Eliya “Akaomba kwa Bidii Mvua Isinye”
SALA ya mtu mwenye haki, mwenye msimamo unaokubaliwa na Yehova Mungu, ina nguvu. Inaleta matokeo. (Yak. 5:16) Hivyo ndivyo mwanafunzi Yakobo alivyoonyesha alipoandika hivi: “Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinye; na mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake.”—Yak. 5:17, 18.
Ingawa Eliya alikuwa nabii, yeye alikuwa mwanadamu na hakuwa tofauti na mwanadamu ye yote mwenye haki. Alikuwa na mawazo yale yale ya moyoni, magonjwa yale yale na makosa yale yale ya mwanadamu mwingineyo. Lakini Yehova Mungu alijibu sala zake. Bila shaka atajibu watumishi wake pia wakimtolea dua kupatana na mapenzi yake.
Tukumbuke kwamba Maandiko ya Kiebrania hayataji waziwazi kwamba Eliya ‘aliomba’ mambo yanayotajwa na Yakobo. Lakini, kuna ushuhuda wa kuonyesha kwamba alifanya hivyo. Tunasoma yafuatayo juu ya alilofanya Eliya muda mfupi tu kabla ukavu uliokuwako muda mrefu haujakwisha: “Akapanda juu mpaka kilele cha Karmeli; akasujudu kifudifudi, akainama uso mpaka magotini.” (1 Fal. 18:42) Eliya alisujudu, nalo tendo hilo linaelekea kuonyesha alimkaribia Mungu katika sala. Basi, ni busara kusema kwamba alisali na kutoa dua kuhusu tangazo alilokuwa amemtolea Ahabu: “Kama [Yehova], Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu.”—1 Fal. 17:1.
Bila shaka, mwanafunzi Yakobo aliandika mambo hayo kwa kuongozwa na Mungu, kwa hiyo aliweza kuandika mambo yasiyotajwa waziwazi katika Maandiko ya Kiebrania, lakini yanapatana nayo kabisa. Mfano mmoja ni anaposema Eliya aliomba.
Mambo ambayo Yakobo aliandika juu ya Eliya yanapasa yatutie moyo tudumu katika sala. Tunaweza kuwa na hakika kwamba tutapokea cho chote tuombacho, ikiwa kinapatana na mapenzi ya Mungu.—Yohana 14:13, 14.