Ubora Uliojaribiwa wa Imani Waleta Uvumilivu
“Ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu waleta uvumilivu.”—Yak. 1:3, NW.
1. Imani ni nini, kama inavyoelezwa katika Biblia?
IMANI ni nini? Ufafanuzi unaofaa zaidi unapatikana katika kitabu cha Biblia cha Waebrania. Twasoma: “Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana.”—Ebr. 11:1.
2, 3. (a) Nguvu ya usemi huu “hakika ya mambo” katika kueleza maana ya imani ni nini? (b) Imani ni “bayana ya mambo yasiyoonekana” namna gani?
2 Usemi “hakika ya mambo” yatarajiwayo umetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki linalomaanisha msingi, tegemezo, tumaini hakika, na uhalisi pia, uthabiti, kwa kutofautishwa na jambo lisilo halisi au la kuwazia tu.
3 Yesu alimwambia mwanamke Msamaria hivi: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli,” si kulingana na hadithi za uongo wala maoni ya kuwazia tu. (Yohana 4:24) Mwandikaji wa barua kwa Waebrania aliendelea pia kusema kwamba imani ni “bayana ya mambo yasiyoonekana.” Basi, imani hufanya mtu atende kama kwamba mambo yasiyoonekana ni halisi, kama kwamba ameyaona. Sababu ni kwamba mambo hayo ni halisi kabisa, naye mtu mwenye imani ya kweli ajua hivyo, ingawa mambo hayo hayaonekani wakati huo. Ile ambayo huenda ikaitwa “imani” lakini isiyo na msingi wa mambo halisi si imani, bali ni ujinga.—Linganisha Waebrania 11:27.
4. Toa mfano wa namna imani ilivyo kwa kutumia mambo ya kila siku.
4 Kwa mfano, wewe unaamini kwamba miji fulani kama Moscow na Peking iko, ingawa pengine hujapata kuwa huko. Huenda ikawa hata hujaona picha ya miji hiyo. Lakini umesikia na ukasoma habari za miji hiyo na ukaona ilipo katika ramani. Kwa sababu ya imara ya imani yako, isiyotegemea dhana au maoni ya kuwazia tu, usingesita kupanda ndege ufikie mmoja wa miji hiyo ukiona ni lazima ufunge safari hiyo. Ungekuwa na hakika kwamba tumaini lako la kuuona mji huo litatimizwa ndege ituapo. Au, ikiwa una rafiki mpendwa ambaye hajapata kukudanganya, unaamini anayokuambia nawe utayafanya kama mambo halisi, isipokuwa kama anayosema yanatofautiana kabisa na mambo ya hakika na vilevile kama yanatofautiana na utu wake, ambao wewe waujua sana. Wewe una mifano mingi ya nyakati zilizotangulia alipokuambia kweli, na hivyo una msingi wa kuamini.
5. Mwandikaji wa Biblia anaposema imani ni “bayana ya mambo yasiyoonekana,” anaonyesha nini juu ya imani?
5 Anapoonyesha wazi zaidi imani ni nini, mtume atumia neno la Kigiriki la “karipio” au “kukaripia,” lililotafsiriwa na watafsiri mbalimbali kama “wonyesho wa wazi,” “kusadiki,” ‘kuhakikisha,’ na kadha wa kadha. (Ebr. 11:1; 2 Tim. 3:16; Kingdom Interlinear, Diaglott, New English Bible) Tunapokaripia mtu tunachunguza jambo sana sana, tukiliangalia kila upande. Tunatokeza mambo ya hakika na sababu zenye nguvu kuhusu habari hiyo na kuihakikisha, hata msikiaji anasadikishwa kabisa na ushuhuda huo thabiti. Kwa hiyo, lazima msingi wa imani uwe ushuhuda wenye kusadikisha. Mtu akijisikia tu ana imani, hiyo si imani. Lazima imani iwe na mambo ya hakika, lazima mtu awe aliona mambo zamani au ushuhuda usiopingwa ndipo awe na tumaini hakika. Halafu mambo anayoamini au anayotumainia hayatamkatisha tamaa.—Linganisha Warumi 9:33; 10:11.
IMANI YATAKA USHUHUDA THABITI
6, 7. Ni “mashahidi” gani wawili, ndiyo, watatu wanaothibitisha kuwa na imani ya kwamba kuna Mungu?
6 Ili kuamini kitu kisichoonekana lazima tuwe na ushuhuda kutoka vyanzo vyenye kutegemeka. Tunaamini Mungu Muumba yuko kwa sababu tunashuhudia uumbaji—ambao ni wa ajabu mno wanadamu dhaifu wasiweze kuuelewa kabisa. Twaona uhai duniani, pamoja na viumbe vyenye kutegemeana, vinavyohitajiana kabisa. Halafu tuna Biblia, inayotuambia Mungu aliumba vitu hivyo, na kusudi lake lilikuwa nini. Kwa hiyo tunao ushuhuda wa viumbe vyenyewe, na Neno la Mungu lililonenwa kupitia kwa watu wengi wenye ukamilifu na uaminifu, si kupitia kwa mmoja tu.—Rum. 1:19, 20; Matendo 4:24.
7 Tunao pia uwezo wa kutumia akili zetu wenyewe, unaotuonyesha kwamba bila shaka Muumba hawezi kujulikana kabisa na wale alioumba. Tunapotazama anga kubwa sana la ulimwengu wote tunamoishi, tunaweza kufahamu sehemu ndogo sana yake. Je! Muumba wake asiwe mbali zaidi, hata tusiweze kumwona? Nabii Isaya ahakikisha hilo akisema: “Ni nani aliyeyapima maji kwa konzi ya mkono wake, na kuzikadiri mbingu kwa shubiri, na kuyashika mavumbi ya dunia katika pishi, na kuipima milima kwa uzani, na vilima kama kwa mizani?” “Mtamlinganisha Mungu na nani? au mtamfananisha na mfano wa namna gani?”—Isa. 40:12, 18.
8. Mungu kwa fadhili alimpa Ibrahimu sababu mbili zenye nguvu au ushuhuda wa kuwa na imani katika ufufuo namna gani?
8 Wakati imani ya Ibrahimu ilipojaribiwa juu ya kumtoa mwanawe Isaka awe dhabihu, Ibrahimu alikuwa na sababu zisizopungua mbili za kuamini kwamba Mungu angemfufua Isaka. Alikuwa ameahidiwa na Mungu kwamba kupitia kwa Isaka taifa kubwa lingetokea, na sababu hiyo ilitosha. Lakini alijua pia kwamba alikuwa amepewa Isaka kwa mwujiza, wakati nguvu za Ibrahimu na Sara zilipofanyizwa upya. Kazi hiyo ya Mungu ilikuwa mwujiza mkubwa ulio sawa na ufufuo. Kwa sababu hizo, na kwa sababu Mungu alishikamana na Ibrahimu na alimpenda, Ibrahimu aliamini kwamba Mungu angemfufua Isaka wake mpendwa.—Rum. 4:17-21; Ebr. 11:17-19.
ROHO YA MUNGU NI YA LAZIMA ILI TUWE NA IMANI YA KWELI
9, 10. (a) Hata ijapokuwa kuna ushuhuda wa imani, ushuhuda huu unaonekana namna gani kwa mtu asiye na imani? (b) Mungu anataka watu wake wawe na imani ya namna gani? (c) Zaburi 27:1-3 inaonyesha namna gani imani hii? (d) Maneno ya Yesu katika Mathayo 13:11-15 yalionyesha namna gani sababu “si [watu] wote walio na imani” kama inavyoelezwa katika 2 Wathesalonike 3:2?
9 Sehemu moja ya imani katika mambo yanayohusu Mungu, yaani, ahadi zake, mambo ya hakika yanayotimiza unabii wake, na kadhalika, ni kwamba mtu asiyemjua Mungu huenda akaona mambo ya hakika juujuu na kudhani yanatofautiana au yanapingana na imani ya Mkristo wa kweli. Hiyo ni kwa sababu Mungu ataka watu wake wamwamini, kama vile mwana anavyoamini baba mwema, na kuhakikisha imani yao, ingawa mambo ambayo Mungu ameahidi yaonekana yako mbali na kutimizwa au hayawezi kutimizwa kulingana na maoni ya kibinadamu tu. Yeye hataki kuwa na waabudu ambao lazima waone kila kitu ndipo waamini. Angalia kwamba mara nyingi Yesu alitoa mifano aliyoeleza baadaye kwa wale waliopendezwa naye na kumwamini kutosha kiasi cha kumwuliza. Lakini wale wasiokuwa na mioyo minyofu, ya kuchunguza, yaani wale wasioamini sana, walienda zao bila kufahamu na bila imani. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi:
10 “Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa maana ye yote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini ye yote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mifano; kwa kuwa wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema.” (Mt. 13:11-15) Na hali, Wayahudi walizungukwa na ushuhuda mwingi kwamba Masihi alikuwa amefika.
11, 12. Toa mfano wa “bayana ya mambo yasiyoonekana” ambayo ulimwengu wote umefichwa.
11 Leo, msomaji wa Biblia amezungukwa na matukio yanayoonyesha kwamba ufalme wa Kimasihi umekaribia. Lakini wenye kuutumaini ulimwengu huu wanadhani mambo yataendelea kama yalivyo kwa wakati usiojulikana. Yesu alipokuwa duniani ndivyo hali ilivyokuwa, ingawa mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi ungefika baada ya miaka michache tu. Yesu aliwaambia:
12 “Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo. Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo. Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?”—Luka 12:54-56.
13. 1 Wakorintho 2:12-14 linafunua namna gani sababu mtu wa kimwili hawezi kuona mambo yaliyo waziwazi sana kwa Mkristo?
13 Huenda mtu akasema, Mbona msingi wa imani ni ushuhuda thabiti hivyo, hata watu wengine hawawezi kuona mambo kama Mkristo ayaonavyo? Mtume aeleza hivi: “Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali [roho itokayo] kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu. . . . Basi mwanadamu wa tabia ya asili [mwenye kuwaza mambo ya kimwili, NW] hayapokei mambo ya [roho ya Mungu]; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi [ya kiroho].”—1 Kor. 2:12-14.
14. Toa mfano wa kuonyesha sababu gani wale wasio na imani wanaeleza mambo ya hakika katika njia isiyo ya kweli.
14 Kwa mfano, dini nyingi sana zinaamini kwamba mtu afapo, hasa ikiwa ni kitoto, ‘Ameitwa na Mungu.’ Twasikia lalamiko hili, ‘Kwa sababu gani Mungu ameita mtoto wangu (au, mume wangu)?’ Juujuu huenda ikaonekana kwamba kila jambo linalotukia linaongozwa na Mungu, kwa sababu yeye ni mwenye nguvu zote. Walakini, watu hao hawafahamu kwamba Adamu ndiye aliyeingiza kifo katika jamaa yake alipomwasi Mungu na kupotezea wazao wake uzima, wala si Mungu aliyeingiza kifo. (Rum. 5:12) Wanakosa kufahamu kwamba Shetani Ibilisi alilaumu enzi kuu ya Mungu baadaye, akasema hakuna mtu angeendeleza ukamilifu kwa Mungu akijaribiwa. (Ayubu 2:4, 5) Hawafahamu kwamba Mungu ameruhusu kuwe na uovu na huzuni kwa muda mfupi kwa sababu ya suala hilo. Hawajui kwamba wafu wamepumzika kaburini, wakingojea kufufuliwa kupitia kwa Yesu Kristo, na huo ni mpango wa Mungu wenye rehema. (Yohana 11:11-14, 24) Lakini, hasa, wao hawaujui utu wa Mungu, hawajui kwamba yeye hawezi kamwe kuwa mkatili na mchoyo hivyo hata ‘aite’ mtu anayehitajiwa na mkewe au wazazi wake.—Kut. 34:6, 7.
SABABU IMANI YENYE NGUVU NA YENYE KUDUMU INATAKIWA
15. Kupotea au udhaifu wa imani ni “dhambi ile ituzingayo kwa upesi” namna gani?
15 Kwa sababu ukamilifu wa Mkristo na mwendo wake unategemea imani, na kwa sababu kupotoka kwa njia yo yote kutoka mwendo unaofaa kwaonyesha imani yake ni dhaifu, mtume aendeleza mazungumzo yake ya imani, akitoa mifano, na kusema hivi: “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” (Ebr. 12:1) Kwa hiyo, lazima imani ya Mkristo iwe yenye nguvu nyingi.
16, 17. Toa mifano miwili inayoonyesha sababu gani wale wanaotumainia kuishi katika “nchi mpya” wanatakiwa wawe na imani na ukamilifu bora sana.
16 Kwa sababu gani ni lazima imani ya Mkristo iwe yenye nguvu nyingi hivyo hata iweze kudumu ikishambuliwa vyo vyote na upande wo wote? Kwa mfano, chukua kisa cha “mkutano mkubwa” watakaoiokoka ‘dhiki kubwa’ wakati itakapoharibu taratibu hii ya mambo ya ulimwengu. (Ufu. 7:9-14) Wakiingia katika dunia watakuwa “msingi” wa jamii ya “nchi mpya.” Kwa kuwa wao ndio msingi, lazima wawe wenye nguvu. Lazima wamwakilishe Yehova Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote bila kuyumba-yumba. Wataishi wakati Ufunuo 20:11-15 utakapokuwa ukitimizwa, na kwa hiyo watakuwa na daraka la kufundisha watakaofufuliwa njia inayofaa, wamfahamu Yehova na Mwanawe Yesu Kristo. Kati ya watu hao watakaofufuliwa, waliokuwa wakiishi maisha ya namna zote, bila shaka wengine watapinga kweli, na itakuwa lazima “mkutano mkubwa” wawe na imani yenye msingi imara. Hawataondolewa katika mwendo wa uaminifu kwa kukazwa wala kwa kuongozwa na maoni yao wenyewe.
17 Halafu, mwishoni mwa utawala wa miaka elfu wa Kristo, jaribu la mwisho litakalokuwako Shetani afunguliwapo litajaribu imani ya wote watakaokuwa duniani. Jaribu hilo litaonyesha kama kila mtu anaendelea kuwa mkamilifu kwa Mungu na kumwamini, hata litaonyesha kama mtu ana kiwazo kidogo zaidi sana cha kutoaminika. Jaribu hilo ni la lazima kwa sababu watakaolipita watapewa uzima wa milele. Kwa sababu ya kuonyesha imani yao haivunjiki, Yehova na ulimwengu wake wote atajua kwamba hawatadhoofika kamwe wala hawataiacha kweli.—1 Kor. 15:24-28.
18. Petro na Yakobo wanaonyesha namna gani kwamba si ajabu kwa Mkristo ikiwa imani yake inajaribiwa katika njia mbalimbali, hata vikali?
18 Kwa kuwa tunaona kwamba imani yetu yapaswa kuvumilia shambulio lo lote, tusishangae juu ya mambo yanayoweza kutokezwa yatujaribu—hata mambo yaliyo tofauti na tunayotazamia. Mtume Petro anaambia Wakristo hilo, akisema: “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho.” (1 Pet. 4:12) Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu, akubali, hivi: “Ndugu zangu, oneni yote kuwa furaha mpatwapo na majaribu mbalimbali, mkijua mnapofanya hivyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu waleta uvumilivu.”—Yak. 1:2, 3, NW.
19. Mkristo anaweza kuijaribu imani yake mwenyewe namna gani?
19 Kwa hiyo imani yaweza kutofautiana ubora. Kila mmoja wetu anaweza kuichunguza imani yake mwenyewe. Mtume Paulo anashauri hivi: “Jijaribuni wenyewe kwamba mmekuwa katika imani; jithibitisheni wenyewe.” (2 Kor. 13:5) Mkristo anaweza kuyafikiria majaribu na matatizo ambayo amepata na namna ameyatatua. Anaweza kufikiria namna anavyotatua matatizo yake ya sasa na kutimiza madaraka yake. Je! anafanya maendeleo ya kuzaa matunda ya roho? Je! anafanya kadiri awezavyo asaidie wengine? Je! anayowatendea ndugu zake yanawafaidi sikuzote? Je! anatangaza imani yake?
MUNGU ANAUPA UVUMILIVU THAWABU YA KIBALI
20. Kushinda majaribu kwa uvumilivu kunamtendea Mkristo nini?
20 Yakobo anasema kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yako unatokeza uvumilivu. Mtume Petro anasema juu ya majaribu ambayo Wakristo wanapata, na kutoa sababu yake: “Ili ubora uliojaribiwa wa imani yenu, iliyo na thamani kubwa zaidi sana kuliko dhahabu inayoharibika ijapokuwa inajaribiwa kwa moto, uonekane kuwa sababu ya sifa na utukufu na heshima katika ufunuo wa Yesu Kristo.” (1 Pet. 1:7, NW) Kwa kadiri tunavyopita majaribu ya imani yetu ndivyo tunavyokuwa wenye nguvu zaidi—twaweza kuvumilia. Pia tunapokea kibali ya Yehova na kumfurahisha yeye na Mwana wake, kwa sababu tunakuwa mashahidi wa Yehova katika ulizo la ukamilifu.—Rum. 5:3, 4.
21. Imani yenye kuendelea ina ubora gani?
21 Kwa kweli, kuwa na imani yenye nguvu, yenye kuvumilia ni bora kuliko kuwa mshindi mkubwa, kwa sababu mtume Yohana anasema hivi: “Huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Ni ukamilifu, si nguvu. Kuvumilia pamoja na imani ni kuufuata mfano wa Yesu Kristo, yeye aliye na imani kuu zaidi na mshindi mkuu kuliko wote wa ulimwengu.—Yohana 16:33.
22. 1 Petro 1:7 linaonyesha namna gani kudumu kwa imani iliyojaribiwa na kudumu kwa aliye nayo?
22 Ndiyo, kitu cho chote, hata dhahabu, chaweza kuharibika kwa kuliwa na kutu. Lakini imani, ikiisha kujaribiwa na kuonekana kuwa yenye nguvu, yenye ubora mkubwa, ‘haiharibiki.’ Haiwezi kuharibiwa, kwa sababu msingi wake ni Mungu wa milele, Mwenye Nguvu Zote. Mtume anasema kwamba haiwezekani kumpendeza Mungu pasipo imani. (Ebr. 11:6) Mtu asiye na imani hawezi kuisadiki kweli. Yeye haioni kweli iliyo kubwa kuliko zote katika ulimwengu wote, enzi kuu halali ya Yehova Mungu. Hawezi kumpendeza Mungu kwa sababu yale anayofanya hayapatani na ulimwengu wote. Mwanamume au mwanamke mwenye imani iliyojaribiwa atavumilia milele, kwa sababu, Mungu anayeishi milele, anapenda na analinda uhai wa watu hao.—Zab. 145:18-20; Ufu. 7:15-17.
[Picha katika ukurasa wa 59]
Yehova alijaribu imani ya Ibrahimu kwa kumjaribu amtoe mwana wake Isaka dhabihu