Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 11/1 kur. 485-491
  • Vile Unavyoweza Kutia Wengine Nguvu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vile Unavyoweza Kutia Wengine Nguvu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! WEWE WAWEZA KUTIA WENGINE NGUVU?
  • KUSHINDWA KWA PETRO
  • MASOMO TUNAVOPASWA KUJIFUNZA
  • VILE PETRO ALIVYOPATA NGUVU MPYA
  • MIFANO YA KUIGA
  • TIA NDUGU ZAKO NGUVU SASA!
  • Tianeni Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake
    Igeni Imani Yao
  • Acheni Tuishike Sana Imani Yetu Yenye Thamani!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 11/1 kur. 485-491

Vile Unavyoweza Kutia Wengine Nguvu

“Mara urudipo, watie nguvu ndugu zako.”​—⁠Luka 22:32, NW.

1, 2. (a) Kwa sababu gani kuna uhitaji wa pekee leo kusaidia wengine? (b) Watumishi wa Mungu huhuzunika na kuhitaji kutiwa nguvu wakati wo wote?

KWA hakika kuna uhitaji wa kusaidia wengine. Hakuna wakati mwingine wo wote katika historia watu wengi hivyo wamepata kuhuzunishwa na hali za kusikitisha sana ulimwenguni​—⁠maoni mabaya juu ya watu wengine yasiyo na msingi, udhalimu, kuwa na nyumba mbaya mbaya, kusongamana kwa watu, na kadhalika. Wengine wanahuzunika kwa kushindwa kupata vitu walivyotumainia, kwa sababu ya afya mbaya, kujiona wameshindwa kufanikiwa, au kuwa na shuku za kwamba wengine hawawataki.

2 Watumishi wa Mungu pia huenda wakajiona wenye huzuni bila ya wao kutazamia, na huenda wakashangaa na kuvurugika wanapokuwa hivyo. Nyakati nyingine Wakristo wameuliza hivi kwa kukata tamaa: “Sababu gani jambo hili linanipata? Nimefanya nini? Napaswa kuwa nikitia wengine nguvu, lakini siwezi kujitia nguvu mwenyewe. Nimetenda dhambi isiyosameheka? Mungu ameniacha?”

3, 4. (a) Kuna mifano gani ya watumishi wa Mungu wa nyakati zilizotangulia Ukristo waliohitaji kutiwa nguvu? (b) Kuna ushuhuda gani kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walihitaji pia kutiwa nguvu?

3 Walakini, Mkristo kama huyo asishangae sana, kama kwamba yeye peke yake ndiye hujiona hivyo. Watumishi wengine wa Mungu wamejiona ivyo hivyo, na hivyo walikuwa na uhitaji wa kutiwa nguvu. Kwa mfano, mtunga zaburi za Biblia, akiwa mwenye huzuni na kujiona ameachwa, aliandika hivi: “Nitamwambia Mungu, mwamba wangu, Kwa nini umenisahau? Kwa nini ninakwenda nikihuzunika, adui wakinionea?” (Zab. 42:9) Mke mpendwa wa Elkana, Hana, alikata tamaa sana kwa kutoweza kuzaa na kwa kuchokozwa sana na mke mpinzani hata “akalia, asile chakula.”​—1 Sam. 1:5-7.

4 Walikuwako pia Wakristo wa karne ya kwanza waliohitaji kutiwa nguvu, wakamfanya mtume Paulo alishauri kundi la Thesalonike kwa kusema: “Watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge.” (1 The. 5:14) Baada ya kufa kwa Yesu Kristo, Kleopa na mwenzake walihuzunika sana. Walipokuwa katika njia ya kwenda Emau, ‘walisimama wamekunja nyuso zao’ wakamimina habari za kukatika kwa tumaini lao, kwa maana walikuwa wametumaini kwamba Yesu atakomboa Israeli. Na ni nani asiyekumbuka vile Petro ‘alivyotoka nje akalia kwa majonzi’ baada ya kumkana Kristo mara ya tatu? Alijisikia vibaya sana kwa kuruhusu kuogopa wanadamu kumfanye akane Bwana wake.​—⁠Luka 24:13-21; 22:62.

5. Yesu alimpa Petro amri gani, na kwa sababu gani alifaa kupewa?

5 Walakini, Yesu alijua kwamba Petro angemkana, kwa sababu alikuwa na nguvu za kimungu za kutangulia kujua yatakayotukia. Kwa kweli, saa chache tu kabla, Yesu alimwambia Petro jambo hilo, kwa kusema: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isilegee; na wewe, mara urudipo, watie nguvu ndugu zako” (Luka 22:32, NW) Kwa sababu ya jambo baya sana lililompata, Petro alifahamu kabisa vile mtu huwa anapokuwa na huzuni nyingi, na anapohitaji kutiwa nguvu. Kwa hiyo, ilifaa sana kwamba Petro ndiye aliyeamriwa na Yesu hivi: “WATIE NGUVU NDUGU ZAKO”!

JE! WEWE WAWEZA KUTIA WENGINE NGUVU?

6. Kwa sababu gani yaweza kusemwa kwamba amri hii iliwafaa pia Wakristo wote wa kweli?

6 Chini ya hali hizo ni Petro ndiye aliyepewa amri hiyo na Yesu. Walakini, inawafaa Wakristo wote wa kweli. Mara kwa mara Yesu alisema na mtu mmoja au wachache tu, akiwatumia kama njia ya kutoa mafundisho yake kwa wengine. Wakati mwingine alimwambia Petro moja kwa moja hivi, “Chunga kondoo zangu wadogo.” Agizo kama hilo lilihusu mitume wengine waliokuwako, na lilirudiwa kwa wachungaji wote wa Kikristo. (1 Pet. 5:1, 2; Matendo 20:28) Na ingawa Yesu aliwapa wafuasi wake wa kwanza tu amri hii, “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,” amri hiyo yahusu Wakristo wote wa kweli.​—⁠Yohana 21:15-17; Mt. 28:19, NW.

7. Ni maulizo gani yanayotokezwa hapa?

7 Kwa hiyo ikiwa wewe wataka kufanya hivyo na una nguvu, unaweza kutia wengine nguvu. Yesu haombi wafuasi wake wafanye lo lote wasiloweza. Lakini Yesu alimaanisha nini alipotoa amri hii, “Watie nguvu ndugu zako”? Alikuwa akimaanisha nguvu gani tunazopaswa kutia ndugu zetu wa Kikristo?

8, 9. (a) Yesu alimaanisha nini kwa kuamuru “watie nguvu ndugu zako”? (b) Maneno ya kwanza ya Kigiriki yaliyotafsiriwa ‘tia nguvu’ na ‘kutia nguvu yahakikishaje hilo?

8 Yesu hakumaanisha hasa kutoa msaada wa kimwili, kama chakula, unaoweza kutia mwili nguvu. (Matendo 9:19) Sivyo, bali alimaanisha yatupasa kuwapa ndugu zetu mambo wanayohitaji watiwe nguvu akilini na kiroho. Alimaanisha tuseme au tutende kwa njia ya kuongeza matumaini ya Wakristo wenzetu, kuwafariji, kuwaimarisha au kuwasimamisha katika njia ya Kikristo. Maneno ya kwanza ya Kigiriki yanayotafsiriwa ‘tia nguvu’ au ‘kutia nguvu’ katika Biblia yana maana hiyo.

9 Kwa mfano, wakati Yesu alipomwambia Petro “watie nguvu ndugu zako,” alitumia neno la Kigiriki stērizō, nalo lina maana ya “kuimarisha kabisa, kukaza kikiki, kuthibitisha, kutegemeza, kusaidia.” Hivyo neno hilo la Kigiriki linatafsiriwa pia katika New World Translation kama ‘kuimarisha.’ (Rum. 1:11; 16:25; 2 The. 2:17; 1 Pet. 5:10) Maneno mengine ya Kigiriki yaliyotafsiriwa ‘tia nguvu’ na “kutia nguvu” katika Maandiko yana maana ya “kuburudisha, kusaidia au kuimarisha, kufariji,” kama tutakavyoona. Lakini kwanza, acheni tuone sababu gani Petro aliingia katika uhitaji wa kutiwa nguvu kiroho. Uchunguzi huo huenda ukatusaidia tusifanye makosa kama yake.

KUSHINDWA KWA PETRO

10. Petro alionyeshaje wazi kwamba alikuwa akijitumainia kupita kiasi juu ya nguvu zake za kiroho, lakini Yesu alitabiri nini?

10 Elekeza fikira zako kwenye matukio yaliyotangulia tu kukanwa kwa Kristo na Petro. Yesu alipowaambia mitume wake jioni yake ya mwisho nao kabla hajauawa, “Ninyi nyote mtachukizwa kwa ajili yangu usiku huu,” Petro alijivuna: “Wajapochukizwa wote kwa ajili yako, mimi sitachukizwa kamwe.” (Mt. 26:31-35) Kulingana na maandishi ya Luka juu ya yaliyofuata, Yesu alimwonya Petro mitume wengine wakisikia akamwambia hivi: “Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano.” Lakini Petro akadai kwa nguvu: “Bwana, niwapo pamoja nawe, mimi ni tayari kwenda gerezani au hata kifoni.” Walakini, Yesu akajibu: “Nakuambia, Petro, jogoo hatawika leo, kabla wewe hujanikana mara tatu ya kuwa hunijui.” (Luka 22:31-34) Inapendeza kuona vile maneno ya Yesu yalivyotimia usiku huo huo.

11, 12. Petro na mitume wengine walishindwa-shindwaje kumtii Yesu katika bustani ya Gethsemane?

11 Baada ya sala ndefu, Yesu na mitume wake waliondoka chumba cha orofani walikokuwa wameadhimishia sikukuu ya Kupitwa, wakatoka wakaenda bustani ya Gethsemane. (Yohana 16:33–18:1) Huko, kabla hajawaacha ili aende akasali faraghani, Yesu alimwambia Petro na mitume wake wawili wengine hivi: “Kaeni hapa mkeshe.” Walifanya hivyo? Maandishi ya Biblia yasema: “Akaja akawakuta wamelala usingizi.” Ndipo Yesu akamgeukia Petro akasema: “Je! Simoni, umelala? Hukuweza kukesha saa moja? Kesheni muombe, msije mkaingia majaribuni.”​—⁠Marko 14:32-38.

12 Je! Petro na mitume wengine walitii? Maandishi ya Biblia yaendelea kusema: “Akaenda zake tena, akaomba, akisema neno lilo hilo. Akaja tena akawakuta wamelala.” Hawakusikiliza! Kabla hajaenda akasali tena, bila shaka Yesu aliwatia moyo kwa haraka zaidi wakeshe na kusali. Walakini, Yesu “akaja mara ya tatu, akawaambia, [Wakati kama huu mnalala na kupumzika!] yatosha, saa imekuja; tazama, Mwana wa Adamu anatiwa mikononi mwao wenye dhambi.”​—⁠Marko 14:39-41.

13. (a) Yesu alipokamatwa akapelekwa, Petro alifanya nini? (b) Ni chini ya hali gani Petro alimkana Kristo, na Petro alijionaje baadaye juu ya alilotenda?

13 Muda mfupi baadaye, Petro alijionyesha kuwa ameamka kweli kweli. Alichomoa upanga, akakata sikio la Malko mtumwa wa kuhani mkuu, aliyekuwa pamoja na waliokuja kumkamata Yesu. (Yohana 18:10, 11) Yesu alikamatwa akapelekwa, mitume wakakimbia. Walakini, Petro alifuata kwa mbali, yaelekea akiwa na woga wa kuuawa mwenyewe na vilevile akitaka sana kujua litakalompata Yesu. Wakafika makao ya kuhani mkuu, naye Petro akakana mara tatu kwamba hata hamjui Yesu, akiwa katika ua wa makao hayo, hata akataka yeye mwenyewe alaaniwe au aadhibiwe ikiwa alimjua Yesu. Papo hapo jogoo akawika, Yesu akageuka akamtazama Petro, naye akatoka nje akalia kilio kichungu.​—⁠Luka 22:47-62; Marko 14:71, 72, The Jerusalem Bible.

MASOMO TUNAVOPASWA KUJIFUNZA

14. (a) Ni onyo gani la Biblia linakaziwa na kushindwa kwa Petro, likikazia somo gani? (b) Tuna ushuhuda gani kwamba Petro alijifunza somo?

14 Petro alikuwa amekuwa na hakika sana kwamba ana nguvu za kiroho, hata hivyo alianguka, akashindwa kuendelea katika mwendo mwaminifu wa Kikristo. Jambo hilo lakazia sana ubora wa onyo hili: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Kor. 10:12) Naam, somo tunalopaswa sote kujifunza hapa ni kwamba hakuna ye yote kati yetu apaswaye wakati wo wote kujitumainia kupita kiasi juu ya nguvu zake za kiroho, akidhani kwamba hawezi kuanguka. Twaweza kuanguka. Petro alijifunza hivyo, na kwa hiyo baadaye aliandikia Wakristo wenzake hivi: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”​—1 Pet. 5:8.

15. (a) Yatupasa sote tujifunze somo gani jingine kutokana na jambo hili? (b) Chanzo kikuu cha msaada wa kutia nguvu ni nini?

15 Somo jingine tunalopaswa kujifunza kutokana na yaliyotukia usiku huo ni kwamba sote twahitaji msaada wa kututia nguvu. Wakati Yesu alipokuwa katika bustani ya Gethsemane, alijitahidi kutoa msaada huo uliohitajiwa kwa kusihi wanafunzi wake wasali. Wao hasa waliuhitaji msaada ambao Mungu aweza kutoa. Kama mtume Paulo alivyosema, Mungu ‘aweza kuwafanya imara,’ yaani, aweza kututia nguvu au kutusimamisha imara tushinde mikazo yo yote. (Rum. 16:25) Hata Yesu Kristo alihitaji kutiwa nguvu hivyo, kama inavyoonyeshwa na lililotukia huko katika bustani wakati mitume walipokuwa wamelala.

16, 17. (a) Ilikuwaje Yesu alipokuwa akisali kwa Mungu katika bustani? (b) Kwa wazi malaika alimtiaje Yesu nguvu?

16 Yesu mwenyewe, kama tulivyoona, alikuwa akisali. Masimulizi ya Biblia yasema kwamba “akapiga magoti, akaomba, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea AKAMTIA NGUVU [eniskhúō]:, (Luka 22:41-43) Naam, Yehova Mungu alitoa msaada wa kimalaika huko katika bustani wakati huo wa hatari katika maisha ya Yesu!

17 Kwa wazi malaika alisema na Yesu, akampa habari zilizomtia nguvu, zikamtia nguvu mpya. Hiyo yaonyeshwa na neno la Kigiriki eniskhúō lililotafsiriwa hapa ‘akamtia nguvu.’ Mahali pengine pa pekee linapoonekana katika Biblia ni Matendo 9:19, na mtume Paulo asemekana kuwa “akapata nguvu” kwa kula chakula. Lakini Yesu, kwa upande mwingine, alitiwa nguvu, si na chakula cha kimwili, bali na kuwapo kwa malaika, na bila shaka na maneno ya malaika yenye kutia moyo. Walakini, mitume walikuwa wamelala, na hivyo hawakuwa katika hali ya kutiwa nguvu hivyo.

18. (a) Twahitaji nini ndiyo tuwe na nguvu za kiroho, nasi twaweza kuzipata wapi? (b) Mengine ya maulizo mazuri ya kujiuliza ni nini?

18 Namna gani wewe? Je! uko macho kupokea misaada ya kiroho ya kukutia nguvu? Kumbuka, Biblia yasema: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mt. 4:4) Maneno hayo ya Mungu yenye kutia nguvu kwa kawaida hayatolewi kupitia kwa malaika, kama yalivyotolewa kwa Yesu. Bali, yanapatikana katika Neno la Mungu Biblia, ambalo hurudiwa kwa kawaida na kuzungumzwa katika mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Je! wewe huwa macho na husikiliza unapokuwa katika mikutano hiyo? Nyakati hizo wewe hupokea nguvu za kiroho unazohitaji kutokana na yanayosemwa? Uzima wetu wenyewe wategemea nguvu tunazotoa katika chakula hiki cha kiroho.

VILE PETRO ALIVYOPATA NGUVU MPYA

19, 20. (a) Kwa makano yake, Petro alijitia katika hali gani? (b) Yesu alichukua hatua gani amrudishe Petro?

19 Kwa makano yake ya kurudia-rudia, Petro hakumwacha Yesu tu, bali na Yehova Mungu pia. Lakini Yesu alikuwa na hakika kwamba Petro angerudi. Alijua kwamba kwa kawaida Petro alikuwa na moyo mwema, lakini alikuwa ameshindwa kwa sababu ya kuogopa wanadamu tu. Kwa hiyo Yesu alifanya nini? Je! alimtazamia Petro ajirudishe mwenyewe, bila msaada wo wote au kutiwa moyo?

20 Hapana, Yesu alijitahidi alivyoweza akamsaidia Petro. Kwanza, aliomba dua kwa ajili ya Petro, akasali kwamba imani yake isimalizike kabisa. (Luka 22:32) Lakini zaidi ya hilo, muda fulani baada ya ufufuo wake Yesu alimtokea Petro kwa njia ya pekee, wanafunzi wakaripoti kwa furaha nyingi hivi: “Bwana amefufuka kweli kweli, naye amemtokea Simoni.” (Luka 24:34) Kutokana na aliyosema mtume Paulo pia, kwa wazi hiyo ni mojawapo ya mara za kwanza Yesu alipoonekana baada ya kufufuliwa. (1 Kor. 15:4-8) Kwa sababu gani Yesu alimfikiria Petro hivyo kwa njia ya pekee, mtu aliyekuwa amemkana kwa ukali hivyo?

21. (a) Kusudi la Yesu kumfikiria Petro kwa njia ya pekee lilikuwa nini? (b) Hilo lapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

21 Kusudi lilikuwa kumtia nguvu, kumhakikishia Petro kwamba alimpenda bado na alimtaka awe mwanafunzi wake. Je! hatuvutwi na rehema hiyo aliyoonyeshwa Petro? Tendo la Yesu latukumbusha habari ya baba ya mwana mpotevu, aliyemkubali mwana wake mwenye kutubu kwa mikono mikunjufu. (Luka 15:11-32) Wadhani tendo la Yesu lilikuwa na matokeo gani juu ya Petro? Wewe ungalionaje? Petro alitiwa nguvu; alipata nguvu zaidi za kiroho kuliko alizopata kuwa nazo. Alirudi. Na wakumbuka Yesu alitaka Petro mwenye kurudi, na vilevile sisi sote, afanye nini? “WATIE NGUVU NDUGU ZAKO,” Yesu alisema. Ndiyo kusema, saidia kwa imara kuwathibitisha au kuwasimamisha katika imani. Twawezaje kufanya hivyo?

MIFANO YA KUIGA

22. Twawezaje kutia ndugu zetu nguvu kwa njia bora?

22 Njia bora ni kufuata mfano wa Yesu, kuiga vile alivyotendea Petro na wengine waliohitaji kutiwa nguvu. Na kama tuwezavyo kuona, Yesu alikuwa mwenye kurehemu na kusamehe. Twaweza kutia ndugu zetu nguvu, kuwakaza kikiki katika imani, kwa kuwatendea ivyo hivyo. Yatupasa kutii shauri la Biblia: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”​—⁠Efe. 4:32.

23. (a) Yawapasa wazee hasa waangalie nini katika mfano wa Yesu? (b) Wazee wanawezaje kuonyesha wanaiga mfano wa Yesu?

23 Hasa wazee katika kundi la Kikristo wana daraka la kuwapa ndugu zao msaada wenye kutia nguvu, na kwa hiyo yawapasa wachunguze kwa uangalifu mfano wa Yesu. Yeye alikuwa tofauti kabisa na Mafarisayo wa kidini ‘waliofunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao.’ Yesu alisema, “Nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 23:4; 11:28, 30) Kwa hiyo, wazee, mwigeni yeye kwa kutowafunga ndugu zenu na sheria za maoni yenu wenyewe juu ya mambo, zinazoweza kuwa kama “mizigo mizito” ya kuwalegeza. Badala yake, sitawisheni ndani ya ndugu zenu kumthamini sana Yehova ili wavutwe na moyo kutaka kumpendeza Yeye. Hilo ndilo litakalowakaza kikiki katika imani.

24. (a) Petro alitiaje ndugu zake nguvu? (b) Wakristo wengine walitiaje ndugu zao nguvu?

24 Petro alifaulu kutia ndugu zake nguvu. Kama hivi, mfano wake mwema wa ujasiri na ushujaa katika kuhubiri kujapokuwa na dhihaka na upinzani uliwatia moyo. (Matendo 2:14–5:42) Barua zake zenye kujenga zilitia nguvu pia, na ya kwanza iliandikwa “kutia moyo”! (1 Pet. 5:12) Wazee wengine wa karne ya kwanza walitia ndugu zao nguvu pia kwa kuwatia moyo, nayo Biblia yasema juu ya Paulo na Barnaba hivi: “Wakarudi Listra na Ikonio na Antiokia, wakitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo wabaki katika imani.” Vilevile, Yuda na Sila “wakatia ndugu moyo kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.” Baadaye Paulo “alipitia Shamu na Kilikia, akitia nguvu makundi.”​—⁠Matendo 14:21, 22; 15:32, 41, NW.

25. (a) Maneno haya ‘kutiwa nguvu’ na ‘kutia nguvu’ yana maana gani? (b) Kwa hiyo wazee wa kisasa wanawezaje kutia ndugu zao nguvu?

25 Neno la Kigiriki epistērizō (namna iliyopanuliwa ya stērizō) lililotafsiriwa ‘kutiwa nguvu’ na ‘kutia nguvu’ hapa katika Matendo lina maana ya kuimarisha au kusaidia. The Bible in Living English ya Steven Byington yatafsiri Matendo 14:22 hivi: “Wakiimarisha nafsi za waongofu.” The Jerusalem Bible yasema: “Wakatia moyo mpya katika wanafunzi.” Ninyi wazee mwapaswa kuiga mfano huu. Kwa kuweka mfano wa kuwa na juhudi katika utumishi wa shambani, kwa kuonyesha ushujaa wakati wa upinzani, kwa kutia moyo na kwa hotuba zenu za kuchochea, mtaimarisha ndugu zenu, mkiwatia moyo mpya na kuwathibitisha katika imani.

26. Kila mshiriki wa kundi la Kikristo awezaje kutia nguvu ndugu zake?

26 Lakini si wazee tu wanaopaswa kutia ndugu zao nguvu. Kila Mkristo apaswa kujitahidi kufanya ivyo hivyo. Wewe wawezaje? Hasa kwa kuweka mfano mwema wa kutii matakwa ya Yehova; kwa mfano, kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa kawaida. Uwapo mikutanoni, tabasamu la kirafiki au salamu ya uchangamfu yaweza kutia nguvu ndugu mwenye huzuni. Majibu yako wakati wa mikutano ya kundi yaweza kujenga wengine sana. Ukiyatoa kwa moyo, hata ujisikie unatoa madogo namna gani, yanaweza kugusa mioyo ya ndugu zako, kuwatia nguvu. (Ebr. 10:23-25) Vilevile, kwa kuwa mwenye bidii kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu kujapokuwa na vizuizi kama hali mbaya ya hewa au magonjwa ya kimwili, unaweza kutia wengine moyo waige mfano wako mwema.

27. Wenzi watatu wa Paulo walikuwaje msaada wa kumtia nguvu, kama inavyoonyeshwa na neno la Kigiriki lililotumiwa hapa?

27 Hata wale walio imara katika imani wanaweza kuhitaji kutiwa nguvu, kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu mwenyewe. (Luka 22:43) Twaweza kufuata mfano wa Aristarko, Yusto na Marko kwa kutoa msaada huo. Mtume Paulo, aliyekuwa gerezani Rumi, aliandika hivi juu yao: “Watu hawa hawa wamekuwa msaada wa kunitia nguvu.” (Kol. 4:10, 11, NW) Naam, walimsaidia Paulo kweli kweli. Kwa njia gani? Neno la Kigiriki paregoria, lililotafsiriwa hapa ‘msaada wa kutia nguvu,’ lamaanisha kutuliza au kufariji. “Kiarifa cha neno hilo chamaanisha dawa zinazomaliza kuwasha,” yasema kamusi An Expository Dictionary of the New Testament Words ya W. E. Vine. Kwa hiyo kwa kushikamana na Paulo, kwa kumfariji na kumtia moyo, wanaume hawa walikuwa msaada wa kumtia nguvu.

28. Kulingana na mfano huu wa Biblia, twawezaje kutia ndugu zetu nguvu?

28 Vivyo hivyo leo, kwa kufariji wale walio na huzuni au wanaojaribiwa, utakuwa msaada wa kuwatia nguvu. Utawajenga kwa kuwajulisha unawajali, unawapenda. Mara nyingi mtu huhitaji mwingine wa kusema naye, rafiki wa kumiminia mambo yanayomsikitisha. Hivyo kwa kuwa msikilizaji mwenye huruma waweza kutia ndugu zako nguvu. Kwa kuwa kila mtu aweza kufaidika kwa kutiwa moyo, je! isingekuwa vizuri tuwe tukijiuliza hivi: “Leo naweza kukumbuka kutendea mtu fulani angaa jambo moja la upendo​—⁠pengine kumwambia neno la fadhili, kutoa wazo la huruma kwa mtu fulani aliyeudhika, mwenye huzuni au anayehitaji kutiwa moyo?” Naam, ni jambo la maana sana tufanye kama Biblia isemavyo, “Farijianeni na kujengana kila mtu na mwenzako.”‏​—1 The. 5:11.

TIA NDUGU ZAKO NGUVU SASA!

29. Kwa sababu gani hasa sasa ni lazima tutie ndugu zetu nguvu?

29 Ni lazima hasa sasa tufikirie kutiana nguvu. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kama vile katika karne ya kwanza Petro na mitume wengine walivyopatwa na majaribu makali, sisi leo huenda pia tukapatwa na majaribu makubwa zaidi ya imani yetu kadiri tukaribiavyo zaidi mwisho wa taratibu hii ya mambo. Hivyo ni jambo la maana zaidi sasa kuliko nyakati zote tutolee ndugu zetu msaada wa kuwatia nguvu, nao pia watufanyie hivyo. Basi, wakumbuke wale wanaofanya vema kundini kujenga na kutia wengine nguvu, na ufuate mfano wao. Lakini hasa, ufikirie mfano wa Yehova Mungu na Mwanawe.

30, 31. (a) Yehova Mungu na Mwanawe wanawekaje mifano myema ya kutia wengine nguvu? (b) Uamuzi wako umepaswa kuwa kufanya nini, nawe waweza kutazamia nini?

30 Linalotokeza tunapofikiria mifano yao ni vile upendo usio wa kichoyo unavyoweza kutia wengine nguvu. Na angalia vile Mungu anavyochukua hatua ya kwanza kuonyesha upendo wake. Kwa kweli, Biblia yasema: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Rum. 5:8) Naam, tulipokuwa bado tukifanya machukizo juu ya Mungu, pengine hata tukikana kuwako kwake na kuvunja sheria zake bila kujali, Mungu alitupenda akatufanyia mpango wa kufurahia uzima wa milele. (Yohana 3:16) Naye Mwanawe hutendea wanadamu namna iyo hiyo. Kwa mfano, hata wakati Petro alipokuwa akimkana, Yesu hakuacha kumpenda Petro. Baadaye, kama tulivyoona, alimtokea yeye kwa njia ya pekee baada ya kufufuliwa, na hiyo ilimhakikishia alimpenda.

31 Kwa hiyo basi, na uwe kama Yehova Mungu na Mwanawe. Watie nguvu ndugu zako. Wapende sana sana kwa moyo. Chukua hatua ya kwanza kufanya hivyo. Ukifanya hivyo, nawe pia utapendwa na kutiwa nguvu nao. Litakuwa jambo zuri namna gani!

[Picha katika ukurasa wa 486]

Amri ya Yesu “watie nguvu ndugu zako” ilikusudiwa kwa Wakristo wote. Wewe hutia wengine nguvu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki