Yakupasa Ufunike Kichwa Wakati wa Kusali?
ILIKUWA siku yenye baridi na upepo, siku ambayo rafiki za mjane aliyekufa walisimama katika theluji wakiwa wamezunguka kaburi lililokuwa wazi. Mhudumu aliyekuwa ameanza kuwa na upara alisema maneno machache ya faraja kisha akasali.
Kama wewe ungalikuwako, ungalidhani wote waliokuwapo walipaswa kuondoa cho chote kilichofunika vichwa vyao wakati wa sala? Huenda ulizo hilo likahusu sana wakati huo wenye baridi. Lakini, je! wewe wadhani kwamba wakati wo wote unaposali yakupasa uondoe kitu kilichofunika kichwa? Au, unadhani kwamba wakati wa kusali yakupasa kabisa uwe na kitu cha kufunika kichwa?
Sala ni ya maana. Mungu atutaka tusali. (Zab. 145:18; 50:14, 15) Sala zetu zapaswa kuwa zenye kufaa, na yatupasa tumtolee Yule anayefaa, kumweleza mambo yanayofaa na kwa njia inayofaa. Ingawa Biblia haitoi orodha ya sheria nyingi sana juu ya kusali, inatoa mashauri yaliyo wazi juu ya kufunika kichwa wakati wa kusali.
Mashauri hayo hayamo katika Maandiko yaliyoandikwa kabla ya Ukristo, kwa maana Mungu hakuwataka Waisraeli wote wafunike vichwa wakati wa kusali, ingawa labda wengine walifanya hivyo kwa sababu ya kumheshimu. Lakini, aliagiza makuhani Waisraeli wavae kitu cha kufunika kichwa, hata kuhani mkuu akawa na kilemba cha pekee. (Law. 8:13; Kut. 28:40; 39:27-29) Bila shaka walivaa vitu vya kufunika kichwa kama ishara ya kunyenyekea Mungu muda wote walipokuwa wakitumikia hekaluni, si wakati wa kusali tu.
Huenda watu wengine wakauliza, ‘Lakini Wayahudi leo hawafuniki vichwa wanaposali?’ Ndiyo, sasa wengi wanafanya hivyo. Lakini muhtasari ya kale ya sheria na mafundisho ya Wayahudi inayoitwa Talmud yaonyesha kwamba ilikuwa juu ya mtu mwenyewe kuchagua kama atafunika kichwa au hatafunika wakati wa kusali. Hivyo Mtaalamu Jacob Lauterbach alisema: “Sheria siyo inayofanya watu wawe na desturi ya kusali kwa kutofunika kichwa au kwa kukifunika. Inategemea kama watu wanaona inafaa au haifai.”
Hata hivyo, kwa Wakristo sala si desturi ya kuamuliwa na watu wa mahali ambapo mtu anaishi wala dini. Maandiko ya Kikristo (au, “Agano Jipya”) yanatoa mashauri yaliyo wazi juu ya habari hiyo, kwa kusema: “Kila mwanamume, asalipo, au anapohutubu, naye amefunikwa kichwa, yuaaibisha kichwa chake. Bali kila mwanamke asalipo, au anapohutubu, bila kufunika kichwa, yuaaibisha kichwa chake; kwa maana ni sawasawa na yule aliyenyolewa. Maana mwanamke asipofunikwa na akatwe nywele.”—1 Kor. 11:4-6.
Sababu ni nini? Nayo mashauri hayo yatumika wakati gani?
SABABU GANI TUJIFUNIKE AU TUSIJIFUNIKE?
Ili kuelewa aliyoandika mtume Paulo juu ya kufunika kichwa na kusali, fikiria mstari uliotangulia: “Nataka mjue ya kuwa kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Kor. 11:3) Naam, Paulo alikuwa akisema habari za kanuni ya kimungu ya ukichwa, na hasa jinsi inavyotumika katika ibada inayofanywa hadharani.
Kama mtume alivyoeleza, Muumba alimpa mwanamume aliyemwumba kwanza ukichwa na mamlaka juu ya mke wake, ambaye alifanywa kutokana na ubavu wa mwanamume. Kwa habari ya ukichwa, mwanamume alikuwa “mfano na utukufu wa Mungu” kwa maana yeye hakupewa mtu mwingine duniani awe kichwa chake. Lakini, mke wake na watoto wake wana kichwa cha kidunia wanachopaswa kutii kwa kiasi.—1 Kor. 11:7-10; Efe. 5:22-24; 6:1.
Kanuni ya ukichwa yahusika pia katika utendaji wa kundi. Paulo aliandika kwamba wanawake wanapaswa kuheshimu na kujitahidi kushirikiana na wanaume, ambao ndio wanapaswa kufundisha ya na kusali. (1 Kor. 14:33-35; linganisha 1 Timotheo 2:11, 12.) Kwa hiyo, nyakati nyingi, mwanamke asingeweza kuhubiri wala kusali kundini, huko nyuma katika karne ya kwanza W.K.
Basi, kwa sababu gani Paulo alisema habari za kufunika kichwa? Ni wakati gani ilifaa kukifunika na ni wakati gani haikufaa? Na hilo lahusuje siku hizi?
Paulo aliandika kwamba mwanamke anaposali anapaswa kuvaa kifuniko kichwani, kofia, kitambaa au shela, kama “dalili ya kumilikiwa.” (1 Kor. 11:10) Kifuniko hicho kingeonyesha anatambua kanuni ya ukichwa. Lakini ni wakati gani anapopaswa kufunika kichwa? Fikiria hali tatu hizi:
Siku za Paulo roho takatifu ya Yehova iliwapa Wakristo fulani karama za miujiza, kama uwezo wa kutabiri au kusema kwa lugha mbalimbali. Kwa mfano, labda katika mkutano fulani wa karne ya kwanza roho ingeweza kufanya mwanamke Mkristo atabiri. (1 Kor. 12:4-11; Matendo 21:8, 9) Au, labda wanawake peke yao wangeweza kuwa wamehudhuria mkutano fulani wa kundi. Mwanamke Mkristo angeweza kuongoza wengine katika sala au kuwafundisha, maana hakukuwa na mwanamume aliyebatizwa. Halafu tena, labda mke Mkristo alikuwa na mume asiyeamini na nyakati fulani akatazamiwa asali au afundishe watu Biblia mumewe akiwapo. Katika yo yote ya hali hizo mwanamke angepaswa kuvaa kifuniko kichwani, “dalili ya kumilikiwa,” aonyeshe alitambua kanuni ya ukichwa.
“KICHWA” CHAKO NI NANI?
Tunaweza kuthamini zaidi uhitaji wa wanaume na wanawake Wakristo kufuata maagizo ya Mungu juu ya kufunika kichwa tukiangalia matokeo ya kutofanya hivyo yangekuwa nini.
Kumbuka kwamba mtume aliandika kwamba mwanamume asaliye “naye amefunikwa kichwa” afanya jambo fulani. Jambo gani? Andiko la asili la Kigiriki lasema kwamba “anaaibisha kichwa cha yeye,” au, “yuaaibiisha kichwa chake.” Vivyo hivyo, mwanamke ‘asaliye au kutabiri’ bila kufunika kichwa “anaaibisha kichwa cha yeye,” au, “yutaaibisha kichwa chake.” Ni nani au ni nini kinachotajwa kuwa “kichwa” kila mara?
Twaweza kuelewa hilo kwa kusaidiwa na mstari uliotangulia. Hapo Paulo alisema kwamba “kichwa cha kila mwanamume ni Kristo” na “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Kor. 11:3) Kwa hiyo, inaweza kusemwa kwamba mwanamume asaliye akiwa amefunika kichwa anamdharau Kristo kwa njia fulani. Mwanamume akifunika kichwa anaposali angekuwa akitenda kama kwamba yeye ni mke wa kichwa fulani kinachoonekana duniani, badala ya Kristo kuwa kichwa chake. Vivyo hivyo, mwanamke aliyesali bila kufunika kichwa angeweza kusemwa kuwa yuaaibisha “kichwa” chake katika mpango wa Kikristo, yaani, mumewe (ikiwa ameolewa), baba yake au ukichwa wa wanaume Wakristo kundini.
Wafafanuzi wengine wanatoa maoni mengine. Wanaonyesha kwamba Wakorintho wa Kwanza 11:4, 5 yasema kwamba kila mwanamume asaliye au atabiriye “naye amefunikwa kichwa” yuaaibisha “kichwa chake,” na mwanamke asaliye au atabiriye “bila kufunikwa kichwa” chake yuaaibisha “kichwa chake.” Katika visa viwili hivyo, kabla tu ya kutaja kwamba “kichwa” kinaaibishwa, kichwa halisi cha mtu mwenyewe kinatajwa. Kwa hiyo, wafafanuzi hao wanasema kwamba labda Paulo alimaanisha kwamba mwanamume au mwanamke Mkristo asiyetenda ifaavyo kwa habari ya kufunika kichwa anajiaibisha mwenyewe.
Katika Maandiko ya Kiebrania twasoma habari za watu waliorudishiwa au wakaletewa mashutumu, ubaya, matata, jeuri, hatia ya damu na madhara juu ya vichwa vyao wenyewe. (Neh. 4:4; 1 Sam. 25:39; Zab. 7:16; 2 Sam. 1:16; 1 Fal. 2:32, 44) Katika mifano hiyo kichwa chamaanisha mtu mwenyewe, kwa maana ndicho sehemu ya mwili inayomwongoza sana katika matendo yake.
Zaidi ya hilo, Paulo alipokuwa akinena habari ya kufunika kichwa, alisema kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu, “ni aibu kwake.” Tena akaandika kwamba “ni aibu mwanamke kukatwa nywele zake,” kama kwamba ni mtumwa au amepatikana akifanya uasherati; mwenye kuaibishwa ni mwanamke mwenyewe.—1 Kor. 11:14, 6.
Kulingana na vile Paulo anavyoanza habari yote hiyo akikazia mpango wa kimungu wa ukichwa, inaelekea kuwa wazi kwamba wakati mwanamume Mkristo anapodharau kanuni hiyo ya ukichwa, anamdharau Kristo; vivyo hivyo, huenda mwanamke akadharau mumewe, au baba yake au wanaume walio kundini. Lakini, ni kweli kwamba mtu anayedharau mpango wa Mungu wa ukichwa na utii ajiaibisha kichwa chake mwenyewe.
KUFUNIKA KICHWA WAKATI WA SALA
Paulo alikuwa akisema habari ya mambo yanayofaa katika “makanisa ya Mungu,” hasa mikutanoni. (1 Kor. 11:16, 20-34) Kwa hiyo, maagizo yake juu ya kufunika kichwa wakati wa kusali hayahusu sala ya mtu anapokuwa peke yake, bali kunapokuwa na watu wengi hasa, katika ibada ya hadharani. Hiyo yaonekana wazi kwa sababu kutabiri (kuhutubu, UV) kunatajwa pamoja na sala. Haielekei kwamba huko nyuma mtu alitabiri akiwa peke yake chumbani mwake, ambamo angeweza kutoa sala zake mwenyewe.—Mt. 6:6.
Kwa hiyo, kulingana na Maandiko si lazima mwanamume wala mwanamke afuate maagizo ya kufunika kichwa anapomtolea Mungu sala akiwa faraghani. Mwanamke akiwa katika kazi za nyumbani kisha asimame kidogo asali, si lazima afunike kichwa. Vivyo hivyo, huenda mwanamume Mkristo anayetembea barabarani akamtolea Mungu sala. Mawazo yake mwenyewe yakimhimiza avue kofia, yampasa afanye hivyo. Lakini mashauri ya Mungu juu ya kufunika kichwa hayasemi ni lazima aivue.
Namna gani sala katika utendaji wa kundi au katika jamaa? Kulingana na kanuni ya ukichwa, ikiwa mwanamume aliyebatizwa yupo, apaswa atoe sala bila kufunika kichwa. Ndivyo itakavyokuwa katika jamaa hata wakati mume na mke peke yao wanaungana kusali.
Hata hivyo, huenda zikawako nyakati ambazo mwanamke Mkristo atalazimika kufunika kichwa asali. Kama ilivyokuwa karne ya kwanza, huenda dada akalazimika kusali kwa sauti kubwa mkutanoni kwa sababu akina ndugu hawako. Au, huenda mume asiyeamini akaomba mkewe Mkristo asali kwa sauti kubwa ili jamaa ile chakula. Katika hali hizo dada atakuwa akishughulika na kazi ambayo kwa kawaida ingefanywa na mtu aliye na ukichwa juu yake, yaani, ndugu kundini au mumewe. Kwa hiyo, yampasa avae kitu cha kufunika kichwa. Kwa kufanya hivyo ataonyesha anaiheshimu kanuni ya kimungu ya ukichwa na kuepuka ‘kuaibisha kichwa chake.’—1 Kor. 11:5.a
Mwisho, je! yakupasa ufunike kichwa ukiwa kati ya watu wengi lakini si wewe unayesali kwa sauti kubwa? Kwa mfano, fikiria sala ile iliyotolewa kaburini. Je! kama mwanamke angalikuwapo wakati sala hiyo ilipokuwa ikitolewa, ingalimpasa kufunika kichwa? Sivyo, kwa maana si yeye angekuwa akiongoza katika ibada ya hadharani wala si yeye angekuwa akifanya kazi ambayo mshiriki mwanamume wa kundi atazamiwa kufanya kwa kawaida. Yeye angekuwa akiisikiliza sala na kusema “Amina.” Kwa hiyo, akifunika kichwa au asipofunika asingekuwa akidharau kanuni ya ukichwa. Vivyo hivyo, si lazima mwanamume anayesikiliza sala kaburini afunike au asifunike kichwa. Aweza kufanya lo lote la mambo hayo, lakini inaelekea atafikiria mawazo yake mwenyewe na kuangalia asiudhi watu. Mwanamume akiona yampasa avue kofia wakati mtu mwingine anapotoa sala, aweza kufuata anavyoambiwa na dhamiri yake mwenyewe.
Ni vizuri sana kwamba Yehova ameweka katika Neno lake uongozi wa sala bila kutuwekea sheria nyingi mno. Tukikumbuka hivyo tunaweza kumfikia Mkuu wa Wote katika ulimwengu wote, huku tukiiheshimu mojawapo kanuni zake kubwa, yaani, ukichwa.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata maelezo zaidi juu ya mwanamke kufundisha kundini au mbele ya ndugu au mumewe, angalia Mnara wa Mlinzi wa Januari 15, 1973, kurasa 42-44.