Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 4/1 kur. 164-166
  • Saburi Huthawabisha Sana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Saburi Huthawabisha Sana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Zinazolingana
  • Wewe Unathamini Vile Mungu Anavyokusubiri?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Iga Subira ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Endelea Kuwa Mwenye Subira
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Je! Waweza Kuonyesha Saburi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 4/1 kur. 164-166

Saburi Huthawabisha Sana

KATIKA ulimwengu huu kuna udanganyifu, udhalimu, uonezi na hali nyingine nyingi zisizofaa. Kwa sababu hiyo, watu wengi wanachukizwa sana. Wanapokabiliwa na hali yenye kuhuzunisha, wanaelekea kuwa na harara, wakitaka faraja mara moja. Lakini mtu anatimiza nini hasa kwa kukasirika au kuwa mwenye harara?

Kwa hakika tukiudhika au kuwa na harara, hiyo haitaubadili ulimwengu wala haitaondoa kutokamilika kwa wanadamu. Maadamu taratibu hii inaendelea kuwako, kutakuwa na matata na magumu. Kwa kujiachilia tuudhiwe na mambo hayo nyakati zote, twaweza kujiumiza wenyewe. Twaweza kuhuzunika na mwishowe tuharibu afya yetu.

Mwendo wenye hekima zaidi ni kufuata shauri la mwanafunzi Mkristo Yakobo: “Vumilieni . . . Tazama, mkulima hungoja mazao ya nchi yaliyo ya thamani, huvumilia kwa ajili yake hata yatakapopata mvua ya kwanza na ya mwisho.”​—Yak. 5:7

Mkulima hawezi kunyesha mvua anayohitaji. Anaweza kupanda na kujaribu kung’oa kabisa magugu katika shamba alilolima. Lakini wasiwasi wake juu ya kunya kwa mvua hautamsaidia apate mavuno bora. Kwa kweli, wasiwasi usiofaa unaweza kumwondolea nguvu na furaha ya kufanya kazi yake. Kwa hiyo lazima mkulima aonyeshe saburi.

Watumishi wa kale wa Mungu walituwekea mfano mwema wa saburi. Baada ya mwanafunzi Yakobo kutoa mfano wa mkulima, alielekeza fikira kwenye manabii waaminifu: “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu. Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”​—Yak. 5:10, 11.

Manabii waliotumwa kwa taifa la Israeli hawakuitikiwa vizuri. Biblia yatuambia: “[Yehova] aliwashuhudia Israeli, na Yuda, kwa kinywa cha kila nabii, na cha kila mwonaji, akisema, Geukeni, na kuziacha njia zenu mbaya, mkazishike amri zangu na hukumu zangu, sawasawa na ile sheria yote niliyowaamuru baba zenu, nikawapelekea kwa kinywa cha manabii watumishi wangu. Walakini hawakutaka kusikia.” (2 Fal. 17:13, 14) Zaidi ya kutoitikiwa, wengi wa manabii walitukanwa, wakatendwa vibaya kimwili na hata wakauawa. Kwa sababu ya kumbukumbu hilo lenye aibu la kutendwa vibaya, Yesu Kristo aliweza kuutaja mji mkuu Yerusalemu kama “uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako!” (Mt. 23:37) Hata hivyo manabii hao waliendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, wakavumilia mateso kwa saburi.

Je! saburi yao iliwaletea thawabu? Ndiyo. Juu ya yote, manabii hao waliendelea kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu na wanadamu. Walifurahi kujua kwamba utumishi wao ulimpendeza Yehova Mungu. Na, ingawa sasa wamekufa, kwa maoni ya Mungu wanaishi, kwa maana yeye anakusudia kuwafufua. (Rum. 4:17) Wataona yakitimizwa juu yao wenyewe maneno aliyoambiwa nabii Danieli: “Wewe utastarehe, nawe utasimama katika kura yako mwisho wa siku hizo.”​—Dan. 12:13.

Kama vile mwanafunzi Yakobo alivyoandika, kisa cha Ayubu chaonyesha vizuri kwamba Aliye Juu Zaidi anawaonea shauku ya upendo wale wanaovumilia kwa saburi.Yehova alionyesha alimpenda Ayubu kwa kumkubali awe mtumishi wake. Yeye aliwaambia wenzi watatu wa uongo wa Ayubu hivi: “Ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu, kama alivyonena mtumishi wangu Ayubu. Basi sasa, jitwalieni ng’ombe waume saba, na kondoo waume saba, mkamwendee mtumishi wangu Ayubu, mjisongezee sadaka ya kuteketezwa; na huyo mtumishi wangu Ayubu atawaombea ninyi; kwa kuwa nitamridhia yeye [tu].”​—Ayubu 42:7, 8.

Yehova alimwonyesha Ayubu upendo na rehema pia. Kwa huruma zake Aliye Juu Zaidi aliuondoa msiba ambao alikuwa ameruhusu Shetani amletee mtu huyo mwaminifu. Na, ingawa Ayubu alishindwa kumtukuza Mungu kabisa kama yeye mwenyewe alivyokubali, alirehemiwa sana kwa sababu ya nia yake ya kutubu. (Ayubu 42:2-6) Biblia yasema hivi: “[Yehova] naye akampa Ayubu mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo kwanza. . . . Akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake.”​—Ayubu 42:10-12.

Hata ikiwa mtu hatapata thawabu kubwa kama aliyopata Ayubu, kwa sababu ya kuvumilia wakati huu wa maisha yake, hatakosa baraka ya Yehova. Bado ana tumaini la kufufuliwa apate uzima katika hali zenye haki. Kuamini kwa imara thawabu hiyo ndiko kulikowezesha wengi zamani waendelee kuwa washikamanifu wakati walipotishwa na kifo. Waebrania 11:35 yasema hivi: “Wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi [wasikubali kushindwa kwa kuacha yaliyo haki], ili wapate ufufuo ulio bora.” Kwa sababu kuna ufufuo, hakuna kitu kinachoweza kuzuia mtu asipewe thawabu ya kuvumilia kwa saburi.

Zaidi ya kuwa na hakika kwamba hali zote zisizofaa zitabadilika wakati ujao, mtu anayevumilia kwa saburi mambo yasiyopendeza anapata thawabu nyingi hata sasa. Anaendelea kuwa na dhamiri njema na ni mwenye furaha kwamba anafanya yanayompendeza Muumba. Pia, anapojizuia akasirishwapo anaweza kuzuia magomvi. Ni kama vile Mithali 15:18 isemavyo: “Mtu wa hasira huchochea ugomvi; bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.”

Lakini siri ya kuendelea kuwa na saburi unapokazwa sana ni nini? Mwanafunzi Yakobo alitokeza ulizo kama hilo kisha akatoa jibu. Aliandika hivi: “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? na aombe.”​—Yak. 5:13.

Kwa kumwomba Yehova Mungu atusadie, ‘tunamtwika mzigo wetu.’ Matokeo ya kufanya hivyo yanaelezwa na Zaburi 55:22: “Naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” Kujifunza Neno la Mungu, pamoja na kusali, kwatufahamisha sababu mambo yako yalivyo katika taratibu hii. Hiyo inatusaidia tuepuke kusumbuliwa bure na mambo yasiyoweza kubadilishwa. Tena, Yehova Mungu hutumia roho yake kutukumbusha mambo ambayo tumekwisha angalia katika Neno lake, na kutupa faraja ya kiroho tunayohitaji ili tusubiri tunapokuwa na magumu. Tatizo likizidi hata tuelekee kuwa bila tumaini, Yehova aweza kutumia roho yake iongoze wengine waje kutusaidia. Maadamu tunamtegemea, tunaweza kuwa na hakika kwamba hatatuacha kamwe tupatwe na uharibifu wa kiroho na kupoteza thawabu inayotokana na kuvumilia kwa saburi.

Kwa hiyo, acheni tuendelee kuonyesha saburi katika ulimwengu wenye uasi. Hivyo tunaweza kuendelea kuwa na dhamiri njema mbele za Mungu na wanadamu, twaweza kutuliza ugomvi, kuendelea kuwa wenye furaha hali zijapokuwa zisizopendeza na kuepuka kuharibu afya yetu kwa sababu ya kusumbukia bure mambo tusiyoweza kubadili. Halafu, tena, tunaweza kutazamia tumaini zuri sana la kupata uzima usiokoma katika hali zenye haki. Kusubiri kunathawabisha kweli kweli.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki