Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Wengine wa Wakristo waliotiwa mafuta wakiokoka waingie katika Taratibu Mpya, watakuwa wazee kisha wafe, au maisha yao ya kidunia yatakwishaje?
Kwa wazi, Biblia haisemi. Vyo vyote itakavyokuwa maisha ya kidunia ya Wakristo hawa waliotiwa mafuta kwa roho yatapaswa kumalizika ili waweze kupokea thawabu yao ya uzima mbinguni.—1 Kor. 15:35-38.
Mfano wa Yesu wa ngano na magugu waonyesha kwamba “wana wa ufalme” wengine watakuwa hai duniani wakati wa ‘mwisho wa taratibu ya mambo.’ (Mt. 13:24-30, 37-43, NW) Vilevile, vielelezo vingine vya Biblia vyaonyesha kwamba huenda wengine wa watiwa mafuta hawa wakaokoka “dhiki kubwa” yenye uharibifu. (Mt. 24:21) Angalia vichache vya vielelezo hivyo.
Ezekieli sura ya 9 yaeleza “mtu” mwenye kidau cha wino cha katibu aliyepaswa ‘kutia alama’ watu mmoja mmoja ambao wangeokoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Inafahamika kwamba hiyo inafananisha wakati wetu kazi ya kutia alama ambayo jamii nzima ya “wana wa ufalme” waliotiwa mafuta inaongoza kufanya. Masimulizi ya Ezekieli yaonyesha kwamba “mtu” aliyemaliza kutia alama alimletea Yehova ripoti baada ya kazi ya kuua kufanywa Yerusalemu. Hiyo yaonyesha kwamba wengine wa jamii ya waliotiwa mafuta wataiokoka kazi ya kuua itakayofanywa juu ya kizazi hiki, wakiwa duniani. (Eze. 9:4, 8,11) Wonyesho mwingine unaohusiana na huu ni kwamba nabii Ezekieli mwenyewe aliendelea kuishi Babeli baada ya uharibifu wa Yerusalemu wa kale.
Tena, mke wa Nuhu (anayefananisha jamii ya waliotiwa mafuta walioposwa na Nuhu Mkuu, Yesu) aliokoka gharika. (Mt. 24:37-42; Efe. 5:25-30) Mfikirie pia Elisha, aliyeishi baada ya kazi ya kuharibu iliyofanywa na Yehu, kama mabaki ya waliotiwa mafuta leo wanaotumaini kuiokoka kazi ya kuharibu ya Yehu Mkuu, Yesu Kristo. (Tazama “New Heavens and a New Earth,” kurasa 95 na 321, na “Let Your Name Be Sanctified,” kurasa 351-365.) Kwa hiyo, mabaki ya Wakristo waliotiwa mafuta huenda wakaishi duniani baada ya mwisho wa taratibu hii mbovu ya mambo ili wamalize kazi yao ya kuhubiri na kufundisha kizazi cha duniani, pengine hata wengine wa watakaofufuliwa.—Zab. 71:18; 91:16.
Ikiwa ufahamu huu ni wa kweli, Wakristo waliotiwa mafuta watakaokuwa duniani katika Taratibu Mpya watapaswa kufikia mwisho wa maisha yao ya kidunia wakachukue mahali pao katika ‘ufalme wa mbinguni.’—2 Tim. 4:18.
Wakristo wengi wanaona kwamba haielekei kuwa watiwa mafuta hao watakaokuwa katika Taratibu Mpya wataendelea kuzeeka kisha wafe mwishowe kama watu wengi leo. Wanaowaza hivyo wanaona isingekuwa sawa jambo hilo kuwapata ndugu za kiroho wa Kristo kwa sababu wakati huo wanadamu wenye kuokoka watakuwa wakisonga mbele wakafikie ukamilifu wa kimwili. Kwa hiyo wametaka kujua kama Mungu atamaliza maisha za kidunia za watiwa mafuta kwa mwujiza, kama alivyofanyia Henoko hata Henoko akakosa kupatwa na maumivu yo yote ya kifo. (Mwa. 5:24; Ebr. 11:5) Bila shaka, Mungu aweza kufanya hivyo. Lakini Maandiko hayasemi waziwazi kwamba ndivyo itakavyokuwa. Wala Biblia haionyeshi jibu jingine lo lote la ulizo hilo.
Kwa hiyo, lazima tumtumaini Mungu. Hakuna sababu ya kufikiri-fikiri juu ya hili na lile. Kama Yehova angaliona habari hizo ni za lazima, bila shaka angaliweza kuwa amezitia katika Neno lake. Lakini hakufanya hivyo. Wakati wo wote na vyo vyote watiwa mafuta watakavyomaliza maisha yao ya kidunia, watafufuliwa papo hapo wakiwa na mwili usiokufa wa kiroho. Huo utakuwa ushindi juu ya mauti. (1 Kor. 15:51-57) Hivyo wataweza kuungana na wengine wa “bibi-arusi” wa Kristo, watakaokuwa wakitawala naye katika utawala wake wa miaka elfu moja.—Ufu. 20:6.