Endelea Kuwa Thabiti Kama Kwamba Unamwona Yeye Asiyeonekana
“Kwa imani aliondoka Misri, wala si kwa sababu aliogopa hasira ya mfalme; kwa maana alikuwa mshupavu, kama yeye aliyemwona Mungu asiyeonekana.”—Ebr. 11:27, “New English Bible.”
1. (a) Ni ushuhuda gani unaotuhakikishia Yehova aishi? (b) Kwa sababu gani kutoonekana kwa Mungu hakuleti shaka lo lote juu ya kuwako kwake?
HAKUNA mtu anayeishi sasa wala aliyeishi duniani wakati uliopita amepata kumwona Mungu kwa macho yake halisi. Yehova ni mwenye utukufu mwingi mno kutoweza kuonekana na wanadamu dhaifu. Walakini, kutoonekana kwake hakupaswi kutufanye tuwe na mashaka juu ya kuwako kwake, wala hakufanyi isiwezekane kwetu ‘kumwona’ yeye kama Mtu kwa macho ya imani. Sifa na uwezo wake zinaweza kuonekana pia. Pande fulani za utu wake zinaonekana kwa kutazama kazi zake za uumbaji, kama mtume Paulo anavyosema katika barua yake kwa Warumi: “Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.” (Rum. 1:20) Kutoonekana kwake hakuleti mashaka juu ya kuwako kwake, wala hakufanyi isiwezekane kwetu kumheshimu yeye kama Mtu, wala kuthamini sifa, njia na matendo yake kwa watu wengine, hasa kwa watu wake mwenyewe. Inaonekana pia kwamba sifa na kanuni zake hazibadiliki. Hiyo yahakikishwa kwa maneno yake mwenyewe: “Mimi, [Yehova], sina kigeugeu.” (Mal. 3:6) Kutoonekana kwa Yehova kusipunguze imani yetu katika sifa zake za kipekee, katika mwenendo wake, na vilevile katika njia yake ya kushughulika na wale wampendao.
2, 3. Imani imebadilije maisha za watu wa Yehova?
2 Watu wa Yehova wamemwamini sana hivyo hata bila ya kumwona Yeye kwa halisi hata wakavutwa kubadili maisha zao kabisa wafanye mambo yanayompendeza. Hiyo inaonekana kutokana na uhakika wa kwamba Mashahidi wa Yehova wengi walikuwa wafisadi, wadanganyifu, wenye jeuri, wenye kupenda anasa za kilimwengu, wenye kutafuta faida za vitu vya kimwili, na vilevile wenye kutia bidii nyingi wajipatie “jina,” kabla hawajawa Mashahidi.—1 Kor. 6:9-11.
3 Baada ya ‘kumwona’ yeye, watu wengi wanyofu wamebadili mwendo wao wa maisha ‘wakageuka’ ili waishi kulingana na kanuni ambazo Yeye ameweka, kwa kuwa waaminifu na kuthamini mambo ya kiroho, na vilevile kutanguliza zaidi katika mioyo yao utendaji wa mapenzi ya Yehova.—Matendo 3:19; 1 Pet. 4:3, 4.
4. Ni nini kimeongoza watu wa Mungu watembee katika njia yake?
4 Na kwa sababu gani wamefanya badiliko hilo? Kwa sababu wamemwona Yehova Mungu kuwa mwenye upendo kwa macho yao ya ufahamu, na hilo ndilo jambo ambalo limewaongoza kutembea katika njia inayompendeza. Imani hiyo nyingi sana na yenye kudumu ndiyo imewaongoza kuzihubiri “habari njema” mwaka baada ya mwaka bila kuchoka, ingawa huenda wakavunjika moyo nyakati nyingine kwa sababu ya mateso na kwa sababu watu walio wengi hawataki kusikiliza. Kwa sababu sisi ‘tumemwona,’ tunamtumaini kabisa nasi tu wenye furaha katika utumishi wake.—Efe. 1:18; Matendo 5:42; Mt. 5:8, 10-12.
WAAMINIFU KATIKA IMANI YAO
5. Nia ya wale ambao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa muda mrefu ni nini?
5 Wengi ambao wameitikia amri ya Yehova kuzihubiri habari njema ulimwenguni pote wamekuwa wakifanya hivyo kwa miaka 20, 30, 40 au zaidi. Kadiri ambavyo wamezidi kuufanya utumishi huu, ndivyo wamezidi kuzithamini kazi Zake za ajabu na zenye utukufu. Wamemfahamu zaidi. Wale ambao wamekuwa wakimtumika Yehova kwa muda mrefu hawataki kuacha wala kupunguza mwendo katika mgawo waliopewa na Mungu. Wamekata maneno kusonga mbele, wakaipate thawabu waliyoahidiwa.—Yak. 1:12.
6. Waaminifu wa Mungu wamevumilia nini, nao wameyaonaje majaribu hayo?
6 Ingawa huenda wakawa wamepatwa na mateso makali, wanaendelea kuwa na imani yenye nguvu. Wao wamevumilia upinzani na wataendelea kuuvumilia, tena wamekata maneno kuendeleza ukamilifu kwa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Waaminifu wa Yehova wameteswa vikali sana katika sehemu nyingi za ulimwengu, hasa katika Ujeremani wakati wa utawala wa kishetani wa Nazi na pia hivi karibuni chini ya mtawala mtumia nguvu wa Malawi asiye na huruma. Ingawa majaribu yamekuwa makali sana, wanaume, wanawake na watoto wa Kikristo wameendelea kuwa waaminifu kwa Mungu wao wa kimbinguni, tena wamefurahia kufanya hivyo kama Wakristo wa karne ya kwanza. Wameliona kuwa pendeleo kuhakikisha wao ni waaminifu kwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote.—1 Pet. 4:12, 13; Zab. 145:10.
7-9. (a.) Mashahidi wa Yehova wameonyeshaje imani yao katika Ujeremani na Malawi? (b) Ni nini kimewawezesha kuvumilia?
7 Wakati wa utawala mwovu wa Hitler maelfu ya Mashahidi wa Yehova walipoteza kazi zao, biashara zao na nyumba zao. Wengi walinyang’anywa mali zao, wakanyimwa mishahara yao ya uzeeni, wakapoteza vitu vingine vya kipekee. Watoto 860 walitenganishwa na wazazi wao; jumla ya 6,019 walikamatwa, na wengi kati ya Mashahidi hao walikamatwa mara mbili, tatu, au hata zaidi hivi kwamba, visa vya kukamatwa vilivyoandikwa vilikuwa 8,917 kwa ujumla; nao walitumikia vifungo vya jumla ya miaka 13,924. Wengi wa wanaume na wanawake hao waaminifu walitiwa katika kambi za mateso na wote pamoja walikaa humo miaka 8,078 wakiteswa vibaya sana. 635 walifia gerezani, 253 wakahukumiwa kufa, lakini waliouawa kati ya hao ni 203.
8 Katika miaka ya karibuni zaidi mtawala mwenye kutumia nguvu aitwaye “Mkristo” wa nchi ya Afrika ya Malawi amefuata nyayo za Hitler kwa kutesatesa Mashahidi wa Yehova katika nchi hiyo. Mwaka wa 1972, zaidi ya Wakristo hao 30,000 na wenye kujifunza Biblia nao walilazimika kukimbilia nchi ya Msumbiji iliyo jirani wapate kuokoa maisha zao. Lakini Agosti na Septemba wa 1975 “walirudishwa” Malawi kutoka Msumbiji wakati utukuzo wa taifa ulipotokea tena baada ya nchi hiyo kujipatia uhuru. Huko tena, wameteswa kinyama, wakapigwa na kuibiwa pesa, mali na mavazi. Wamevuliwa nguo wakaachwa uchi, na wengi wa wanawake wao wakanajisiwa. Oktoba 1975, makundi mazima ya Mashahidi watu wazima yalizingirwa yakatiwa katika kambi za mateso kama za Hitler. Wazazi wamelazimishwa kuwaacha watoto wao nje ya kambi, hata vitoto vichanga vyenye kunyonya! Wakati polisi walipoulizwa sababu ya rais wa Malawi kuagiza hayo yatendwe, walijibu: “Ninyi ndinyi wa kulaumiwa kwa kufundisha watoto wenu mambo yasiyofaa. Kwa hiyo watatunzwa na Malawi, nasi tutawalazimisha kuwa raia wa Malawi.” Huo si ushetani? Mashahidi wa Yehova wa Malawi wameachwa bila nchi, bila nyumba hata watoto. Je! nchi ya Malawi inarudia yaliyotendwa na utawala wa Nazi kwa kutesa watu ambao “uvunjaji wa sheria” wa pekee waliofanya ni kulitii Neno la Mungu, Biblia, kwa kutokuwamo katika “ulimwengu” na siasa zake?—Yohana 17:16.
9 Hayo ni matendo ya kishetani! Lakini ni nini kimewezesha Wakristo hao wavumilie kutendwa maovu hayo? Wao wameitegemea Biblia Takatifu, Neno la Mungu. Humo wameona mifano ya watu waaminifu na wenye uvumilivu kama Musa, Yoshua, manabii na Wakristo wa karne ya kwanza. Wameukumbuka hasa mfano wa uaminifu uliowekwa na Bwana na Mwokozi wetu, Yesu Kristo.—Ebr. 12:1-3.
‘KUONA’ KWA JICHO LA IMANI
10. (a) Musa alikuwa na mambo gani yenye faida mwanzoni mwa maisha yake? (b) Alionyesha uaminifu gani kwa Yehova?
10 Kulingana na maoni ya kilimwengu Musa alikuwa katika cheo chenye faida nyingi sana za kimwili. Yeye alikuwa mwana wa kulelewa wa binti Farao, naye alikuwa katika hali ya kuweza kula vyakula vilivyo bora na kuvaa mavazi yaliyo bora, vilevile kuishi kifalme katika mazingira ya starehe kabisa. (Kut. 2:1-10) Alikuwa mtu mwenye fahari na wa kuheshimika, na mwishowe angalirithi mali nyingi sana. Alipata elimu iliyo juu zaidi, “akafundishwa hekima yote ya Wamisri” akawa “hodari wa maneno na matendo.” Bila shaka, basi, alikuwa na cheo chenye pendeleo kubwa sana huko Misri. (Matendo 7:20-22) Hata hivyo, Musa alifikiria zaidi uhusiano wake na Yehova. Kwa kufanya hivyo aliwekea Wakristo wote, wa miaka 1,900 iliyopita hata wa leo mfano unaofaa. Uaminifu kwa Mungu na watu wake ulimfanya aamue kukataa “kuitwa mwana wa binti Farao.” Maandishi ya Biblia yaliyoandikwa na mtume Paulo yaonyesha busara na ufahamu wa Musa yanaposema hivi: “Kwa imani aliondoka Misri, lakini si kwa kuiogopa hasira ya mfalme, kwa maana yeye aliendelea kuwa thabiti kama kwamba anamwona Yeye asiyeonekana. Kwa imani alikuwa amekwisha adhimisha kupitwa na kupaka damu, ili mwenye kuharibu asiwaguse wazaliwa wao wa kwanza. Kwa imani walipita katika Bahari ya Shamu kama katika nchi kavu, lakini Wamisri walipojaribu kufanya hivyo wakafunikwa.”—Ebr. 11:23-29, NW.
11. Musa alitayarishwaje kwa ajili ya mgawo wake wa wakati ujao?
11 Tamaa kuu ya Musa ilikuwa kutumiwa na Yehova kuwakomboa watu Wake. Alikaa Midiani miaka 40 akipewa mazoezi ya kimungu. Alipaswa kusitawisha sifa za saburi, upole, unyenyekevu, ustahimilivu, kutokuwa mwepesi wa hasira, kujiweza, na kujifunza kumngojea Yehova. Alipokuwa mchungaji jangwani alitayarishwa kuvumilia mambo yenye kukatisha tamaa na magumu ambayo yangemkabili. Vilevile alijifunza kwamba ilikuwa lazima awe mtulivu na kuonyesha imara, kwa sababu sifa hizo zingekuwa za lazima katika mgawo wake wa wakati ujao, atakapoondoa watu wa Yehova utumwani.—Matendo 7:29, 30.
12. (a) Kwa sababu gani iliwapasa Musa na Haruni waonyeshe ushujaa kwa kumtegemea Yehova? (b) Yehova aliwasaidiaje Waisraeli?
12 Je! Musa hakutakiwa kuwa hodari na shujaa kuweza kwenda mbele ya mfalme mkubwa kama Farao na kumpa neno mkataa kwamba lazima awaache watu wa Mungu waende zao? Yeye na Haruni, ndugu yake wa kimwili, walifanya hivyo mara nyingi. Mwishowe Farao aliwaacha Waisraeli wakaenda zao, lakini karibuni akabadili nia akawafuata. Ilielekea kwamba hawakuokoka kutoka mamlaka ya Farao. Jeshi la Misri lilikuwa likikaribia nyuma yao, kisha Bahari ya Shamu iliyo kuu ilikuwa mbele yao. Lakini Yehova akamwambia Musa: “Ukanyoshe mkono wako juu ya bahari.” Halafu Yeye akatumia upepo mkali wa mashariki urudishe bahari usiku kucha, sakafu ya bahari ikawa eneo pana la nchi kavu. Waisraeli wakaanza kupitia nchi kavu. Walipokuwa wakiendelea kutoka baharini, Wamisri wakafuata. Ndipo Yehova alipomwambia Musa: “Nyosha mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi tena juu ya Wamisri, juu ya magari yao, na juu ya farasi zao.” Hivyo Yehova aliokoa Israeli na mikono ya Wamisri! “Israeli akaiona ile kazi kubwa aliyoifanya [Yehova] juu ya Wamisri, ndipo hao watu wakamcha [Yehova], wakamwamini [Yehova], na Musa mtumishi wake.”—Kut. 14:15-31.
13. (a) Yoshua na Waisraeli walipataje ‘kumwona’ Yehova? (b) Ni nani aliyekuwa ndani ya Yeriko ‘aliyemwona’ Yehova, na kwa sababu gani?
13 Mrithi wa Musa Yoshua alionyesha imani pia. Yeye pia ‘alimwona’ Yehova. Wakati makuhani wenye kuchukua sanduku la agano walipokanyaga Mto Yordani, maji yaliyoshuka kutoka juu yalisimama kwa mwujiza. Waisraeli wakatembea katika bonde kavu la mto huku makuhani wakiwa wamesimama katika nchi kavu katikati ya Yordani. Waisraeli hao waliamini kabisa kwamba Yehova alikuwapo. Haya! moja kwa moja mpaka Yeriko! Walipofika huko waliuzunguka-zunguka mji mara moja kila siku, mpaka siku ya saba. Makuhani walipozipuliza pembe na watu wakapiga kelele, kuta za Yeriko zilizoelekea kutoanguka zilivunjwa-vunjwa. Kwa kweli Waisraeli wangeweza ‘kumwona’ Yehova katika tukio hilo, (Yos. 3:15-17; 6:10-16) Lakini mtu fulani aliyekuwa ndani ya Yeriko ‘alimwona’ pia Yehova wakati huo. Huyo alikuwa Rahabu. Kwa sababu ya kuuamini uwezo mkuu wa Yehova, aliachiliwa pamoja na jamaa yake. Alikuwa ameonyesha imani yake kwa matendo kwa kuwaficha wajumbe wa Yoshua.—Yos. 2:1-21; 6:25; Yak. 2:25; Ebr. 11:30, 31.
14. Mjane mmoja katika Sarepta ‘alimwonaje’ Yehova?
14 Wakati fulani baadaye nabii Eliya alitembelea mjane mmoja katika Sarepta. Mtoto wa mwanamke huyo alipatwa na ugonjwa akafa. Eliya akamwambia mwanamke: “Nipe mwanao.” Kisha “akamchukua juu chumbani mle alimokaa mwenyewe, akamlaza kitandani pake.” Halafu “akajinyosha juu ya mtoto mara tatu, akamwomba [Yehova], akanena, Ee [Yehova], Mungu wangu, nakusihi, [nafsi] ya mtoto huyu imrudie ndani yake tena . . . ikamrudia, akafufuka.” Je! mjane huyo ‘alimwona’ Yehova kweli? Ndiyo, lakini hakumwona kwa macho halisi. Alimwona kwa macho yake ya imani, kwa maana alimjibu Eliya akisema: “Sasa najua ya kuwa wewe ndiwe mtu wa Mungu, na ya kuwa neno la [Yehova] kinywani mwako ni kweli.”—1 Fal. 17:7-24; Ebr. 11:35.
15. Twaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa “wingu kubwa la mashahidi”?
15 Watu waaminifu wa kale, yaani, Habili, Henoko, Nuhu, Ibrahimu na wengine kufika wakati wa Musa, wote wale wanaotajwa katika sura ya kumi na moja ya Waebrania na wengine wasiohesabika, wana ushuhuda wa kwamba ‘walimwona’ Mungu. Waebrania 12:1 yasema hivi juu ya watu hao: “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” Kwa kuonyesha imani, watu hao walitoa ushuhuda usioweza kupingwa kuhusu Mungu na makusudi yake yasiyobadilika. ‘Walimwona’ Mungu hasa, si kwa macho halisi, bali kwa macho yao ya imani. Je! wewe, pia, una imani yenye nguvu kama yao?
IMANI HUONGOZA MTU KUCHUKUA HATUA
16. ‘Twaonaje’ kwa jicho la imani?
16 Tunapofahamu jambo fulani kwa kuona yanayopata wengine au yanayotimizwa nao, tunaonyesha sifa hiyo ya imani ijapokuwa hatukuliona jambo lenyewe kwa macho yetu halisi. Twaweza kusema kwamba twaikubali au ‘twaiona’ taratibu mpya ikikaribia sana. Haimaanishi tumeonyeshwa taratibu hiyo kwa halisi, ingawa tunaifurahia kidogo katika paradiso yetu ya kiroho ya siku hizi; bali hiyo yamaanisha kwamba tumeiona kwa macho yetu ya imani. Tunaelezwa jambo hilo na Paulo katika Warumi 1:19, 20: “Mambo ya Mungu yanayojulikana yamekuwa dhahiri . . . Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata [wasioamini] wasiwe na udhuru.” Imani hutegemea ushuhuda thabiti. Kutegemeka kwa neno la Mungu na kutimia kwa usahihi kwa unabii wake mbalimbali kunafanya tuwe na imani kamili mioyoni mwetu.
17. Twawezaje kuonyesha ‘uthabiti katika kumwona Yeye asiyeonekana’?
17 Yehova anataka ‘watu wote wafikie toba.’ (2 Pet. 3:9.) Kwa hiyo lazima tuwe thabiti tunapohubiri wengine. Huenda tukajiona hatuna uwezo mwingi wa kuhubiri, lakini hiyo si sababu ya kuacha kazi hiyo yenye kujenga imani. Yehova ataka watu wote wanaoyakubali “maji ya uzima” wayatoe kwa wengine pia. Kama Musa, acheni tuendelee ‘kuwa thabiti kama kwamba tunamwona Yeye asiyeonekana,’ tusaidie wengine pia ‘wamwone’ Yeye. Katika Ufunuo 22:17 twaambiwa hivi: “Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” Ikiwa tuna imani yenye nguvu, tutatoa ukaribishaji huo kwa moyo wote.
18. Twawezaje kuondoa udhaifu wetu?
18 Musa hakujiona anafaa kutimiza agizo alilopewa. Alitoa udhuru, akisema kwamba hakuwa mwepesi wa kusema. (Kut. 4:10) Hata hivyo, alifanikiwa kwa kusaidiwa na Yehova. Sisi pia twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatutia nguvu tutimize agizo tulilopewa ingawa huenda tukawa na udhaifu fulani. Je! si wengi wamejiona hivyo, pengine zaidi ya wakati mmoja? Wewe ulipoanza kuhudhuria mikutano ya kundi ya Mashahidi wa Yehova, je! ulisema hivi: “Mimi siwezi kusema kama wale wengine”? Je! pengine ulidhani hivi pia: “Mimi siwezi kamwe kuhutubia wasikilizaji, wawe wengi au wachache”? Lakini je! sasa hufanyi mambo hayo yote uliyodhani hayawezekani? Hiyo ni kwa sababu umejifunza Neno la Mungu na wajua kwamba roho yake i pamoja nawe na kwamba yatutia nguvu.—2 Kor. 12:10.
19. (a) Sisi tunashiriki katika kazi ya nani? (b) Ni mfano gani mwema unaohakikisha hivyo?
19 Lazima tukumbuke kwamba kazi ambayo Yehova amewapa watu wake si yao. Ni kazi yake, naye ndiye mwenye kufungua mioyo ya watu waitikie. Hii yaonyeshwa vizuri na aliyoona Paulo alipohubiri Filipi: “Mwanamke mmoja, jina lake Lidia, mwenye kuuza rangi ya zambarau, mwenyeji wa Thiatira, mcha Mungu, akatusikiliza, ambaye moyo wake ulifunguliwa na [Yehova], ayatunze maneno yaliyonenwa na Paulo.” Naam, Yehova ndiye aliyeufungua moyo wa Lidia ‘akabatizwa, yeye na nyumba yake.’—Matendo 16:14, 15.
20, 21. (a) Twawezaje kushinda kipingamizi cha eneo la watu wasioitikia? (b) Jina la Yehova lahusikaje?
20 Imetupasa tutumie uwezo na sifa zo zote tulizo nazo tuvute watu wenye mioyo minyofu, bila kujali hali yao ya maisha. Tutegemee nguvu za kutoka wapi? Yehova ndiye atakayetutia nguvu, kama alivyowatia Musa na Haruni, hata tutaweza kutenda kwa ujasiri na uhodari bila kujali wakati ni wa aina gani au tumekabiliwa na jambo la aina gani. Tukiendelea ‘kumwona’ Yehova, tutaendelea kuzitangaza “habari njema,” hata watu wengi wasipoitikia. (1 Tim. 4:10) Hata watu wakose kuitikia namna gani, sisi hatuwezi kujua watakavyofanya wakati ujao. Huenda wakabadilika. Kwa kuonyesha saburi, Yehova awapa nafasi ya kutosha wabadilike. (2 Pet. 3:9) Kama vile Musa alivyokwenda mbele ya Farao mara nyingi, je! haitupasi sisi kutembelea mara nyingi watu wasioitikia? Tutafanya hivyo tukimweka Yehova mbele yetu sikuzote, tukikumbuka kwamba jina lake lahusika.—Zab. 16:8.
21 Hata watu wakikataa kubadilika, jina la Mungu linajulishwa. Onyo la kutosha linatolewa kabla yeye hajatoa hukumu. Halafu, mwishowe kabisa, mataifa yote ‘yatapaswa kujua’ Mungu huyo ni Yehova.—Eze. 39:7.
22. Ni nini linalotukia katika sehemu nyingi za dunia, nalo hili litutie moyo tufanye nini?
22 Katika sehemu nyingi za dunia watu leo wanaliitikia Neno la Mungu kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia. (Isa. 60:8, 22) Mahali pengine watu hujia Mashahidi wa Yehova, wakitaka kufunzwa Biblia nyumbani kwao. Ikiwa wanafanya hivyo katika eneo lako, je! hilo halikuongozi kupanga mambo yako uweze kusaidia watu zaidi? Je! hilo halikutii moyo utumie wakati zaidi kutembelea watu nyumbani kwao na pia kuwasaidia zaidi kwa kujifunza nao? Kwa njia hiyo unaweza kupanua kazi yako ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Pengine hatua ya pili unayoweza kuchukua ni kufanya upainia wa muda au wa kawaida (utumishi wa wakati wote), kwa njia hiyo usaidie watu zaidi ‘wamwone’ Mungu kwa macho ya imani. Sasa kuna uhitaji mkubwa zaidi wa wafanya kazi zaidi na juhudi ya kufanya kazi ya mavuno zaidi kuliko wakati mwingine wo wote!—Luka 10:2, 3.
23, 24. (a) Eneo likimalizwa mara nyingi kunakuwa na matokeo gani? (b) Inapendekezwa tuwe na nia gani?
23 Bila kujali hali ikoje katika ujirani wako, imekupasa kujua kwamba kadiri ambavyo watu wanazidi kusikia kweli ndivyo wanavyopata nafasi zaidi ya kutwaa maarifa yatakayowapa uzima wa milele. (Yohana 17:3) Tusingetaka ulegevu wetu ufanye wengine wasipate nafasi ya kujifunza na kujua mambo mengi zaidi juu ya Mpaji wa uzima, sivyo?—Eze. 33:8, 9.
24 Kwa kuwa tunajua vile hali ya watu ilivyo mbaya, haitupasi kuwahurumia? (Mt. 9:35-38) Je! haitupasi kuwa na nia ya kujinyima wakati fulani na kujitahidi kuwasaidia wajifunze kweli juu ya Yehova?—Efe. 5:15-17.
IMARA KUJAPOKUWA NA UPINZANI
25. (a) Ni mambo gani yamepata wengi wa Mashahidi wa Yehova wa Kikristo katika sehemu mbalimbali za dunia? (b) Jambo hilo liwe na matokeo gani juu yetu?
25 Mashahidi wa Yehova katika sehemu mbalimbali za ulimwengu wamepatwa na majaribu makali; hata mara nyingi wamefikia kiasi cha kupoteza maisha zao. Tumesimulia vile Mashahidi wengi Wajeremani walivyopoteza maisha zao makumi machache ya miaka iliyopita. Hata sasa, kuna mateso makali sana sana Malawi na katika nchi nyingine za Afrika, na vilevile katika nchi kadha za Kikomunisti. Mtu akipatwa na upinzani anaweza kutiwa moyo na mifano ya waaminifu hao. Wao wamesimamia kweli na kanuni zake zenye haki kwa uthabiti! Wana ushuhuda wa kuonyesha kwamba Mungu yu pamoja nao.—Yer. 1:19; 15:20, 21.
26, 27. (a) Ni jambo gani limewapata watumishi waaminifu wa Yehova nyakati zilizopita? (b) Tunaweza kutazamia nini, na imetupasa kutendaje kwa sababu hiyo?
26 Watumishi wengi waaminifu wa Yehova wamevumilia dhihaka walizofanyiwa isivyo haki nyakati zilizopita. Kumbuka vile Ayubu alivyofanyiwa mzaha na kuchekwa kwa sababu ya kuendelea kushika ukamilifu wake. (Ayubu 12:4; 17:2) Pia, Daudi alifanyiwa mzaha na kuchekwa.—Zab. 22:7; 35:16.
27 Yeremia alidhihakiwa na kuchekwa, hata alionyesha nia ya kuacha kusema juu ya Yehova. (Yer. 20:8, 9) Lakini hakuacha. Kwa sababu gani? Kwa sababu aliufahamu ukubwa na wema wa Yehova na kutambua kwamba Yehova alikuwa naye, hata akamwokoa asiuawe na waliotaka kumwua. Basi, je! sisi pia tusitazamie baraka kama hizo tukiendelea kuwa thabiti, kama Yeremia? Je! sisi, Mashahidi wa Yehova wa kisasa, hatuchukiwi na ulimwengu kama yeye? Kwa kweli, tunaweza kufarijika kwa sababu kama jamii tumeokoka mateso na mambo ya aibu. Tunaweza kuona kabisa kwamba Yehova amesaidia watu wake wakayapita majaribu hayo. (Yer. 20:11, 13) Kwa hiyo, ungekuwa upumbavu na jambo la kutoonyesha imani namna gani kama tungeukataa ukuu wa Yehova upitao ukuu wa wote au hata kama tungepunguza bidii ya kuendeleza faida za kweli!
28. (a) Eleza jaribu lililowapata Waebrania watatu waaminifu. (b) Twaweza kupata somo gani kutokana na yaliyowapata wao na pia kutokana na maneno ya Paulo?
28 Hata tukiwa chini ya jaribu kali, hali yetu si ngumu kama ya Shadraka, Meshaki na Abednego. Hata walipotaka kutupwa ndani ya tanuru yenye moto mkali sana walisema hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme.” (Dan. 3:17) Wala hawakuachia hapo. Waliendelea kusema hivi: “Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.” (Dan 3:18) Tunaweza kufarijika sana tukijua kwamba Yehova aweza kuondoa dhara lo lote ambalo huenda Shetani akatuletea. Kwa hiyo je! kuteseka kwa muda ni nini kunapolinganishwa na uzima wa milele katika hali za ukamilifu? Maneno ambayo Paulo aliwaambia Wakorintho yanafariji sana nayo yaonyesha maoni tunayopaswa kuwa nayo: “Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”—2 Kor. 4:17, 18.
29, 30. (a) Imetupasa tufuate mfano gani wa uvumilivu? (b) Twapata mfano gani katika uaminifu wa Ayubu?
29 Mashahidi wa Yehova wenzetu wanapoonewa na kuteswa sisi tunahuzunika. Musa alihuzunika pia alipoona Waisraeli wakitendwa kikatili na Farao. (Kut. 5:22, 23) Haitupasi kutiwa hofu na mateso yanayowapata ndugu zetu, ingawa kweli tunawasikitikia wanapoteswa. (1 Kor. 12:26) Sisi pia tukipatwa na mateso kama hayo, tutafuata mfano wao wa uvumilivu, tukiwa na hakika kwamba imani yetu itashinda. Ni kama inavyosemwa katika 1 Petro 1:6, 7: “Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali; ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.”
30 Ni jambo la maana tukumbuke kwamba tukiendelea kuwa na imani tunapojaribiwa twamhakikisha Ibilisi kuwa mwongo. Ayubu alikuwa mfano mwema wa kufanya hivyo. Shetani alikuwa ametoa shtaka la kwamba angeweza kumfanya Ayubu ‘amkufuru Mungu mbele za uso wake,’ lakini Ayubu ‘alishikamana na utimilifu wake’ katika majaribu yake yote. Aliendelea kumheshimu Mungu wa kweli.—Ayubu 2:4, 5, 9, 10; tazama pia Mithali 27:11.
31. Twaweza kutazamia nini kwa imani?
31 Tunaweza kutazamia yaliyoko mbele kwa macho yetu ya imani. Twaweza kumwona Yehova akiwashinda adui zake na kukomboa watu wake katika dhiki. Alipokuwa akiwaandikia Wathesalonike, Paulo alitaja litakalowapata watenda maovu na watesi: ‘Wataadhibiwa kwa maangamizi ya milele, kutengwa na uso wa Bwana na utukufu wa nguvu zake.’—2 The. 1:9.
32. Kwa sababu gani tusiogope yale ambayo adui aweza kutuletea?
32 Tunaweza kufarijiwa sana na mifano ya imani ambayo tumewekewa katika Neno la Mungu Biblia. Kwa hiyo, hata tuwe tutapatwa na nini kwa sababu ya kuchukiwa na mataifa au serikali, tunaweza kuuthamini ubora wa kuendelea kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova ana uwezo wa kutusaidia. Hiyo yatia ndani uwezo wake wa kutulinda tunapomtumikia kwa uaminifu. Acheni tusonge mbele, basi, tuendelee kuwa thabiti, ‘kama kwamba tunamwona Mungu asiyeonekana,’ Yeye ambaye aweza kutufanya tushiriki baraka za ushindi wake mkuu.
[Picha katika ukurasa wa 344]
Musa aliunyosha mkono wake juu ya Bahari ya Shamu maji yakagawanyika, Waisraeli wakapita katika nchi kavu