Kutumikia Pamoja na “Mtumwa” Mwaminifu
“Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake [ya nje].”—Ufu. 16:15.
1. Isaya 6:8 na Warumi 10:18 zimehusuje watu wa Yehova leo kwa njia ya pekee?
“MIMI HAPA, nitume mimi.” Miaka ya majuzi umati mkubwa wa watu wenye mioyo minyofu wamejitolea kumtumikia Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu wakiwa na roho ya maneno hayo ya nabii Isaya. Matokeo yakawa nini? Habari njema zenye kufurahisha zimetangazwa “duniani mwote” kwamba Yehova amesimamisha ufalme wake wa mbinguni akauweka mikononi mwa Mwanawe Yesu Kristo. Wale ambao wamejinyima mambo mengi washiriki kabisa katika kazi kubwa hii wamebarikiwa sana.—Isa. 6:8; Rum. 10:18.
2. (a) Maneno ya Isaya, ‘Ee Yehova, hata lini?’ yapaswa kutumiwaje? (b) Jibu la Yehova latuonyesha nini leo?
2 Wakati huo yamekuwako mtajaribu na mateso makali, na wengi wetu tumekua wazee tukimtumikia Yehova. Kama Isaya mwaminifu, tumelazimika kuvumilia mara nyingi tukitolea ushuhuda watu ambao mioyo yao ‘haikufahamu,’ masikio yao ‘hayakusikia’ na macho yao ‘yametiwa kibandiko pamoja’ (NW) hata wakawa hawawezi kutambua ujumbe mtukufu wa ufalme wa Mungu unaofanya kazi sasa. Kama Isaya, pengine nyakati nyingine tuliuliza ulizo hili, ‘Ee Yehova, hata lini watu hawa wataendelea kuonyesha ugumu wa mioyo yao?’ Yehova ajibu: “Hata miji itakapokuwa ukiwa, haina wenyeji, na nyumba zitakapokuwa hazina watu, na nchi hii itakapokuwa ganjo kabisa; hata [Yehova] atakapowahamisha watu waende mbali sana, na mahame yatakapokuwa mengi ndani ya nchi.”—Isa. 6:10-12.
3. (a) Tukiendelea kutumikia Ufalme kwa juhudi matokeo yatakuwa nini? (b) Kusudi letu la kumtumikia Yehova lapaswa kuwa nini?
3 Lazima tuendelee kusubiri na kuutoa ushuhuda wa Ufalme kwa juhudi kadiri ambavyo Yehova anakusudia. Nasi tunaposhikamana sana na “utimilifu wa matumaini” twaweza kuwa na hakika ‘Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yetu, na pendo lile tulilolidhihirisha kwa jina lake.’ (Ebr. 6:10-12) Lo! jinsi tulivyo na pendeleo kuu kumtumikia Mungu wetu Yehova kwa sababu ya upendo mtupu!—Marko 12:28-31; 1 Tim. 1:5.
4. (a) Yatupasa tuwe na uhakika gani juu ya makusudi ya Yehova? (b) Kwa hiyo sasa tuna pendeleo gani kuu’
4 Makusudi mazuri sana ya Ufalme wa Yehova yatatimizwa kabisa kwa wakati wake. (Isa. 55:11; Ebr. 10:37) Kwa upande wetu lazima tuendelee kusifu jina lake zuri kwa shukrani, huku tukitazamia sana kutimizwa kwa ahadi bora za Ufalme duniani.—1 Nya. 29:11-13; Isa. 9:6, 7; 2 Pet. 1:4, 11.
5. (a) Sikuzote wafuasi wa Yesu wamekuwa wakitazamia nini? (b) Paulo atoa onyo na shauri gani katika Wathesalonike wa Pili?
5 Wafuasi wa kweli wa Kristo Yesu wametumikia sikuzote wakiutazamia “mwisho.” Katika Luka 19:11 twasoma kwamba wanafunzi wa Yesu “walidhani ya kuwa ufalme wa Mungu utaonekana mara.” Baadaye, Yesu alipowatokea baada ya kufufuliwa, wanafunzi hawa walimwuliza hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” (Matendo 1:6) Baadaye Paulo aliandikia Wakristo wenye kutazamia akawaambia: “Ndugu tunakusihini, kwa habari ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo, na kukusanyika kwetu mbele zake, kwamba msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo.” Bali, walipaswa ‘kufanywa imara katika kila neno na tendo jema.’—2 The. 2:1,2, 17.
6. Wakristo wa karne ya kwanza walifanyaje “siku ya Bwana” ilipokosa kufika?
6 Ingawa waliishi wakitumaini kuiona “siku ya Bwana,” hakuna mmoja wa Wakristo hao wa karne ya kwanza aliyeiona muda wa maisha yake. Je! walipunguza juhudi na imani yao? Hata kidogo! Hata taratibu mbovu iishe wakati gani, “habari njema za ufalme” zilikuwa tukufu bado, nao uhusiano wao na Yehova na Kristo wake ulikuwa wenye thamani bado. Ingawa hawakuuona “mwisho” muda wa maisha yao, bado waliweza kuzihubiri habari njema “katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu,”—Kol. 1:23.
7. (a) Matokeo ya saburi ya Yehova yamekuwa nini leo? (2’Pet. 3:15) (b) Kwa sababu gani hakuna ye yote wa watumishi waaminifu wa Yehova atakayekuwa na jambo la kukatia tamaa?
7 Lakini namna gani leo? Je! watu wa Mungu wamepata hasara kwa sababu siku ile kuu ya Yehova haijawazukia waovu wa dunia? Sivyo, kwa maana watu karibu milioni mbili sasa wamesimama mahali pa usalama wa kiroho wakiwa na mabaki waliotiwa mafuta wa Mashahidi wa Yehova. (Zab. 91:9, 10) Ingawa huenda wengine wakafa wakati ujao kutokana na mateso, uzee au mambo mengine, wamehakikishiwa watafufuliwa. (1 The. 4:13, 14) Wanaoendelea kujilisha Neno la Mungu na kumtumikia Mungu kwa juhudi hawatakata tamaa.—Rum. 10:11.
8. Kama ilivyoonyeshwa na The Watch Tower mwaka 1914, ni jambo gani ambalo sikuzote watu wa Yehova wameona kuwa la maana kupita yote?
8 Gazeti hili limeendelea kuwatia moyo wafanye utumishi huo wa Ufalme kwa moyo wote, tangu lilipoanza kuchapwa mwaka wa 1879. Kwa mfano, kifungu kinachofuata kilikuwa katika The Watch Tower la Januari 1, 1914, ukurasa wa 3:
“Kulingana na uamuzi wetu, 1914 ndio mwaka wa mwisho katika yanayoitwa na Biblia ‘Majira ya Mataifa’—kipindi ambacho Mungu ameruhusu mataifa ya dunia wajitahidi wawezavyo kutawala ulimwengu. . . . Twaamini mwaka 1914 waonyesha zaidi ya mwaka wo wote uliotangulia wa mavuno kwamba kuna uwezekano mwingi wa kutumikia kweli. . . . Kwa hiyo, na tuwe macho zaidi tutumiwe na kuwa wenye faida katika utumishi wa mfalme wetu. Na tukumbuke kwamba nyakati hizi ni za maana, kwamba hata tuwe na shughuli ngapi za maisha, sikuzote twaweza kupata wakati fulani wa kuitumikia kweli.”
Sikuzote watu waaminifu wa Yehova wameuchukua “utumishi wa mfalme wetu” kuwa wa maana zaidi kupita mambo yote.
9. Mwaka 1914, ni ushuhuda gani wa wazi uliokuwako kwamba “ishara” ilitimizwa?
9 Naam, kwa zaidi ya miaka 30 mpaka 1914, kikundi cha Wakristo waaminifu kilikuwa kimekuwa kikitumikia kama “mtumwa mwaminifu mwenye akili” wa kisasa kwa kutolea watumishi wenzao wa nyumba ya Mungu chakula cha kiroho. (Mt. 24:45; Efe. 2:19-22; Gal. 6:10) Halafu tangu 1914, unabii mbalimbali waliokuwa wameonyesha ulianza kutimizwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipotokea pamoja na “utungu” mwingine, nao wenyewe wakateswa na mataifa yenye kuwaka vita. “Ishara” ilikuwa wazi kwamba Kristo alikuwa amefika ‘kuketi katika kiti cha utukufu wake cha mbinguni’ na kuanza kuhukumu mataifa. (Mt. 24:3, 7-9; 25:31, 32) Kulikuwa na mambo gani mbele ya jamii ya “mtumwa”?
“HERI MTUMWA YULE”
10. Sasa Bwana alitimiza unabii gani juu ya “mtumwa”! (Luka 12:42-44)
10 Hapo ndipo Bwana alipoamua kwamba “mtumwa” astahili mapendeleo zaidi, kupatana na ahadi yake ya unabii:
“Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.”—Mt. 24:45-47.
11. “Mtumwa” aliitikiaje alipowekwa na Bwana? (Linganisha Matendo 1:8.)
11 Maneno hayo yametimizwa vizuri ajabu! Mwaka 1919 watu wa Mungu walifunguliwa kabisa katika utumwa wa dini na siasa walimokuwa wamefungwa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, nao walifurahi sana roho ya Yehova ilipomiminwa juu yao ikawatia nguvu, walipokuwa wamekusanyika katika Cedar Point, Ohio, U.S.A. Walianza kazi kwa bidii wakitumia chombo kipya cha utumishi, gazeti Golden Age (linaloitwa leo Amkeni!). Walifurahi hata zaidi katika kusanyiko la Cedar Point la 1922, wakati mwito ulipotolewa: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni Mfalme na ufalme wake.” Kweli Bwana-alikuwa amemkabidhi “mtumwa” huyu, si Jumuiya ya Wakristo isiyoamini, “vitu vyake vyote,” yaani, kutimiza daraka la Ufalme duniani. Matokeo ya utendaji ulioongezwa wa “mtumwa” huyu mwenye furaha yangekuwa nini?
12. (a) Utendaji wa “mtumwa” wenye bidii ulithawabishwaje? (b) Kama ilivyotajwa katika The Watchtower mwaka 1944, watumishi wa Yehova wanaona jambo gani kuwa la maana kupita yote? (Mt. 24:14)
12 Yehova alikuwa amethawabisha Mashahidi wake waliotiwa mafuta walipoendelea kwa uaminifu kuutangaza Ufalme miaka hiyo. (Mt. 25:21, 23) Na baadaye furaha yao ilifurika wakati “mkutano mkubwa” wenye matumaini ya kuishi milele juu ya dunia hii ulipoanza kujiunga nao. (Ufu. 7:4, 9) Kufika mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Wakristo hao wenye kushika ukamilifu walikuwa wameongezeka wakawa karibu 140,000. Sasa walijifunza kwamba kulikuwa na kazi kubwa ya kufanya, nao walitimiza daraka hili wakiwa na nia inayoelezwa katika The Watchtower la Septemba 15, 1944, ukurasa wa 280:
“Wenye kukesha . . . hawasemi, ‘Umebaki wakati mrefu kabla ya mwisho, na kulingana na ufahamu wa sasa wa hesabu ya tarehe za Biblia, miaka elfu sita ya kuwako kwa mwanadamu itakwisha kwanza katika miaka ya sabini inayokuja, na mpaka wakati huo muda ni mrefu wa kumtumikia Bwana bila kuacha wala kugawanya fikira.’ Sivyo; wakeshaji waaminifu na watumishi hawajishughulishi na tarehe, iwe ni zamu ya pili ya usiku au ya tatu, au hata ikiwa wakati utaongezewa siku moja zaidi, mpaka kesho. Wao wanakaza macho na moyo wao juu ya ufalme wa Yehova, si juu ya wakati.”
Mpaka leo hii, Ufalme ndilo jambo la maana kupita yote. Lazima jamii ya “mtumwa” na wafanya kazi Wenzao wote waendelee kukesha wanaposhikamana na furaha ya utumishi wa Ufalme, wakifahamu kwamba wo wote wanaolegea wamo katika hatari ya kupoteza vyote.—Marko 13:35-37; Mt. 25:26, 29.
13. “Mtumwa” ana sababu gani leo ya kufurahi?
13 Leo, wako watu zaidi ya 2,000,000 wanaoshiriki kwa bidii kuutangaza Ufalme, tena twatazamia mpanuko zaidi, kwa maana katika mwadhimisho wa 1976 wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu, jumla ya wahudhuriaji ilikuwa 4,972,571 katika makundi karibu 40,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote, na kati ya hesabu hiyo watu 10,187 walidai kuwa wa jamii iliyotiwa mafuta ya “mtumwa.” Lo! jinsi “mtumwa” huyu alivyo na furaha kwamba ‘uvumilivu’ wa Yehova umeruhusu watu wengi zaidi ya ilivyotazamiwa wakusanywe!—2 Pet. 3:9; Isa. 60:8, 22.
KUENDELEA KUMNGOJEA BWANA KWA KUKESHA
14. “Mtumwa” anaangalia “vitu” gani sasa?
14 Mwaka 1971, Baraza Inayoongoza ya jamii ya “mtumwa” ilianza kupanuliwa ili kutoa usimamizi mwingi zaidi wa kiroho juu ya “vitu” vya Bwana hapa duniani. Hiyo yatia ndani kuangalia faida za “mkutano mkubwa.” Yatia ndani kuangalia matayarisho ya vitabu vya Ufalme, kufundisha watu wa Mungu na kuwasaidia katika utumishi wao shambani.
15. (a) Baraza Inayoongoza ya “mtumwa” imebarikiwaje miaka hiyo yote? (b) Ni nini kimesaidia kudumisha tengenezo?
15 Miaka yote iliyopita, Baraza Inayoongoza ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” sikuzote ilishirikiana sana na shirika halali linalojulikana sasa kama Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, lililokubaliwa kisheria mwaka 1884, nalo linasimamia mambo ya lazima ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Hakuna shaka kwamba msimamizi wa kwanza wa shirika hilo, C. T. Russell, alitumiwa sana na Yehova katika kipindi ambacho kweli za msingi za Biblia zilikuwa zikirudishwa kati ya waabudu wa kweli wa Mungu duniani. Halafu, kutoka mwaka 1917 mpaka 1942, J. F. Rutherford alitumikia kama msimamizi, akapinga kishujaa jitihada za Jumuiya ya Wakristo kuharibu sifa ya watu wa Mungu waliotengenezwa duniani na kuwamaliza. Kutoka mwaka 1942, N. H. Knorr, ambaye bado anatumikia kama msimamizi wa Watch Tower Society, amejitahidi sana kupeleka kwenye miisho ya dunia shughuli kuu ya kuelimisha watu Biblia. Usimamizi wa wanaume hao waaminifu na wafanya kazi wenzao katika Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova umebarikiwa ajabu na Yehova. Hiyo yaonyesha mbingu zinawaongoza, na tengenezo litadumu na ni lenye imara, kwa maana kwa muda wa karibu miaka mia moja, ni wanaume watatu tu mbalimbali ambao wametumikia kama wasimamizi wa Watch Tower Society, na kila mmoja alikuwa na uwezo wenye kufaa sana mahitaji ya wakati huo.
16. (a) Mahitaji ya mpanuko yalitimizwaje mwaka 1971, na 1974? (b) Ni badiliko gani kubwa lililopangwa mwaka 1975, nalo lilianza kufanya kazi wakati gani?
16 Ili matakwa zaidi ya mpanuko yatimizwe, mwaka 1971 mpango ulifanywa kuongeza hesabu ya “wanaume wazee” wanaotumikia kama Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova wawe jumla ya washiriki kumi na mmoja, badala ya kuwa saba (ambao ndio wasimamizi wa Watch Tower Society). Mpanuko zaidi ulitokea mwaka 1974, wakawa washiriki kumi na wanane; tangu wakati huo, John Groh aliyekuwa kati yao amemaliza mwendo wake wa kidunia. Halafu mwaka uliofuata wa 1975 kukafikiriwa badiliko kubwa kupita yote katika historia ya miaka 100 ya mashahidi wa kisasa wa Yehova. Baada ya mazungumzo kufanyika karibu mwaka wote huo, washiriki wale kumi na saba wa Baraza Inayoongoza waliinua mikono kwa ujumla kulikubali badiliko hilo Desemba 4, 1975. Lilianza kufanya kazi tangu Januari 1, 1976.
17. (a) Sikuzote Kichwa cha jamii ya “mtumwa” ni nani? (Mt. 23:8, 10) (b) Walikabidhiwaje madaraka, kupatana na Mithali 11:14?
17 Ni mambo gani yaliyokuwamo katika badiliko hilo? Kama kawaida, Kristo Yesu aliendelea kutambuliwa kuwa Kichwa cha jamii ya “mtumwa,” yaani, kundi lake lililopo duniani. (Efe. 1:22; 5:23) Washiriki waliotiwa matuta wa Baraza Inayoongoza wanatumikia katika vyeo vilivyo sawa wakiwa chini ya Kichwa hicho kimoja, nao hupokezana zamu ya uenyekiti kila mwaka kulingana na herufi ya kwanza ya majina yao. Madaraka ya usimamizi yamegawanywa kati ya Halmashauri ya Mwenyekiti yenye washiriki watatu (mwenyekiti wa mwaka huu, wa mwaka uliopita na wa mwaka unaokuja), na halmashauri tano za kudumu zenye washiriki kuanzia watano mpaka saba, zinazoangalia utendaji mbalimbali wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Kila moja ya halmashauri hizi inapokezana zamu ya uenyekiti kila mwaka na ina msawazishi au katibu wa kudumu.—Mit. 11:14.
18. (a) Halmashauri zimegawanaje madaraka? (b) Sasa tengenezo liko tayari sana kushughulika na nini? (Isa. 60:5; 32:1, 2)
18 Halmashauri ya Uandikaji inasimamia matayarisho ya vitabu vyote! Halmashauri ya Kufundisha inatayarisha mambo ya kutumiwa katika zile shule mbalimbali, mikutano na makusanyiko ya watu wa Mungu; Halmashauri ya Utumishi inaangalia mambo yote yanayohusiana na kuuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi; Halmashauri ya Uchapaji inashughulika na kazi zote za uchapaji vitabu na mambo ya biashara; nayo Halmashauri ya Utumishi wa Betheli inaangalia faida za watu wote wanaotumikia katika makao ya Betheli na viwanda vya Mashahidi wa Yehova. Hivyo madaraka yanagawanywa kama ilivyokuwa kati ya ‘wanaume wazee’ katika kundi la Kikristo karne ya kwanza. Tena, tengenezo sasa liko tayari sana kushughulika na mpanuko zaidi, na vilevile matatizo yanayoweza kutokea kwa sababu ya hatari za ulimwengu zinazoongezeka.—Matendo 15:1, 2, 6-29; 1 Kor. 14:40.
19. Maafisi ya matawi ya Watch Tower yamefanyiwaje mabadiliko, kupatana na Mithali 15:22?
19 Februari 1, 1976, mpango kama huo ulianzwa katika maafisi yote ya matawi ya Watch Tower Society duniani mwote. Hakuna mwangalizi wa tawi tena, bali ‘wanaume wazee’ watatu au zaidi wenye ujuzi wanatumikia kama halmashauri, wakiwa chini ya Baraza Inayoongoza, kuangalia faida za Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo. Halmashauri hizo pia zinapokezana zamu za uenyekiti kila mwaka, lakini mshiriki mmoja anatumikia daima kama msawazishi.—Mit. 15:22.
20. (a) Ni matunda gani ya ajabu ambayo yamezaliwa na wafanya kazi waaminifu shambani? (Mt. 13:23) (b) Wathesalonike wa Kwanza 5:1-4 inatutiaje moyo tuendelee kuzaa matunda hayo?
20 Kwa baraka ya Yehova, kazi ya Mashahidi wake wenye kujinyima imezaa matunda mazuri ajabu, nalo tengenezo limepanuka. Wako wafanya kazi waaminifu shambani ambao wameshikamana na Yehova wakimtumikia miaka 40, 50, 60 na zaidi, na wanaendelea kuwa mifano bora kwa kundi zima. Halafu wako wale wamejitoa “wapainie” katika maeneo magumu, kupeleka ujumbe wa Ufalme katika miji na nchi mpya, na kutumikia kwa siri makumi ya miaka katika nchi ambako Mashahidi wa Yehova ni marufuku. Sote tuendeleapo kutumikia kwa juhudi, twaweza kuwa na hakika kwamba tutapata matunda mazuri mpaka ‘siku ya Yehova itakapoleta uharibifu wa ghafula juu ya ulimwengu huu mwovu.—1 The. 5:1-4.
21. (a) Ni katika hali gani Bwana na “mtumwa” wake anaonya kwa upole wote wanaomtumikia Mungu kwa juhudi? (b) Kuna thawabu gani za kutumikia kwa juhudi? (Mit. 18:10; Isa. 26:20, 21)
21 Ni wazi kwamba sasa “roho za mashetani” zinawaendea “wafalme [watawala] wa ulimwengu wote, kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Katika hali hiyo ndipo Bwana wetu anapoongeza onyo: “Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake [ya nje, NW], asiende uchi hata watu wakaione aibu yake.” Ungekuwa msiba huo! Kwa hiyo, jamii ya “mtumwa” itaendelea kutia moyo wote wapendao kweli wayavae daima “mavazi” yanayoonyesha wanamtumikia Mungu kwa juhudi na “katika haki na utakatifu wa kweli.” Utumishi huo wenye juhudi na ushikamanifu utatudumisha katika mahali pa usalama wa kiroho, kisha tutaokolewa tusiharibiwe katika Har–Magedoni.—Ufu. 16:14-16; Efe. 4:24.
[Chati katika ukurasa wa 250]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
YEHOVA MUNGU
Yesu Kristo
“Jamii ya “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”—Mt. 24:45-47
BARAZA INAYOONGOZA
Halmashuri ya Halmashuri ya Halmashuri ya Halmashuri ya Halmashuri ya Halmashuri ya
Mwenyekiti Uandikaji Kufundisha Utumishi Uchapaji Utumishi wa Betheli