Kuthamini Uhusiano Wetu na Yehova
“Mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.”—Mt. 5:45.
1. Kwa sababu gani tunathamini sana rafiki mwema, na kwa sababu gani lazima tumwone Yehova kama rafiki yetu aliye bora kupita wote?
RAFIKI mwenye kutumainika amepaswa ahesabiwe kati ya vitu vyenye thamani zaidi tulivyo navyo. Mtu wa namna hiyo ni mwenye kufariji sana wakati wa shida nasi tunamfurahia sana tunapokuwa na baraka za kushiriki pamoja naye. Ikiwa sisi tuna rafiki wengi waaminifu tu matajiri kweli kweli. Lakini wewe wamwona nani kuwa rafiki yako bora kuliko wote? Pengine ni yule unayeshirikiana sana naye ambaye uhusiano wake nawe unatosheleza zaidi mahitaji yako. Sote tunaweza kufikiria rafiki tunaowathamini sana, lakini hatuwezi kupata ye yote kati yao anayelingana na Yehova kama rafiki anayeweza kutosheleza kabisa mahitaji yetu. “Humwongezea nguvu yeye asiyekuwa na uwezo,” akitupa vitu vyote vinavyotakiwa ili kututosheleza. (Isa. 40:29-31) Wale wanaothamini uhusiano wao na Yeye wanashikamana kabisa na Yeye kama mwenzi wa karibu.
2, 3. (a) Tunawezaje sisi wenyewe kufahamiana na Yehova? (b) Kuwa rafiki Yake kunaleta daraka gani?
2 Kutokana na maoni ya kibinadamu, huenda wengine wakaona haiwezekani kuwa na uhusiano naye. Nawezaje kuwa rafiki wa karibu wa mtu aliye mbali hivyo? Mimi mwenyewe nina nafasi gani ya kukadiri sifa zake? Ni wachache kati yetu tulio na tumaini la kushirikiana naye tukionana naye hasa, lakini hiyo haimaanishi kwamba hatuwezi kamwe kujua alivyo. Yeye alitoa habari halisi za utu wake kupitia kwa Mwanawe. Yesu alijulisha hivi: “Aliyeniona mimi amemwona Baba.” (Yohana 14:9) Wanafunzi wa Yesu waliweza kuona ndani yake sifa zile zile zilizomo katika Baba yake. Kuwapo kwake katikati ya wanadamu na matendo yake kati yao yalitupa nafasi isiyo na kifani ya kufahamiana na Baba yake sisi wenyewe. Yesu alisema, “Heri macho yaonayo mnayoyaona ninyi. . . . Manabii wengi na wafalme walitamani kuyaona mnayoyaona ninyi wasiyaone.” (Luka 10:23, 24) Hata Musa aliyezungumza mwenyewe na Yehova hakuwa mwenye baraka kama wale walioweza kumwona na kumsikia Yesu.
3 Yesu alifanya iwezekane kwetu kujua Yehova alivyo. Alituonyesha namna ya kumfikia Baba yake tupate upendeleo Wake. Alitupasha habari alizojua juu ya Baba yake. Mtume alisema hivi: “Ndani yake yeye hazina zote za hekima na maarifa zimesitirika.” (Kol. 2:3) Kuchunguza mafundisho yake na sifa zake mwenyewe kunatusaidia kumfahamu na kumthamini Baba yake kama rafiki mwenye kutumainika. Kadiri tunavyozidi kuwa karibu naye, ndivyo furaha yetu inavyozidi kuongezeka. Vile vile, daraka letu linaongezeka. Wajibu wetu kwake unaongezeka. Mtu anayempa Yehova kisogo kwa makusudi akiisha kumkubali kama rafiki anachukuliwa kama mtu “aliyemkanyaga Mwana wa Mungu, na . . . [kuifanyia jeuri roho ya] neema” (Ebr. 10:28, 29) Badala ya kutuvunja moyo, kujua hivyo kunatufanya tutafute hata zaidi urafiki wake.
YESU ANATHAMINI KABISA UHUSIANO WAKE NA YEHOVA
4. Yesu alikuwa na nafasi gani ya kupata kumjua Baba yake, naye alipewa mgawo gani?
4 Yesu alionyesha kwa kila njia kwamba aliuthamini sana uhusiano wake na Baba yake. Yote aliyosema na kufanya yalionyesha kwamba alimjua Baba yake vizuri sana na alitaka kuwa kama yeye katika kila njia. Aliendelea kuwa mbele za Baba yake kale na kale kabla hajawa mwanadamu, akaweza kumwona yeye mwenyewe na kuwa na uhusiano wa karibu naye kama vile kati ya baba mwenye upendo na mwana mwaminifu. Mgawo wake wa kazi ulikuwa kutimiza makusudi ya uumbaji wa Baba yake. Kwa sababu hiyo, “vyote vilifanyika kwa huyo.” (Yohana 1:3) Yeye alitimiza kazi mbalimbali zisizo na kikomo kwa usawa kabisa, hata hatuwezi kuuwazia ubora wazo. Alipewa nguvu yenye uwezo kupita nguvu zote aitumie: roho takatifu. Aliitumia kwa kutii mapenzi ya Baba yake kwa uaminifu, akatimiza yote ambayo Yeye alikuwa amekusudia.
5. (a) Yesu aliendeleaje kutumia mamlaka hata alipokuwa duniani? (b) Alitumia mamlaka yake kutimiza makusudi gani mawili?
5 Mwana anao uwezo mkuu. “Yu juu ya yote,” naye Baba “amempa vyote mkononi mwake.” (Yohana 3:31, 35; Mt. 28:18) Alipokuwa duniani aliendelea kutumia kadiri fulani ya mamlaka hiyo. Wakati mtume Petro alipotumia jeuri Yesu alipokamatwa, alimkemea Petro akauliza hivi: “Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika?” (Mt. 26:53) Alipokuwa akishughulika na mitume wake, alisema kwa mamlaka. Walipomwita “Bwana,” alikubali akisema hivi: “Mwanena vema, maana ndivyo nilivyo.” (Yohana 13:13) Maneno yake na njia ya kutenda havikutia shaka kwamba hakuwa msimamizi. Walakini, sikuzote yeye alitumia mamlaka kwa upole, kutimiza makusudi mawili: kwanza, kumtukuza Baba yake na kufunua makusudi Yake, na, pili, kufaidi wale ambao wangetii. Kushughulika kwake na mambo kulikusudiwa kuelekeza fikira zinazofaa juu ya Baba yake, kutukuza jina Lake mbele ya wengine. Alijaribu kwa bidii kujulisha sifa nzuri sana za Baba yake na mipango yake yenye upendo. Alisema mara nyingi bila kusitasita kwamba alimtii Yehova Mungu, akakata maneno sikuzote ‘kufanya yale yampendezayo.’—Yohana 8:29.
6. Yesu alionyeshaje kwamba alifikiria wengine kwa unyofu?
6 Alitaka sana kuona wengine wakiwa na hali njema, akataka sana kuwasaidia wastahili kupata kibali ya Baba yake. Yeye hakutumia mamlaka yake kwa njia yo yote kuwafanya wamtumikie yeye kwa faida yake mwenyewe. Kuwa kwake na mali haba za kimwili kulionyesha kwamba hakutamani kujitajirisha mwenyewe kwa kuwatumia wao. Hakuamuru wengine kibwana-mkubwa wafanye hivi na vile; alitenda kwa huruma na upole. Wote waliomfikia walipokewa namna ile ile moja, bila kupendelea matajiri wala kudharau maskini.
7. Yesu alionaje juu ya mamlaka ya Baba yake, nayo hiyo ikawa na matokeo gani juu ya wanafunzi wake?
7 Yeye aliona yote yaliyokuwa mema, ya haki na adilifu katika Baba yake. Yeye hakuona kutii kama wajibu; alitaka Baba yake awe Bwana wake. Kwa sababu Yesu alizionyesha sifa hizo katika utu wake mwenyewe kwa usawa kabisa wanafunzi wake nao walitaka kufanya vivyo hivyo. Pia, mambo waliyoona ndani wake yaliwafanya wamtake Yesu awe Bwana wao. Petro alizungumza kwa ajili ya waamini wote aliposema Yesu ni “Mtakatifu wa Mungu” na kwamba ndiye aliye na “maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:67-69) Kwa sababu yeye alisihi kwa upendo, wao walivutwa kwake kwa vyepesi. (Yohana 15:12) Ukamatano uliotokezwa na upendo huo uliendelezwa kwa kadiri ya kwamba wangeweza hata kuufia. Wakashikamana wasiweze kutenganishwa, wakaungana pamoja kumtii Baba kwa uaminifu.—Yohana 17:20, 21.
8. Yesu alionyeshaje matumaini kamili katika Baba yake?
8 Yesu alimwamini na kumtumaini kabisa Baba yake. Alisadiki kwa nafsi yote kwamba Baba yake asingemkatisha tamaa. Hakutilia mashaka wema, uadilifu, thamani wala kufaulu kabisa kwa kazi za Baba yake. Alijitoa kwa kupenda na bila kusita-sita atumiwe na Baba yake, “si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” (Mt. 26:39) Ndivyo alivyoazimia yeye ajuaye Baba kuliko mtu mwingine ye yote. Ni wazi kwamba alistaajabiwa kwa sababu ya uzuri wa sifa alizoonyesha akiwa ameziona katika Baba yake.
KRISTO ALIMFUNUA YEHOVA KUWA RAFIKI
9. Yesu alitusaidiaje tufahamu namna Baba yake anavyotupenda sisi sana?
9 Ingekuwa baraka kama nini kwetu tukimjua Baba kama Yesu alivyomjua! Yeye alitaka sana sana kutusaidia tufanye hivyo, halafu mwishowe tupate furaha iliyo nyingi zaidi ya urafiki wa Baba yake. Kupitia kwa mwenendo wake, sifa nzuri ajabu za Baba yake zilifunuliwa wote wapate kuziona. Iliyo kubwa zaidi kati ya sifa hizo ni upendo wake usio na kikomo. Yohana 3:16 inasema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee” kama ukombozi. Tunaanza kufahamu wingi wa upendo huo tunapomwona Yesu akijitolea kwa sababu ya upendo uo huo “kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Tunajiona kuwa wenye deni ya kumshukuru Yesu kwa sababu ya alilofanya. Tunapothamini kwamba mpango wote uliwezeshwa na Baba yake kwa kupata hasara ya Mwanawe mpendwa sana, tunavutwa kwa Yehova mioyo yetu ikiwa imejawa sana na shukrani.
10. Yesu alimfuataje Baba yake katika kuonyesha unyenyekevu?
10 Wenye kumjia Yesu walimwona kuwa mwenye kuambilika, tayari kusikiliza maneno yao na mwenye kupendezwa nao kwa unyofu sikuzote. (Yohana 4:6, 30-34) Wengi walistaajabu kumwona akiwa na unyenyekevu wa kweli usioonekana sana katika wenye mamlaka. Inachangamsha moyo sana kujua kwamba tunaweza kumfikia Baba, Yehova Mungu, tukiwa na uhakikisho uo huo kwamba atatupokea kwa upole, akifikiria mahitaji yetu kwa unyofu. Unyenyekevu wa kustaajabisha unaweza kuonekana hata katika Baba na kutuvuta karibu naye bila kipingamizi.—Zab. 18:35.
11. Ni kitu gani kilichovutia watu wawe wanafunzi wa Yesu, na hii ikawa na matokeo gani juu ya uhusiano wao na Baba yake?
11 Ingawa Yesu alikuwa mwanadamu mkamilifu mwenye sifa nyingi za utu mume, Yesu hakuvuta watu kwa sababu hiyo. Wasiopenda haki au sifa za wema hawakuvutwa na mambo waliyoona akifanya, sawasawa na vile unabii ulivyokuwa umekwisha sema. (Isa. 53:1, 2) Wale ambao wakawa wanafunzi wake walikuwa watu wenye kuthamini sana wema na haki, wenye kuona kabisa kwamba yeye alikuwa na sifa hizo. Kwa kuona sifa hizo za kutamanika alizo nazo Yesu sisi wenyewe tunazidi kumheshimu Baba yake kwa maana sisi pia tunapata kuvutiwa na Yeye mwenyewe. Nasi tumepata kuipenda haki aliyoonyesha katika njia zake zote.
KRISTO ALIFUNUA UHUSIANO WETU NA YEHOVA
12. (a) Huenda tukaelekea kulionaje wazo la kwamba tunaweza kuwa rafiki za Yehova? (b) Ni kujua nini kunakotutia moyo tukaribie?
12 Tunaposikia mara ya kwanza kwamba tunaweza kuwa rafiki wa karibu wa Yehova tunajiona hatustahili kuwa hivyo. Hata hivyo, anatuita kwa uchangamfu tumwendee, sawa na vile baba anavyoita watoto wake. Yeye ndiye Baba yetu kweli kweli, nasi tuna nafasi katika jamaa yake ya wana wa kibinadamu. Tunapomfikia kupitia kwa Yesu hatupaswi kubadili umbo la mwili wetu, kwa maana hapo mwanzo tuliumbwa kwa ‘mfano wake na sura yake,’ tukiwa na kadiri fulani ya sifa zake. (Mwa. 1:26) Kwa sababu tuna ukamatano huo, tunaweza kuwa na uhusiano wenye maana naye. Mahali panapotufaa kuwa ni ndani ya jamaa yake; tukiwa nje mahali penginepo tunakuwa mbali naye, tunakuwa mbali tusiweze kupata vitu vya lazima vinavyotufanya kuwa hai. Adamu ndiye aliyefanya kuwe na pengo katika uhusiano wetu wa jamaa pamoja na Mungu; dhambi yake ya makusudi ilitufanya tulaaniwe kuwa watenda dhambi waliotengwa. Kwa rehema Yehova alitupa njia ya kupata tena kilichopotezwa. Yesu alitufunulia tunachokosa akatuonyesha sawasawa mabadiliko tunayopaswa kufanya katika nyutu zetu tuweze kukubalika tena kuwa sehemu ya jamaa ya Mungu.
13. Ni kitu gani kimezuia uhusiano wetu Naye, nacho kitaondolewaje?
13 Bila shaka, hatuwezi kwa nguvu zetu wenyewe kushinda kizuizi cha dhambi tuliyorithi hata tukijaribu namna gani. Maadamu kizuizi hicho kipo, nyutu zetu zitaonyesha maelekeo yenye dhambi yasiyoweza kukubaliwa na Mungu. Paulo alisema hivi waziwazi: “Lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo.” Alifurahia kufikiria faida za ukombozi zilizotumiwa, ambazo mwishowe zingeondoa vizuizi vyote vyenye kutufanya tusikuze utu mpya. (Rum. 7:19, 24, 25) Wenye kustahili kuzipata faida zote za ukombozi wanajifunza kuonyesha utu huu mpya kwa njia inayompendeza Mungu.
14. Wale walio na uhusiano mwema na Yehova wanapewa pendeleo gani?
14 Kupata tena uhusiano mwema naye kunafanya upate tena mapendeleo uliyopoteza katika utumishi wake. Anatutolea nafasi ya kushiriki katika kazi anayofanya sasa, yaani, kueneza ujumbe wa Ufalme. Anatukaribisha tushiriki tukiwa ‘wafanya kazi pamoja naye,’ si tukiwa watumwa wadogo. (1 Kor. 3:9) Tunapewa heshima ya ‘kufanya kazi pamoja naye.’ (2 Kor. 6:1) Leo, zaidi ya ‘wafanya kazi wenzake’ 2,000,000 wanalifurahia pendeleo la kushiriki pamoja naye katika kazi hiyo ya kuokoa uhai.
15. Hata ingawa tunafanya kazi kwa bidii, lazima tutambue nini juu ya matokeo?
15 Ingawa tunajitahidi sana, Mungu ndiye anayefanya kazi iliyo kubwa zaidi. Mgawo wetu ni kupeleka habari njema tu kwa wale walio karibu yetu, tukifanya tuwezayo tufundishe wale wanaoitikia. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Tunaweza kuwa wenye shukrani kwamba Yeye anatupa utendaji huo wenye kufaa unaotupa nafasi ya kuzoeza akili zetu na uwezo wetu mbalimbali kwa ukamili. Tunafanya yote tuwezayo, lakini tunatambua kwamba yangekuwa majivuno kwetu kujipatia sifa ya matokeo yanayopatikana. Yehova ndiye amefungua mioyo ya mamia ya maelfu ambao wameitikia, akaviondoa vizuizi ambavyo vimekuwa vikiwafanya wajinga. Sheria yake inapatikana katika mioyo yao kwa sababu yeye ndiye aliyeitia humo kulingana na agano Lake jipya. (Ebr. 10:16) Sifa ya mabadiliko makubwa ambayo wamefanya katika maisha zao yaweza kutolewa kwa utendaji wa roho yake takatifu yenye nguvu, si kwa ufundi wetu kama waalimu.
16. Ni kwa kadiri gani inatupasa tumpe Yehova sifa kwa sababu ya kupata wanafunzi wapya?
16 Tunapoona waamini wapya wakiwa imara, kwa njia hiyo tunashuhudia utendaji wa roho ya Mungu. Ni mwujiza wa Mungu kweli kila mara moyo wa mtu unapofunguliwa akubali kweli ya Biblia. Tunalazimika kustaajabu kila mara mtu anapoponywa upofu wa kiroho na kutolewa katika mtego wa Ibilisi. Wakati watu mwishowe wanapoweka maisha zao wakf na kubatizwa katika maji wawe wanafunzi wa Yesu, sifa yote lazima imwendee Baba. Yesu mwenyewe alikubali hivyo alipotangaza hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba.” (Yohana 6:44) Ni pendeleo kama nini kwa mtu kupewa madaraka ya kuwa mfanya kazi pamoja naye, licha ya kukubaliwa kuwa rafiki yake! Kuthamini kunatufanya tuwe wenye shukrani nyingi sana.
KRISTO ALIFUNUA MADARAKA YETU KWA MUNGU NA WANADAMU
17. (a) Katika uhusiano wetu, Yehova anatazamia nini kwetu? (b) Yesu aliweka mfano gani mkamilifu katika habari hii?
17 Kwa mfano na mafundisho yake, Yesu alitusaidia tuone hali yetu katika uhusiano wetu na Baba yake na madaraka tunayochukua katika hali hii yenye upendeleo. Baba yake anatutazamia tumtumaini Yeye. Yesu hakutegemea uamuzi wake kwa vyo vyote. Alitafuta uongozi na msaada wa Baba yake katika mambo yote, akasali Kwake sikuzote. (Luka 6:12) Utii ni wa lazima pia. Zaidi ya hayo, utii wa namna inayofaa ni wa lazima. Mungu hataki utumwa mnyonge wa mtumwa mpumbavu, wala hataki utii unaoongozwa na kuogopa tu kuadhibiwa. Yesu aliweka mfano kwa kuwa mtu ‘mwema,’ si ‘mwenye haki’ tu. Yeye hakuepuka kufanya mabaya kwa sababu tu sheria ya Mungu inakataza kuyafanya. Alifanya hivyo kwa sababu yeye mwenyewe asingeweza kuyakubali. Kama vile Baba yake, yeye ‘alipenda haki, akachukia maasi.’ (Ebr. 1:9) Yeye hakuweza kufikiria kufanya jambo baya.—Mt. 16:22, 23.
18. Wanadamu watakapokuwa wakamilifu, ni kwa kadiri gani watakavyohitaji sheria za kuandikwa?
18 Kuchunguza kusudi la Yesu la kuweka mfano mkamilifu aliouweka kunainua kuwaza kwetu ili tuthamini kanuni ya juu ambayo kwayo Baba yake atashughulika nasi wakati mwishowe tutakapofikia ukamilifu. Wakati wanadamu wanapoonyesha sifa ya kimungu ya wema aliyoionyesha Yesu, kunakuwa hakuna haja ya kuweka sheria ndefu ndefu. Paulo alihakikisha hivyo, akisema hivi: “Sheria haimhusu mtu wa haki, bali waasi, na wasio wataratibu.” (1 Tim. 1:9) Baada ya kueleza matunda ya roho ya Mungu, aliendelea kusema hivi: “Juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” (Gal. 5:22, 23) Wakati wanadamu wanapoongozwa na maelekeo ya haki yaliyo ndani yao, hawazuiwi kwa vyo vyote na sheria zilizoandikwa. Tutakapofikia ukamilifu, tutafanya yaliyo haki kwa maana tukiwa wanadamu wakamilifu tutachagua kupenda yaliyo haki. ‘Tutawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata tuingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.’ (Rum. 8:21) Sheria nyingi sana zitakuwa kuukuu. Uongozi wote unaohitajiwa na mwanadamu utajumlishwa katika amri nyepesi ya “kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” (Mik. 6:8) Sulemani aliieleza amri hii kwa maneno machache, akisema kwamba ‘hii ndiyo jumla ya maneno: Mche Mungu, nawe uzishike amri zake.’—Mhu. 12:13.
19. Ikiwa tunamfuata Yesu, tutaonaje juu ya kutenda mabaya?
19 Imetupasa tujitahidi kukaribia kanuni kamilifu ya Yesu kama iwezekanavyo. Tukiwa na nia yake, hatutakuwa na maoni mabaya juu ya sheria ya Mungu, tukiitii kwa sababu ni lazima tu na bila moyo wa kupenda. Kwa sababu tunapenda haki na kuchukia uasi, hatutakuwa na maoni ya kwamba jambo lo lote linafaa maadamu kundi la Kikristo haliwezi kutuadhibu kwa sababu yake. Wala hatutajaribu kusogea tuone tunaweza kukaribia kufanya ubaya kadiri gani bila kuvunja sheria fulani, wala hatutajaribu kuendelea kufanya jambo lenye kutiliwa mashaka ati kwa sababu wazee hawawezi kutuamuru tufanye vingine. Kwa sababu tunampenda Yehova, ‘tutauchukia uovu’ na kujiepusha nao kama iwezekanavyo.—Zab. 97:10.
20, 21. (a) Kuthamini kunatuongoza kufanya nini? (b) Kwa sababu gani ni lazima kufanya hivyo ili tuwe na uhusiano mwema na Yehova?
20 Hakuna jambo lililo zuri zaidi kwa mwanadamu kuliko kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Thawabu yake ni bora zaidi sana kuliko hazina yo yote ya kimwili. Thamani ya mambo yanayostahili sifa ya kuonyesha wengine wema na kuwapenda hailinganiki. Kuthamini kunatuvuta tukaribishe wengine wajiunge nasi katika uhusiano huu wa jamaa pamoja na Mungu. Kwa shauku tunawapungia mkono kusema ‘njoni! mtwae maji ya uzima bure.’ (Ufu. 22:17) Baada ya nyutu kubadilishwa na upendo wa kweli ambao Yesu alitufundisha, sasa tunaacha maelekeo yasiyokamilika ya kujifikiria wenyewe bila kujali wengine. Upendo huo unatufundisha kwamba kukataa kushiriki faida za fadhili zake zisizostahilika ni kukosa kusudi lake. (2 Kor. 6:1) Tunapozidi kuthamini sifa hiyo ya kimungu, tunataka zaidi kuona watu wengine wakiwa na hali njema.
21 Hatuwezi kuendelea kuwa na uhusiano na Baba wa kimbinguni bila kufikiria wengine hivyo. Kuwa na hali yenye kukubalika mbele zake kutategemea milele juu ya nia yetu kufuata upendo wake tunaposhughulika na wengine. Kila wonyesho wa fadhili ambao yeye alionyesha ulionyeshwa mara nyingi kwa mambo aliyotufanyia Yesu, hiyo ikatia mkazo wa kwamba Baba yake anawapenda wanadamu sana. Mtu ye yote asiyejali mwanadamu mwenzake kwa kujifikiria mwenyewe hawezi kuwa anampenda Mungu kwa ukamili. Ni lazima tufikirie watu wengine ikiwa tutakuwa na uhusiano wenye kufaa pamoja naye.
22. (a) Tunawezaje kuonyesha upendo wa kweli kwa ndugu zetu? (b) Upendo huo unawezaje kuonyeshwa kwa wale walio nje ya kundi?
22 Kwa kufahamu hivyo, tunapendezwa na wengine kwa unyofu wa moyo. Imetupasa tuwafikirie zaidi wale walio karibu nasi katika kundi la Kikristo. Tunataka sana “tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Gal. 6:10) Tunajaribu kwa kila njia kutoa msaada tunapoona ndugu zetu wakiwa na mahitaji ya kiroho au ya kimwili. Lakini upendo wetu hauhusu ndugu zetu wa kiroho tu; unakunjuliwa kutia ndani wanadamu wote, hata wale walio mbali sana na Mungu. Tunawahurumia, na hii inatufanya tujaribu kuwafanyia mambo wapendayo zaidi kama ambavyo sisi tunataka wengine watufanyie. (Mt. 7:12) Wakiyajua mambo aliyoyafundisha Yesu watakuwa wameijua njia ya uzima. Kuhubiri kwetu ujumbe wa Ufalme kunawasaidia wawe na uhusiano unaofaa na Yehova na kunaonyesha kwamba tunataka sana sana kuona wakiwa na hali njema. Kwa furaha tunatumia kila nafasi tushiriki, kwa kuwa hatutosheki na kujitahidi kidogo tu. Tunaendelea kufikiria namna tunavyoweza kutumia wakati wetu na nguvu zetu na mali tulizo nazo tukiwa na mradi wa kupata nafasi zaidi za kuhubiri. Tunaona kufanya upainia, kutumikia katika sehemu zilizo na uhitaji mkubwa na kadhalika kuwa mapendeleo ya pekee sana yanayoturuhusu tuonyeshe hasa sifa ya kweli ya upendo wetu.
23. Ni faida gani zinazotokana na jitihada ya kuendeleza uhusiano mwema na Yehova?
23 Kazi hii inaleta faida kwa mtu anayehusika. Yehova anafurahia utii wetu wa kupenda na jitihada yetu kulishuhudia jina lake. Yesu anafurahia tuwe wanaotazamiwa kuwa raia chini ya utawala wake wa miaka elfu. Ndugu zetu wa kiroho wanatukaribia sisi katika kifungo cha umoja chenye uchangamfu. Wenye mfano wa kondoo wanajiona kuwa wenye deni ya kushukuru daima kwa sababu ya mambo ambayo tumewafanyia. Mioyo yetu inafurahi kweli kweli kuziona baraka zinazotokana na uhusiano wetu na Yehova! Tu wenye furaha namna gani kwa kuwa tumeruhusiwa ‘kufanya urafiki’ naye na kupokea uhakikisho wake juu ya kuishi wakati ujao katika “makao ya milele”!
24. Kwa sababu gani imetupasa tuuthamini uhusiano wetu na Yehova?
24 Kweli Yehova amejihakikisha kuwa rafiki bora zaidi na aliye wa kutumainiwa zaidi kuliko ye yote tutakayekuwa naye. Hakuna jambo lenye faida zaidi katika maisha yetu kuliko kupata kumjua yeye kama mwenzi wa karibu. Akiwa ndiye “Mungu mwenye furaha,” tayari anatimiza ahadi yake ya kutufanya sisi wenye furaha pia. (1 Tim. 1:11, NW) Tukiweza kuimarisha kifungo cha urafiki huo tutaendelea kuwa wenye furaha milele. Kwa sababu ya kuthamini usalama, amani ya akili na tumaini ambalo tumepata katika uhusiano wetu, tunavutwa kuonyesha shukrani zetu zilizo nyingi zaidi na za moyoni kwa rafiki yetu bora, Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 510]
Yesu alisaidia wengine waingie katika uhusiano na Yehova, akapokea watu wote kwa msingi ule ule mmoja, bila kupendelea matajiri wala kudharau maskini