‘Mlango Unaoongoza Kwenye Utendaji Wafunguka’
“Mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji umefunguliwa.”—1 Kor. 16:9, tafsiri ya Kiingereza ya New World.
1. Kulingana na Matendo 14:15; 17:30; Tito 3:4, 5 na 1 Yohana 5:13, Yehova Mungu alifanya nini katika karne ya kwanza W.K., nao watu mmoja mmoja walipata pendeleo gani?
ZAIDI ya miaka mia kumi na tisa iliyopita kipindi kipya kilianza. Kilifungua nafasi nzuri ajabu ambazo hazijafungwa mpaka leo hii. Mungu Aliye Juu Zaidi alimtumia Mwanawe mzaliwa wa kwanza akawapa watu wa makabila yote, mataifa na lugha zote pendeleo la kumtumikia milele na milele.—Matendo 14:15; 17:30; Tito 3:4, 5; 1 Yohana 5:13.
2. (a) Yehova Mungu alikuwa ameshughulika na nani peke yao muda wa karne nyingi kabla ya Wakati wetu wa Kawaida? (b) Kwa sababu gani Wayahudi peke yao ndio waliomjua Yeye waliyekuwa wakimwabudu?
2 Karne nyingi kabla Yesu hajaja duniani, Yehova Mungu alishughulika na Waisraeli au Wayahudi peke yao. Wao peke yao ndio ‘waliokabidhiwa mausia matakatifu ya Mungu.’ (Rum. 3:2) Waisraeli wa asili peke yao au Mataifa wenye kushirikiana nao katika ibada ndio wangeweza kufahamu kusudi la Yehova lililofunuliwa. Ndiyo sababu Yesu aliweza kumwambia mwanamke Msamaria hivi: “Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho.” (Yohana 4:22) Wasamaria walivikubali vitabu vitano vya Musa, lakini wakayakataa Maandiko ya Kiebrania yale mengine yaliyoongozwa na Mungu. Kwa hiyo, walikuwa na kasoro katika maarifa yao juu ya Mungu wa kweli Yehova. Hawakumjua kiasi alichokuwa amejifunua. Lakini, Wayahudi walioyakubali Maandiko ya Kiebrania yote yaliyoongozwa na Mungu na kujitahidi kuabudu kulingana na njia iliyoonyeshwa katika Maandiko hayo walimjua kweli Yeye waliyekuwa wakimcha. Waliabudu kulingana na mpango uliokusudiwa na Mungu uliotegemea hekalu Yerusalemu.—Kum. 12:5, 6; 1 Fal. 14:21.
3. (a) Yesu Kristo alikuwa akitaja badiliko gani la ibada alipokuwa akisema na mwanamke Msamaria? (b) Ni mambo gani katika Maandiko ya Kiebrania yanayoonyesha kwamba baadaye mpango wa ibada safi ungebadilika?
3 Lakini, Yesu alionyesha kwamba badiliko lingetukia karibuni alipokuwa akiongea na mwanamke huyo Msamaria. Alisema: “Saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu [Gerizimu, ulioonwa na Wasamaria kuwa mtakatifu], wala kule Yerusalemu.” (Yohana 4:21) Dalili ndogo juu ya badiliko hilo zilikuwa zimekwisha tolewa katika Maandiko ya Kiebrania. Yehova Mungu alikuwa amemtumia nabii wake Yeremia akatangaza kwamba agano jipya lingefanywa badala ya agano la zamani la Torati. (Yer. 31:31-34) Aliye Juu Zaidi alimtumia mtunga zaburi Daudi kufunua kwamba cheo cha kuhani mkuu kingepewa kwa mtu asiye wa ukoo wa Haruni. Huyo angekuwa kuhani-mfalme kama Melkizedeki wa Salemu wa kale. Katika Zaburi 110 tunasoma hivi: “[Yehova] ameapa, wala hataghairi, ndiwe kuhani hata milele, kwa mfano wa Melkizedeki.” Badiliko hilo la ukuhani lilihitaji kuwe na dhabihu tofauti pia. Jambo hilo pia lilikuwa limeonyeshwa kwa unabii. Zaburi 40:6 inatuambia hivi: “Dhabihu na matoleo hukupendezwa nazo, masikio yangu umeyazibua [“lakini mwili ulitayarisha,” Septuagint Version], kafara na sadaka za dhambi hukuzitaka.”
4. Kwa sababu gani ibada inayokubalika inaweza kutolewa kupitia kwa Yesu Kristo peke yake?
4 Kutokana na Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki tunajifunza kwamba Yesu Kristo ndiye Mpatanishi wa agano jipya, kwamba yeye ndiye kuhani-mfalme kulingana na mfano wa Melkizedeki, na kwamba mwili wake mkamilifu wa kibinadamu ndiyo dhabihu yenye kulipia dhambi inayokubaliwa na Mungu. (Ebr. 7:15-28; 8:6; 9:15; 10:1-10) Kwa hiyo, ikawa lazima watu wote wanaotaka kuabudu ifaavyo wakubali kwamba Yesu Kristo ndiye njia ya pekee ya kumfikia Baba. Mwana wa Mungu alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6) Badiliko hilo la ibada lilikuja pamoja na nafasi ya watu mmoja mmoja ya kuwa sehemu ya taifa jipya la Israeli wa kiroho, lenye “uraia” katika ufalme wa mbinguni.—Flp. 3:20, tafsiri ya Kiingereza ya New World.
5. Iliwapasa wanafunzi wa Yesu wafanye nini ili watu wengine wajifunze njia ya kumwabudu Mungu kwa njia anayoikubali? (Rum. 10:10-15)
5 Lakini watu wangejuaje hivyo? Jibu linapatikana katika agizo ambalo Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake baada ya kufufuliwa kwa wafu: “Basi, enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, . . . na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20) Naam, kulikuwa na kazi ya kutangazia watu kweli ya Mungu na kuwafundisha. Miaka mitatu na nusu ambayo Yesu Kristo alifundisha hadharani, mitume na wanafunzi wengine walikuwa wamezoezwa kuifanya kazi hiyo ya maana. Kwa sababu ya utendaji huo wa maana sana, watu waliokuwa na uwezo na nia ya kufanya utumishi walipata nafasi nyingine nyingi.
KUNDI LA KIKRISTO LAANZA KUFANYA KAZI
6. Kundi la Kikristo lilianzwa wakati gani, naye Yehova alionyeshaje kwamba hakuwa akilitumia tena kundi la Kiyahudi?
6 Ikaja siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. Hiyo ndiyo siku ambayo kundi la Kikristo lilianzwa. Siku hiyo ilionyeshwa waziwazi kabisa kwamba kundi ambalo Mungu alikuwa akitumia sasa lilikuwa na wanafunzi wa Mwanawe. Siku hiyo, Aliye Juu Zaidi alimtumia Bwana Yesu Kristo kumimina roho takatifu juu ya wanafunzi karibu 120 waliokusanyika katika chumba cha orofa ya nyumba moja katika Yerusalemu. Kabla ya roho kumiminwa kulitokea “uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi.” Uvumi (au kelele) huo ulifanya Wayahudi na waongofu wengi wakusanyike karibu na nyumba walimokuwa wanafunzi. Wanafunzi hao waliotiwa nguvu na roho takatifu walianza kusema kwa lugha za kigeni “matendo makuu ya Mungu.” Wayahudi na waongofu waliokuwa wamekuja Yerusalemu kutoka mahali pengi pa mbali walistaajabu kusikia Wagalilaya wakisema lugha zao wenyewe.—Matendo 2:1-12.
7. Wayahudi na waongofu wangewezaje kuwa washiriki wa kundi la kweli la Kikristo?
7 Ndipo mtume Petro alipowaeleza waliokusanyika kwamba roho ya Mungu ilikuwa imemiminwa ili kutimiza unabii wa Yoeli. Aliendelea kuonyesha kwamba Yesu waliyekuwa wamemtundika mtini alikuwa amefufuliwa kwa wafu na kwamba alikuwa ndiye Kristo hasa, Bwana wa Mfalme Daudi, akiwa ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Waliyaonaje maneno ya Petro? Masimulizi yanatuambia hivi: “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?” Petro akajibu: “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha [roho takatifu].” Karibu watu 3,000 walifanya jinsi walivyotiwa moyo wafanye.—Matendo 2:14-41.
8. Ni mipango gani iliyofanywa ili kuwezesha waliokuja Yerusalemu kutoka mbali waendelee kukaa huko ili kufaidika kutokana na mafundisho ya mitume?
8 Waamini hao wapya na wengine wengi walioanza kushirikiana na kundi la Kikristo baada ya hapo walikuwa na mengi ya kujifunza. Bila shaka mitume, ambao walikuwa wamezoezwa na Yesu Kristo mwenyewe, ndio waliokuwa katika hali bora ya kuwafundisha. Lakini mitume wasingeweza kwenda sehemu zote za mbali za dunia ambako Wayahudi na waongofu walikuwa wametoka na kuja Yerusalemu. Kwa hiyo, ili waongofu hao wapya waweze kujitoa wafundishwe na mitume, walirefusha muda wao wa kukaa mjini. Walisaidiwa kufanya hivyo wakati waamini wengi wenzao walipojitolea kuuza mali zao na kupelekea mitume pesa walizopata wawagawie wenye shida.—Matendo 2:44, 45; 4:34, 35.
9. Kundi la Yerusalemu lilipoongezeka ukubwa, ni akina nani waliowekwa, na kwa sababu gani?
9 Ukuzi wa kundi la Yerusalemu ulifungulia wengine wasio mitume nafasi za kuangalia mahitaji ya watu wote. Mwanzoni mwanzoni mwa kundi hilo tunasoma habari ya vijana waliofanyia mitume kazi za mikono. Pengine walipatikana nyakati zote ili kupeleka ujumbe wa maana. (Matendo 5:6, 9, 10) Vijana hao walikuwa wakizoezwa vizuri sana kwa ajili ya wakati ujao kwa kushirikiana sana na mitume. Baada ya muda fulani, kazi ya kusaidia wenye shida ya kimwili iliwalemea sana mitume. Wakati tatizo lilipotokea juu ya kugawia wajane wenye shida chakula, mitume walijua kwamba isingefaa kuachilia madaraka yao ya kufundisha ili kufanya jambo hilo lisilokuwa na maana sana. Kwa hiyo, waliwaomba ndugu kundini wachague kati yao wenyewe wanaume saba wenye kustahili wawe wakigawa chakula kila siku. Baada ya mitume kusali, waliwawekelea wanaume hao mikono wafanye kazi hiyo. Wote saba walikuwa wanaume wenye sifa nzuri sana za kiroho, ‘wenye kujawa na roho, na hekima.’ (Matendo 6:1-6) Vilevile, kundi lilipoendelea kukua, bila shaka mitume waliweka wanaume hodari ‘wenye kujawa na roho, na hekima,’ watumikie pamoja nao kama wazee wa kutimiza mahitaji ya kiroho ya wanafunzi.
WAPASHANA HABARI NA MAKUNDI MAPYA
10. (a) Kulikuwa na matokeo gani juu ya kueneza “habari njema” wakati mateso makali yalipolipata kundi la Yerusalemu? (b) Baraza ya wazee katika Yerusalemu ilipashanaje habari na makundi mengine?
10 Muda mfupi baada ya kuanzwa kwa kundi Yerusalemu, mateso makubwa yalilipata, wengi wa wanafunzi wakalazimika kuondoka mjini. Waliotawanyika waliitumia nafasi hiyo kuzieneza “habari njema.” Kwa hiyo, makundi yalianzwa katika miji kama Samaria na Antiokia. (Matendo 8:1, 4-8; 11:19-21) Wakati habari juu ya makundi hayo na mahitaji yao zilipofika Yerusalemu, baraza ya wazee ya huko ilifanya mipango ya kuwapa msaada wa kiroho. Mitume Petro na Yohana walitumwa kwenye mji wa Samaria, nao walipokuwa wakirudi Yerusalemu wakazitangaza “habari njema” katika vijiji vingi vya Wasamaria. (Matendo 8:14-17, 25) Tunasoma pia kwamba baadaye Petro alitembelea makundi katika Lida na Yafa. (Matendo 9:32-43) Wakati Petro alipokuwa Yafa, ndipo roho ya Mungu ilipomwagiza kwenda Kaisaria akafungulie Mataifa wasiotahiriwa nafasi ya kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo kwa mara ya kwanza, yaani, Kornelio, nyumba yake na rafiki zake wakubwa.—Matendo 10:23-48.
11. Kwa sababu gani Barnaba alikwenda Antiokia, naye alipataje msaada wa kulijenga kundi la huko?
11 Kundi la Yerusalemu lilimtuma mwanafunzi Barnaba aende Antiokia, naye alipofika aliwatia sana moyo waamini wenzake. (Matendo 11:22-24) Kwa kuwa Barnaba alihitaji msaada wa kuendeleza ibada ya kweli katika mji huo, alijiamulia kumtafuta Paulo katika Tarso akamwomba amsaidie kazi katika Antiokia. Pengine wakati huo karibu miaka kumi na miwili ilikuwa imepita baada ya Paulo, aliyekuwa amekuwa mtesi wa wafuasi wa Kristo, kuwa mwamini. (Matendo 11:25, 26) Wakati huo manabii kutoka Yerusalemu walikuwa wakilitembelea kundi la Antiokia. (Matendo 11:27) Mmojawapo manabii hao, Agabo, alitabiri njaa kubwa. Kwa hiyo kundi la Antiokia lilifanya haraka kukusanya vitu vya kusaidia ndugu katika Uyahudi, likatuma Paulo na Barnaba Yerusalemu wakiwa na michango yao. (Matendo 11:28-30) Watu hao wawili walirudi Antiokia pamoja na Yohana Marko, binamu ya Barnaba.—Matendo 12:25.
12. (a) Kwa sababu gani Paulo na Barnaba waliondoka Antiokia wakafungue maeneo mapya? (b) Makundi mapya waliyoanza yalipataje baraza za wazee? (c) Kundi la Antiokia lilipataje habari za utendaji wa Paulo na Barnaba?
12 Baada ya hapo roho takatifu iliagiza kwamba Paulo na Barnaba wapewe kazi ya pekee. (Matendo 13:1, 2) Kupatana na uongozi wa roho, Paulo na Barnaba walisafiri wakapitia Kipro na sehemu za Asia Ndogo, wakizihubiri “habari njema” na kuanza makundi mapya. Walipoyatembelea tena makundi hayo waliweka wazee wa kutimiza mahitaji ya kiroho ya wanafunzi. (Matendo 14:21-23) Waliporudi Antiokia, ‘walikutanisha kanisa, wakawaeleza mambo yote aliyoyafanya Mungu pamoja nao, na ya kwamba amewafungulia Mataifa mlango wa imani.’—Matendo 14:27.
13. (a) Kwa sababu gani tatizo lilitokea katika kundi la Antiokia juu ya waamini Mataila? (b) Kwa sababu gani ilifaa tatizo hilo likaamuliwe Yerusalemu?
13 Halafu tatizo likatokea. Ndugu fulani kutoka Uyahudi walikuja Antiokia, wakasisitiza kwamba watu wasio Wayahudi walioanza kufuata Ukristo walipaswa kutahiriwa na kuagizwa waitii sheria ya Musa. Ama sivyo wasingeweza kupata wokovu. (Matendo 15:1) Tatizo hilo lingeweza kutatuliwa wapi? Mahali palipofaa zaidi ni Yerusalemu, maana hilo ndilo kundi ambalo mitume walishirikiana nalo. Zaidi ya hilo, huko ndiko kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ilikotoka ikaenea kote ambako makundi yalikuwa. Kwa hiyo, wazee wa kundi la Yerusalemu walikuwa ndiyo baraza kuu ambayo ingeweza kupelekewa maulizo na wazee wengine, Basi Paulo na Barnaba walitumwa wawaendee “mitume na wazee kwa habari ya swali hilo” la tohara.—Matendo 15:2.
14. (a) Baraza kuu ya wazee katika Yerusalemu ililimalizaje ulizo la tohara? (Matendo 15:6-21) (b) Makundi mengine yalipashwaje habari za uamuzi uliofikiwa? (Matendo 15:22-29)
14 Baraza kuu ya wazee, kutia na mitume, ililizungumza sana jambo hilo. Ushuhuda ulitolewa kuonyesha kwamba Mungu mwenyewe alikuwa amewakubali watu wasio Wayahudi wakiwa katika hali yao ya kutotahiriwa, akawamiminia roho yake. Hivyo ikafahamika wazi kwamba kuingizwa kwa Mataifa katika kundi la Kikristo kulitimiza unabii wa Maandiko ya Kiebrania. Walifikia uamuzi kisha wakauandika katika barua. (Matendo 15:6-21) Barua hiyo ilisema hivi:
“Mitume na ndugu wazee, kwa ndugu zetu walioko Antiokia na Shamu na Kilikia, walio wa Mataifa; Salamu. Kwa kuwa tumesikia ya kwamba watu waliotoka kwenu wamewasumbua kwa maneno yao, wakipotosha roho zenu, ambao sisi hatukuwaagiza; sisi tumeona vema, hali tumepatana kwa moyo mmoja, kuwachagua watu na kuwapeleka kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo, watu waliohatirisha maisha yao, kwa ajili ya jina la Bwana wetu Yesu Kristo. Basi tumewatuma Yuda na Sila, watakaowaambia wenyewe maneno yayo hayo kwa vinywa vyao. Kwa maana [iliipendeza roho takatifu] na sisi, tusiwatwike mzigo ila hayo yaliyo lazima, yaani, mjiepushe na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati, Mkijizuia na hayo, mtafanya vema. Wasalamu.”—Matendo 15:23-29.
15. Maamuzi ya baraza kuu ya wazee katika Yerusalemu na ziara za ndugu waaminifu ziliyasaidiaje makundi?
15 Barua hizo za baraza kuu ya wazee katika Yerusalemu pamoja na ziara za ndugu mbalimbali waaminifu zilijenga makundi na kuyatia nguvu yaendelee kuzitangaza “habari njema” na kusaidia waamini wenzao waendelee kuwa imara katika imani. (Matendo 15:30-32; 16:4, 5) Tena barua zilizoongozwa na Mungu, za Paulo, Petro, Yuda na Yohana ziliwaimarisha sana wanafunzi kiroho.
16. (a) Ni nafasi gani za utumishi ambazo wanafunzi wote, wanaume na wanawake, walifunguliwa na kipindi cha Kikristo? (Mt. 28:19, 20: Gal. 2:9; 6:10; 1 Tim. 5:10; Tito 2:3-5) (b) Wanaume hodari waliotaka kutumikia wenzao walipata nafasi gani nyingine za utumishi?
16 Kweli kuanza kwa kipindi cha Kikristo kulifungua nafasi nyingi kubwa za utumishi. Wanafunzi wote, wanaume na wanawake, walikuwa na pendeleo la kuzitangaza “habari njema,” na kutia waamini wenzao moyo na kuwasaidia wakati wa magumu au kwa njia za kiroho. Wainjilisti walihitajiwa ili kuzitangaza “habari njema” katika maeneo mapya. Ndugu hodari walihitajiwa pia waweze kutembelea makundi na kufanya kazi nayo muda fulani ili kuyatia nguvu na kuweka wazee na watumishi wa kundi. Kwa kuwa ndugu hao wenye kusafiri walikuwa na daraka kubwa sana, walisaidiwa na vijana ambao wangeweza kuwapelekea ujumbe na kuwatumikia kwa njia nyinginezo. Namna gani leo? Je! hata sasa nafasi za namna hiyo zingali wazi?
[Picha katika ukurasa wa 484]
Petro awaeleza Wayahudi na waongofu waliokusanyika juu ya utimizo wa unabii wa Yoeli
[Picha katika ukurasa wa 486]
Wakati Mataifa walipoingizwa katika kundi la Kikristo, baraza kuu ya wazee ilitoa maagizo ya kudumisha umoja