‘Tukiwa Hatuna Kitu Lakini Tukiwa na Vitu Vyote’
“Kama maskini lakini tukitajirisha wengi, tukiwa kama hatuna kitu lakini tukiwa na vitu vyote.”—2 Kor. 6:10, NW.
1. Ni kwa njia gani pesa zinatimiza uhitaji?
KWA hakika pesa ni za lazima katika maisha ya kila siku. Bila hizo, ungewezaje kuishi katika taratibu iliyopo ya mambo? Ungewezaje kujipatia riziki? Katika sehemu nyingi za dunia zinaweza kusaidia mtu apate uangalizi hospitalini, zinaweza kumsafirisha, zinaweza kununua umeme, joto na maji ya mifereji, vitu ambavyo vina mafaa kwa mwanadamu. Lakini kama usingekuwa na pesa, ungewezaje kujilisha na kujivika mwenyewe na jamaa yako? Ungewezaje kupata mahali pa kuishi na kupatunza? Ni kama vile Mhubiri 10:19 inavyosema kwa hekima sana: “Karamu hufanywa kwa ajili ya kicheko, na divai huyafurahisha maisha; na fedha huleta jawabu la mambo yote.”
2. Imepasa Mkristo ajihadhari na nini sikuzote? Kwa sababu gani?
2 Kwa hiyo, maadamu taratibu iliyopo ya mambo ipo, pesa zinaweza kutumiwa vizuri sana na Wakristo watimize mahitaji yao ya kila siku, hasa kwa habari ya kuendesha utumishi wao wa Ufalme. Walakini, kwa sababu ya mafaa yazo na vitu vingi zinavyoweza kununua, lazima Mkristo aendelee kujiweza, sikuzote awe na maoni yanayofaa juu ya pesa (utajiri, mali za kimwili), yaani azione kama chombo cha kumsaidia, kama mtumishi. Zisiruhusiwe kamwe ziwe chombo cha kupendwa na mtu, ziwe ‘kipenzi chake cha moyo.’ Kwa hiyo, ni jambo la lazima namna gani kwa Mkristo leo kupata na kuendeleza maoni yanayofaa juu ya mali, tukifikiria wakati tunamoishi sasa!
3. (a) Paulo anatusaidia kuonaje mali za kimwili? (b) Yeye aliweka moyo wake wapi?
3 Kwa sababu mtume Paulo alikuwa wa kabila la Benyamini, Mwebrania wa dini ya Mafarisayo (waliokuwa na sifa ya kuwa “wapenda fedha”), angeweza kusema atusaidie tuwe na usawa wa kiroho akiwa na ujuzi wa aliyokuwa akisema. (Flp. 3:5; Luka 16:14) Kwa sababu ya uwezo wake mbalimbali na elimu, akiwa amefundishwa na Farisayo Gamalieli mwenye elimu ya juu, bila shaka angaliweza kufanikiwa sana katika ukusanyaji wa utajiri wa kimwili. (Matendo 5:34; 22:3) Lakini, Paulo alionyesha kuliko na utajiri wa kweli. Baada ya kutumia zaidi ya miaka 25 katika kazi ya kuhubiri wakati wote, na kutupwa gerezani kwa sababu ya kazi hiyo, aliandika habari za kusadiki kwake, uamuzi wake wa kuacha maisha ambayo pengine yalikuwa ya kujipatia faida nyingi za kimwili, akisema hivi: “Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo; tena nionekane katika yeye . . . ili nipate kwa njia yo yote [kuufikia ufufuo wa mapema zaidi kutoka kwa wafu].” Paulo alionyesha alikuwa ameweka moyo wake wapi, na kilichokuwa cha thamani halisi katika maisha yake. (Flp. 3:8-14; Ebr. 6:10-12) Kwa kuwa nia yake juu ya utajiri wa kimwili ilifaa, angeweza kuendeleza maoni yanayofaa. Maishani mwake aliona matokeo yenye kudhuru wengi yaliyotokana na kupenda utajiri.—2 Tim. 4:10.
TANZI (MTEGO) YA TAMAA YA KICHOYO
4. Timotheo alikuwa akionywa juu ya hatari gani?
4 Paulo alimwandikia kijana Timotheo kwa kumfikiria kwa unyofu Timotheo akiwa Efeso, Asia Ndogo, ambao wakati huo ulikuwa mji wenye utajiri mwingi sana wa kibiashara. Akimwonya juu ya kusitawisha tamaa ya utajiri wa kimwili na matokeo yake yenye msiba, alisema hivi: “Hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru, ziwatosazo wanadamu katika upotevu na uharibifu. Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:9, 10) Je! wewe unathamini shauri hilo? Je! unalitii? Je! umeona ukweli walo katika maisha za wengi leo?
5. (a) Ni kwa njia gani tamaa ya utajiri wa kimwili inavyoweza kuwa “tanzi”? (b) Kwa sababu gani mtu hawezi kutumikia mabwana wawili?
5 Wakati kupendezwa kwako na pesa za kujiruzuku kunapogeuka kuwa tamaa yenye kuwaka ya kuwa tajiri, au kujipatia vitu usivyovihitaji, pesa zinaacha kuwa chombo cha matumizi yako, zinaacha kuwa mtumishi wako. Badala yake, zinakuwa bwana wako! Sasa zinakuwa “tanzi.” Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.” (Mt. 6:24) Biblia haikatazi kuwa na mali; inakataza kuwa kwako mtumwa wake. Kwa sababu gani? Kwa sababu tamaa yako ya faida ya kimwili inapokuwa nyingi sana hata unakuwa mtumwa wake, Yehova Mungu si Bwana wako tena. Kwa hiyo huwezi ‘kumpenda Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa nafsi yako yote, na kwa akili zako zote.’ (Mt. 22:37) Wengine wanatamka kwamba “pesa zinasema.” Lakini, uwapo mtumwa wazo, ndizo zitakazokuwazia pia!
6. (a) Ni matokeo gani yenye kudhuru ambayo kupenda pesa kunaweza kuwa nayo juu ya Mkristo? (b) Wengine wanaonaje pesa?
6 Tamaa hiyo ya pesa (mali) inaweza kuwasha sana nafsi ya mtu hata kuziondoa sifa za Kikristo. Inaweza kushusha mtu akawa wa kinyama. Inaweza kufanya mtu aache kuona haja ya kuwa na haki, kweli, uaminifu, kuwa mkarimu na kuonyesha rehema. (Kum. 16:19, 20; Kut. 23:8) Kutamani sana wingi wa vitu vya kimwili kunaongoza mtu kwa vyepesi ajitie katika mazoea ya ulimwengu ya udanganyifu wa kibiashara. “Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.” (Mit. 28:20) Lakini huenda ukasema, “Hivyo sivyo mimi nilivyo; mimi naweza kuzuia tamaa hiyo. Ningewezaje kusitawisha upendo wa pesa? Ingawaje, pesa ni karatasi tu!” Ni kweli, lakini je! unatumia wakati na jitihada ya kadiri gani uzipate? Je! zinakuwa bwana wako? Katika kitabu chake The Paper Economy, David T. Bazelon anakubali hivi kwa uaminifu: “Pesa ni ndoto. Ni kipande cha karatasi ambacho kimeandikwa ndoto ya vitu vyote zinavyoweza kununua kwa wino isiyoonekana . . . Wengi wetu Amerika tusioshindwa kabisa kutafuta sana pesa tunazipenda sana kuliko cho chote cha vitu zinavyoweza kununua. Kwetu pesa si kitu cha kutusaidia, ni tamaa.” Tunaishi katika wakati aliouonyesha Paulo kwa unabii katika 2 Timotheo 3:1, 2, ambao alisema hivi juu yake: “Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa . . . wenye kupenda fedha.” Kwa hiyo, ni jambo la maana kama nini Mkristo aendeleze usawa, akijihadhari na tamaa isiyotoshelezeka ya utajiri wa kimwili!
7. Mara nyingi kujitaabisha kwa ajili ya mali kumekuwa na matokeo gani?
7 Kujitaabisha huko kwa ajili ya mali na kuzipenda kumeleta maumivu ya moyo yasiyo na kikomo, msiba, taabu, huzuni, fadhaa na umwagaji wa damu. Wale ambao wamekosa kiasi ni wa kuhurumiwa, wale ambao wamesitawisha mioyo yenye tamaa. Acheni tufahamu kama Paulo, kwamba “yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi” na kwamba ni ya “kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.”—Rum. 15:4; 1 Kor. 10:11.
“UDANGANYIFU WA MALI”
8. (a) Ni nia gani ya moyo aliyoonyesha Akani? (b) Tunajifunza somo gani kutokana na hilo?
8 Acheni tukumbuke wakati Yehova Mungu alipokuwa akiongoza Waisraeli kupitia jangwani walipoelekea kuwa tayari kuimiliki Nchi ya Ahadi. Waliambiwa mji wa Yeriko “lazima uwe kitu kilichowekwa wakf kwa uharibifu . . . ni wa Yehova,” ukiwa kama malimbuko ya ushindi. Maagizo ya Mungu yalikataza kuteka nyara (kuchukua vitu vya watu walioshindwa), kama ilivyokuwa ikifanywa kwa kawaida wakati wa kuteka mji, lakini ulipaswa kuchomwa kwa moto. Fedha na dhahabu zilipaswa kutiwa “katika hazina ya Yehova.” (Yos. 6:17-19, NW) Walakini, Akani, wa kabila la Yuda, aliacha moyo wake uwe wenye tamaa. Baadaye aliungama hivi: “Nilipoona katika nyara joho nzuri ya Babeli, na shekeli mia mbili za fedha, na kabari ya dhahabu, uzani wake shekeli hamsini, basi nalivitamani, nikavitwaa.” (Yos. 7:21) Kupenda utajiri kulimwongoza Akani kuwa asiyeaminika, akawa mdanganyifu, akamwibia Yehova. Israeli waIipokuwa wakijaribu kuteka mji uliofuata, Ai, Yehova aliondoa roho yake kwa Israeli mpaka Akani alipoonyeshwa wazi mbele ya watu kuwa mtenda kosa. Walipotolewa kati ya watu wengine, Akani, jamaa yake na mifugo yake yote walipigwa kwa mawe na kuchomwa kwa moto. Looo! ni hasara gani iliyowapata kwa sababu ya hazina yenye kuharibika!—Yos. 7:1-26.
9. (a) Gehazi alionyeshaje kwamba ‘alipenda fedha’? (b) Vivyo hivyo, ni nini kilichofanya Anania na Safira wapoteze maisha zao?
9 Mfikirie pia mtumishi wa Elisha, Gehazi. Elisha alipokwisha kumponya jemadari Mshamu Naamani ukoma wake, Naamani alitaka kuonyesha shukrani na kumpa Elisha zawadi, lakini akaikataa. Walakini, Gehazi alikuwa mpenda mali. Alijaribu kujipatia faida kutokana na mwujiza huo. Ikamfanya atunge uongo wa kumwambia Naamani na Elisha pia. Matokeo yakawa nini? Elisha alisema: “Kwa hiyo ukoma wa Naamani utashikamana nawe na wazao wako kwa wakati usiojulikana.” (2 Fal. 5:20-27, NW) Halafu tena Anania na mkewe Safira ‘waliomwambia Mungu uongo’ wakazuia kwa siri sehemu ya thamani ya kiwanja chao, walipoteza maisha zao kwa sababu hiyo.—Matendo 5:1-10.
10. Moyo wenye tamaa unaweza kumwingiza mtu katika hali gani za kupita kiasi?
10 Halafu tunao mfano wa mtu aliyekuwa na pendeleo la ajabu la kuwa mmoja wa mitume wa Yesu, Yuda Iskariote. Bila shaka kwa sababu ya kuwa mwaminifu na mwenye kutegemeka kwanza, alianza kutunza pesa za kawaida za Yesu na wale thenashara; lakini baadaye akawa mwizi mwenye pupa, mwizi wa mazoea. (Yohana 12:6) Moyo wake wenye tamaa ukamwongoza kumsaliti Bwana wake kwa vipande 30 tu vya fedha. Matokeo? Alipoona Yesu amehukumiwa, akatoka nje “akajinyonga.” (Mt. 27:3-5) Hiyo ndiyo hatari kwa wale wanaokuwa watumwa wa mali!
11. Ni kwa njia gani mali za kimwili ni zenye udanganyifu? Eleza.
11 Biblia inazungumza juu ya “udanganyifu wa mali.” (Mt. 13:22) Sababu ya kuwa kwake na udanganyifu ni kwamba mtu anayezitafuta kwa kawaida anashindwa kujua upungufu wake. Anadanganyika kwa sababu hapati hasa uradhi anaotaka sana kutokana na mali hizo anazotafuta kwa bidii nyingi. Sikuzote anadhani kwamba vitu asivyoweza kupata akiwa na utajiri mdogo ataweza kuvipata akiwa na utajiri zaidi. Kwa hiyo sikuzote anaona njaa ya mali zaidi na zaidi, naye hatosheki kamwe. Linalopendeza ni kwamba njaa yake inaongezeka kadiri anavyozidi kuzitafuta. Kama vile alivyokubali kwa unyofu msimamizi wa mambo ya kiserikali Mwamerika Benjamin Franklin: “Pesa hazijapata kufanya mwanadamu akawa mwenye furaha, wala hazitamfanya. Hakuna cho chote katika pesa cha kuleta furaha. Kadiri mtu alivyo na zaidi, ndivyo anavyotaka zaidi. Badala ya kujaza nafasi zinatokeza nafasi zaidi. Zikitosheleza uhitaji mmoja, kwa njia nyingine zinaufanya uhitaji huo uongezeke maradufu na mara tatu. Hiyo ni mithali ya kweli ya mtu mwenye hekima, uitegemee. ‘Afadhali vichache pamoja na kumcha BWANA kuliko hazina kuu pamoja na taabu.’”—Mit. 15:16, AV.
12. Kufahamu kwetu upungufu wa mali za kimwili kutatusaidiaje tuendeleze maoni yanayofaa juu yake?
12 Kujua upungufu wa mali za kimwili kutatusaidia tuendelee kuwa na kiasi. Utajiri wa kimwili haufai mahitaji ya kibinadamu yanapozidi sana. Kama Yesu alivyosema, uzima wa mtu hautegemei mali zake za kimwili. (Luka 12:15-21) Mtu afiwapo na mpendwa, je! pesa zinaweza kumpunguzia huzuni? Je! kuna kiasi cho chote unachoweza kutoa umrudishe huyo kutoka Sheol, kaburini? Mtu aondokewapo na ujana wake na kuingiliwa na uzee, je! rasilmali na fedha iliyowekewa amana inaweza kuyaondoa makunyanzi, kumfanya mtu awe kijana na mwenye nguvu tena? Afya ya mtu iharibikapo, kuwa na benki nzima yenye kujawa na mapesa kunaleta furaha gani? Ikiwa ulizaliwa kipofu, je! pesa zote zilizomo ulimwenguni zingekuonyesha ishara mbalimbali za upendo zilizo usoni pa wazazi wako, zingekuonyesha machweo ya jua yenye kupendeza au vitoto vya wanyama vikicheza-cheza? Ikiwa ulizaliwa kiziwi, je! kuwa na dhahabu kama maji ni afadhali kuliko kusikia wimbo wenye ulinganifu wa sauti zenye kupendeza, mlio wa bahari kuu au hata sauti yako mwenyewe? Lo! namna ulivyo mchache uwezo wa hazina za kimwili!
13. Mithali 30:8, 9 inatupa maoni gani?
13 Kupata kibali na baraka ya Yehova hakutegemei vitu ambavyo huenda tukawa navyo wala ambavyo huenda tukawa hatunavyo, bali kunategemea namna tunavyotumia na kuona vile tulivyo navyo. “Usinipe umaskini wala utajiri; unilishe chakula kilicho kadiri yangu. Nisije nikashiba nikakukana, nikasema, [Yehova] ni nani? Wala nisiwe maskini sana nikaiba, na kulitaja bure jina la Mungu wangu.” (Mit. 30:8, 9) Tusipokuwa na kiasi na kuendeleza maoni yanayofaa, kuwa kwetu na chache au nyingi za mali za ulimwengu huu kunaweza kuwa hatari.
14. (a) Wengine walio maskini wa bidhaa za ulimwengu huu wana maoni gani? (b) Kuwaza huko ni sawa?
14 Mtu asiye na mali za kimwili anaweza kuonyesha upendo mwingi sana wa mali. Kwa kuwa hana kitu, huenda akajiona ana haki ya kuiba, au kuwa mdanganyifu kwa njia nyingine ndiyo apate kitu anachotamani sana. Kwa sababu ya kuonea kijicho vitu walivyo navyo wengine, huenda akajiona yu mwenye haki kabisa kutumia wakati wake wote na kujitahidi sana apate kitu anachotamani. Au, pengine aweza kuona kwamba ulimwengu una deni ya riziki yake, kama waonavyo watu wengi leo. Lakini, jambo hili linategemea maoni ya mtu. Mtu huyu huyu anayejiona kuwa maskini huenda akaonekana kuwa tajiri na mtu mwingine anayeishi katika nchi nyingine. Lazima tuthamini tulivyo navyo na kuvitumia inavyofaa. “Mwenye hekima asijisifu kwa sababu ya hekima yake, wala mwenye nguvu asijisifu kwa sababu ya nguvu zake, wala tajiri asijisifu kwa sababu ya utajiri wake.” (Yer. 9:23) Nia inayofaa imeonyeshwa hapo bila kujali kama mtu ni mwenye hekima, mwenye nguvu au tajiri. Si kwamba lazima mtu awe mmoja wa hao, bali amepaswa kuwa na kiasi. Na ajisifie kumjua Yehova.—1 Kor. 1:31.
15. (a) Paulo anaonyeshaje kwamba si vibaya kuwa na wingi? (b) Walakini, ni hatari gani zinazokabili wale walio na wingi?
15 Neno la Mungu halihukumu mtu kwa sababu ya kuwa na wingi wa bidhaa za ulimwengu huu. Alipokuwa akitambua uhakika wa kwamba wengine walikuwa matajiri katika siku zake, Paulo hakumwagiza Timotheo ashauri ndugu hao matajiri wajiondolee utajiri wao, wawe maskini na kuishi maisha ya umaskini. Sivyo! Bali, aliwasihi waendeleze nia inayofaa juu ya mali. “Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha. Watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.” (1 Tim. 6:17-19) Paulo anaonya juu ya hatari ya kuwa na mali nyingi kupita kiasi. Huenda mtu akawa na maelekeo ya kuweka tumaini lake katika mali. Zinaweza kuondoa fikira za mtu katika mambo ya kiroho. Mtu angeweza kuwa mtumwa kwa kuzitunza, kuzilinda. Mtu awe tajiri au maskini, kuna kikomo cha kadiri anavyoweza kula au kuvalia. Imetupasa kuridhika na cho chote tulicho nacho, kukitumia kuendeleza faida za Ufalme, kushika sana “uzima ulio kweli kweli.”
KUTAFUTA MALI ZA KWELI
16. Imetupasa tuwe na maoni gani juu ya wakati ujao kwa habari ya mali za kimwili?
16 Ni kwa kadiri gani basi imetupasa kuhangaikia mali za kimwili? Paulo alishauri hivi: “Hatukuja na kitu duniani, tena hatuwezi kutoka na kitu; ila tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Tim. 6:7, 8) Alipokuwa akifundisha wanafunzi wake kusali, Yesu alisema: “Utupe riziki yetu ya siku kulingana na uhitaji wa siku.” (Luka 11:3, NW) Hasemi tuweke lundo la vitu. Anasema uhangaikie matakwa yako ya kila siku tu, si kufikiria-flkiria utakachokuwa nacho wakati ujao kana kwamba ndilo jambo kubwa. Sababu gani ujiwekee utajiri kwa ajili ya wakati ambao huenda usiuone kamwe? Sababu gani uweke hazina katika ulimwengu unaopita?—1 Yohana 2:15-17.
17, 18. (a) Tunawezaje kujilinda na kusumbukia vitu? (b) Maana ya mifano ya Yesu ni nini?
17 Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ataona umepata riziki ukitanguliza faida za ufalme maishani mwako. Yesu anatoa maoni yanayofaa: “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? (Mt. 6:25) Yesu anakazia mambo ya maana, mambo ya kiroho, maisha ya mtu, si vitu vya kimwili vinavyoweza kuleta masumbufu hayo! Anatuambia ‘tuangalie sana ndege,’ namna Yehova “huwalisha hao,” na ‘tufikiri maua ya mashamba, hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo.’ Akionyesha wazi sana jambo halisi la kusumbukia, anasema: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Babu yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mt, 6:26-33) Je! wewe unaamini hivyo?
18 Hiyo haimaanishi tujikalie kitako, tusifanye lo lote, kisha tungoje mpaka Mungu atakapotupa chakula na mavazi. Mfano wa Yesu unaonyesha namna ndege wanavyotafuta wanachotaka. Yehova anawapa uwezo na nguvu za kufanya hivyo. Atatupa na sisi pia. (Flp. 4:13) Linalokaziwa ni kutokuwa kwetu na hangaiko linalozidi juu ya vitu vya kimwili, bali tufanye utumishi wetu kwa Mungu kuwa hazina. Kufanya hivyo kutaleta baraka zisizohesabika. Mtu akifanya hivyo anapokea thawabu ya vitu ambavyo pesa haziwezi kununua, mali zisizolinganika!—Rum. 11:33.
19. Kwa sababu gani mali za kiroho si za kulinganishwa na za kimwili?
19 Thamani nyingi zaidi ya mali hizo inafafanuliwa vizuri kwa ajili yetu katika Mithali 3:13-18: “Heri mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Maana biashara yake ni bora kuliko biashara ya fedha, na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi. Yeye ana thamani kuliko marijani, wala vyote uvitamanivyo havilingani naye. Ana wingi wa siku katika mkono wake wa kuume, utajiri na heshima katika mkono wake wa kushoto. Njia zake ni njia za kupendeza sana, na mapito yake yote ni amani. Yeye ni mti wa uzima kwao wamshikao sana; ana heri kila mtu ashikamanaye naye.” Kutokana na mali hizo inakuja amani na furaha ya kweli, hata uzima wetu wenyewe wa wakati ujao!
20. (a) Ni mfano gani alioweka Yesu juu ya mali za kimwili? (b) Alifanya nini kipatikane?
20 Je! wewe unathamini hazina hizi? Yesu alizithamini! Hazina yake ilikuwa kuyafanya mapenzi ya Baba yake. Hata alisema hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 4:34; 6:38) Aliweka kila kitu kingneecho nyuma katika maisha yake. Kwa kufaa alithamini ubora wa mali za kweli. Ingawa alikuwa Mwana wa Mungu, hatusomi kwamba Yesu alikuwa na wingi wa mali za kimwili duniani. Sivyo! “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana vioto, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake.” (Luka 9:58) Walakini, ingawa alikuwa maskini alikuwa tajiri. Fikiria maisha yake nawe utaona kwamba alikuwa mwenye furaha, mwenye kuridhika. Alikuwa kama mtu mwenye bidhaa chache za ulimwengu, lakini aliweza kukomboa taifa lote la kibinadamu, akafanya mali zilizo kuu zaidi zipatikane, yaani, tumaini kwa wafuasi wake la kuwa “wana wa Mungu.” Tena, walipata mali nyingine za kiroho.—2 Kor. 8:9; Rum. 8:14, 19; Yak. 2:5; Kol. 1:27; 2:2, 3.
21. (a) Mitume wa Yesu walionyeshaje kuthamini hazina ya kimbinguni? (b) Tunaweza kufikiria maulizo gani?
21 Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya mitume. Wao pia waliendeleza maoni yanayofaa kwa kutanguliza hazina za kimbinguni. Petro na ndugu yake Andrea walikuwa wavua samaki, lakini walipokaribishwa na Yesu, waliitikia “mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata.” (Mt. 4:20) Ndivyo Yohana na Yakobo walivyoitikia. “Mara wakakiacha chombo na baba yao, wakamfuata.” (Mt. 4:22) Lo! waliithaminije nafasi ya kumtumikia Yehova Mungu pamoja na Mwanawe aliyemtuma! Ungalikuwako wakati huo, ungalifanya nini? Ungaliacha nyavu zako papo hapo? Au ungalichelewesha uamuzi wako, ukiwaza kwamba, kwa kuwa biashara ya samaki ilikuwa yenye kuleta faida, utaendelea nayo kidogo hata uwe na pesa zilizo nafuu ndiyo umfuate? Imetupasa sana leo tufahamu iliko hazina ya kweli. Je! kwa mwendo wako wa maisha unahakikisha sasa kwamba hazina hizo za kiroho ndilo jambo la maana zaidi maishani mwako? (Mt. 13:44-46) Je! wewe unakua katika kuthamini hazina za kiroho, katika kuthamini utafutaji wa upendeleo na baraka za Yehova? Je! unatambua faida zote za kiroho zinazotumiminikia kupitia kwa tengenezo la Mungu na kuzitumia kwa faida kamili?
KUELEKEZA “JICHO” LETU PANAPOFAA
22. (a) Ni kwa njia gani jicho letu ni “taa ya mwili’’ Eleza. (b) Maana yake nini kuelekeza ‘macho ya moyo’ wetu panapofaa?
22 Yesu alisema: “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi [nyofu; lenye kutazama mahali pamoja tu, likiwa la ukarimu], mwili wako wote utakuwa na nuru. Lakini jicho lako likiwa bovu [lenye choyo Moffat] ,mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo!” (Mt. 6:22, 23) Shauri hilo linafaaje! Je! sote hatuwezi kufurahia nuru mahali penye giza ituzuie tusijikwae au kugonga kitu, na kujidhuru wenyewe? Ili tuwe na maono yanayofaa, lazima jicho letu liwe safi, yaani, litazame mahali pamoja tu linapofanya kazi. Lazima lielekee panapofaa, likinasa barabara miale yote ya nuru linayoweza kunasa katika chombo fulani hata kionekane namna kilivyo kabisa. Ndivyo yalivyo ‘macho ya mioyo yetu.’ (Efe. 1:18) Lazima nayo yaelekee panapofaa, lazima yatazame mahali pamoja tu. Lazima tuone mambo yanavyofaa kuonwa ndiyo tufanye maamuzi yanayofaa. Kuwa na jicho nyofu (la ukarimu) kutatusaidia tusijihangaikie wenyewe kupita kiasi. Tutataka kugawana vitu na wengine. (Flp. 2:4) Kuwa na ‘jicho baya’ au lenye kutazama-tazama huku na huku kutatufanya tufuatie mwendo wa anasa, tukifanya uchaguzi mbaya. Mwili wetu wote utakuwa na “giza” tititi.
23. (a) Tukiwa kama maskini, tunawezaje kutajirisha wengi? (b) Tunaweza kuwa na maoni gani juu ya utumishi wa wakati wote?
23 Tukiwa na ‘jicho la ukarimu’ hilo, tunaweza kufahamu maneno ya Paulo ya kwamba yeye alikuwa ‘kama maskini lakini akitajirisha wengi, akiwa kama hana kitu lakini akiwa na vitu vyote.’ (2 Kor. 6:10, NW) Paulo hakuwa na wajibu uliomtaka awe na pesa hata afanye kazi ya kawaida ya kutengeneza hema, lakini nyakati nyingine alitengeneza hema asilemee makundi ya alikokuwa kwa habari ya pesa. Hakuna kiasi cha pesa kinachoweza kulingana na hazina ya kumtumikia Yehova kwa fikira zako zote. Kama Paulo, kuna maelfu leo wanaotumia wakati wao wote kuhubiri na kufundisha wakiwa mapainia, waangalizi wa pekee na wafanya kazi katika makao ya Betheli, kwa kuendelea kuwa na jicho “safi.” Kwa kuwa na maoni yanayofaa juu ya pesa, wanaziona baraka hizo za kiroho kuwa zenye thamani kubwa zaidi kuliko mali za kimwili ambazo wangaliweza kuwa nazo kama wangalikuwa wakitumia mwingi wa wakati wao katika shughuli za kimwili.
24. Kutoa kunawezaje kuwa hazina?
24 Tukielekeza macho yetu ‘panapofaa,’ tunaweza kuithamini furaha iliyo nyingi zaidi ya kusaidia wengine wazijue kweli za Mungu za ajabu na kuona badiliko zinaloleta katika maisha zao. Huu ndio msingi wa furaha halisi! Kama alivyosema Yesu: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Furaha na baraka ya kusaidia wengine, hasa kiroho, inatajirisha mtu zaidi kuliko kiasi cho chote cha utajiri wa kimwili. Je! wewe ‘unaona’ na kuthamini hivyo?
25. Ni kwa njia gani “matunda ya roho” ni hazina hasa leo?
25 Fikiria pia hazina ya roho takatifu ya Mungu. Haiwezi kununuliwa. (Matendo 8:18-20) Wala kiasi cho chote cha pesa hakiwezi kununua matunda ya roho ya Mungu. Ikieleza habari za hazina hiyo, Biblia inasema hivi: “Matunda ya roho ni upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Gal. 5:22, 23, NW) Katika siku hii yenye ugomvi ulimwenguni pote, ebu fikiri sifa hizo ni zenye thamani ya kadiri gani! Ni jambo lenye thamani kama nini kuwa na “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.” “Itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Flp. 4:7) Kwa kuepuka roho ya kupenda fedha ya ulimwengu, kwa kujipatanisha na mapenzi ya Mungu, kwa kusali sikuzote, kwa kuomba roho yake na ufahamu na kwa kuiacha iwe nguvu kuu katika maisha yako, wewe pia unaweza kuzipata baraka za hazina hiyo.
26. Thawabu ya “kondoo wengine” wanaoendelea kuwa na jicho “safi” ni nini?
26 Ukiwa na maono safi ya kiroho, je! wewe unaweza kuiona hazina nyingine hii—tumaini la kupata uzima wa milele? Naam! Wazia, kuishi milele juu ya dunia ya paradiso! Hiyo ndiyo thawabu ya “kondoo wengine” wale wanaoendelea kuweka jicho lao likiwa “safi,” likitazama mahali pamoja tu. (Yohana 10:16; Tito 1:2; 1 Yohana 2:17; 1 Tim. 6:12) Hakuna kiasi cho chote cha mali za kimwili kingeweza kuipata thawabu hiyo. (Luka 12:15-21) Kwa maana “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Hiyo ndiyo ahadi ya Mungu kwa wale wanaompenda na kufanya mapenzi yake, kutia na “kondoo wengine.”
27. (a) Kwa sababu ya wakati tunamoishi, imetupasa tuendeleze maoni gani juu ya utajiri wa kimwili? (b) Yetu ni furaha na pendeleo gani?
27 Basi, sote na tuendelee kuwa na maono safi ya kiroho kwa kuendeleza maoni yanayofaa juu ya mali, tukikumbuka kwamba mapesa yote ya taratibu hii ya mambo yanakusudiwa kutoweka, kuwa ya bure. (Eze. 7:19; Luka 16:9) Karibuni, wakati “dhiki kubwa” itakapokomesha mataifa yote ya dunia, thamani ya mali za ulimwengu huu itatoweka, kwa wafu na kwa waokokaji wa “dhiki” pia. Acheni tulitii shauri la Yesu na kutumia tulivyo navyo kumtukuza Mungu. (Yohana 15:8) Na tuonyeshe kwamba tunatanguliza mali za kiroho kwa kutumia kwa faida kamili mipango mingi ambayo Yehova amefanya, si kwa maneno tu, bali kupitia kwa matendo yetu. Acheni tueleze wengine habari njema za Ufalme, tukiwasadia wapate mali za kiroho, na kuendelea kuwa na maoni yanayofaa juu ya mali zetu za kimwili na kukuza kumbukumbu jema kwa Baba yetu aliye katika mbingu. Yetu na iwe furaha na pendeleo la kuwa “kama maskini lakini tukitajirisha wengi, tukiwa kama hatuna kitu lakini tukiwa na vitu vyote.”—2 Kor. 6:10, NW.
—Kutoka The Watchtower, Sept. 15, 1975.