Endelea Kusubiri
“Mimi, nitamtazamia [Yehova]; nitamngojea Mungu wa wokovu wangu; Mungu wangu atanisikia.”—Mik. 7:7.
1. Ni faida gani njema zimetokana na subira ya Yehova?
SUBIRA ina malipo mengi. Kusubiri kwa Mungu kumefungulia wanadamu nafasi kubwa ya kupata uzima wa milele wakiwa watumishi wake anaowakubali. (Yohana 17:4; 2 Pet. 3:9; 1 Tim. 2:3, 4) Kumewapa watu mmoja mmoja wakati wa kujifunza matakwa yake na kuanza kujipatanisha nayo. Wengi wamefanya hivyo. Kwa hiyo, watu hao sasa wanafurahia zaidi maisha yenye kusudi, wanaepuka migogoro na matata yanayopata watu wanaopuza kanuni za Mungu zenye haki.
2. Tukisubiri wengine, twafaidikaje sasa?
2 Watu mmoja mmoja pia wanapata thawabu wanaposubiri. Mtu mwenye subira hajiachi audhike upesi, na hivyo haelekei sana kufanya mambo haraka-haraka. Hivyo anaendelea kuwa na dhamiri njema na kuepuka ugomvi na mapigano ya bure tu. Anafaidika afya pia. Mithali ya Biblia yasema: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.” (Mit. 14:30) Utulivu na subira, hata katika hali zenye kujaribu, unaongeza afya ya mwili mzima. Kwa upande mwingine, kuudhika-udhika na kukasirika-kasirika ni kama ugonjwa unaoweza kudhoofisha mwili wa mwanadamu. Kwa sababu ya faida zinazotokana na kusubiri, bila shaka yatupasa tuonyeshe sifa njema hii.
3. Kwa sababu gani yatupasa tuone kusubiri wengine kama wajibu?
3 Bado kuna sababu nyingine nzuri ya kusubiri. Yatupasa tuuone kama wajibu. Kwa sababu gani? Angalia kanuni aliyotaja Yesu Kristo: “Yo yote mtakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Sasa, je! twataka watu watusubiri? Sisi huthamini wakati wengine wanapotusikiliza kwa subira tunapowaeleza jambo la maana. Tunafurahi kushirikiana na wale wanaotueleza kwa subira mambo tusiyofahamu. Ni vyepesi zaidi kushughulika na watu walio na nia ya kuachilia makosa yetu madogo, wanaotusubiri tujapokosa mara nyingi. Kwa hiyo, je! hizo si pande ambazo sisi pia twapaswa kusubiri?
4. Sababu yetu kubwa ya kutaka kusubiri yapaswa kuwa nini?
4 Kwetu sisi Wakristo, sababu kubwa zaidi ya kutaka kusubiri yapaswa kuwa kumpendeza Yehova Mungu. Kwa kuwa ni mwenye subira, twaagizwa tumwige katika kila jambo. Biblia yatusihi hivi: “Mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa.” (Efe. 5:1) Lakini ni nini litakalotusaidia tuonyeshe zaidi subira ya Mungu?
TAMBUA UZITO WA KUTOSUBIRI
5. Mhubiri 7:8 yashirikisha kutosubiri na tabia gani isiyotamanika, nayo tabia hiyo yaweza kuonekanaje?
5 Yatupasa tuepuke kudhani kutosubiri ni kajambo kadogo tu. Biblia yasema: “Heri . . . mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi. Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako, maana hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.” (Mhu. 7:8, 9) Angalia kwamba mwenye subira anatofautishwa hapa na mwenye kiburi, mwenye majivuno. Huenda mwenye kiburi akawaza hivi: Ati yanipasa mimi nivumilie wengine wanaponiudhi na kunikasirisha kwa upumbavu na uchoyo wao? Wao wanadhani mimi ni nani? Vilevile, mwenye majivuno ni mwepesi kuudhiwa na kila jambo na kumhamakia mtu ye yote anayemwonyesha kosa. Anaweka kinyongo moyoni, anakiweka karibu naye kama kwamba kipo “kifuani” pake mwenyewe.
6. Kwa sababu gani yaweza kusemwa kwamba mtu mwenye kiburi, asiyesubiri, ni ‘mpumbavu’ pia?
6 Kwa kweli, mtu wa namna hiyo ni ‘mpumbavu.’ Haraka haraka yake ya kuudhiwa inamfanya aropoke maneno au atende mambo bila kufikiri, kisha ajiumiza mwenyewe na wengine. Vilevile hana kiasi kwa vile anavyojiona. Hiyo ni wazi kutokana na shauri la mtume Paulo katika Warumi 12:3, ZSB: “Ninamwambia kila mutu wa kwenu, asiwaze kujisifu kupita ilivyomupasa kuwaza, lakini awaze kwa akili.” Tena, huenda mtu anayeacha kiburi na kutosubiri kumtawale akahatirisha uhusiano wake na Yehova Mungu. Kwa sababu gani? “Kwa sababu Mungu anashindana na wenye kiburi, lakini anawapa wanyenyekevu neema.”—1 Pet. 5:5, ZSB.
7. Je! tuseme kwamba kutosubiri kunaletwa na kiburi katika mambo yote? Kwa sababu gani?
7 Bila shaka, si namna zote za kutosubiri zinazoletwa na kiburi. Kwa mfano, huenda jamaa ikawa imefanya mpango wa kwenda kula chakula katika nyumba ya rafiki zao wakati halisi uliowekwa. Huenda baba na mama wakawa tayari mapema ili wafike huko bila haraka. Lakini, huenda binti akawa amechelewa kujitayarisha apaswavyo kwa sababu hana shauku ya kwenda, au kwa sababu nyingine. Hivyo, huenda wazazi wakamsihi afanye haraka zaidi wasichelewe. Hatuwezi kusema sauti yao ya kumharakisha bila subira yatokana na kiburi. Bali, huenda wakawa wanahangaika kwa sababu binti hafikirii mambo, tena huenda wakawa hawataki waudhi waliowakaribisha kwa kuchelewa. Hilo pia laonyesha ubora wa kuepuka hali zinazoweza kuwapa wengine sababu halali za kutotusubiri. Tena, kanuni yahusika: “Kana mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Luka 6:31.
8. Twajifunza nini kutokana na 1 Samweli 13:3-14 juu ya hatari ya kutosubiri?
8 Kwa hiyo ingawa nyakati nyingine huenda kukawa na sababu halali ya kutosubiri, yatupasa tutambue uzito wa kutosubiri kunakoletwa na kiburi au kunakotufanya tutende haraka-haraka, bila kufikiri. Hatari ya kuacha kutosubiri kututawale yaonyeshwa vizuri na kisa cha Mfalme Sauli. Baada ya Yonathani mwana wa Sauli kuua jeshi la Wafilisti katika Geba, Wafilisti walikusanya jeshi kubwa wakapiga kambi Mikmashi wajilipie kisasi. Wakati huo Sauli alikuwa Gilgali katika bonde la Yordani, akimngojea nabii Samweli. Nabii alipokosa kufika wakati aliotazamiwa, Sauli hakusubiri. Alihofu kwamba Wafilisti wangemjia kabla hajaweza kutafuta msaada wa Yehova kwa kutoa dhabihu ya kuteketeza. Tena, kwa sababu watu wake walikuwa wakimwacha, hakutaka kuendelea kukawia asipoteze jeshi lake lote. Sauli alishindwa kusubiri, akajitanguliza akatoa dhabihu, akadharau amri ambayo Yehova alimpa kupitia kwa Samweli, kwamba angoje. Muda mfupi baada ya hapo Samweli alifika. (1 Sam. 13:3-12) Tendo moja hilo la haraka-haraka lilileta matokeo mabaya sana. Samweli alimwambia Sauli: “Umefanya upumbavu; hukuishika amri ya [Yehova], Mungu wako aliyekuamuru; kwa maana [Yehova] angaliufanya ufalme wako kuwa imara juu ya Israeli milele. Lakini sasa ufalme wako hautadumu.” (1 Sam. 13:13, 14) Wazia hilo! Kutosubiri kwa Sauli, kulikomwingiza katika dhambi, ni mojawapo sababu kubwa zilizomfanya Yehova aondoe ufalme katika ukoo wake. Kwa hiyo tusidhani kwamba kutosubiri hakuwezi kutuletea matata makubwa.
JIFUNZE KUTOKANA NA MFANO WA YEHOVA
9. (a) Mfano wa Yesu juu ya watumwa wawili na deni zao waonyesha kusamehe kwahusianaje na subira? (b) Tusitazamie Yehova atufanyie nini tusiposubiri ndugu zetu na tukikosa kuwarehemu?
9 Mara nyingi kusubiri hutia ndani nia ya kusamehe wengine makosa wanayotutenda. Tukiiga mfano wa Yehova twaweza kusaidika sana tusubiri wanadamu wenzetu. Mfano mmoja aliotoa Yesu Kristo wakazia sana jambo hilo. Mtume Petro alikuwa ameuliza hivi: “Ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? hata mara saba?” Yesu alimjibu: “Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini [Mpaka mara sabini na saba, NW].” Ndipo aliposimulia mfano wa watumwa wawili. Mmoja wao alikuwa na deni ya mfalme ya dinari 60,000,000. Wakati ulipofika wa kulipa deni, mtumwa huyu alimsihi sana mdai wake: “Nivumilie, nami nitakulipa yote pia.” Mfalme alimhurumia akafuta deni yote. Lakini ndipo mtumwa huyu alipomwendea mtumwa mwenzake, akadai amlipe deni ya dinari 100. Mtumwa huyo alimsihi sana: “Nivumilie, nami nitakulipa yote pia.” Lakini mtumwa ambaye alikuwa amefutiwa deni yake kubwa zaidi hakutaka kusubiri. Aliagiza mtumwa mwenzake atiwe gerezani. Mfalme aliposikia hilo, alibadili nia akaagiza mtumwa asiyesubiri, asiye na rehema, atiwe katika jela. Yesu aliutumia mfano huo akasema: “Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi, msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake.”—Mt. 18:21-35.
10.Yatupasa tuoneje makosa ya ndugu zetu kwa vile ambavyo Mungu ametusamehe dhambi zetu?
10 Kosa lo lote ambalo huenda ndugu Mkristo akawa ametutenda ni dogo sana likilinganishwa na deni kubwa ya dhambi ambayo Yehova Mungu ametusamehe kwa sababu ya dhabihu ya Mwanawe. Kwa hiyo ikiwa ndugu ametubu, tuna haki gani ya kutomsubiri au kutaka akione kwa sababu ya alilotutenda?
11. (a) Yehova alikuwa na nia ya kufanya nini aweke msingi wa kusamehe wanadamu dhambi zao? (Rum. 5:6-8) (b) Mfano wa Mungu wa kutoa kipatanisho watuhusuje? (1 Yohana 4:11)
11 Tusisahau kamwe kwamba Yehova Mungu alijipatia hasara kubwa kwa kuweka msingi anaotumia kusamehe watu. Alimpenda sana Mwanawe. Yesu Kristo mwenyewe alisema: “Baba ampenda Mwana.” (Yohana 5:20) Hata hivyo, Aliye Juu Zaidi alikuwa na nia ya kumpa kwa wanadamu awe “kipatanisho” kwa dhambi zetu. (Yohana 3:16; 1 Yohana 2:2) Hakuna mwanadamu amepata kujinyima kitu kikubwa hivyo ili kuwe na msingi wa kurudia uhusiano mwema na mtu aliyekuwa amemtenda dhambi. Lo! Yehova ametuwekea mfano bora namna gani kwa kututia moyo tuwasubiri wale watutendao dhambi!
KUWAONA WENGINE IFAAVYO
12. (a) Twaweza kupata somo gani juu ya ndugu zetu katika Warumi 12:4-8 na 1 Wakorintho 12:14-26, na hilo laweza kutusaidiaje tuwasubiri? (b) Shauri la Wafilipi 2:3 laweza kutusaidiaje tuwe na subira?
12 Jambo jingine linalotusaidia kusitawisha subira ni kuwaona wengine ifaavyo. Yatupasa tukumbuke kwamba watu na hali zao hutofautiana. Kwa mfano, huenda wengine wakawa wakawivu wa kufahamu mambo, lakini huenda wengine wakawa wanaweza kufahamu maagizo magumu upesi. Hata hivyo, hilo halionyeshi kwamba watu walio wakawivu au wenye kufanya mambo kwa uangalifu sana si wenye maana sana! Huenda wakawa wanatupita katika mambo mengine ya maisha—fadhili, urafiki na ukarimu. Kwa hiyo yafaa tutazame watu pande zao zote. Shauri ambalo mtume Paulo aliwapa Wafilipi lafaa sana: “Kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.” (Flp. 2:3) Ni kweli kwamba hakuna mwanadamu asiye mkamilifu mwenye sifa zote zinazotamanika. Ikiwa yeye ni mnyenyekevu, ataona vyepesi kwamba wengine wanampita katika mambo ambayo yeye ni dhaifu na kwamba yeye pia huenda akawaudhi nyakati nyingine.
13. Ni nini linalohakikisha kwamba Yesu aliwasubiri mitume wake?
13 Bila shaka Yesu Kristo alionyesha maana hasa ya kuwaona wengine ifaavyo. Aliwasubiri mitume wake walipokuwa na ugomvi mdogo-mdogo na walipokawia kufahamu mambo. Yeye hakuwahamakia kamwe. Bali, alitumia subira kuwaonyesha masomo aliyotaka wajifunze. (Marko 9:33-37; Yohana 13:5-17) Hakuna maandishi yanayoonyesha kwamba Yesu Kristo aliwagombeza wenzake. Ingekuwa vizuri namna gani tukiiga mfano bora wake!
NIA YA KUNGOJEA
14. Kwa sababu gani huenda ndugu wengine wakakosa subira kuhusu madaraka ya kundi?
14 Lakini, si makosa ya wengine peke yake yanayoweza kujaribu subira yetu. Mara nyingine tunatakiwa kuwa na nia ya kungojea jambo linalotamanika. Ulizo ni hili: Je! tutakosa subira kama mtoto anayetaka kupata vyote mara moja, au tutakuwa na nia ya kusubiri mpaka wakati unaofaa? Pengine wewe ni ndugu katika kundi la Kikristo. Kwa sababu hujawa mtumishi wa huduma, je! unaona ni vigumu kungojea wakati ambao utakuwa ‘umejaribiwa’ kabisa akaonekana unafaa? (1 Tim. 3:10) Ikiwa umekuwa mtumishi wa huduma labda mwaka mmoja hivi, wajisikia kwamba wakati umefika wa kupendekezwa uwe mzee? Au, una nia ya kungojea, ukitumia wakati wako vizuri kupata ufahamu mwingi na bora wa Neno la Mungu, na kuonyesha unataka kushirikiana na wengine katika mambo, unategemeka, unafikiria wengine na umejitoa kabisa umtumikie Yehova?
15. (a) Kwa sababu gani mtu apaswa kujichunguza pia anapotaka madaraka? (Yak. 3:1, 2) (b) Ndugu anayetaka kushiriki kuchunga kundi aweza kujiulizaje?
15 Bila shaka, ni jambo la kusifika ndugu ‘wanapofikilia’ madaraka makubwa zaidi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Usemi huo ni wenye kuaminika. Ikiwa mwanamume ye yote anafikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.” (1 Tim. 3:1, NW) Hata hivyo, mtu akipata madaraka anakuwa na wajibu mwingi zaidi. Yesu Kristo aliitaja kanuni: “Naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi.” (Luka 12:48) Kwa hiyo, ikiwa watamani kupata madaraka zaidi, kwanza yakupasa ujichunguze uone kama maisha yako ya Kikristo yaweza kuchunguzwa sana na washiriki wengine wa kundi bila ya kuonea mashaka mfano unaoweka. Waweza pia kujiuliza hivi: Kweli nataka kutumikia ndugu zangu? Je! nina hekima ya kimungu na busara ya kuamua mambo yanayohusu maisha za watu? Naweza kutoa mashauri ya Maandiko yatakayosaidia wengine na matatizo yao ya kipekee na ya jamaa? Je! kweli wengine wananiona kuwa “mzee” kwa sababu ya ujuzi wangu wa kuishi Kikristo? Uchunguzi mzito huo huenda ukatuliza maelekeo yo yote ya kutosubiri. Huenda ukakuonyesha sana ubora wa kusubiri mpaka wakati utakapoweza kabisa kutumikia vizuri ndugu zako.
16. Maneno ya mtume Paulo katika 1 Timotheo 5:22, 24, 25 yaweza kusaidiaje ndugu asubiri kwa unyenyekevu mpaka wengine watakapoweza kuona kwamba anastahili madaraka makubwa zaidi?
16 Huenda pia ukasaidika kwa kufikiria daraka zito ambalo wazee wanakuwa nalo wanapofanya mapendekezo ya ndugu watakaotumikia kama waangalizi. Mtume Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Usimwekee mtu mikono kwa haraka, wala usizishiriki dhambi za watu wengine. Ujilinde nafsi yako uwe safi.” (1 Tim. 5:22) Kama Timotheo angalikosa kuhakikisha kwamba mtu mwenye kuwekwa alikuwa ametimiza kweli matakwa ya Maandiko, angalikuwa na lawama fulani kwa makosa yo yote ambayo mwanamume huyo asiyestahili angetenda. Ndivyo na leo. Basi mbona usisubiri kwa unyenyekevu mpaka wengine watakapoweza kuona kazi njema zako? Kumbuka kwamba, kama vile makosa yanavyokuja kuonekana wazi mwishowe, kazi njema hazitakosa kuonekana daima. Mtume Paulo alimwonyesha Timotheo hilo alipomwandikia hivi: “Dhambi za watu wengine zi dhahiri, zatangulia kwenda hukumuni; wengine dhambi zao zawafuata. Vivyo hivyo matendo yaliyo mazuri ya dhahiri; wala yale yasiyo dhahiri hayawezi kusitirika.”—1 Tim. 5:24, 25.
17. Yatupasa tujitahidi kusitawisha nia gani ya nabii Mika, na ni katika mambo gani ya maisha yatupasa tuwe wenye subira?
17 Basi, katika mambo yote ya maisha, yatupasa tutii maneno ya Maandiko yanayotutia moyo, “Umtarajie [Yehova], tangu leo na hata milele.” (Zab. 131:3) Tusikose subira kwa sababu siku kuu ya Mungu ya kufikiliza hukumu haijafika. Bali, yatupasa tuonyeshe tuna hakika kama Mika: “Mimi, nitamtazamia [Yehova]; nitamngojea Mungu wa wokovu wangu; Mungu wangu atanisikia.” (Mik. 7:7) Zaidi ya hilo, na tuendelee kusubiri wengine, kuwasamehe makosa yao madogo waliyotutenda na kufikiria udhaifu na hali zao. Naam, tusihatirishe kamwe uhusiano wetu na Mungu wetu mwenye subira, Yehova, kwa sababu ya kutosubiri na kuwa na kiburi.
—Kutoka The Watchtower, Feb. 1, 1977.
[Picha katika ukurasa wa 306]
Yesu aliweka mfano mwema wa kusubiri, akavumilia makosa ya mitume wake, hata akaonyesha masomo aliyotaka wajifunze