Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 11/1 kur. 489-494
  • Kuzuia Mtengano Kati Yako na Watoto Nyumbani Mwako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuzuia Mtengano Kati Yako na Watoto Nyumbani Mwako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IWEKE WAZI NJIA YA KUPASHANA HABARI
  • KULINGANISHA KUSIKOFAA KWAELEKEA KUTOKUFAA KITU
  • TUMIA WAKATI UKIWA PAMOJA NA WATOTO WAKO
  • KUANGALIA USHIRIKA WAO
  • BARAKA ZA MALEZI YAFAAYO
  • Wazazi Na Watoto—wasilianeni Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kuendelea Kupashana Habari
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Zoeza Mtoto Wako Tangu Utoto Mchanga Sana
    Siri ya Furaha ya Familia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 11/1 kur. 489-494

Kuzuia Mtengano Kati Yako na Watoto Nyumbani Mwako

“Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”​—Mit. 22:6.

1, 2. (a) Nani wasioweza kuepuka kushiriki lawama ya mtengano wa wazazi na watoto, na kwa sababu gani? (b) Ni maelezo gani yaliyotolewa juu ya vijana wengi wa leo?

WATU wazima leo hawawezi kuepuka kushiriki lawama kwa sababu ya mtengano kati ya wazazi na watoto uliopo ulimwenguni pote. Kwa mfano, wazazi wengi wamewaendekeza mno watoto wao, matokeo yakiwa mabaya. (Mit. 29:15) Si kwamba tu mtengano kati yao na watoto umetokea, bali pia vijana ambao “wamefuata njia yao wenyewe” mara nyingi wameharibu maisha zao. Kwa kweli, sasa twaishi katika ambacho kimeitwa “Kizazi cha Wazembe.” Majuzi, Theodore M. Black, mwanachama wa New York State Board of Regents, alisema wazo hili alipokuwa akizungumza juu ya mitihani ya Manaibu kama kanuni ya kuamulia yaliyotimizwa kwa njia ya elimu:

2 “Kwa kadiri fulani twajikuta tukiishi katika ambacho inanilazimu nikiite Kizazi cha Wazembe kwa sababu ya kutojali kwetu wenyewe​—wakati ambapo uzembe katika afya ya kipekee, sura, usemi na tabia, ufisadi na uchafu unaoonyeshwa waziwazi, kutopendezwa kwa uvivu na kufanya kazi za mtu na kujifikiria mwenyewe daima kunakojionyesha wazi si katika kukosa adabu tu bali pia katika kudharau haki za wengine na mambo ya uhusiano wa kibinadamu katika jamii iliyostaarabika kweli kweli​—yote yanaelekea kuwa ndiyo kawaida ya siku hizi.”​—New York Times, Juni 24, 1972.

3. Ikiwa mtoto atakua akiwa na sifa njema za Kikristo, lazima wazazi wafanye nini, na wakati gani?

3 Wazazi wanaopendezwa na watoto wao hawataki wakue namna hiyo. Lakini ikiwa mtoto atakua akiwa na kanuni bora za adili, akionyesha sifa za Kikristo, kutia na bidii, fadhili, wema na upendo, mzazi wa Kikristo hatangoja mpaka mtoto afikie umri wa kwenda shuleni ndipo amlee katika njia ifaayo​—njia ya Mungu. Sivyo, bali ni vema leo kufanya kama vile katika habari ya kijana wa Kikristo Timotheo. Mtume Paulo alisema hivi juu yake: “Tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.” (2 Tim. 3:15) Ni jambo la maana basi kuanza kuzoeza watoto wakiwa vitoto vichanga. Watoto hawazaliwi wakiwa na kanuni za kimungu. Bali, “ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.” (Mit. 22:15) Tangu wanapokuwa wenye umri mdogo wanahitaji malezi na kutiwa adabu ili kuzuia maelekeo mabaya.

4, 5. (a) Mithali 22:6 inatoa shauri gani jema? (b) Wakati yanapokuwapo matukio ya pekee yasiyolingana na yanayotajwa katika Neno la Mungu, kwa sababu gani hii hailibatilishi andiko hili?

4 Ndiyo sababu Biblia inashauri hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mit. 22:6) Au kama vile New English Bible inavyoutafsiri mstari huo: “Mshikishe mvulana njia ifaayo, na hata katika uzee hataiacha.” Tafsiri nyingine ya mstari huu inasema hivi: “Mwelimishe mtoto kulingana na matakwa yake ya maisha; hata azeekapo hatageuka kutoka kwayo.”​—The New Berkeley Version.

5 Walakini, huenda wazazi wengine wakasema: “Mimi nawajua watoto waliolelewa kulingana na njia za Biblia, lakini wakawa wabaya.” Je! kugeuka kwa vijana wengine kutoka kweli za Mungu kunalibatilisha andiko hili? Sivyo! Ile ambayo Biblia imesema katika Mithali 22:6 ni kanuni ya kawaida tu. Yako matukio ya pekee, kama vile kulivyo na matukio ya pekee yasiyolingana na yasemwayo katika Mithali 15:1: “Jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.” Hii sivyo ilivyo sikuzote; nyakati nyingine mtu ataendelea kukasirika hata jawabu letu liwe la upole namna gani. Lakini kanuni hii ni njema nayo yaleta matokeo mazuri sana mara nyingi.

6, 7. Kwa sababu gani malezi ya mapema ya watoto ni ya lazima, yakielekea kuwa na matokeo gani?

6 Kanuni ya kawaida yatumika: kuna faida kubwa katika kulea mvulana au msichana katika njia za Yehova tangu utoto mchanga. Malezi ya mapema ni ya lazima, kwa maana miaka minne au mitano ya kwanza ya maisha ya mtoto ni ya maana. Wakati huu njia zake za uwezo wa kufikiri zinaimarika. Dr. Joseph M. Hunt wa Chuo Kikuu cha Illinois asema hivi: “Ukuzi wa mtoto ni wa haraka zaidi na unaweza kurekebishwa zaidi wakati wa miaka minne au mitano ya kwanza ya maisha. Wakati huu mtoto anaupata uwezo utakaokuwa msingi wa uwezo wake wa baadaye. Pengine kiasi cha 20 kwa mia cha uwezo huo wa msingi kinakuzwa kabla ya mwaka wake wa kwanza tangu alipozaliwa, pengine nusu yake kabla hajafikia umri wa miaka minne.”

7 Basi, kutumia wakati kutia kanuni za kimungu katika watoto wachanga ni kwa lazima. Atafuata njia ifaayo atakapokuwa mkubwa zaidi, ikiwa mtoto mwenyewe ana moyo mwema. Anasaidiwa kutopatwa na matokeo ya mtengano wa wazazi na watoto ulioenea sana.​—Efe. 6:4; Kum. 6:6, 7.

IWEKE WAZI NJIA YA KUPASHANA HABARI

8. Wazazi wanaweza kufanya nini waimarishe na kuiendeleza njia ya kupashana habari na watoto wao?

8 Yako mambo mengi ambayo wazazi wanaweza kuyafanya kuimarisha na kuiendeleza njia ya kupashana habari na watoto wao. Kwa ujumla, vifungo vya jamaa ni vyenye nguvu zaidi wazazi wakitoa usimamizi mwingi wa kipekee, badala ya kutegemea sana malezi ya shule, watu wa ujamaa, mayaya, na kadhalika. Ni jambo la maana kuanza mapema iwezekanavyo kuzungumza na mtoto bila vizuizi. Vile vile ni jambo la maana kuyajibu maulizo ya mtoto, hasa kwa Biblia, iwezekanapo. (2 Tim. 3:16, 17) Hii yahitaji kusikiliza kwa kuyaheshimu anayoyasema mtoto. Kwa hiyo imewapasa ninyi wazazi mjifunze kusikiliza. Jaribu kuyajua matatizo ya mtoto wako. Usifikiri kwamba matatizo yake ni madogo mno hata usiweze kuyahangaikia.

9, 10. (a) Mtoto awezaje kutayarishwa ayakabili maisha kama yalivyo? (b) Wazazi wanawezaje kuwatia watoto wao moyo na kuendeleza kupashana habari kusiko na vizuizi?

9 Kupashana habari kunaendelezwa kwa njia bora wazazi wanapokumbuka kwamba watoto si wakamilifu, kama vile wao wenyewe wasivyo wakamilifu. Kwa kweli, mtoto anapaswa kutayarishwa kwa ajili ya makosa​—yake mwenyewe, ya jamaa yake, na ya wengine. Kwa hiyo inafaa kumlea mtoto ukijua kabisa kwamba atafanya makosa. Hii haiepukiki tukiwa katika kutokamilika na katika hii taratibu ya mambo. (Zab. 51:5; Rum. 3:23; Yak. 3:2) Lakini wazazi wanaweza kumtia mtoto wao moyo azidi kufanya maendeleo, na kuzidi kujitahidia kusitawisha sifa za Kikristo. (Kol. 3:12-15) Toa sifa wakati inapostahiliwa.

10 Ili kurahisisha kupashana kwa habari kusiko na vizuizi kati ya wazazi na watoto, inafaa jamaa ishiriki vyakula pamoja badala ya kukuza tabia ya kula mbali mbali. Mazungumzo ya kawaida nyakati za chakula yanaendeleza kupashana habari kwa jamaa.

11. Wazazi wanaweza kufanya nini waiweke wazi njia ya kupashana habari na kuzuia watoto wao wasijifikirie wenyewe tu?

11 Imewapasa wazazi waonyeshe na kutia moyo upendo uendelee kuwapo. Kifungo chenye nguvu cha upendo kitaunganisha jamaa za Kikristo. (Efe. 5:25; Tito 2:4) Upendo ukiwapo njia ya kupashana habari inazidi kuwa wazi. Nyakati nyingine watoto wanapata kuwa wenye kujifikiria wenyewe tu ikiwa wazazi wanazungumza kwa kulaumu wengine sikuzote, wakidharau wengine, au kutafuta makosa. (Mit. 12:18; 16:27) Lakini wazazi wanaorahisisha makosa ya wengine, na wanaokuwa na nia ya fadhili na ya upendo, wanasaidia watoto wao kuwa wenye upendo na wenye kusamehe, na kupendezwa na watu wengine. (Efe. 4:32) Wakati wazazi wanapoonyesha ukarimu, hata wakiwauliza watoto wao, “Twaweza kumfanyia Fulani nini?” si kwamba tu wanasitawisha furaha ya kutoa bali pia wanaiweka wazi njia ya kupashana habari, iliyo ya lazima sana katika kuzuia mtengano wa wazazi na watoto. Wazazi wakijifunza kweli ya Mungu wakati watoto wanapokuwa wamepita umri wa miaka kumi na mitatu, jitihada ya kawaida itasaidia kuziweka wazi tena njia za kupashana habari.

KULINGANISHA KUSIKOFAA KWAELEKEA KUTOKUFAA KITU

12, 13. Vijana wengine wametoa maelezo gani wakizungumza matatizo yao katika kupashana habari na wazazi wao?

12 Inapendeza kusikia wanavyosema vijana kunapokuwa na mazungumzo ya kikundi juu ya matatizo yao katika kupashana habari na wazazi wao. Msichana mmoja alieleza wazi: “Dada yangu hujitolea sikuzote asaidie. Kwa kweli​—anapenda kazi ya nyumbani. Halafu mama’angu huniambia, ‘Tazama kazi anayoifanya dada yako. Sababu gani usiwe kama yeye?’ “Msichana huyu aliona kulinganisha huko kuwa kwenye kuvunja moyo na kwenye kuzuia kupashana habari na wazazi wake.

13 Msichana mwingine alieleza: “Haifai. Mimi nakwenda kutupa takataka na kuosha vyombo na kutengeneza chumba changu, na kesho yake mama anasema, ‘Maskini, hata mbwa anafanya kazi hapa zaidi yako.’ Watoto wengine wanalinganishwa na ndugu na dada zao, lakini miye hata nalinganishwa na mbwa.”

14. (a) Wanapojaribu kuwatia watoto wao moyo, huenda wazazi wakasahau nini nyakati fulani? (b) Vijana wanaonaje shuleni wanapolinganishwa na wengine isivyofaa?

14 Kwa kweli, wazazi wengi wanajua kwamba watoto wa jamaa moja wanatofautiana katika wayapendayo na wasiyoyapenda na katika utu na sifa. Lakini nyakati fulani, hasa wanapokuwa chini ya mkazo, huenda wazazi wakasahau hivyo, wakijaribu kumvuta mtoto mmoja aige wengine ambao tabia yao yapendeza zaidi katika jambo fulani. Lakini inaelekea jitihada hizo hazitafaa kitu. Kitabu Today’s Teen-Agers chasema: “Waalimu wameona kwamba kulinganisha kusikofaa kwaelekea kuvunja moyo badala ya kuwatia wanafunzi moyo darasani.”

15-18. (a) Huenda wazazi wakafaidikaje kutokana na mfano wa wazee katika kundi la Kikristo na maoni yaliyotajwa na Yesu yaliyoandikwa katika Mathayo 13:23? (b) Wote waliomo katika kundi la Kikristo wanatiwa moyo watumainie nani kama mfano? (c) Kwa hiyo, imewapasa wazazi wa Kikristo watake kuwatendeaje watoto wao?

15 Inafaa wazazi wawaige wazee katika kundi la Kikristo wanaojaribu sikuzote kutumia kanuni za Biblia. Wazee hawa wanajua namna ambavyo lingekuwa jambo lisilo la hekima kulinganisha Mkristo mmoja na mwingine, au kuuliza ulizo: “Sababu gani usifanye mengi zaidi? Ndugu Fulani, aliye na madaraka zaidi kuliko wewe, anafanya hivi na hivi.” Je! kulinganisha huko kungemtia moyo Mkristo ye yote? Au kungemvunja moyo?

16 Na namna gani kulinganisha huko kusikofaa kukifanywa mbele ya watu wengi, wengine wakisikia? Je! hii isingekuwa na matokeo yenye kuvunja moyo hata zaidi, isifae kitu kama njia ya kumtia mtu moyo?

17 Wazee katika kundi la Kikristo hawalinganishi hivyo. Wao wanajua kwamba Bwana Yesu Kristo alizungumza juu ya wale Wakristo wanaoshiriki habari njema za Neno la Mungu kwa njia inayofaa, wawe wanashiriki mara 30, 60 au 100. (Mt. 13:23) Zaidi ya hayo, katika kundi la Kikristo, wazee wanalitia kundi moyo ‘wawe waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa,’ pia wawe waigaji wa Kristo na kuwaiga Wakristo wenzao namna tu wanavyomwiga Kristo. (Efe. 5:1, NW; 1 Kor. 11:1) Kutokana na haya twaona kwamba wale tupaswao kuwatumainia na kujilinganisha nao wamepaswa wawe Yehova Mungu na Bwana Yesu Kristo. Mfano wa uaminifu wa Wakristo wenzetu waweza kututia moyo, lakini tusilinganishwe na Wakristo wengine kutufanya tufikiri tu hafifu au bora kuliko wengine. (2 Kor. 10:12; Gal. 6:4) Tunawaiga walio mifano bora.

18 Kwa hiyo, kwa kuwa kulinganisha kusikofaa badala ya kutendea wote kama watu kumeonekana kuwa jambo lisilo la hekima katika kundi la Kikristo, na pia katika madarasa ya kilimwengu, inafaa wazazi wa Kikristo wanaotaka kuepuka kutengana na watoto wao wafikiri sana kabla ya kulinganisha hivyo.

TUMIA WAKATI UKIWA PAMOJA NA WATOTO WAKO

19-21. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana wazazi waonyeshe kupendezwa na watoto wao kwa kutumia wakati wakiwa pamoja nao, na mashahidi fulani wamesema nini juu ya matokeo ya kutojali kwa wazazi?

19 Imewapasa wazazi waonyeshe kupendezwa na watoto wao. Hawawezi kutazamia watoto wao wawe wema ikiwa wao wenyewe ni wapenda anasa au utajiri kuliko kuwa wapenda watoto wao wenyewe. (1 Tim. 6:9, 10) Hivyo, kwa habari ya kijana aliyepata kutengana na wazazi wake akaharibika, twaambiwa hivi: “Leon alitengwa mbali na wazazi wake, ambao walifanya kazi wote wawili na waliokuwa na shughuli nyingi mno wasiweze kumwangalia alivyotaka.”

20 Njia ya leo ya maisha pamoja na mikazo yake mingi na mashaka inafanya iwe vigumu kwa wazazi kutumia wakati wakiwa pamoja na watoto wao. Lakini unapaswa wakati utumiwe. Mtaalamu Urie Bronfenbrenner anashikilia kauli ya kwamba wazazi wengi mno wamejitenga na maisha za watoto wao wakiacha wazi nafasi inayojazwa na wenzi wao na televisheni katika kitabu Two Worlds of Childhood: U.S. and U.S.S.R. Daktari huyu Bronfenbrenner anaandika hivi:

“Hatufaulu katika tendo la kuwafanya wanadamu wawe wanadamu bora. Linalohitajiwa ni badiliko katika njia zetu za maisha zitakazowarudisha watu wazima tena kwenye maisha za watoto na watoto kwenye maisha za watu wazima. . . . Watu wazima wasiporudia kujitia katika maisha za watoto wetu, mashaka yatafuata.”

21 Naye McCann aliandika hivi katika Delinquency​—Sickness or Sin?: “Orodha za mahakma zetu za vijana . . . zaonyesha wazi jambo la kawaida katika mtoto mmoja baada ya mwingine: ubaridi wa wazazi, kutojali, kutupiliwa mbali.”

22. Wana wa mkaribishaji wa televisheni walipatwa na nini aliposhindwa kutumia wakati wa kutosha akiwa pamoja nao, naye aliisimuliaje hali hii kwa habari yake na mababa wengi?

22 Mashaka yalimpata mkaribishaji mmoja maarufu wa televisheni mwenye umri wa miaka 44 ambaye wana wake walianza kutumia dawa za kulevya. Baadaye aliieleza idara ya uchapaji hivi: “Baba wa kawaida haishi kama mimi niishivyo, lakini hakuna tofauti. Anakwenda kazini, anarudi nyumbani, anasema hataki kuyasikia matatizo madogo madogo kwa maana amekuwa na matatizo afisini, kufungua televisheni kisha anakwenda kulala. . . . Naona watu waliofanikiwa wakisimamia kampuni zenye mamia ya watu; wanajua namna ya kushughulika na kila hali, namna ya kutia adabu na kuthawabisha kazini. Lakini kazi kubwa wanayosimamia ni jamaa yao nao wanashindwa kuisimamia. . . . Nilidhani nilijua kila jambo kwa sababu nilifanikiwa nikiwa mwenye umri mdogo. Kumbe sikujua lo lote.”​—New York Times, Agosti 1, 1972, uk. 26.

23. Mpelelezi mmoja aligundua nini juu ya matokeo ya ubaridi wa wazazi?

23 Hivyo, watoto waachwapo peke yao na kupendezwa nao na mambo wanayoyafanya kusionyeshwe, wanatengana na wazazi, matokeo yakiwa mabaya sana. Majuzi uchunguzi wa mpelelezi mwenye maarifa wa dawa za kutia usingizi wa San Antonio, Texas, ulitangazwa wazi. Baada ya miezi tisa akiwa kama mpelelezi, aligundua kwamba vijana wengi wanaotumia dawa za kulevya hawakuelekea kujaribu kuficha kwamba wao hawatumii dawa za kulevya. Mkataa uliofikiwa na mpelelezi huyu ni kwamba matumizi ya vijana ya dawa za kulevya yamesababishwa sana na ubaridi wa wazazi. Alisimulia juu ya vijana wanaosema wazazi wao wanawapa pesa na kuwaacha peke yao wafanye kama watakavyo mwishoni mwa juma. “Inaelekea kuwa watoto hawakuweza kuelewa sababu ya wazazi wao kutotaka kutumia wakati wakiwa pamoja nao,” alisema mpelelezi huyo.​—San Antonio News, Januari 28, 1972.

24-26. (a) Wazazi wanaweza kutumia wakati kwa njia yenye kufaidi wakiwa pamoja na watoto wao lini? (b) Ni kanuni gani aliyoiweka Mungu katika Israeli wa kale inayohusiana na “watoto” katika jamaa za Kikristo leo?

24 Kwa hiyo, ni jambo la maana namna gani wazazi watumie wakati wakiwa pamoja na watoto wao! Kutumia wakati pamoja kunafanya kupashana habari kuwe jambo la kawaida, nako kunasaidia wazazi wapate maoni ya vijana. Matokeo yanakuwa mema sana wakati baba anapotumia wakati akiwa pamoja na wana na binti pia wakifanya kazi nyumbani. Kushiriki katika kazi, na katika tafrija pia, kunaizoeza jamaa kufurahia mambo pamoja na wengine, si kufuata mapendezi ya kipekee tu.

25 Na, bila shaka, kutumia wakati pamoja faraghani na katika mafunzo ya Biblia ya kundi ni kwa lazima. Mungu aliiweka kanuni hiyo katika Israeli wa kale. Aliwaamuru wazazi kwenda pamoja na watoto wao makusanyikoni yaliyofanywa kwa kusudi la kumwabudu na kumsifu Yehova, si kuwafundisha njia za Mungu nyumbani tu. Amri ya kimungu iliyopewa kupitia kwa Musa ilikuwa: “Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto . . . wapate kusikia na kujifunza, na kumcha [ Yehova], Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii.” “Watoto” hawakuachwa nyumbani. Vivyo hivyo na leo imewapasa watoto wahudhurie mikutano ya kundi la Kikristo pamoja na wazazi wao.​—Kum. 31:12, 13; Neh. 12:43; Luka 2:41-50; Mt. 19:13, 14.

26 Wazazi wanaofuata Neno la Mungu wana hekima ya kimungu kuwasaidia walee watoto wao, nao wakiwalea watoto wao katika njia iwapasayo kufuata, wakitumia wakati wakiwa pamoja nao, wakiwafundisha wawe waigaji wa Mungu na wa Mwanawe mpendwa, inaelekea watafaulu.

KUANGALIA USHIRIKA WAO

27-29. (a) Ni kanuni gani ya Maandiko aliyoitaja mtume Paulo juu ya ushirika? (b) Ushirika ni nini, nao ni mbaya wakati gani?

27 Wazazi wanaotaka watoto wao wasipate kujitenga nao, na kuingia katika mazoea ya kutumia dawa za kulevya au ufisadi, imewapasa wauthamini ubora wa kuyaangalia mashirika ya watoto. Biblia inaitaja waziwazi kanuni ya kufaulu: “Msipotezwe. Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.”​—1 Kor. 15:33, NW.

28 Hapa mtume Paulo haonyi juu ya kuonana tu na walimwengu. Namna gani hivyo? Basi, ushirika ni nini? Neno la Kigiriki lina maana ya “kuhusiana na” au “kuwa na urafiki na.” Neno la Kiingereza limetolewa kutoka neno la Kirumi lenye maana ya “-liounganishwa na,” “-liopatana na.” Yaani, unakuwa mwenzi au rafiki ya mtu fulani ambaye urafiki wake unautafuta. Ni kuandamana, kuingia katika shughuli na anasa za wale unaoshirikiana nao. Hili ni jambo baya ikiwa ushirika ni pamoja na walimwengu, kwa maana adili na mazoea mema yataharibika.

29 Nyakati nyingine wazazi wanapata kujua kwamba kuangalia ushirika wa watoto wao ndilo jawabu la kuepukia maumivu ya moyoni baada ya kupatwa nayo. Lakini sababu gani ujifunze mambo ukiisha kuumia? Neno la Yehova lina uongozi wanaouhitaji wazazi ili kulea watoto kwa kufaulu.

BARAKA ZA MALEZI YAFAAYO

30. (a) Ni thawabu gani wanazozipata wazazi wanaowapa watoto wao malezi yafaayo tangu utoto mchanga? (b) Hii yaonyeshwaje na lililotukia katika shule ya masomo ya juu?

30 Lo! ni thawabu kama nini zilizopo kwa wazazi wanaolea watoto wao katika njia iwapasayo kufuata! Wanapata furaha nyingi na kuiepuka huzuni na maumivu ya moyoni na aibu ambavyo bila shaka vitatokea mtoto akijitenga na wazazi na kufuata njia yake mwenyewe. (Mit. 17:21; 29:15) Wakati wa mazungumzo ya wasichana ya darasani katika shule ya masomo ya juu shauri la mtengano wa wazazi na watoto liliingizwa katika habari juu ya matatizo ya kijamii. Mazungumzo yalikuwa ya kupendelea, kwa hiyo wasichana hao wakaombwa waje na wazazi wao kipindi kitakachofuata. Wazazi wa mwanafunzi Shahidi walipanga wawepo. Baba alisema hivi:

“Sisi tu ndio tuliokuwa wazazi wa pekee kufika. Waalimu wawili walikuwapo pia. Mazungumzo yalianza wasichana wakiinua mikono yao na kuuliza maulizo tulipowaomba wafanye hivyo. Wasichana hao walipendezwa na maoni yetu juu ya kutia adabu, kuadhibu, kuruhusu uhuru, tafrija, sababu za mtengano wa wazazi na watoto, na kadhalika. Msingi wa majibu yetu ulikuwa Biblia, ambayo tulitaja ndicho kitu kinachohitajiwa.

“Tulionyesha kwamba wakati jamaa inapoishi kulingana na kanuni za Biblia mtengano wa wazazi na watoto haupo. Wasichana walielekea kupendezwa sana, na mwishoni mwa kipindi cha dakika 40 wakauliza kama tungeweza kukaa wakati wa kile kipindi cha pili, nasi tukafanya hivyo.

“Ilikuwa wazi kwa wasichana hao kwamba nyumbani kwetu hatukuwa na kizuizi cha kupashana habari. Baada ya kuondoka kwetu, wasichana wengine walimwambia binti yetu kwamba ingaliwezekana wangebadilishana wazazi naye. Wengi walikubali kwamba waliona ni afadhali kuishi katika nyumba ambamo mna adhabu pamoja na upendo kuliko katika nyumba ambamo wazazi na watoto hawawezi kupashana habari.”

31. Zitaje tena kanuni njema zitakazowasaidia wazazi wazuie mtengano kati yao na watoto wao nyumbani mwao?

31 Ndiyo, kanuni bora za Biblia zinatoa njia ya ambavyo wazazi na watoto wanaweza kupashana habari, wakijua kwamba watu wazima na vijana pia ni watoto wa Baba Mkuu ajuaye kuadhibu kwa upendo. Kwa hiyo waleeni watoto tangu utoto mchanga, mjitahidi sana kuiweka wazi njia ya kupashana habari, mkiwatia moyo, si kwa kulinganisha kusikofaa kitu, bali kwa Mifano Bora Zaidi itupasayo kuiiga. Mtumie wakati mkiwa na watoto wenu, na mwuangalie ushirika wao. Hivyo mtapata baraka za malezi hayo, kwa maana “baba yake mwenye haki atashangilia; naye amzaaye mtoto mwenye hekima atamfurahia.”​—Mit. 23:24, 25.

​—Kutoka The Watchtower, May 1, 1974.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki