“Iweni Wafadhili Ninyi Kwa Ninyi”
LO! Ni furaha sana kushirikiana na watu wafadhili! Wao wanatofautiana sana na wachoyo wakali wasio na adabu kwa kuhurumia wengine na kupendezwa kuona wakiwa na hali njema.
Wale wanaotaka kumpendeza Mungu wana sababu nzuri ya kufikiria kuonyesha fadhili. Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu, anatutaka sote tusitawishe sifa hii kabisa. Fadhili ni tunda la roho yake. (Gal. 5:22) Biblia inasihi wale wanaompenda Mungu wafanye hivi: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.”—Kol. 3:12.
Mfano ambao Yehova Mungu ameweka katika kuonyesha fadhili umepaswa utuongoze kuonyesha sifa hiyo ya kutamanika katika maisha zetu wenyewe. Juu ya jambo lilo hilo, mtume Paulo anatuonya kwa upole, akisema: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”—Efe. 4:32.
Kwa hakika Yehova Mungu amekuwa mwenye fadhili kwa kutusamehe makosa yetu. Ni kama vile Maandiko yanavyosema: “Alitusamehe makosa yetu yote kwa fadhili.” (Kol. 2:13, NW) Kwa hiyo, lingekosa namna gani kuweka kinyongo moyoni au kuona uchungu juu ya wenzetu kwa sababu ya makosa madogo waliyotutendea! Kwa kweli isingekuwa fadhili kuwaepuka au kukataa kusema nao kwa sababu walituudhi kwa njia fulani. Je! sisi tungetaka wengine watende hivyo kwa sababu ya makosa yetu madogo? Nasi tungekuwa wapi kama Yehova Mungu angetuhesabia makosa yetu yote yaliyo mengi?—Zab. 130:3.
Ikiwa tunataka Mungu aendelee kutufaidi kwa fadhili zake, lazima tuwe na nia ya kufunika makosa yetu madogo madogo sisi kwa sisi. Kama vile Yesu Kristo alivyoonyesha: “Mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.”—Mt. 6:14, 15; tazama pia Luka 6:35, 36.
USEMI NA MATENDO YA KUFIKIRIA WATU
Walakini, fadhili juu ya wengine hazihusu kusamehe tu. Zinatia ndani usemi na matendo ya kufikiria watu pia. Nyakati nyingine huenda mtu akaelekea kujirahisisha afanye lo lote kwa wale alio na uhusiano wa karibu nao, watu wa ukoo wake na marafiki. Anaposhughulika na wageni, huenda akawa mwangalifu sana, akisema “tafadhali” na “asante,” na kuonyesha anafikiria sana mawazo yao ya moyoni. Lakini anaposhughulika na washiriki wa jamaa na marafiki, huenda akakosa kujali juu ya maneno na matendo yake. Huenda akawaza kwamba wale wanaomjua kweli watafahamu sababu gani anafanya hivyo hata liwe ni jambo gani analofanya au kusema. Ingawa hiyo huenda ikawa kweli kwa kadiri fulani, je! inafanya maisha yawe ya kupendeza zaidi na ya kufurahika kwa washirika hao wa karibu? Badala yake, je! haiharibu fadhili zao kidogo?
Fikiria vile malaika waaminifu wamefanya walipokuwa wakishughulika na wanadamu kwa fadhili na heshima. Ingawa ni wakuu zaidi kwa nguvu na uwezo, wakati wo wote malaika hawaonyeshwi katika Maandiko kama walisema vyo vyote tu walipokuwa wakizungumza na wanadamu duniani. (2 Pet. 2:11) Walikuwa wenye heshima sana, wakiwapa waliokuwa wakisema nao fahari iliyowastahili. Kwa mfano, malaika mwenye kumwakilisha Yehova alisema “tafadhali” alipokuwa akisema na Ibrahimu. (Mwa. 13:14, NW) Je! tusiwe wenye nia ya kufanyia wanadamu wenzetu ivyo hivyo, tukiwapa fahari na heshima inayowastahili kwa fadhili?
Naam, katika ulimwengu huu usio na fadhili si vyepesi kuonyesha fadhili. Huenda mtu akajikuta akilazimika kushughulika na wakosa adabu wasiofuata kanuni. Lakini je! hiyo inaonyesha kwamba hao hawastahili kuonyeshwa fadhili? Hata kidogo.
Fikiri juu ya Lutu na hali aliyokabili katika Sodoma. Alipokaribisha malaika wageni nyumbani mwake, kundi la watu wenye ghasia lilizunguka nyumba yake, wakadai awape wageni wake wawafanye ufisadi. Yeye alifanya nini? Je! alikosa kujiweza akalinenea kwa hasira kundi hilo la watu wenye ghasia? Sivyo, Lutu alijizuia sana, akalisihi kundi hilo kwa maneno ya fadhili: “Basi, nawasihi, ndugu zangu, msitende vibaya hivi.”—Mwa. 19:7.
Kwa kuwa Lutu alisema kwa fadhili sana na watu waovu kupindukia, bila shaka imetupasa tutake kufanya ivyo hivyo kwa walio wenzi wetu katika kumtafuta Mungu, hata ikiwa wanafanya mambo yasiyo ya akili kwa njia fulani. Imetupasa tujitahidi kuwaonyesha fadhili kuu, kama tunavyowaonyesha wasiopendezwa kamwe kamwe na ujumbe wa Biblia. Kwa njia hiyo, tutakuwa tukitenda kupatana na onyo la upole lililoongozwa na Mungu: “Kwa kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”—Gal. 6:10.
Mwandikaji wa shauri hilo lililoongozwa na Mungu, mtume Paulo, alifanya lilo hilo. Alipomwandikia Filemoni ampokee mtumwa wake mtoro Onesimo, ambaye alikuwa ndugu aliyeongolewa karibuni, Paulo mwenyewe alionyesha fadhili kuu. Paulo angaliweza kumwagiza Filemoni afanye ile yeye, kama mtume, alivyoona inafaa. Lakini mtume Paulo alichagua kumsihi Filemoni atumie upendo wake wa haki. Aliandika hivi: “Nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza likupasalo; lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi, kwa kuwa ni kama nilivyo, Paulo mzee.”—Flm. 8, 9.
Kwa hakika njia hiyo ya uchangamfu ya kushughulika na jambo hilo ilikuwa na matokeo mazuri zaidi kufikia moyo wa Filemoni kuliko vile ingekuwa kama angalitumia amri ya mamlaka. Fadhili kama hizo zinavuta mtu atake kumwitikia vizuri yule anayezionyesha. Fadhili zinasaidia pia kukuza vifungo imara vya upendo na shauku.
Sifa hiyo inaweza kuwa na matokeo mema yenye nguvu hata juu ya watu wasio na fadhili. Kama vile Biblia inavyosema: “Adui yako akiwa na njaa, mlishe; akiwa na kiu, mnyweshe; maana ufanyapo hivyo, utampalia makaa ya moto kichwani pake.” (Rum. 12:20) Maneno yako na matendo yako yenye fadhili kwa mtu asiye na fadhili huenda yakamwaibisha juu ya vile ametenda. Huenda akalainisha nia yake juu yako. Huenda moyo wake ukaongozwa kuitikia kwa fadhili, kutokeza mambo bora yaliyomo ndani yake. Je! hiyo isingekuwa baraka kuu yenye kuthawabisha kwa kuonyesha fadhili?
Kwa sababu ya faida zinazotokana na kuonyesha fadhili, imetupasa kweli tujitahidi kusitawisha zaidi sifa hiyo. Hiyo itaongeza furaha ya wengine na yetu wenyewe pia. Neno la Mungu linasema, “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) La maana zaidi ni kwamba, kwa kuisitawisha sifa hiyo tunapata na kuendeleza kibali ya Baba yetu wa kimbinguni mwenye fadhili, Yehova Mungu.