Kufaidika Kutokana na Ukichwa wa Kristo
YESU Kristo peke yake ndiye Kichwa cha kundi la Kikristo, wala si mwanadamu wala kikundi cho chote cha wanadamu. Yeye hakujichukulia cheo hicho mwenyewe wala hakukipata kwa kuchaguliwa na watu wengi. Aliyempa cheo hicho si mwingine ila Baba yake. Akiandikia waamini wenzake katika Efeso, mtume Paulo alisema kwamba Mungu ‘alimweka Yesu awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa.’—Efe. 1:22.
Inafaa kabisa Yesu Kristo awe na cheo hicho cha kuwa kichwa cha kundi. Mafundisho yake na maisha yake, hasa kifo chake cha kuwa dhabihu, ndiyo mambo yaliyowezesha kundi lenyewe liwepo. Hakuna mtu anayeweza kuwa mwanakundi bila kumtegemea Yesu Kristo. Yesu alisema, “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”—Yohana 14:6.
Je! Kristo anatumia ukichwa wake kuonea watu wakati wo wote? Yeye hafanyi hivyo, bali njia aliyotumia kushughulikia mambo alipokuwa mwanadamu duniani inahakikisha kwamba anatumia ukichwa wake kwa upendo na huruma. Aliwaeleza wanafunzi wake mambo magumu kwa subira, wala hakuwalemea kamwe kwa kuwaeleza mambo mengi mno ambayo wasingeweza kufahamu. Alitumia upendo kuangalia mahitaji yao, akahakikisha kwamba wamepumzika na kuwa katika hali ya faragha nyakati zilizofaa. Wakati mmoja, kulipokuwa hakuna “nafasi ya kula,” Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo.” (Marko 6:31) Mwishowe, Yesu aliwafia wanafunzi wake. Ni kama vile yeye mwenyewe alivyokuwa amesema, kwamba “hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.”—Yohana 15:13.
Yesu Kristo hakutumia ukichwa wake kamwe kuonyesha kwamba hakutumaini wafuasi wake. Aliamini kwamba walitaka kuifanya kazi na mapenzi ya Baba yake. Kwa mfano, wakati mmoja alisema hivi: “Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya.”—Yohana 14:12.
Bila shaka wanafunzi walipata moyo walipoyasikia maneno hayo. Wakiwa mmoja mmoja, hakuna mwanafunzi ye yote wa Yesu angeweza hata kukaribia kufanya mambo yote aliyoyafanya Bwana wao. Lakini, wakiwa wote kwa ujumla, waliweza kufanya kazi kubwa kuliko zake. Katika wakati wake Mungu, waliweza kupelekea Wayahudi na watu wasio Wayahudi “habari njema” mbele ya Uyahudi, Galilaya na Perea, ambako Yesu alihubiri. Walitumiwa kufanya wanafunzi wengi kuliko wale waliofanywa na Yesu wakati wa huduma yake ya duniani ya miaka mitatu na nusu. Hakika Yesu hakuwa amewatumaini wanafunzi wake wa kweli bure.
JINSI YESU ANAVYOTUMIA UKICHWA LEO
Yesu Kristo hajapunguza maongozi yake juu ya wanafunzi wake kwa sababu ya kutokuwapo leo akiwa mwanadamu. Wao wanapata msaada, uongozi na ulinzi wake kama kwamba yupo hapa duniani. (Mt. 28:20) Jambo hilo linawezekanaje?
Kwanza, kundi la Kikristo lina maandishi yenye kuaminika kuhusu mafundisho ya Yesu na maisha yake, nayo yameandikwa na watu wanne mbalimbali, yaani, kuna Injili ya Mathayo, ya Marko, ya Luka na ya Yohana. Vilevile sehemu ile nyingine iliyobaki ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo inamtaja sana Yesu na kuonyesha kusudi la mafundisho yake. Kwa hiyo tunapoyasoma Maandiko hayo yaliyoongozwa na Mungu na kuyatumia, tunaonyesha kwamba tunaukubali ukichwa wa.Kristo.
Tena, Yehova Mungu amempa Mwanawe mamlaka ya kusimamia nguvu fulani iliyo na uwezo mwingi, yaani, roho takatifu yake. Jambo hilo linaonekana wazi kutokana na maneno ambayo mtume Petro alisema juu ya kumiminwa kwa roho hiyo siku ya Pentekoste mwaka 33 W.K.: “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake. Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya [roho takatifu], amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia.”—Matendo 2:32, 33.
Kwa kuwa Yesu Kristo alimiminia wanafunzi roho, anaweza kuitumia pia awaongoze. Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapopatwa na matatizo au majaribu yenye kuwafadhaisha, wanaweza kuwa na hakika kwamba Bwana wao atawasaidia. Anaweza kuitumia roho takatifu ya Mungu kuwakumbusha Maandiko yanayofaa kuwaongoza na kuwawezesha kuona mwendo wanaofaa kufuata.
Hivyo wazee wanaoona kwamba hakuna mmoja wao aliye mkubwa kuliko mwenzake, na kumtegemea Kristo kichwa chao, wanasaidiwa kufanya maamuzi mazuri wanapofikiria mambo ya kundi kwa kusali. Maoni yao mazuri juu ya mmoja na mwenzake, pamoja na kuukubali kabisa ukichwa wa Kristo, yanaruhusu roho ya Mungu ifanye kazi juu yao bila kizuizi. (Efe. 4:15, 16) Kuwa hivyo kunazuia mambo mabaya yasitokee kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, pamoja na maelekeo ya kuwa na kiburi au kutaka makuu, wanapojaribu kutatua matatizo au kufanya maamuzi mazito wakiwa baraza nzima.
Licha ya kutumia roho ya Mungu, Yesu Kristo anaweza kutumia malaika wasaidie kundi lake. Alipokuwa duniani, alikuwa na mamlaka ya kuomba malaika waje kumsaidia. Alimwambia Petro hivi: “Wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi [au, lejioni, NW] kumi na mawili ya malaika?” Lejioni moja ya wakati huo ilikuwa na askari 6,000 kwa kawaida. Kwa hiyo Yesu angeweza kuomba asaidiwe papo hapo na zaidi ya malaika 72,000.
Tunaweza kufahamu jinsi malaika hao walivyo na nguvu nyingi tukikumbuka kwamba mmoja wao tu aliua askari 185,000wa jeshi la Kiashuru wakati wa Hezekia Mfalme Myahudi. (2 Fal. 19:35) Yesu Kristo anaweza kutumia malaika zake hodari alinde wanafunzi wake wasiingiliwe na wapinzani wabaya na kuhakikisha kwamba hawatazuiwa kutimiza amri aliyowapa wafanye wanafunzi, wajapopingwa kwa njia iliyo mbaya zaidi. Tunahakikishiwa kwamba malaika wanatumiwa kulisaidia kundi kwa sababu marufuku hata mateso mabaya sana yameshindwa kuisimamisha kazi ya kufanya wanafunzi. Wanakundi wanaweza kujibu ulizo lifuatalo, lililo katika Waebrania 1:14, kwa kusema NDIYO: “Je! hao wote si roho watumikao, wakitumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu?”
CHEO CHA WAZEE KUHUSIANA NA KRISTO
Yesu Kristo anatumia ukichwa wake kwa kutumia wanaume pia watumikie kundi ulimwenguni pote, nalo kundi hilo lina maelfu ya vikundi vya wanafunzi. (Efe. 4:7, 8, 11-13) Kila kimojawapo vikundi hivyo vya wanafunzi kwa kawaida kinakuwa na baraza ya wazee. Wakati wazee hao wanapojitahidi kuiga mfano wa Yesu na kuonyesha kikweli nia ya Kristo katika kufundisha kwao, hapo makundi yanakuwa yakifundishwa, kushauriwa na kusahihishwa na Yesu Kristo. Mtu anayefuata maonyo ya upole ya wazee, na kufahamu kwamba yanatokana na Maandiko, anaonyesha anaukubali ukichwa wa Kristo. Anaonyesha anajua kwamba wao hawaneni kwa mamlaka yao wenyewe, kwa sababu wanashikamana na Maandiko.
Lakini je! hiyo ina maana ya kwamba kila jambo lisemwalo na mzee lionekane kama kwamba limetoka kwa Kristo mwenyewe? Si nyakati zote. Mzee ni mwanadamu asiyekamilika kama mwanakundi mwingine ye yote, tena anaweza kufanya makosa kwa kunena na kutenda. Ni kama vile mwanafunzi Yakobo alivyokubali: “Twajikwaa sisi wote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yak. 3:2) Kwa hiyo lazima wazee wajiangalie wasiingize maoni yao wenyewe katika mafundisho, mashauri na masahihisho wanayowapa watu, kwa sababu wao pia wana udhaifu na hali za kutokamilika.
Wazee wakishughulikia mambo kwa maoni yao wenyewe na kufanya maamuzi kwa kutegemea mambo ambayo wao wenyewe wanapenda au wasiyoyapenda, watakuwa na hatia ya kuupuza ukichwa wa Kristo. Kwa kufanya hivyo watakuwa wakijiinua juu ya Yesu Kristo, kuonyesha kwamba uongozi anaolipa kundi una walakini. Watakuwa wakionyesha kwamba maoni yao wenyewe yanahitajiwa kuliko mafundisho ya Yesu Kristo.—Linganisha 1 Wakorintho 3:4-11.
Ingekuwaje mzee akishindwa kukubali ukichwa wa Kristo kwa njia hiyo? Ingekuwa juu ya wazee wale wengine kumsaidia awe na maoni ya kiasi juu yake mwenyewe kuhusiana na Yesu Kristo na ndugu zake. (Flp. 2:2-5) Hakika inampasa mzee aliyefanya kosa hilo atii shauri la wazee wengine linalotokana na Biblia, kisha aonyeshe kwamba anaukubali ukichwa wa Kristo. Je! kosa hilo lingefanya mzee huyo asistahili kuendelea kutumikia katika cheo hicho? Lingemfanya akiendelea tu kuyapuza masahihisho anayopewa na wazee wenzake kutokana na Biblia.
Kisa cha mtume Petro (Kefa) kinaonyesha vizuri kwamba mzee akifanya kosa kubwa katika uamuzi si lazima aondolewe Papo hapo. Wakati mtume Petro alipofanya kosa kwa kuacha kushirikiana na Wakristo wa Mataifa, mtume Paulo alimkaripia. Kwa habari ya jambo hilo, Paulo aliandika hivi: “Kefa alipokuja Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu. Kwa maana kabla hawajaja watu kadha wa kadha waliotoka kwa Yakobo, alikuwa akila pamoja na watu wa Mataifa; lakini walipokuja wao, akarudi nyuma akajitenga, huku akiwaogopa waliotahiriwa. Na hao Wayahudi wengine wakajigeuza pamoja naye, hata na Barnaba pia akachukuliwa na unafiki wao. Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi?” (Gal. 2:11-14) Petro alikubali karipio hilo, akafanya kama alivyoambiwa na kuendelea kutumikia kama mzee na mtume mwaminifu.
Lakini namna gani ikiwa wewe si mzee na unaona kwamba mzee mmoja au wengi kundini wanajaribu kuagiza wengine wafuate maoni yao wenyewe? Hapo inakupasa usali na kufikiri uone kama kweli maoni yako yanapatana na Maandiko. Ikiwa kweli kuna tatizo, uwe na hakika kwamba Yesu Kristo hataliacha kundi lipatwe na madhara yo yote ya kiroho. Yeye anajua linalofanyika. (Linganisha 2 Timotheo 2:18, 19 na Ufunuo 2:2-7.) Dhamiri yako ikiendelea kukusumbua, unaweza kuongea na mmoja wa wazee ili utulie moyoni na akilini. Uendelee kusali ili uzidi kuenenda kama mwanafunzi mshikamanifu wa Yesu Kristo, halafu ufaidike kutokana na ukichwa wake.
Hakuna shaka kwamba Yesu anatumia ukichwa wake juu ya kundi la Kikristo. (Kol. 1:13, 14, 18) Tunapoukubali tunapata faida nyingi sana kwa kulindwa, kuongozwa na kusaidiwa kwa njia nyinginezo. (1 Kor. 11:3) Basi, acheni tumnyenyekee Bwana wetu na kuendelea kupata baraka anapotumia ukichwa wake. —Yohana 14:23.