Hakuna “Upungufu wa Nguvu” wa Kiroho kwa Wenye Busara
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Pana tofauti gani wakati huu wa “upungufu wa nguvu”?
LEO kuna “upungufu wa nguvu” katika nchi nyingi. Kwa watu wengine hii yamaanisha kutosafiri sana kwa magari, kwa maana petroli si nyingi. Mafuta yahitajiwa pia kuendesha mashine kubwa zinazofanyiza umeme. Kwa hiyo, watu wengi wanajaribu kuhifadhi nguvu kwa kuzima taa zisizohitajiwa.
2 Hata hivyo, kuna nuru isiyotegemea vyanzo vinavyotumiwa na watu wengi. Wenye shukrani waliyo nayo wanakataa kuizima nuru yao hata kuipunguza. Kwa njia ya kiroho, ‘wanaacha nuru yao iangaze.’—Mt. 5:14-16.
3. Mfano wa Yesu wa wanawali kumi ulikuwa sehemu ya jibu la nini?
3 Yesu alikuwa akiwafikiria wao alipoufananisha ufalme wa Mungu na wanawali kumi walioalikwa kwenye karamu ya arusi. Mfano wake ulikuwa sehemu ya jibu kwa ulizo hili: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW) Ushuhuda wahakikisha kwamba sasa twaishi katika “siku za mwisho,” kwa hiyo utimizo wa “ishara” iliyotabiriwa wapaswa utufanye tupendezwe.
4. Vikundi viwili vya wanawali vilitofautianaje?
4 Wanawali wote kumi walikuwa na taa, pengine vyombo vyenye mdomo na utambi upande mmoja na mkono upande mwingine. Pengine hivi vilijazwa mafuta ya mizeituni, yaliyotumiwa sana siku hizo kwa kuwasha taa. Kwa sababu bwana-arusi alikawia, wanawali walilala, wakaamshwa usiku wa manane na tangazo la kwamba alikuwa anakuja. Wanawali “wenye busara” watano walikuwa na mafuta ya ziada katika vyombo walivyovichukua, lakini wale “wapumbavu” hawakuleta mafuta ya ziada na iliwapasa waende zao wakayanunue. Wakati huo, wanawali “wenye busara” walimlaki bwana-arusi wakaingia naye kwenye karamu ya arusi. Wanawali “wapumbavu” walijaribu kuingia baadaye, lakini wasiweze.—Mt. 25:1-12.
5. (a) Ni akina nani waliofananishwa na “bwana arusi” na ‘wanawali wenye busara’? (b) Ni katika maana gani wanawali hawa wamekuwa na “mafuta” ya kutosha?
5 Yesu Kristo aliyetukuzwa ndiye “bwana arusi,” nao wanawali “wenye busara” wanakuwa “Bibi-arusi” wake wa kimbinguni, mwishowe hesabu yao ikiwa 144,000. (Ufu. 14:1-4; 19:7, 8; 20:6; 21:9) Wanapokuwa duniani, wana “mafuta” tele, Neno la Mungu na roho takatifu yake. Kwa hiyo wao hawapatwi na “upungufu wa nguvu” wa kiroho ambao ungeweza kuipata taa. Hata hivyo, wanawali “wapumbavu” wamekosa “mafuta” ya kutosha kuendeleza taa zao zenye kuwaka tangu “warithio pamoja na Kristo” wa kwanza walipozaliwa kwa roho siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E. mpaka Bwana-arusi alipotokea akawa akiingia katika karamu ya arusi.—Rum. 8:17.
KUMNGOJEA BWANA-ARUSI
6, 7. Kulikuwako vichocheo gani vya mapema kwa habari ya kurudi kwa Kristo? Kwa matokeo gani?
6 Wanawali kumi wote wa mfano walilala kwa kitambo. (Mt. 25:5) Lakini wakati wa karne hizo lazima kuwe kulikuwako vichocheo fulani, hasa vya wanawali “wenye busara.” Hasa ndivyo ilivyokuwa baada ya kuamka kwa kidini kwa mapema karne ya kumi na sita C.E., wakati jitihada kubwa ilipofanywa Ulaya kuyarudisha Maandiko Matakatifu kama kitabu cha pekee cha kweli ya kimungu. Ahadi ya kurudi ya Kristo Bwana-arusi iliwavuta wanafunzi wa Biblia wenye mioyo minyofu, waliojua kwamba huku kungeutangulia utawala wa miaka elfu ambao ungeonyeshwa na kufungwa kwa Shetani katika “shimo kubwa.”—Ufu. 20:1-6, NW.
7 Wakati wa miaka 50 ya kwanza ya karne ya kumi na nane, mwanadini wa Kilutheri Johann Albrecht Bengel wa Ujeremani alitabiri kwamba utawala wa miaka elfu ungeanza mwaka wa 1836. Baadaye, katika United States, William Miller aliwafundisha wafuasi wake kwamba Kristo angetokea katika mwili na kuwapeleka kwenye makao yao ya kimbinguni mwaka wa 1843. Lakini, tarehe hizo zilipita kusitokee lo lote, nayo maandishi wala misemo ya Bengel wala Miller haikuwa kweli kulingana na kelele ya usiku wa manane iliyotabiriwa: “Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki.”
8. Ni mambo gani mengine yaliyotukia kati ya wanafunzi wa Biblia kwa habari ya kuwapo kwa Kristo?
8 Walakini, miaka iliyoanza na wa 1870 kikundi kidogo cha watu wasioshiriki na madhehebu za Kristendomu kilianza kujifunza Biblia katika Pittsburgh (Allegheny), Pennsylvania. Kati yao alikuwako Charles Taze Russell. Walijifunza kwamba Kristo angerudi kama roho na kwamba hii ingeanzisha kuwapo kusikoonekana ambako kungedhihirishwa na mashuhuda yenye kuonekana.
9. C. T. Russell na washirika wake walitambua nini juu ya mwaka wa 1914 C.E.?
9 Hao wanafunzi wa Biblia walizishirikisha “nyakati za Mataifa” zilizotajwa na Yesu na “nyakati saba” zilizotajwa katika Danieli. (Luka 21:24, King James Version; Dan. 4:16, 23, 25, 32) Walifahamu kwamba hizo “nyakati saba” za kutawaliwa kwa dunia na Mataifa zilianza mwishoni mwa karne ya saba B.C.E. na zingeendelea kwa miaka 2,520. Kwa hiyo, C. T. Russell mwenye umri wa miaka 24 alitoa makala akapelekea Bible Examiner la Oktoba 1876, ambamo aliandika hivi: “Nyakati saba zitakoma A.D. 1914.”
10. (a) Ni kwa njia gani mwanzo wa miaka ya kuanzia wa 1870 ulivyodhaniwa ulilingana na orodha ya tarehe na historia ya kibinadamu? (b) Hii ilisahihishwaje baadaye?
10 Mwaka wa 1877, Russell alijiunga na Nelson H. Barbour kuchapa kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World. Kilionyesha kwamba mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914 ungetanguliwa na kipindi cha miaka 40 ambacho kingeanza na mavuno ya miaka mitatu u nusu mwaka wa 1874 C.E. Kulingana na orodha ya tarehe za Biblia iliyofuatwa baada ya hapo, ilifahamiwa kwamba hiyo miaka 6,000 ya kuwapo kwa mwanadamu duniani ilikwisha mwaka wa 1872, na kwa hiyo miaka 6,000 ya dhambi ya mwanadamu ilikwisha na mwaka wa 7,000 ukaanza 1874. Kuwapo kwa Kristo kulidhaniwa kulikuwa kumeanza Oktoba wa mwaka wa 1874, mwanzoni mwa Yubile kuu iliyofananishwa.—Law. sura 25; Ufu. 20:4.a
11. Iliaminiwaje kwa habari ya kuwapo kwa Kristo?
11 Kulingana na ufahamu huo, ilidhaniwa kwamba jamii ya “bikira safi” ilianza kwenda kumlaki Bwana-arusi mwaka wa 1874. (2 Kor. 11:2) Kwa hiyo, wakati C. T. Russell alipoanza kuchapa gazeti jipya la kidini Julai wa mwaka wa 1879, liliitwa “Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence.” Lilikuwa likikutangaza kuwapo kwa Kristo kwamba kulianza mwaka wa 1874. Kuwapo huku kusikoonekana kulitazamiwa kuendelee mpaka Majira ya Mataifa yamalizike mwaka wa 1914, wakati ambapo mataifa yasiyo ya Kiyahudi yangeharibiwa na mabaki ya jamii ya “bikira safi” watukuzwe pamoja na Bwana-arusi wao mbinguni kwa kufa na kufufuliwa wakaishi wakiwa wa kiroho. (1 Kor. 15:42-44) Kwa njia hiyo jamii ya ‘wanawali wenye busara’ ingeingia mlangoni kwenye arusi.
12. Majira ya Mataifa yalipokwisha, jamii ya “bikira safi” ilitazamia nini, lakini walipatwa na nini?
12 Jamii ya “bikira safi” ilijaribu kuacha nuru yao iangaze walipoukaribia wakati ambao walitazamia kumlaki Bwana-arusi wao mbinguni. Mwishowe, siku hiyo ilifika—Oktoba 1, 1914. Majira ya Mataifa yalikwisha, lakini kutukuzwa kwa kimbinguni kwa kanisa kulikotazamiwa hakukutokea. Kwa kweli, hakukuwa kumetokea wakati Russell mwenyewe alipokufa Oktoba 31, 1916. Bali, taabu kuu na mateso yaliwapata wale waliotamani kumlaki Bwana-arusi. Upeo ulifikiwa wakati wa hari ya mwaka wa 1918, wakati ambapo msimamizi mpya wa Watch Tower Society, J. F. Rutherford, na wanaume wengine saba wa Kikristo walioshirikiana na makao makuu waliposhtakiwa isivyo haki na kutiwa gerezani.
13. Mwaka wa 1919 kulitokea mambo gani ya maana?
13 J. F. Rutherford alikaa miezi tisa tu gerezani, si miaka ishirini, kama alivyohukumiwa. Yeye na wenzi wake saba waliachiliwa Machi 25, 1919, na mwishowe wakatolewa hatiani kabisa. Lakini mwaka wa 1919 ulikuwa wenye maana kwa sababu nyingine. Kama vile wanawali wenye kusinzia walivyoamshwa na kelele ya usiku wa manane kwamba bwana-arusi alikuwa anakuja, ndivyo na mwaka wa 1919 C.E. kuwapo kwa kimbinguni kwa Bwana-arusi katika Ufalme kulivyoonyeshwa kwa wote waliojidai kuwa wanawali wenye kumngojea.
KUZITENGENEZA “TAA” ZAO
14, 15. Kuna ushuhuda gani kwamba jamii ya “bikira safi” ilitengeneza “taa” zao? Kwa matokeo gani?
14 Mara hiyo jitihada zilifanywa kuutia nguvu ujasiri wa Wakristo wa kweli waliokuwa wamekuwa wakimtazamia Bwana-arusi. Kusanyiko kuu lilifanyiwa Cedar Point, Ohio, Septemba 1-8, 1919. Shauku nyingi sana iliamshwa Septemba 5, wakati Msimamizi J. F. Rutherford alipotangaza kuchapwa kwa gazeti jipya, The Golden Age, tangu Oktoba 1, 1919, na kuendelea. Watu wa Mungu ‘waliowekwa wakf’ walitiwa moyo washiriki kupata maandikisho yake, wakitazamia wakati ambapo nakala 4,000,000 za toleo moja zingeenezwa. Leo, gazeti hili linaloitwa “Awake!,” linachapwa nakala 8,000,000 kila toleo kwa wastani.
15 Bila shaka, mwaka wa 1919 haukuwa usio na maana sana katika historia ya jamii ya Mungu ya “bikira safi.” Ndipo kazi ya kuuhubiri Ufalme ya ulimwenguni pote ilipoanza. Jamii ya ‘wanawali wenye busara’ iliamshwa wakati huo nayo haijapata kusinzia tangu wakati huo!
16. Kwa sababu gani wanawali “wenye busara” wasingeweza kugawana “mafuta” yao na wanawali “wapumbavu”?
16 Huo ndio wakati hasa ‘waliondoka wanawali hao wote, wakazitengeneza taa zao.’ (Mt. 25:7) Taa zilikuwa karibu kuzimika. Lakini wanawali “wenye busara” walikuwa na vyombo vilivyojazwa mafuta, wanawali “wapumbavu” hawakuwa na mafuta ya ziada. Hata hivyo, “wenye busara” wasingeweza kuwagawia mafuta yao, kwa maana kama wangaliigawanya akiba iliyobaki ya wote kumi ingalikwisha. Kwa hiyo ilikuwa lazima wanawali “wapumbavu” waondoke wakajaribu kujinunulia mafuta saa hiyo ya usiku.
17. (a) Ni nini kinachofananishwa na “mafuta”? (b) Ni kwa njia gani jamii ya wanawali “wapumbavu” haina “mafuta” ya kutosha?
17 “Mafuta” ya mfano yanafananisha Neno la Mungu na roho takatifu yake, inayolimulika Neno hilo na kutokeza katika wenye “mafuta” ‘tunda la roho’ la kimungu. Kukataa kugawana “mafuta” yao na wanawali “wapumbavu” kwamaanisha kwamba wanawali “wenye busara” hawataridhiana na jamii hiyo. Wanawali “wapumbavu” wanajidai kufuata Ukristo, na hali hawatimizi matakwa yake. Huenda wakaongozwa kidogo na maarifa yao ya Biblia, lakini si kwa kiasi cha kuwa na roho yenye nguvu ya Mungu ndani yao na kutokeza tunda lake. Ijapokuwa wanatazamia kwenda mbinguni, maendeleo yao ya kidini hayawawezeshi kuutimiza mwito wa kelele ya usiku wa manane: “Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki.” Wao wana upungufu wa mafuta ya taa. Yao ni nuru inayoshindwa.
18. Jamii ya wanawali “wenye busara” ilichukua hatua gani zaidi kutogawa “mafuta” yao?
18 Mwaka wa 1919 jamii ya ‘wanawali wenye busara’ ilichukua hatua ya kutoka katika Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Wasingeweza kuridhiana na jamii ya ‘wanawali wapumbavu,’ kama vile kwa kujiunga na Babeli Mkuu kuiabudu ‘sanamu ya mnyama,’ Ushirika wa Mataifa, ambaye Babeli Mkuu alimpanda mwaka wa 1919. (Ufu. 13:14, 15; 14:11, 12; 17:1-18; 18:4) Hali yao ya unyofu ilionyeshwa wazi penye kusanyiko la Cedar Point Septemba 7, 1919, wakati J. F. Rutherford alipoitoa hotuba ya watu wote “Tumaini la Wanadamu Wanaotaabika.” Kwa ujasiri alionyesha kuchukizwa kwa Mungu na Ushirika wa Mataifa, ambao viongozi wa kidini waliukubali kama wonyesho wa kisiasa wa ufalme wa Mungu duniani. Jamii ya ‘wanawali wenye busara’ iliamini kwamba ufalme wa Mwana wa Mungu ulikuwa umekwisha simamishwa mbinguni mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914, nao wakakataa kutambua na kuabudu kitu cho chote kama kilicho badala yake. Wasingeweza kutoa kiasi cho chote cha “mafuta” yao ya kiroho wala kuupunguza uaminifu wao kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi.
19. Hivyo jamii hii imeshiriki sehemu gani kwa habari ya Bwana-arusi?
19 Jamii ya ‘wanawali wenye busara’ ilimlaki Bwana-arusi kwa njia hiyo mwaka wa 1919 nao wameendelea kuwa sehemu ya maandamano yanayomheshimu yeye hata mwisho. Wanapoufikia “mlango,” wanaonekana kustahili kuruhusiwa waingie. Bwana-arusi anawakuta waking’aa kwa utu wa Kikristo na kwa hiyo anawakubali hawa wanawali “wenye busara” wa leo kama sehemu ya kundi la Kikristo.—2 Kor. 11:2, 3; Efe. 5:27.
WAKUTA MLANGO UMEFUNGWA
20, 21. Jamii ya wanawali “wapumbavu” itakutaje mlango umefungwa?
20 Waliporudi, wanawali “wapumbavu” walikuta mlango umefungwa. (Mt. 25:10) Lakini, katika utimizo, ni wakati gani unapofungwa rasmi? Ni wakati “dhiki kubwa” ianzapo na uharibifu kuanza juu ya Kristendomu na sehemu nyingine yote ya Babeli Mkuu. Wakati huo itakuwa kuchelewa mno kwa Wakristo wa kujidai kutoka kwake. Wakati huo, pia, hesabu kamili ya “wateule” 144,000 wanaofanyiza “Bibi-arusi” wa Kristo itakuwa imekwisha kamilishwa.—Mt. 24:21, 22.
21 Mfano unamalizia kwa maneno haya: “Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie. Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi.” (Mt. 25:11, 12) Kwa sababu ya upumbavu wao ulioleta “upungufu wa mafuta” wa kiroho, wanawali “wapumbavu” hawakuwa wamemlaki bwana-arusi wala kuongezea uangavu wo wote kwa maandamano yake ya arusi. Kwa hiyo, bila shaka alikuwa na haki ya kuwafungia mlango.
22. “Dhiki kubwa” itakapotokea, hali ya jamii ya wanawali “wapumbavu” itakuwa nini?
22 Vivyo hivyo, wakati “dhiki kubwa” itakapoanza juu ya Kristendomu, jamii ya ‘wanawali wapumbavu’ itajua kwamba hawakuwa wakishirikiana na tengenezo la kidini linalomfanyiza “bikira safi,” “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo.” (Ufu. 21:9) Ndiyo, watamwita Bwana-arusi, lakini mlango hautafunguliwa, kwa maana wakati mwingine Yesu alisema hivi: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.” (Mt. 7:21-23) Katika “dhiki kubwa” Bwana-arusi ataiacha jamii ya ‘wanawali wapumbavu’ nje katika usiku wenye giza sana sana la ulimwengu, wakatoweke pamoja na ‘watendao maasi’ wengine wote. Watakapoharibiwa hawatapata ufufuo wo wote kwenye uzima wa kimbinguni.
“KESHENI”
23, 24. Yesu alikuwa akitilia jambo gani mkazo ambalo lazima sote tulitii?
23 Yesu aliikazia maana ya mfano wake kwa maneno ya wakati ufaao kwa Wakristo waliotiwa mafuta wanaoishi wakati wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” Alisema hivi: “Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa.” (Mt. 25:13) Wale wanaotaka kuwa kama wale wanawali “wenye busara” watano lazima waendelee kung’aa kwa utu wenye juhudi wa Kikristo. Hawatathubutu kuridhiana na wale wanaotaka kuondoa kiasi fulani au “mafuta” yao mengi ya kiroho. Imani yao katika kufika kwa Bwana-arusi na kuwapo lazima iendelee kung’aa, na yawapasa waendelee kuwamo katika maandamano yenye kung’aa yanayozifuata hatua zake mpaka atakapokwisha kulileta kundi lake la kibibi-arusi nyumbani.
24 Kukawia kufika kwa muda mrefu kwa Bwana-arusi kumekwisha. Yeye yupo, katika kuwapo kwake kwenye utukufu. Wakati wa kusinzia na kulala umepita! Huu ndio wakati wa kumheshimu kwa kung’aa na kufurahi pamoja naye katika furaha ambayo Baba yake wa kimbinguni amemwekea, ile ya kujitwalia “Bibi-arusi” wake wa kiroho na kuadhimisha hili kwa karamu ya arusi. Kwa hiyo, lazima Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho wakeshe, kwa maana hawajui siku wala saa ambayo “mlango” wa nafasi utafungwa, usifunguliwe kamwe. Lakini hao wenye kukesha na wenye busara hawatafungiwa nje kwa sababu ya upungufu wo wote ulio hatari wa mafuta ya taa ya kiroho.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.
[Maelezo ya Chini]
a Ilionyeshwa kwamba mwanadamu aliumbwa mwaka wa 4128 na dhambi ikaingia mwaka wa 4126 B.C.E. Orodha hiyo ya tarehe ilifuata tafsiri ya hati yenye makosa ya Matendo 13:20 katika The Emphatic Diaglott, iliyosema kwamba Mungu aliwapa Israeli waamuzi “karibu miaka mia nne na hamsini, mpaka Samweli nabii.” Maelezo ya chini yalisema kwamba hii haikupatana na 1 Wafalme 6:1, ambapo herufi ya Kiebrania daleth (inayodhaniwa kuisimamia namba 4) ilidhaniwa kuwa hivyo badala ya herufi he (5). Kwa hiyo, ilishauriwa kwamba miaka 580 (si 480) ilikwisha kati ya kutoka kwa Israeli Misri na wakati ambao Sulemani alianza kulijenga hekalu la Yehova. Lakini hati za zamani kupita zote zinaonyesha namba zote. Kwa hiyo isingaliwezekana kuwe na kosa la mnakili katika 1 Wafalme 6:1, ambacho kinaonyesha kwa usahihi kipindi hiki kilikuwa miaka 480. Hii inapatana na kusoma kwa usahihi Matendo 13:20, panapoonyesha kwamba kipindi cha “karibu miaka mia nne na hamsini” kinachotajwa hapo kiliutangulia wakati wa Waamuzi.
Katika mwaka wa 1943 kitabu cha Watch Tower Society “The Truth Shall Make You Free” kiliiachilia mbali miaka ya ziada 100 isiyokuwapo kabisa katika kipindi cha Waamuzi na kuonyesha miaka 6,000 ya kuwako kwa mwanadamu itakwisha katika miaka ya kuanzia na wa 1970. Pia kilikuthibitisha kuanza kwa kuwapo kwa Kristo katika mwaka wa 1914 C.E., si mwaka wa 1874.