Mtu Mwenye Ushujaa wa Kusema
NI WATU wangapi walio na ushujaa wa kutetea jambo la haki wakati ambao watu wengine wote wanaowazunguka wanafanya ubaya? Wewe unao? Tuseme kwamba tatizo linalohusika ni la kidini au la kiroho. Je! kuna faida ya kusema kwa ushujaa?
Mwanzoni mwa historia ya kibinadamu alikuwako mtu mwenye ushujaa wa kusema mambo ya kiroho. Huyo alikuwa Henoko, mwana wa Yaredi. Henoko ndiye aliyekuwa mwanamume wa saba katika kizazi kilichotoka kwa Adamu, baba ya taifa la kibinadamu.—Mwa. 5:18; Yuda 14.
‘HENOKO ALITEMBEA PAMOJA NA MUNGU’
Henoko alikuwa mtu wa namna gani? Ingawa alikuwa mtu asiyekamilika kama sisi sote tusivyokamilika, “Henoko aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwa. 5:24, NW) Alifuata mwendo wa haki kulingana na kweli ya Mungu iliyofunuliwa. Maisha yake yalipatana na mapenzi ya Yehova Mungu na kusudi lake. Kwa uhakika Henoko aliamini kwamba baraka nyingi zingeletwa kupitia kwa uzao wa “mwanamke” wa Mungu. (Mwa. 3:15) Hakuna jambo linalotajwa kuonyesha kwamba kuna mtu mwingine ‘aliyetembea pamoja na Mungu’ siku za Henoko. Ingawaje, anaelekea kuwa ndiye mtu wa pekee aliyeonekana kuwa amefanya sana hivyo.
HALI YA KIDINI YA SIKU HIZO
Hali ya kiroho kati ya wanadamu ilikuwa imeharibika sana wakati Henoko alipozaliwa mwaka 3404 kabla ya Wakati wa Kawaida. Miaka ilipokuwa ikipita, matendo ya kutomcha Mungu yalikuwa yameongezeka sana. Habili mwana wa Adamu, aliyekuwa shahidi wa Mungu, alikuwa amelitaja jina la Yehova, akawa ameuawa kwa sababu ya uaminifu wake. (Mwa. 4:4-8; Ebr. 11:4) Zaidi ya karne moja baadaye, Sethi mwana wa Adamu alizaa kivulana jina lake Enoshi. Ni mambo gani yaliyotokea siku za Enoshi? Tunaambiwa katika Maandiko hivi: “Hapo ndipo watu walipoanza kuliitia Jina la [Yehova].” (Mwa. 4:25, 26; 5:3, 6) Je! Hiyo ilikuwa njia ya kurudisha ibada ya kweli?
Hapana sivyo ilivyokuwa. Wanafunzi wa Kiebrania wanashikilia maoni ya kwamba andiko hilo linapasa kusema ‘walianza kwa makufuru’ kuliita jina la Mungu, au, “ndipo makufuru yalipoanza.” Kitabu Targum of Palestine kinasema: “Hicho ndicho kizazi kilichoanza kufanya makosa, na kujifanyia sanamu, wakaziita sanamu zao kwa jina la neno la Bwana.” Ni wazi kwamba hayo yalikuwa matumizi mabaya ya jina la Yehova. Inawezekana kwamba watu walitumia jina hilo kujitaja wao wenyewe au kuhusu watu fulani ambao walisingizia kupitia kwao ndipo waweze kumfikia Yehova katika ibada. Au labda walilitumia jina la kimungu kuhusu sanamu.
Vyo vyote ilivyokuwa, ‘kuliitia jina la Yehova’ kwa makufuru hayo hakukuwarudisha katika ibada safi ya Mungu wa kweli. Watu hao hawakuwa wakitembea pamoja na Mungu. Hakuna maandishi yanayoonyesha kwamba mwanadamu ye yote alitembea na Mungu kabla ya Henoko kuzaliwa, miaka 387 baada ya Enoshi kuzaliwa. Kufika siku za Henoko, matendo mabaya sana ya kutomcha Mungu yalikuwa yakizoewa na watu wengi, tena ibada ya uongo ilikuwa yenye nguvu. Walakini, ijapokuwa Henoko alizungukwa na upotovu wa kiroho, “aliendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.”—Mwa. 5:22, NW.
HENOKO ATUMIKIA KAMA NABII WA MUNGU
Henoko mwaminifu hakunyamaza asitaje makosa ya kidini na mazoea ya kutomcha Mungu. Kwa kuwa alikuwa mtu mwenye imani nyingi ajabu, alikuwa mmoja wa “wingu kubwa la mashahidi” wa Yehova. (Ebr. 11:5; 12:1) Henoko— mwanadamu asiyekamilika aliyekuwa shahidi wa pekee kati ya watenda makosa—alikuwa na ushujaa wa kusema.
Henoko alisema, “Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasimcha Mungu wameyanena juu yake.” (Yuda 14, 15) Naam, Henoko alisema kishujaa akiwa nabii wa kibinadamu aliye mwaminifu kwa Mungu. Inaelekea kwamba Henoko alitangaza unabii wake kwa kuhubiri, kama vile Nuhu alivyokuwa ‘mhubiri’ baadaye. (2 Pet. 2:5, ZSB) Lakini, Henoko hakusema mambo kwa akili zake mwenyewe. Alisema kwa uongozi wa roho takatifu au nguvu ya utendaji ya Yehova. Kwa hiyo, ingawa Henoko alikuwa na ushujaa wa kusema, alifanya hivyo kwa nguvu za Mungu.—Flp. 4:13.
Haielezwi jinsi mwanafunzi Yuda, aliyeyaandika maneno ya Henoko katika karne ya kwanza W.K., alivyopata habari juu ya unabii huo. Haupatikani katika maandiko ya Musa, aliyeyakusanya pamoja masimulizi ya Mwanzo. Hata hivyo, Yuda aliandika kwa uongozi wa Mungu, kwa hiyo unabii wa Henoko ni wa kweli kwa sababu umetiwa katika barua yake.
Yuda alikuwa akisema habari za “watu wasiomcha Mungu” waliokuwa wamepenya katika kundi la Kikristo. (Yuda 4, NW) Alipokuwa akinena habari zao aliutaja unabii wa Henoko unaosema kwamba Yehova angekuja kuleta hukumu juu ya wasiomcha. Maneno hayo yalikuwa na matokeo ya ajabu katika karne ya kwanza.
Lakini ebu yafikirie matokeo ya unabii wa Henoko juu ya watu wasiomcha Mungu walioishi siku zake! Je! unadhani watenda makosa hao walifurahi kusikia kwamba ‘Yehova atakuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya wasiomcha’? Hasha! Hakika alihitaji ushujaa na msaada wa Yehova ili aweze kusema hivyo katikati ya watu hao waovu wenye kuzoea dini ya uongo. Jinsi walivyotaka kuunyamazisha ulimi wa Henoko!
MUNGU AJITIA NDANI
Bila shaka watu hao wasiomcha Mungu walitaka kumwua mtu huyo aliyekuwa akitumiwa Naye kuwaonyesha wazi kwamba walikuwa wakifuata ibada ya uongo na ‘kazi za upotevu.’ Lakini mipango yo yote waliyopanga wafanye hivyo ilizuiwa. Jinsi gani? Tunaambiwa kwamba Henoko ‘alitoweka, maana Mungu alimtwaa.’ (Mwa. 5:24) Yehova hakuwaruhusu wapinzani wamwue Henoko nabii Wake mshikamanifu. Badala ya kuwaruhusu, Mungu “alimtwaa.” Lakini, hiyo maana yake nini?
Kuhusu jambo hilo, mtume Paulo Mkristo aliandika hivi: “Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha: maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu.” (Ebr. 11:5) Dakt. James Moffatt alilitafsiri andiko hilo hivi: “Ilikuwa kupitia kwa imani kwamba Henoko akapelekwa mbinguni, hivi kwamba hakufa kamwe (hakupatwa na kifo, kwa maana Mungu alikuwa amemchukua).” Lakini tafsiri hiyo inawezaje kuwa ya kweli? Zaburi 89:48 inauliza hivi: “Ni mwanamume gani atakayeishi asione mauti?”
Henoko alikuwa mtu asiyekamilika. Alikuwa amerithi dhambi na kifo kutoka kwa Adamu babu yake. Mtume Paulo aliandika akasema, “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Rum. 5:12) Tena, Yesu Kristo alisema hivi: “Hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu.” (Yohana 3:13) Basi, Henoko alikufa, wala Mungu hakumpeleka mbinguni.
Bali, “Mungu alimtwaa” Henoko kwa kumwondoa kati ya watu hao na kumpa kifo chenye amani wakati nabii huyo mwaminifu alipokuwa na umri wa miaka 365. (Mwa. 5:23, 24) Muda alioishi ulikuwa chini sana ukilinganishwa na watu wengi wa marika yake. Henoko hakuuawa kwa jeuri na watesi wake. Wala Maandiko hayaonyeshi po pote kwamba alipatwa na afya mbaya ambayo kwa kawaida inaua watu. Kwa hiyo, ni wazi kwamba Henoko hakuona maumivu wakati wa kufa. Kwa hiyo, yeye ‘hakuiona mauti’ kwa sababu hakujua akifa.
Baada ya nabii huyo shujaa kufa mahali wasipotajwa wazi, Yehova aliuharibu mwili wake kwa siri, kama alivyouharibu mwili wa Musa baadaye. (Kum. 34:5-7) Adui za Henoko hawakuweza kamwe kupata mwili wake wautende vibaya.
‘KUHAMISHWA’ KWA HENOKO
Basi, kwa njia fulani “Henoko alihamishwa, asije akaona mauti” baada ya ‘kushuhudiwa kwamba amempendeza Mungu.’ (Ebr. 11:5) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa hapo kuwa “alihamishwa” lina maana ya ‘kusafirisha mahali pengine’ au ‘kubadili mahali pa.’ Linaonyesha maana ya tukio lililompata mtume Paulo, aliyehamishwa au akachukuliwa na kupelekwa “kwenye mbingu ya tatu,” au “katika paradiso.” Katika hali hiyo, inaelekea kwamba Paulo alipewa na Mungu njozi ya paradiso ya kiroho ambayo ingekuwa katika kundi la Kikristo baadaye.—2 Kor. 12:1-4, NW.
Kwa kuwa Henoko alikuwa nabii, inawezekana kwamba Mungu “alimtwaa” akiwa katika hali kama hiyo yenye furaha nyingi. Labda Yehova alimlaza Henoko katika mauti akiwa katika hali ya usingizi mzito, akifurahia njozi ya paradiso ya taratibu mpya Mungu ambamo Yehova ‘atameza mauti hata milele.’ (Isa. 25:8) Huenda Henoko akafufuliwa akiwa na njozi yake yenye kumfurahisha kisha auone utimizo wa ajabu wa njozi hiyo.—Matendo 24:15.
MAMBO HAYO YANA FAIDA GANI LEO?
Watu wenye kumcha Mungu leo wanaweza kufaidika sana kutokana na habari za Henoko na mfano wake mwema. Wanaweza ‘kutembea pamoja na Mungu’ kwa imani kama yeye, wakiishi kupatana na mapenzi na kusudi la kimungu. Ingawa wao ni watu wasiokamilika kama Henoko alivyokuwa, wanaweza kuwa mashahidi waaminifu wa Yehova, kama vile yeye alivyokuwa.—Ebr. 12:1.
Leo Yehova ‘hatwai’ watu wenye kumcha kama vile ‘alivyomtwaa’ Henoko. Lakini kupitia kwa roho takatifu, Mungu anasaidia watu wake wanapoteswa kwa ajili ya haki. Wanaweza kufurahi wajapopatwa na majaribu mbalimbali, wakiwa na hakika kwamba Mungu hatawaacha wapatwe na mambo mengi kupita yale wanayoweza kuvumilia. (Mt. 5:10; 1 Kor. 10:13; 1 Pet. 1:6, 7) Watu hao wenye kumcha Mungu wakifa wakiwa waaminifu, watakuwa na tumaini la kufufuliwa kama Henoko.—Yohana 5:28, 29.
Ijapokuwa Wakristo hawajaona njozi ya paradiso itakayokuwako duniani, wanajua kwa uhakika kwamba itakuwako. Wanajua kwamba itaanzishwa. (Luka 23:43, ZSB) Hata sasa wanafurahia paradiso ya kiroho.
Kupatana na onyo la Henoko la unabii, Yehova alileta hukumu juu ya wasiomcha wakati wa gharika ya siku za Nuhu. Lakini unabii huo unawatia Wakristo moyo leo pia, kwa maana unaonyesha kwamba wakati wa uharibifu wa Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, na wakati wa vita ya Mungu katika Har–Magedoni, watu wasiomcha wataharibiwa, wakatiliwe mbali na maelfu ya malaika watakatifu wa Mungu. Bwana Yesu Kristo ndiye atakayeisimamia kazi hiyo ya kuwaua.—Ufu. 16:14-16; 18:1-24; 19:11-16.
Basi, leo Wakristo wanautangaza ujumbe wa Mungu kwa ushujaa kama Henoko, uwe unahusu hukumu za kimungu juu ya wasiomcha Mungu au kuhusu kusudi Lake tukufu la kuwabariki wanadamu chini ya utawala wa Ufalme wake wa mbinguni. Mashahidi wa Yehova wana ushujaa wa kusema habari za mambo hayo.