, NE.

6. (a) Kwa sababu gani taifa la Kiyahudi lilimkataa Yesu kama Masihi, na kwa hiyo ujumbe wa kwamba “Yesu ni Bwana” ulitangazwa kwa nani? (b) “Neno la imani” alilolizungumza Paulo lilikuwa na msingi gani?

6 Sheria ambayo walipewa Wayahudi ilipaswa iwe mwalimu wa kuwaelekeza kwenye Kristo. Ilipaswa iwalete kwenye Masihi na kuwasaidia wamtambue na kumkubali yeye kama mwalimu wao na Bwana atakapokuja. (Gal. 3:24) Na hali wengi wao walijikwaa juu ya yule yule ambaye sheria ya Mungu yenye haki iliwaelekeza kwake, yaani, Mwana wa Mungu, kwa sababu hawakuwa na imani. Kwa hiyo, sasa, “neno” au ujumbe wa kwamba “Yesu ni Bwana” ulikuwa ukitangazwa kwa mataifa yote vile vile, si kwa Wayahudi peke yao. “Neno” hili kutoka kwa Mungu linafanywa lipatikane kwa vyepesi kwa watu wa kila mahali. Barua ya Paulo kwa Warumi ilisema kwamba “neno li karibu nanyi: li midomoni penu na moyoni mwenu.” Lakini mtu atafanya nalo nini? Ikiwa kweli “neno” linaingia ndani ndani moyoni mwake ataamini. Atakuwa na imani katika Yesu Kristo kama Bwana na kama yeye ambaye kupitia kwake Mungu atatimiza ahadi Zake zote za ajabu. (2 Kor. 1:20) Ili awe na imani hiyo lazima awe na ujuzi​—⁠kwanza, ujuzi wa Mungu na ujuzi wa aliyoyasema Yeye na akayafanya, kwa maana mpango wa wokovu kupitia kwa Kristo unatokana na Mungu. Mungu mwenyewe ndiye aliyemfufua Yesu kutoka kwa wafu. Hivi ndivyo Paulo anavyojaribu kusadikisha watu, zaidi Warumi katika siku zake. Nyakati nyingine ilikuwa lazima kukazia ubora wa kweli hizi za msingi hata juu ya wale waliojidai kuwa wakf kwa Mungu siku za Paulo. Paulo alikuwa akilitangaza “neno la imani.” Msingi wa imani hiyo ulikuwa nini? Yalikuwako mambo mawili ya wazi sana aliyoyafikiria Paulo, na kwa hiyo lazima nasi tuyafikirie nyuma ya miaka 1,900 kupita. Ili mtu awe Mkristo lazima alisikie “neno la imani” na kusadikishwa (1) Kwamba Yesu, Mwana wa Mungu, ni Bwana, kwamba kwa kifo chake cha dhabihu aliwanunua wanadamu na kwa hiyo lazima yeye akubaliwe na Wakristo kama mwenyeji wao; vile vile, (2) Kwamba Yehova Mungu alimfufua Yesu kutoka kwa wafu. Bila shaka, wewe ungetaka uhakikisho wa mambo haya mawili kwa maana ni ya lazima ili mtu aweze kupata wokovu, yaani, kupata uzima wa milele.​—2 Kor. 5:14, 15.

7. Kwa sababu ya imani yenye nguvu, wanafunzi wa Yesu walijua nini juu ya Yesu, lakini Mafarisayo waliitikiaje?

7 Wanafunzi waliotembea na Kristo Yesu karne kumi na tisa zilizopita walikuwa na nafasi nzuri ajabu ya kupata imani yenye nguvu kwa maana walitembea kweli pamoja na Mwana wa Mungu. Walimsikia yeye akisema alipokuwa angali hapa duniani kama kiumbe cha kibinadamu na vile vile kufuata ufufuo wake. Wakati Yesu alipowauliza wafuasi wake: “Mwaninena mimi kuwa ni nani?” wangeweza kujibu kwa kusadiki kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi, Mwana wa Mungu. (Mt. 16:15, 16) Lakini juu ya shauri hili Mafarisayo wasioamini waliwekwa katika hali ambayo wasingeweza tena kumjibu Yesu. Habari imeandikwa katika Mathayo 22:41-46: “Na Mafarisayo walipokusanyika, Yesu aliwauliza, akisema, Mwaonaje katika habari za Kristo? Ni mwana wa nani? Wakamwambia, Ni wa Daudi. Akawauliza, Imekuwaje basi Daudi katika [roho] kumwita Bwana, akisema, Bwana alimwambia Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwawekapo adui zako kuwa chini ya miguu yako? Basi, Daudi akimwita Bwana, amekuwaje ni mwanawe? Wala hakuweza mtu kumjibu neno; wala hakuthubutu mtu ye yote tangu siku ile kumwuliza neno tena.”

8, 9. (a) Lazima Wakristo wafanye ungamo gani juu ya Yesu waionyeshe imani yao, nao wataonyeshaje kwamba kwa kweli wanaamini hivyo? (b) Kwa hiyo ni hatua gani zaidi ya lazima kuonyesha imani ya mtu?

8 Lakini, katika siku ya Pentekoste Petro alionyesha wazi “Bwana” huyu ni nani na kwamba yuko katika mkono wa kuume wa Mungu. Alisema hivi: “Basi nyumba yote ya Israeli na wajue yakini ya kwamba Mungu amemfanya Yesu huyo mliyemsulibisha kuwa Bwana na Kristo.” (Matendo 2:36) Kama vile mitume na Wakristo wa kwanza walivyofanya ungamo kwa midomo yao kwamba Yesu ni Bwana, ndivyo na Wakristo hata leo hii wanavyofanya. Lakini, ikiwa wao ni Wakristo wa kweli, mengi zaidi kuliko kusema kwa kinywa tu yahitajiwa. Wao wanaonyesha utiifu wao kwa Kristo kama Bwana kwa kuyafanya mapenzi ya Baba yake Yesu, kama Yesu alivyowafundisha wanafunzi wake kufanya. (Mt. 7:21; Yohana 15:8) Lazima Wakristo waamini kitu kingine vile vile, na hilo ni kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu na Mungu. Petro alihakikisha hili siku ya Pentekoste. Alisema hivi: “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake.” (Matendo 2:32) Sasa je! wewe unayaamini mambo haya mawili ya msingi yaliyosemwa na Paulo na Petro vile vile, kwamba “Yesu ni Bwana” na kwamba “Yesu huyo Mungu alimfufua” kutoka kwa wafu? Ikiwa waamini, basi lazima ufanye jambo fulani, yaani, ufanye ungamo la imani yako kwa midomo yako. Wale wanaofanya ungamo hilo kwa moyo imewapasa wabatizwe. Mtume Petro aliwasihi wale waliomsikia akisema siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. wafanye hivyo. “Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile wakaongezeka watu wapata elfu tatu.”​—Matendo 2:40, 41.

9 Ebu wazia: karibu watu elfu tatu kati ya wale ambao Petro alihutubia walibatizwa! Waliongezwa kwenye kundi nao wakaendelea kujitoa kwa fundisho la mitume na wakashiriki kwa kipekee katika kuzihubiri habari njema kwa wengine.​—Mt. 28:19, 20; Matendo 8:1, 4.

10. (a) Mtume Paulo alijaribuje kulitia moyo kundi la Rumi litende kwa bidii? (b) Basi, ingewapasa kufanya nini Waihakikishe imani yao, wakiweka mfano gani kwa Wakristo leo?

10 Miaka mingi kufuata hapo, karibu mwaka wa 56 C.E., mtume Paulo alikuwa akiliandikia kundi la Kikristo katika Rumi. Pengine kundi hilo lilianzishwa na Wayahudi fulani au waongofu kutoka Rumi waliokuwa wametembelea Yerusalemu siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 C.E. Pengine wao walikuwa wamekushuhudia kumiminwa kwa roho takatifu kwa mwujiza wakati huo. (Matendo 2:1-5, 10) Sasa miaka 23 ilikuwa imepita. Wakati huo Paulo alikuwa amekwisha kuwa mtume kwa mataifa, na kwa kuwa alipendezwa na kundi katika Rumi alikuwa akijaribu kuwachochea kwenye utendaji mkubwa zaidi ili habari njema hizi za Ufalme zipate kuhubiriwa mahali pengi zaidi kuliko zilivyokuwa zimehubiriwa wakati huo. Mambo ambayo katika hayo walikiri imani mbele ya ubatizo yalipaswa vile vile kutangazwa waziwazi nyuma ya ubatizo ili wengine wapate kuamini. Paulo aliandika hivi: “Ikiwa midomoni penu pana ungamo, ‘Yesu ni Bwana,’ na moyoni mwenu imani ya kwamba Mungu alimfufua yeye kutoka kwa wafu, basi mtapata wokovu.” (Rum. 10:9, NE) Ikiwa kweli waliamini hili wangekuwa wenye bidii katika kulihubiri kwa wengine. Lazima waihakikishe imani yao kwa mambo yaliyokuwa midomoni pao, kwa kuitaja imani yao kwa wengine kwamba Yesu ni Bwana kweli. Lazima wahakikishe kwa matendo yao kwamba waliamini Yesu alikuwa amekwisha kwezwa kwenye cheo ambacho ukuu wake unapitwa na cha Mungu peke yake na kwamba “kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Flp. 2:9-11) Sisi, vile vile, lazima tutoe ushuhuda wa kwamba tunayo imani hiyo. Bila shaka, ili aamini hivyo, lazima kila Mkristo aamini vile vile kwamba Yesu Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu, na kwamba Yehova Mungu mbinguni ndiye aliyemfanyia Mwanawe hivyo. Paulo anaonyesha katika barua yake kwamba alisadiki hivyo, naye alikuwa akijaribu kuwasadikisha wasomaji wote wa barua yake kwamba imewapasa waitangaze habari ya kwamba Yesu ni Bwana na kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu. Kwa njia hiyo mtu atapata wokovu. Bila shaka, mtu aliyeokolewa ni mshindi. Anaushinda ulimwengu. Atapata uzima wa milele.

11, 12. Warumi 10:10 inaonyeshaje kwamba imani ya kweli lazima iwe yenye msingi imara?

11 Paulo anatilia mkazo umuhimu wa imani, si katika mambo haya mawili tu, kwamba Yesu ni Bwana na ufufuo, lakini, kwa kweli, katika mambo yote aliyoyafundisha Yesu. Lazima imani hii iwe yenye msingi imara, si ya kijuujuu tu; “imani iongozayo kwenye haki imo moyoni, nalo ungamo liongozalo kwenye wokovu lipo midomoni.”​—Rum. 10:10, NE.

12 Ulimwenguni pote leo mashahidi wa Kikristo wa Yehova wanafanya ungamo hili. Watu wa mataifa yote wanaozungumza mamia ya lugha mbalimbali wanajifunza kweli ya Neno la Mungu. Lazima Wakristo wahakikishe kwamba wanayo imani kwa wanayoyatenda.

MANENO BILA MATENDO YANA FAIDA GANI?

13. Ajapokuwa hakuwa mwanafunzi wa Yesu hapo kwanza, ni mwendo gani wa imani ambao Yakobo, ndugu wa mzazi mmoja na Yesu, aliufuata mwishowe?

13 Mwanafunzi Yakobo, ndugu wa mzazi mmoja na Yesu, bila shaka aliyafahamu sana matendo ya nduguye, lakini hakuna jambo lo lote linaloonyesha kwamba yeye alikuwa mwanafunzi aliyemfuata Yesu mnamo huduma yake ya kidunia. Pengine Yakobo alikuwa amekuwa kati ya wale jamaa za Yesu waliosema hivi juu yake: “Amerukwa na akili.” (Marko 3:21) Lakini, yaelekea sana kuwa Yakobo huyu ndiye aliyemwona Yesu alipokwisha kufufuliwa. Kwa wazi Paulo alimmaanisha yeye alipowaandikia Wakorintho hivi: “Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano pamoja . . . Baadaye akamtokea Yakobo; tena na mitume wote.” (1 Kor. 15:6, 7) Kwa hiyo yaelekea kwamba Yakobo huyu ndiye aliyekusanyika asali pamoja na mama yake na mitume na wengine katika chumba cha juu katika Yerusalemu, Yesu alipokufa na mbele ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. (Matendo 1:13, 14) Akaamini kwamba Yesu ni Bwana, na vile vile akajua kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu. Nyumaye Yakobo alipata kuwa mfuasi mashuhuri wa Kristo Yesu naye alikuwa mmoja wa wale walioshiriki katika kuamua mambo kwa ajili ya makundi yote wakati baraza ya wazee ilipokutana katika Yerusalemu miaka ya nyumaye.​—Matendo 15:6, 13.

14. (a) Yakobo alionyeshaje kukamatana kwa imani na matendo mema? (b) Ni maneno gani ya Yesu tuliyo nayo kuuonyesha msingi ambao kwao sasa anabagua watu, kwa kutumainia uzima au kifo?

14 Yakobo aliandika mambo fulani yenye nguvu kwa ndugu zake wa Kikristo, naye alishughulika na shauri hili la imani. Aliliona sawa na alivyoliona Paulo. Yakobo alilitaja hivi: “Ndugu zangu, kuna faida gani kwa mtu kusema anayo imani, na huku hafanyi lo lote kuionyesha?” (Yak. 2:14, NE) Hakuna sababu ya mtu kujivunia imani yake ikiwa yeye hana matendo ya kuitegemeza. Kwa kweli dai lake kwamba anayo imani ni la uongo. Ili kuonyesha mfano wa shauri hili muhimu la matendo yafaayo Yakobo analiuliza kundi ulizo: “Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini?” (Yak. 2:15, 16) Matendo yanahitajiwa kuonyesha kwamba tamaa inayotajwa katika maneno ni ya kweli. Twakumbuka kwamba Yesu alisema hivi: “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake; . . . naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi; atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto. Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari. . . . Nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika; . . . Kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”​—Mt. 25:31-40.

15, 16. (a) Tuna maelezo gani juu ya neno “uchi” linalopatikana katika Mathayo 25:36? (b) Awezaje mtu kuwafanyia “ndugu” za Yesu matendo mema asiwe akisema tu “Heri njema kwenu”?

15 Isingekuwa lazima watu wawe uchi kwa halisi ndiyo wahitaji msaada. Maelezo ya chini ya New World Translation yanasema hivi juu ya Mathayo 25:36: “Au, ‘sikuwa nimejivika vya kutosha’; katika lugha ya kawaida neno la kwanza kwa usemi huu lilimaanisha ‘kuvaa kwa njia hafifu, vazi la ndani peke yake,’ kwa hiyo kuvalia kwa ukosefu, si lazima iwe uchi kabisa.” Bila kujali kama mtu yu uchi au amevalia kwa njia hafifu tu, mtu anayeiona hali ya “mgeni” haimpasi kusema tu, ‘Enenda zako kwa amani, ukaote moto na kushiba.’ Bila shaka, hatuwezi kumtolea Yesu mwenyewe msaada huo, lakini twaweza kufanya hivyo kwa “ndugu” zake, Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho walio hai hapa duniani. Je! wewe unawatolea msaada huo, ukifanya hivyo kwa maana unauona uhitaji wao na kwa maana unajua kwamba wao ni mali ya Kristo?​—Mt. 10:41, 42.

16 Yakobo anaonyesha kwamba maneno yasiyotegemezwa na matendo ni ya bure. Kuyasema tu maneno ‘Ukaote moto’ hakutamfaidi ndugu wala dada yako wa Kikristo. Tafsiri nyingine inayataja maneno ya Yakobo hivi: “Tuseme ndugu au dada amevalia matambaa asiwe na chakula cha kutosha kwa siku, na mmoja wenu asema, ‘Heri njema kwenu, mkajipashe moto, na mle vya kutosha,’ lakini asifanye lo lote kutosheleza mahitaji yao ya kimwili, kuna faida gani?” (NE) Ikiwa mtu anataka kuwaona watu wakijipasha moto, basi itahitaji jitihada kidogo kwa upande wa Mkristo ahakikishe kwamba watu hao wanapashwa moto kwa kuwapa kitu fulani, siyo kwa kusema tu, “Heri njema kwenu,” asifanye lo lote kutosheleza mahitaji yao ya kimwili. Vivyo hivyo, lazima imani ifuatane na matendo. Lazima imani itegemezwe na tendo.

JE! IMANI YAKO IMEKUFA AU I HAI?

17. Nini maana ya Yakobo 2:18?

17 Yakobo anaendelea kusema: “Ndivyo na imani; ikiwa haiongozi kwenye tendo, hiyo yenyewe ni kitu kilichokufa.” (Yak. 2:17, NE) Hiyo ni kweli. Sasa Yakobo anamtokeza mtu wa kuwazika, na kusema: “Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu.” (Yak. 2:18) Jambo linalozungumzwa si kwamba matendo yanayopatana na sheria ya Musa au imani katika Yesu Kristo ndivyo vinavyoongoza kwenye wokovu. Bali, imani iliyo ya kweli na iliyo hai ndiyo inayotofautishwa na imani iliyokufa. Tafsiri nyingine yasema hivi: “Lakini huenda mtu fulani akapinga: ‘Huyu anajidai kuwa na imani na mwingine aonyesha matendo yake.’ Nami najibu hivi: ‘Nihakikishie kwamba imani hii unayozungumza juu yake ni ya kweli ijapokuwa haifuatani na matendo, nami kwa matendo yangu nitakuhakikishia imani yangu.’”​—NE.

18, 19. (a) Tuna ushuhuda gani wa kwamba watu wengi wanaosema wanamwamini Mungu na Kristo hawana imani ya kweli? (b) Yakobo aliwaambia nini wale waliojidai kumwamini Mungu lakini wasiokuwa na imani yenye bidii?

18 Kwa hiyo inampasa mtu ajiulize: Je! Mkristo aweza kuihakikisha imani yake bila ya matendo yo yote? Au ni lazima Mkristo aihakikishe imani yake kwa kuwaonyesha wengine kwa matumizi ya moyo wake, akili, nafsi na nguvu kwamba imani yake ni imani iliyo hai, imani yenye mazao, si iliyokufa? Yakobo anaonyesha kwamba matendo ni uhakikisho wa imani ya mtu. Kuna watu wengi ulimwenguni leo wasemao wanamwamini Mungu, lakini uwaulizapo, ‘Yeye ni nani? Yeye amefanya nini? Yeye anafanya nini?’ mazungumzo yanakomea pale pale. Wao hawamwamini Mungu kabisa, kwa maana wao hawamjui. Wao hawana “hakika ya mambo yatarajiwayo.” Hawaifahamu “bayana ya mambo yasiyoonekana.” (Ebr. 11:1) Wengine wanasema, ‘Mimi namwamini Yesu Kristo,’ lakini unapouliza, ‘Yesu Kristo anafanya nini sasa?’ hawajui kabisa. Wanasema alikufa. Wao hawaamini yeye ndiye Bwana aliyefufuliwa, aliye hai mbinguni, aliyekabidhiwa uwezo mkubwa na anayetawala kama mfalme, ambaye karibuni ataileta taratibu mbovu ya mambo kwenye kikomo chake, na anayejitayarisha kuitimiza kabisa sala ambayo Wakristo wamefundishwa kusali, yaani, “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:10) Watu hao hawajui la kusema wanapokueleza imani yao ni nini. Wao hawawezi kuitegemeza kwa uhakikisho wa Biblia. Hawana tumaini. Kwa kweli, hawaamini kwamba Yesu ni Bwana na kwamba Yehova Mungu alimfufua yeye kutoka kwa wafu na kwamba amefanywa mfalme wa ufalme wa Mungu na kuwekwa katika kiti cha enzi cha kimbinguni awabariki wanadamu wote. Je! wewe waamini?

19 Kwa wazi katika mazungumzo yake na watu waliojidai kuwa wa kundi la Mungu katika karne ya kwanza Yakobo aliona kwamba wengine hawakuwa na imani iliyokuwa hai, iliyokuwa yenye bidii, iliyomvuta mtu kuonyesha upendo wa kweli kwa ndugu zake wa Kikristo na kushiriki katika kutokeza wanafunzi zaidi wa Yesu Kristo. Kwa hiyo Yakobo alisema: “Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema. Mashetani nao waamini na kutetemeka.” (Yak. 2:19) Kwa nini Yakobo alisema hayo?

20, 21. Twajuaje kwamba mashetani wanaamini kuna Mungu, lakini n’nini kilichowapata wakati wa Gharika, na kwa sababu gani?

20 Yeye anaonyesha kwamba mashetani wanaamini kuna Mungu. Kwa kweli, wao wanajua hivyo sana, kwa maana “wanadamu walipoanza kuzidi usoni pa nchi na wana wa kike walizaliwa kwao, wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wo wote waliowachagua.” (Mwa. 6:1, 2) Hawa “wana wa Mungu” walikuwa viumbe vya kiroho lakini wakajivika miili. “Walipoingia kwa binti za wanadamu, wakazaa nao wana; hao ndio waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa.” Kwa sababu ya upotovu wao malaika hawa walioanguka walileta maangamizi makuu duniani, nao wazao wao wa mchanganyiko, “watu hodari,” bila shaka walishiriki sana katika kuleta “maovu” yaliyojaa duniani siku hizo. Kama matokeo, Mungu akasema kwamba angewaharibu wanadamu kwa gharika, akimhifadhi Nuhu peke yake, mkewe na wana wake watatu na wake zao.​—Mwa. 6:4-7, 11-13.

21 N’nini kilichowapata malaika hao waliojivika miili maji ya gharika yalipoanguka? Walilazimishwa kuyarudia makao ya kiroho, lakini si kwenye vyeo walivyogawiwa ambavyo walikuwa wameviacha. Yuda anatuambia hivi: “Malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.” (Yuda 6) Yakobo anawataja malaika hawa kama mashetani. Mashetani hawa waliamini kuna Mungu mmoja, wao waliamini kwamba yupo, lakini hawakuyatenda matendo ya Mungu.

22, 23. Kuna ushuhuda gani kwamba mashetani walimjua Kristo Yesu vile nao wakautambua uwezo wake?

22 Walimjua Mwana wa Mungu vile vile, Kristo Yesu, lakini hawakuyatenda matendo yake. Yesu alipokuwa katika nchi ya Wagerasi alikutana na watu wawili waliopagawa na mashetani wakitoka katika makaburi. Watu hawa walikuwa wakali mno asiweze mtu ye yote kuwa na ujasiri wa kupita njia ile. Mashetani hawa walijua Yesu Kristo alikuwa nani. “Wakapiga kelele, wakisema, Tuna nini nawe, Mwana wa Mungu? Je! umekuja kututesa kabla ya muhula wetu?” Habari yatuambia kwamba Yesu aliwafukuza mashetani hao wawatoke watu hao nao mashetani hawa wakaingia katika kundi la nguruwe.​—Mt. 8:28-32.

23 Bila shaka mashetani hawa waliamini kwamba kuna Mungu na kwamba Yesu ndiye Mwana wa Mungu. Nao walitetemeka walipokumbuka hii maana yake nini. Petro anatuambia hivi: “Mungu hakuwaachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu.”​—2 Pet 2:4.

24. Kwa hiyo, basi, kwa nini kuamini kuna Mungu hakutoshi?

24 Ni wazi sana kwamba hawa wana wa Mungu walipata kuwa mashetani kwa sababu ya kutofanya mapenzi ya Mungu. Walikuwa waasi. Bila shaka walijua kuna Mungu; na sasa Yakobo anasema hivi akisema kwa wale waliomo katika kundi la Kikristo: “Wewe waamini ya kuwa Mungu ni mmoja; watenda vema.” Lakini ikiwa hilo ndilo waliloamini peke yake, basi hawakuwa tofauti sana na mashetani. Mashetani wanampinga Mungu, na hata hivyo wanaamini. Wao wana ujuzi. Wao wanakijua cheo alicho nacho Yehova katika ulimwengu wote, lakini wao hawajipatanishi na mapenzi yake. Vivyo hivyo, mamilioni na mamilioni ya watu papa hapa duniani wanaamini kuna Mungu, nao wanasema wanayo imani, lakini ya wapi matendo yao? Yao ni imani iliyokufa.

USHUHUDA WA IMANI ILIYO HAI

25. (a) Sasa kila mmoja wetu anakutana na maulizo gani? (b) Yakobo anatuambia nini juu ya imani ya Ibrahimu?

25 Kwa hiyo Yakobo analisawazisha shauri hili mbele ya wasikilizaji wake: “Huwezi kuona, ewe mlaghai, kwamba imani iliyotenganishwa na matendo i tasa?” (Yak. 2:20, NE) Mwanamke aliye tasa hazai. Imani yako wewe yakufanyia nini? Je! inayo matendo? Je! inazaa kitu fulani? Je! wewe waishi kupatana na unavyojidai kuamini? Je! imani yako yakusaidia ufanye wanafunzi wa Kristo Yesu? Je! wewe waongezea faida za Ufalme? Ili akazie shauri lake, Yakobo anatupa sisi mfano naye azungumza juu ya Ibrahimu: “Je! haikuwa ni kwa tendo lake, katika kumtoa mwanawe Isaka juu ya madhabahu, kwamba baba yetu Ibrahimu akahesabiwa kuwa haki? Kwa kweli mwaweza kuona kwamba imani ilifanya kazi katika matendo yake, na kwamba kwa matendo haya ukamilifu wa imani yake ulihakikishwa kabisa. Huu ulikuwa utimizo wa maneno ya Andiko: “Ibrahimu alimwamini Mungu, nayo imani hiyo ikahesabiwa kwake kama haki; naye mahali pengine anaitwa ‘rafiki ya Mungu.’ Mwaona basi kwamba mtu anahesabiwa haki kwa matendo wala si kwa imani peke yake.” (Yak. 2:21-24, NE) Je! wewe unayo imani kama ile ya Ibrahimu, namna ya imani inayomvuta mtu akutangulize kufanya mapenzi ya Mungu mbele ya maisha yenyewe?

26. (a) Kama inavyosimuliwa na Paulo, Ibrahimu na Sara walionyeshaje waliziamini ahadi za Mungu? (b) Ni ulizo gani sasa linalojitokeza kwa kila mmoja wetu?

26 Paulo alisema hivi katika barua yake juu ya imani: “Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo.” Vile vile, yeye aliandika juu ya Ibrahimu naye anamtumia Ibrahimu kama mfano wa imani wa mtu aliyeishi kweli. Anasema: “Kwa imani Ibrahimu aliutii mwito wa kwenda kwenye nchi aliyopangiwa yeye na warithi wake, naye akaondoka nyumbani asijue ilikompasa kwenda. Kwa imani alikaa kama mgeni katika nchi aliyoahidiwa, akiishi katika hema, kama walivyofanya Isaka na Yakobo, waliokuwa warithi wa ahadi ile ile. Kwa maana yeye alikuwa akiutazamia mji wenye misingi imara, ambao mwandishi wa ramani yake na mjenzi ni Mungu. Kwa imani Sara mwenyewe alipokea nguvu za kuchukua mimba, ajapokuwa alikuwa ameupita umri, kwa maana yeye aliamua kwamba yeye aliyekuwa ameahidi angedumisha imani; na kwa hiyo kutoka kwa mtu mmoja, na ambaye alikuwa kama mfu, walitokea wazao walio wengi sana kama nyota au kama chembe zisizohesabika za mchanga ufuoni.” (Ebr. 11:8-12, NE) Twajua kwamba Ibrahimu alikufa bila ya kupata utimizo wa ahadi iliyofanywa kwake, lakini bila shaka yeye alikuwa na imani na taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, na katika maisha yake yote alikuwa na ushuhuda wa baraka ya Mungu juu yake. Imani ya Ibrahimu katika “mji . . . ambao mwandishi wa ramani yake na mjenzi ni Mungu” ilimvuta aache nyuma raha za mambo ya kimwili ili afanye mapenzi ya Mungu. Je! matendo yako yanatoa ushuhuda vivyo hivyo kwamba ufalme wa Mungu una maana zaidi kwako kuliko mali za kimwili?​—Luka 12:29-31.

27. Nuhu alionyeshaje kwamba alikuwa mtu mwenye imani yenye utendaji?

27 Kulikuwako mtu mwingine, ambaye aliona yale ambayo wana wa Mungu walikuwa wameyafanya katika ushirika wao na binti za wanadamu mbele ya gharika ya dunia yote kuja, naye Paulo vile vile anamtumia yeye kama mfano wa mtu anayeonyesha imani ya kweli. Twasoma hivi: “Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, aliunda safina, apate kuokoa nyumba yake. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani.” (Ebr. 11:7) Ujenzi wa safina haukutimizwa kwa mwujiza. Ilikuwa lazima Nuhu akate miti, aichonge, na kuweka vyumba mbalimbali katika jengo. Ilimpasa kufunika ndani na nje kwa lami. (Mwa. 6:14) Safina hii haikuwa ndogo; vipimo vyake vilikuwa futi 437 na inchi sita urefu wake, futi 72 na inchi kumi na moja upana wake na futi 43 na inchi tisa urefu wa kwenda juu. Jengo hili kubwa lenye mfano wa sanduku lilijengwa katika nchi kavu. Vile vile Biblia inatoa maelezo ya orodha ya kupendeza ya abiria wake. Mbali na Nuhu, mkewe, wana wake watatu na wake zao, Nuhu aliagizwa aingize viumbe vingine safinani pamoja naye: “Kila kilicho hai chenye mwili, wawili wa kila namna utawaleta ndani ya safina, kuwahifadhi pamoja nawe; wawe mume na mke. Katika vyote virukavyo kwa jinsi yake, na kila namna ya mnyama kwa jinsi yake, kila kitambaacho juu ya nchi kwa jinsi yake, wawili wa kila namna watakuja kwako, ili uwahifadhi. Ukajitwalie chakula cha kila namna kinacholika, ukakusanye, nacho kitakuwa ni chakula chenu na chao. Ndivyo alivyofanya Nuhu, sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwa, 6:19-22) Je! ungesema kwamba Nuhu alikuwa na tendo la kuihakikisha imani yake?

28. Kwa sababu ya imani yake yenye utendaji, Musa alikataa nini?

28 Pana mtu mwingine ambaye wasomaji wa Biblia wamejifunza juu yake katika Maandiko. Kuonyesha kwamba yeye alikuwa na taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, Paulo anasema hivi juu yake: “Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; akihesabu ya kuwa kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri; kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo. . . . Kwa imani akaifanya Pasaka, na kule kunyunyiza damu, ili yule mwenye kuwaangamiza wazaliwa wa kwanza asiwaguse wao. Kwa imani wakapita kati ya Bahari ya Shamu, kama katika nchi kavu; Wamisri walipojaribu kufanya vivyo wakatoswa.”​—Ebr. 11:24-29.

29. Katika namna ambavyo Rahabu aliwatendea wapelelezi wawili n’nini kinachoonyesha yeye alimwamini Yehova?

29 Yakobo hakuwa na wakati wa kuizungumza imani ya watu wengine, kama alivyokuwa nao Paulo. Akiwahutubia ndugu na dada zake, aliwataja Ibrahimu na Rahabu tu. Kwa hiyo alisema hivi: “Ndivyo ilivyo na kwa kahaba Rahabu. Je! yeye hakuhesabiwa haki kwa tendo lake katika kuwakaribisha wajumbe nyumbani mwake na kuwatoa nje kwa njia nyingine?” (Yak. 2:25, NE) Rahabu alikulia katika nchi ambamo miungu mingine iliabudiwa, siyo Mungu wa Israeli. Lakini yeye akapata habari juu ya Mungu wa Israeli naye akamwamini Mungu wao kwa sababu ya yale ambayo Yeye alikuwa amewafanyia Waisraeli. Paulo alimtaja yeye vile vile, sawa na Yakobo, akimtumia yeye kama mfano wa imani. Paulo alisema hivi: “Kwa imani Rahabu, yule kahaba, hakuangamia pamoja na hao walioasi; kwa kuwa aliwakaribisha wale wapelelezi kwa amani.” (Ebr. 11:30, 31) Si kwamba tu Rahabu aliamini aliyoambiwa na wajumbe walipoingia nyumbani mwake, lakini vile vile aliwafanyia kazi. Aliwaficha wajumbe na kuwasaidia watoroke. Vile vile aliikusanya jamaa yake katika mahali pa salama. Yeye aliamini mambo ambayo Waisraeli walimwambia yalikuwa ya kweli.

30, 31. Ni ukamatano gani unaofanywa na Yakobo kati ya mwili na pumzi na imani na matendo, na kwa hiyo n’nini kusudi la maneno ya Yakobo?

30 Yakobo anamaliza mazungumzo yake kwa kusema: “Kama vile mwili ulivyo mfu pasipo pumzi yo yote iliyobakia ndani yake, vivyo hivyo imani iliyotenganishwa na matendo imekufa kama mzoga.” (Yak. 2:26, NE) Siku zilizopita, ikiwa mtu alitaka kuhakikisha hakuna pumzi iliyobakia katika mwili alikuwa akichukua kioo na kukishikilia karibu na kinywa na pua ya mtu. Ikiwa mlikuwa na pumzi katika mwili huo angeweza kuiona kiooni. Ikiwa kusingekuwa na dalili yo yote ya pumzi, angesema mtu yule alikuwa mfu. Kwa hiyo Yakobo anautumia mfano wa mwili. Usipokuwa na pumzi ndani yake, ndivyo mtu anayejidai kuwa na imani lakini asiye na matendo alivyo. Imani inapotenganishwa na matendo na hakuna tendo linaloitegemeza imani hiyo, basi imani ya mtu ni kama mzoga usio na uhai.

31 Jambo moja tunalopaswa kukumbuka ni kwamba Yakobo anahutubia Wakristo, watu walio wakf kwa Yehova Mungu na waliobatizwa na wanaojidai kabisa kwamba wao ni mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Yeye anajaribu kumchochea kila mmoja wao kwenye tendo. Ikiwa wanayo imani imewapasa waionyeshe. Usisahau namna alivyoianza hotuba yake ndefu juu ya imani: “Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo?”​—Yak. 2:14.

32, 33. Ni kwa sababu gani imewapasa mashahidi wa Yehova leo wawe na imani yenye nguvu, na je! wanatoa ushuhuda wa kuwa na imani hiyo?

32 Leo imani yetu imepaswa iwe yenye nguvu kwa maana tunayo Biblia yote. Tunayo Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki. Twaona waliyoyafanya watu waliokuwa katika imani mbele ya Kristo Yesu, Mwana wa Mungu, kutokea duniani. Vile vile twaiona imani ya Wakristo wa kwanza na waliyoyafanya. Wao walimtambua Yesu Kristo kama Mwana wa Mungu; waliutazama mwendo wake wa maisha na bidii yake ya kuzihubiri habari njema za Ufalme kisha wakamwiga yeye kwa kuweka imani yao katika ufalme huo na kuzihubiri habari njema. Sasa Yesu amekwisha kufufuliwa kutoka kwa wafu. Juu ya huyu ambaye Wakristo wa kweli wanajaribu kuuiga mfano wake, Waebrania 1:3 inasema hivi: “Yeye kwa kuwa ni mng’ao wa utukufu wake [Mungu] na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu.”

33 Kwa hiyo leo twawaona mamia ya maelfu ya mashahidi wa Yehova wenye imani yenye nguvu. Kwa midomo yao wanaonyesha wanaamini kwamba Yesu ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu, na moyoni mwao wanaamini kwamba Mungu alimfufua Kristo Yesu kutoka kwa wafu. Wakiwa na namna hii ya imani na kuitangaza waziwazi, wakieleza watu wa mataifa yote na lugha juu yake, wao wanalo taraja lililohakikishwa la wokovu wa kupata uzima wa milele.

34. Ikiwa tunaweka imani katika Yehova, tutatendaje tutakapokutana na hali inayosimuliwa katika Habakuki 3:17, 18?

34 Huenda mkazo mwingi ukaletwa juu yao na taratibu mbovu ya mambo mnamo wakati wake wa kumalizia; huenda wakapatwa na ugumu wa hali ya uchumi; nyakati nyingine huenda kuokoka kwao kwenyewe kuonekane kwenye mashaka. Lakini watakapokutana na haya yote, kwa kuweka imani katika Yehova watakuwa na sababu ya kufurahi. Kama vile nabii Habakuki alivyoongozwa na roho ya Mungu aandike: “Ujapokuwa mtini wenyewe usichanue, na kusiwe na mazao katika mizabibu; . . . hata hivyo, kwangu mimi, mimi nitamfurahia Yehova mwenyewe; mimi nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.”​—Hab. 3:17, 18, NW.

35. Ni utendaji gani hasa katika nyakati hizi utakaoonyesha kwamba sisi tu wenye imani iliyo hai?

35 Leo sisi tu karibu sana na wakati huo wenye hatari. Tunaishi katika siku za mwisho za hii taratibu ya mambo, nasi twauona utimizo wa unabii, zaidi ule ulioandikwa katika sura ya 24 ya Mathayo, unaoyasimulia mambo yale yale ambayo yangetukia mbele ya hii taratibu ya mambo kuja kwenye mwisho. Kama ilivyoandikwa katika Mathayo 24:14, NW, Yesu alisema hivi: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakuja.” Mashahidi wa Yehova wanaamini hivyo. Wao wanayo imani katika ufalme wa Mungu na kwa hiyo wamezitangaza habari njema hizi ulimwenguni pote. Amepaswa kila mtu apendezwe kuona yale ambayo mashahidi wa Yehova waliyafanya mnamo mwaka uliopita wa utumishi.

RIPOTI YA ULIMWENGUNI POTE

36, 37. (a) Orodha ya utumishi iliyomo katika gazeti hili yaonyeshaje imani ya mashahidi wa Yehova? (b) Ni kwa kadiri gani ambavyo wanafunzi wapya wamefanywa mnamo mwaka uliopita?

36 Kwa kuiangalia orodha katika kurasa 306-308 utaweza kuona waliyoyafanya mashahidi wa Yehova wa Kikristo katika kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu mnamo mwaka wa utumishi wa 1973 katika nchi mbalimbali 208 na visiwa vya bahari. Eneo hili lote linaangaliwa kupitia kwa maafisi ya tawi ya Watch Tower Society yaliyowekwa katika nchi mbalimbali 95.

37 Kama Wakristo wajuavyo, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake, “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza.” (Mt. 28:19) Hili lilifanywa kwa matokeo bora mnamo mwaka wa utumishi uliopita. Kulikuwako watu 193,990 waliopata kuwa wanafunzi, wakiweka maisha zao wakf wafanye mapenzi ya Mungu na kuonyesha hili kwa ubatizo wa maji. Sasa wamejitambulisha na mashahidi wa Yehova wa Kikristo nao wanaihakikisha imani yao kwa matendo yao.

38. (a) N’nini kinachoonyesha kadiri ambavyo mashahidi wa Yehova walijitahidi kuzihubiri habari njema mnamo mwaka uliopita? (b) Karibu watu wangapi walikuwa wakijifunza Biblia hasa?

38 Kwa wastani, kulikuwako wahubiri 1,656,673 wa habari njema nje katika utumishi wa shambani kila mwezi, lakini kilele cha watu 1,758,429 wenye kuzitangaza habari njema kilifikiwa wakati wa mwaka huo. Watu hawa walifanya kazi kubwa ajabu, ambayo yaweza kushukuriwa vizuri zaidi labda kwa kujua ni saa ngapi walizozitumia katika kazi ya nyumba kwa nyumba wakifanya ziara za kurudia, wakiongoza mafunzo ya Biblia na kuzungumza nyakati zote zilizofaa na za namna zote juu ya tumaini lao la Ufalme. Watu hawa walio wakf ili wazihubiri habari njema walitumia saa 300,468,676 katika utumishi. Ebu wazia namna wakati huo ulivyo mwingi! Huu haukuwa wakati uliotumiwa wakijisomea Biblia wenyewe tu, lakini kwa kweli ulitumiwa kwa kwenda na kuzungumza na watu wengine juu ya linavyosema Neno la Mungu. Zaidi ya hayo, walifanya ziara za kurudia 131,657,832 kwa watu walioonyesha kupendezwa na Biblia, na wakaongoza mafunzo ya nyumbani ya Biblia kwa kipindi cha miezi sita au zaidi na jamaa mbalimbali 1,209,544 kila juma. Je! funzo la Biblia kama hilo liliongozwa nyumbani kwako? Miezi sita imalizikapo, ikiwa watu wanapendezwa kweli na ufalme wa Mungu kwa kawaida watakuwa wakija kwenye Jumba la Ufalme. Kwa hiyo twaweza kusema kwamba karibu watu mbalimbali 2,400,000 ulimwenguni mwote walikuwa hasa na mafunzo ya Biblia yakiongozwa nyumbani mwao wakati wa mwaka, na, bila shaka, iliwapasa kufanya uamuzi juu ya kama wangepata kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo na kuonyesha imani yao katika ufalme wa Mungu kwa matendo yao. Kama ulivyoona, watu 193,990 walipata kuwa wanafunzi, wakiweka maisha zao wakf kwa Mungu, nao sasa wanashirikiana na mashahidi wa Yehova wa Kikristo katika kuzitangaza habari njema.

39, 40. Kama inavyoonyeshwa na hesabu, watu wa Yehova walitumiaje vitabu mnamo mwaka uliopita?

39 Si kwamba tu mashahidi wa Yehova wanaitumia Biblia katika mafunzo yao na watu, lakini vile vile wao wanatumia vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia. Wamegawa vingi vya hivi wakati wa mwaka. Kwa kweli, Biblia 21,761,877 na vitabu vya kusaidia kujifunza vilienezwa kwa sababu ya kuhubiri kwao habari njema, pamoja na vijitabu 9,965,259.

40 Nyote mnafahamiana na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Awake! nanyi mwajua kwamba mashahidi wa Yehova wanatumia magazeti haya katika marudio ya kawaida nyumbani mwa watu. Mnamo mwaka uliopita waliangusha nakala 235,468,467 za haya katika lugha nyingi. Mnara wa Mlinzi unachapwa katika lugha 77 mbalimbali nalo Awake! katika lugha 31. Vile vile maandikisho mengi ya mwaka mmoja yalichukuliwa. Maandishi yanaonyesha maandikisho 1,894,447 yalitumwa kwa Sosaiti wakati wa mwaka. Ili kutosheleza waandikishaji wote na wasomaji wengine wa magazeti haya, viwanda 37 ambavyo Watch Tower Society inatumia vilichapa jumla ya nakala 198,177,981 za The Watchtower na magazeti 202,520,820 ya Awake! miezi kumi na miwili iliyopita. Hili ni ongezeko la magazeti 15,500,000 kupita mwaka uliotangulia. Kwa hiyo watu wanapendezwa na funzo la Biblia na ujumbe ambao mashahidi wa Yehova wa Kikristo wanajaribu kuwaletea.

41. Hudhurio kubwa penye mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni linaonyesha nini?

41 Mbali na wale ambao ni Mashahidi wenye bidii, watu wengine wengi wanapendezwa sana na wanayoyafanya mashahidi wa Yehova nao wanaihudhuria mikutano ya mashahidi wa Yehova. Kuna makundi 31,850 ulimwenguni mwote. Katika mwadhimisho wa Ukumbusho jioni ya Aprili 17, 1973, walihudhuria watu 3,994,924 penye Majumba ya Ufalme ya mashahidi wa Yehova ulimwenguni mwote, na watu 10,523 walikula na wakanywa mkate na divai, wakionyesha kwamba walijidai kuwa waliotiwa mafuta kwa roho ya Mungu na kutumainia kushirikiana na Kristo Yesu katika utukufu wa kimbinguni. Wale wengine wanatazamia kuishi katika dunia ya paradiso chini ya utawala wa kimungu wa ufalme wa kimbinguni wa Yehova.

42. Watu wa Yehova walitendaje katika huduma yao mwaka uliopita nyuma ya Pazia la Chuma?

42 Nyakati nyingine watu wanauliza kama mashahidi wa Yehova wanaendesha kazi yao nyuma ya Pazia la Chuma. Ndiyo, maandishi yetu yanaonyesha kwamba kuna mashahidi wa Kikristo wa Yehova 150,448 wanaozihubiri habari njema wakiwa katika magumu makali katika nchi kama hizo. Kwa kweli, walikuwa na ongezeko la kiasi cha 5 1⁄2 kwa mia mnamo miezi kumi na miwili iliyopita, na watu 11,334 walibatizwa katika nchi hizi. Kwa kweli, ubatizo huu ulifanywa faraghani kwa maana mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku nyuma ya Pazia la Chuma na katika nchi nyingine kadha. Lakini hii haiwazuii mashahidi wa Yehova wasijaribu kufanya watu hawa kuwa wanafunzi vile vile, wakiwabatiza katika jina la Baba, na la Mwana na la roho takatifu. Wote hawa wanaopata kuwa wanafunzi wanaamini kwamba “imani iliyotenganishwa na matendo imekufa kama mzoga.” Kwa hiyo, kwa furaha, mashahidi wa Yehova wa Kikristo wamejitahidi sana katika nchi 208 za ulimwengu na kwenye miisho ya dunia nao walikuwa na mwaka wa kupendeza sana katika kuzihubiri habari njema za ufalme wa Yehova.

43. Ikiwa mtu anataka awe na imani yenye utendaji kweli kweli, yampasa afanye nini sasa?

43 Namna gani juu yako? Je! unayo imani hiyo, imani iliyo hai katika Mungu inayokuvuta uzungumze na wengine juu ya makusudi yake yenye upendo? Ikiwa hiyo ndiyo tamaa yako, huu ndio wakati wa kujitahidi mwenyewe katika funzo la Neno la Mungu, kushirikiana kwa kawaida na watu ambao matendo yao yanatoa ushuhuda wa kwamba imani yao i hai, na kusali kwa Yehova kwa bidii azibariki jitihada zako upatanishe maisha yako na mapenzi yake.​—1 Yohana 5:14; Luka 13:23, 24.​—⁠Kutoka The Watchtower, Jan. 1, 1974.

[Picha katika ukurasa wa 302]

Je! imani yako i hai?

Je! inakuvuta uwahubiri wengine

[Picha katika ukurasa wa 303]

Rahabu aliwaagiza wapelelezi wawili wa Kiisraeli washuke chini kwa kutumia kamba nyekundu kupitia dirisha la nyumba yake, iliyokuwa juu ya ukuta wa Yeriko

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki