Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! ni afadhali mtu azihubiri habari njema kabla ya kubatizwa?
Ubatizo ni mfano wa wakf wa mtu kwa Yehova nao huonyesha kwamba tangu wakati huo mwenye kubatizwa ataendelea kumfuata Yesu kwa kufanya mapenzi ya Mungu. (Marko 8:34) Ni vizuri kukumbuka kwamba sehemu ya maana ya mapenzi ya Yehova wakati huu ni kwamba watu wa kila mahali wapewe nafasi ya kuzisikia habari njema. Mgawo wa pekee ambao Yehova amewapa mashahidi wake siku hizi ni kazi mara mbili: kwanza, kuzitangaza habari njema za ufalme wa Mungu pamoja na ujumbe wake wa hukumu kwa watu wa mataifa yote na, pili, kufundisha wale wanaoitikia vizuri, kuwafanya wanafunzi.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
Kwa kawaida, mtu anayefikiria kubatizwa apaswa kuwa amekwisha anza kufanya mapenzi ya Mungu kwa kueleza wengine habari njema, kwa njia hiyo akionyesha anataka kushiriki katika kazi hii ya mara mbili. Baada ya kujiweka wakf kwa Yehova afanye mapenzi yake, mtu atataka kubatizwa apatapo nafasi ya kwanza baada ya hapo, na hiyo yaweza kuwa juma chache au miezi kadha baadaye. Kupatana na wakf wake, ni jambo la akili kutazamia kwamba angekuwa mwenye shughuli ya kuhubiri na kufundisha, pengine amwombe mtu fulani amzoeze, angaa wakati wa kipindi kile anapongoja kubatizwa, ikiwa si kabla ya hapo.
Kulingana na maneno ya Yesu yaliyomo katika maandiko yaliyoonyeshwa juu, ‘kufanya wanafunzi’ kunatangulia ‘kuwabatiza.’ Naye mwanafunzi ni nani? Yeye si mtu anayejifunza basi. Ni mtu anayepata kuthamini na kueneza mafundisho ya mwalimu wake. Hasa aishapo kujiweka wakf kwa Mungu na kungoja abatizwe, hapaswi kusita-sita kuyaeneza. Kutangaza kweli hadharani kutakuwa sehemu kubwa ya maisha yake tangu wakati huo, kwa hiyo sababu gani asianze mara moja?
Walakini, namna gani juu ya mifano mingi iliyomo katika Maandiko juu ya watu ambao inaelekea walibatizwa kabla hawajaanza kuzihubiri habari njema juu ya Kristo? Yapaswa iangaliwe kwamba wengi wao walikuwa Wayahudi na waongofu ambao tayari walikuwa sehemu ya watu wa Yehova walio wakf, wenye wajibu wa kuwa mashahidi wake hata kabla ya kubatizwa kwao katika jina la Yesu Kristo. (Isa. 43:10-12) Sana sana, wao walikuwa wamekuwa wakimtumikia Mungu kwa juhudi, hata kabla ya kubatizwa, kulingana na ufahamu wao wa matakwa ya Mungu kwa watu wake chini ya sheria ya Musa.
Wale Wayahudi walioitikia mahubiri ya Petro katika Pentekoste, wakabatizwa, walikuwa wameonyesha juhudi kwa Mungu wao kwa kuja kutoka nchi za mbali washiriki katika karamu za Wayahudi. (Matendo 2:5, 38-41) Kama Wayahudi wengine wengi, Paulo alikuwa ameonyesha juhudi kwa Mungu, “lakini si katika maarifa” sahihi. Baada ya kubatizwa kwake, akawa mwenye juhudi nyingi sana katika kumhubiri Kristo. (Gal. 1:14; Rum. 10:2) Towashi Mwethiopia kwa wazi alikuwa mwanafunzi mwenye makini wa Maandiko ya Kiebrania, naye alikuwa amegeukia ibada ya Yehova: aliposikia “habari njema za Yesu,” alifanya haraka akatumia nafasi hiyo abatizwe na bila shaka alikuwa mwenye juhudi ile ile katika kueleza wengine habari njema tangu siku hiyo alipozifahamu. (Matendo 8:27-31, 35-39) Lidia, pengine mwongofu Myahudi, alikuwa tayari “mcha Mungu” kabla yeye na watu wa nyumba yake hawajabatizwa na Paulo, na hakuna shaka kwamba aliendelea kumtumikia Mungu kwa moyo wote, na vilevile akawa mfano bora wa ukaribishaji. (Matendo 16:14, 15) Wakati Paulo alipohubiri Korintho, Krispo, ambaye alikuwa amemtumikia Yehova akiwa “mkuu wa sinagogi,” akawa mwamini pamoja na watu wa nyumba yake naye alikuwa kati ya Wakorintho wengi waliobatizwa. Twaweza kufahamu kwamba angeendelea kutumikia kwa juhudi akiwa Mkristo.—Matendo 18:8.
Kupatana na mifano hiyo, je! mtu apaswa kuwa amekuwa akihubiri leo kabla hajabatizwa? Hakuna takwa kama hilo. Hakuna sheria zinazowekwa katika habari hii. Walakini, ili mtu abatizwe kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova anatakiwa akutane na wazee wa kundi lake aonyeshe anapozungumza nao kwamba yeye kweli afahamu na kuthamini mafundisho ya msingi katika Biblia. Maandiko yenye kuzungumza mafundisho hayo yamepangwa katika kurasa 21 mpaka 51 za kitabu Tengenezo kwa Kuhubiri Ufalme na Kufanya Wanafunzi.
Wapya wanaojitayarisha kubatizwa leo wanaweza kushiriki katika utumishi huu wenye furaha mara tu walithaminipo pendeleo hilo, mradi wamejitenga na uchafu wote wa kilimwengu. Ziko faida kutokana na kuuhubiri Ufalme mlango kwa mlango hata kabla ya ubatizo. Hiyo itawafanya wazoee kazi ya kutangaza hadharani, kuwaonyesha mambo hasa yanayohusika katika kutembelea watu wengine na habari njema. Hiyo itawaanzisha katika njia ya kukomaa Kikristo. (Ebr. 5:13–6:2; 13:15) Bila shaka ni takwa kwao wafanye tangazo hilo la hadharani tangu kubatizwa, na kwa hiyo inawafaa wajizoeze kazi hiyo hata kabla ya ubatizo.
Mifano ya Biblia ya ubatizo wa Kikristo yaonyesha kwamba waliobatizwa wakawa wateteaji wenye juhudi sana wa ufalme wa Mungu. Walihubiri kwa nguvu sana hata wapinzani wao wakasema ‘wameupindua ulimwengu’ kwa ushuhuda wao. Baada ya miaka inayopungua 30 ingeweza kusemwa kwamba “habari njema . . . zilihubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Matendo 17:6; Kol:1:23, NW) Kama walianza utumishi wao kabla au baada ya ubatizo, ‘walidhihirisha kuendelea kwao kwa watu wote’ na hivyo wakawa mfano mwema kwa wote wanaojiweka wakf leo kwa Mungu na kuuonyesha kwa kubatizwa majini.—1 Tim. 4:15, 16.
Ingawa hakuna takwa kwamba lazima mtu aanze kutangaza habari njema hadharani kabla hajabatizwa, inapendekezwa kwa nguvu kwamba wote wanaopata kuamini “habari njema tukufu” za Ufalme waanze kuzitangaza nyumba kwa nyumba bila kukawia. Imewapasa hasa wawe wakifanya hivyo tangu wanapojiweka wakf, na mpaka na baada ya ubatizo.—2 Kor. 4:4; 1 Tim. 1:11.