Kundi la Kikristo na Utendaji Wake
WAKATI huu wanadamu wamegawanyika sana. Dini, kabila, taifa hali za ujamii na lugha vimekuwa vizuizi visivyoondoleka. Lakini Mungu hakukusudia mgawanyiko huu uwepo. Hapo mwanzoni, Adamu na Hawa, wazazi wa jamii ya wanadamu, walikuwa na umoja wakipatana sana wao kwa wao, na zaidi ya hayo, walikuwa na umoja na Mungu na jamaa yake ya mbinguni ya wana wa kimalaika. (Mwa. 1:27-31; Ayubu 38:7) Mungu anakusudia kurudisha umoja na upatano huu katika ulimwengu wote. Ikisema juu ya “siri [takatifu] ya mapenzi yake” Mungu, Biblia inasema hivi: Ni “sawasawa na uradhi wake, alioukusudia katika yeye huyo. Yaani, kuleta madaraka ya wakati mkamilifu atavijumlisha vitu vyote katika Kristo, vitu vya mbinguni na vitu vya duniani pia. Naam, katika yeye huyo.”— Efe. 1:9, 10.
Bila umoja hakuna amani na furaha inayoweza kuwapo duniani. Lakini hauwezi kuwa umoja unaoletwa na woga, kama vile mataifa yanavyotumaini leo kuupata ili wajilinde na vita ya kutumia makombora ya atomiki. Amani ya kweli yapaswa itegemee umoja unaotokana na moyo—kupendana na kumpenda Mungu. Kukusanywa huku katika Kristo ni kukusanywa pamoja chini ya mamlaka ya Yehova Mungu, kumkiri kuwa Mwenye Enzi Kuu. Kwa muda wa miaka 1,900 iliyopita amekuwa akikusanya watu wa makabila, mataifa na lugha zote wawe kundi la Kikristo pamoja na Kristo akiwa Kichwa. Wakati huu wa mwisho wa taratibu hii ya mambo ya ulimwengu, Mungu anakusanya vilevile watu wanaotumaini kuokoka mwisho huo wa taratibu, waishi duniani milele chini ya enzi kuu ya Yehova. Tena, wakati wa utawala wa ufalme wake wa miaka elfu moja, Kristo atawafufua wafu, awakusanye wote wanaoonekana kuwa na utii katika mwili mmoja unaopatana.—1 Kor. 15:22, 23.
KUNDI NA UMOJA WAKE
Kundi ni nini? Neno hili “kundi” (kanisa) ni tafsiri ya neno la Kigiriki ekklesia, ambalo maana yake ni “mwito kutoka,” yaani, ek, “kutoka katika,” na klesis, “mwito.” Neno hilo lilitumiwa na Wagiriki wa kwanza wa baraza ya wananchi waliokusanyika wazungumze mambo ya Utawala. Maneno ya Kiswahili yanayolingana na neno hilo ni “kusanyiko” na “kundi.” Tafsiri nyingine za Biblia zinatafsiri neno hilo ekklesia kuwa “kanisa.” Neno la Kiebrania linalolingana na hilo ni qahal, linalotumiwa kulitaja kundi la Israeli.—Linganisha Zaburi 22:22, 25 na Waebrania 2:12 katika Tafsiri ya Biblia ya New World.
Neno hili “kundi” katika maana yake kubwa, linatumiwa kwa habari ya jamii nzima ya wanafunzi wa Kikristo walio chini ya Kristo Kichwa. (Kol. 1:18; Rum. 12:5) Linatumiwa vilevile katika Biblia kwa habari ya baraza za Wakristo. (Matendo 15:41; Ufu. 1:4) Ni lazima kila kundi liwe na umoja ndani yake na vile-vile umoja na kundi zima la duniani pote—yote ni kama kundi moja. Ule umoja ambao kundi linapaswa kuwa nao unaelezwa katika 1 Wakorintho 1:10: “Basi ndugu, nawasihi, kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba nyote mnene mamoja; wala pasiwe kwenu faraka, bali mhitimu katika nia moja na shauri moja.”
Upendo ambao ndio msingi wa umoja, ndiyo alama ya kwanza inayotambulisha kundi la kweli la Kikristo. Yesu alisema: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Biblia inaamuru Wakristo hivi: “Jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.” (Kol. 3:14) Ili umoja huu upatikane, yawapasa washiriki wote wa kundi wajifunze Neno la Mungu lililoongozwa na roho na kulifuata. Katika njia hii wanasitawisha nia na roho au nguvu ya Kristo inayoongoza na kuona mambo kulingana na nia yake. (Rum. 8:9; 1 Kor. 2:16) Wanamjua Mungu—utu wake, sifa zake njema na njia zake, nao wanaweza kumwiga yeye. (Efe. 5:1) Jambo hilo linaleta umoja lakini si hali ya kufanana. Kila mshiriki wa kundi hapotezi hali yake inayoonyesha namna alivyo wakati wa ‘kuuvaa utu mpya.’ (Efe. 4:22-24) Bado ana hali yake mwenyewe ya kuchagua anachotaka na asichotaka, anayo majaliwa na uwezo. Jambo hilo linaleta tofauti yenye kupendeza na furaha katika kundi.
BARAZA KUU YA WAZEE
Ili kazi ya kutangaza “habari njema” ifanywe duniani mwote, ni lazima iwepo bidii ya wote pamoja. Wakristo wa karne ya kwanza walifurahia umoja huu, kama mtume Paulo alivyoliandikia kundi la Kikristo katika mji wa Filipi katika Makedonia: “Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo, ili, nikija na kuwaona ninyi, au nisipokuwapo, niyasikie mambo yenu, kama mnasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili.” (Flp. 1:27) Makundi ya karne ya kwanza yalishirikiana na kundi la Yerusalemu. Kwa kuwa ndilo lililokuwa kundi la zamani kuliko yote, na waliokuwa washiriki wa baraza yake ya wazee ni kutia pamoja na mitume, makundi mengine yalitegemea kupata shauri na uongozi kutokana na baraza hiyo.
Mashahidi wa Yehova leo wamefanya bidii wajifunze namna kundi la kwanza la Kikristo lilivyokuwa likitenda na kufuata mfano huo wa Maandiko. Makundi ya shahidi wa Yehova zaidi ya 40,000 katika dunia yote yanashirikiana na baraza kuu ya wazee walioko Brooklyn, New York. Baraza hii ina washiriki ambao ni wanaume Wakristo waliokomaa, washiriki, wa kundi la Kristo, nao wanatokana na mataifa na nchi mbalimbali. Kama inavyoelezwa katika 1 Timotheo 3:1-7 na Tito 1:5-9, wanastahili vilevile kuwa wachungaji na waangalizi wa kundi la Mungu.
Utendaji wa baraza ya wazee ya karne ya kwanza katika Yerusalemu unaonyeshwa katika Matendo sura ya 15. Kama inavyoonyeshwa humo, Mungu alikuwa akitenda na watu wake po pote walipokuwa duniani—kundi lake zima. Kupitia kwa Kichwa cha kundi, Yesu Kristo, Mungu aliongoza watumishi wake Paulo na Barnaba wahubiri katika nchi zilizokuwa si za Kiyahudi, katika hali iliyoleta gumu: Je! Mataifa wanaoukubali Ukristo wanatakiwa watahiriwe kabla ya kukubaliwa katika kundi? Wakristo wengine Wayahudi walisema Ndiyo.
Kwa hiyo mtume Paulo na wengine walipeleka gumu hilo Yerusalemu, walikokuwa wakikaa mitume na wazee wengine wa kundi hilo. (Matendo 15:1, 2) Baraza yote hii ilipokusanyika, Paulo na Barnaba walilitolea ulizo hilo. Yakaanza mazungumzo ambayo katika hayo Petro alisimulia maongozi ya roho yaliyotokeza kuongoka kwa Mtaifa wa kwanza, Kornelio. (Matendo sura ya 10) Kisha, Paulo na Barnaba walitoa ushuhuda uliofanana na hayo.
Kwa njia hiyo roho takatifu ‘ilishuhudia’ kwamba Mungu alipendezwa na jambo hilo. (Yohana 15:26) Kisha, ili ulizo hilo lipate kujibiwa kulingana na Maandiko, roho ya Mungu ilitenda kama kumbukumbu la kumwongoza Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu Kristo kwenye andiko la Amosi 9:11, 12, tena ikawa kama mwalimu kumfahamisha Yakobo maana ya unabii huo. (Yohana 14:26) Kwa njia hiyo, shauri hilo lilimalizika kwa msaada wa roho takatifu. Kwa hiyo, barua iliandikwa ipelekwe kwenye makundi yote ili yaongozwe kupatana na mapenzi ya Mungu—Matendo 15:22-29.
Kwa kutazama namna baraza hiyo ya Kikristo katika Yerusalemu ilivyotenda, twaweza kufahamu namna baraza kuu ya wazee ya kisasa inavyotenda. Uhitaji unapotokea ili kutoa msaada wa ziada, wale wanaume wa baraza kuu ya wazee wanachagua wanaume wengine walio na ujuzi na wanaostahili watumikie katika baraza hii pamoja nao. Vilevile baraza hii inasimamia uchunguzi wa mapendekezo ya wazee yanayofanywa na makundi na kuwekwa kwa wanaume hao katika vyeo. Sehemu nyingine ya utendaji wa baraza hii ni kusimamia kuandikwa kwa magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, Biblia na vitabu vingine vya kusaidia kufahamu Biblia, ikitumia mashirika halali kama Watch Tower Bible and Tract Society ya Pennsylvania na Watchtower Bible and Tract Society ya New York.
Zaidi ya kusimamia mambo hayo, baraza hiyo kuu inapashana habari na makundi katika ulimwengu wote kupitia kwa afisi za tawi. Baraza hiyo inasimamia shule ya Gileadi ya wamisionari katika Brooklyn, New York, inasimamia kazi ya wamisionari katika dunia yote na kuhakikisha kwamba watangazaji wa “habari njema” ya Ufalme wanafikia maeneo yaliyo peke yao. Washiriki wa baraza hii wanatembelea nchi nyingine mara kwa mara. Jambo hili linasaidia umoja wa wazo na tendo uendelezwe ulimwenguni pote. (1 Kor. 1:10) Wanaume hawa wanashirikiana na makundi ya New York na kutumikia kama wazee. Wao si watawala au “mabwana” wa maisha au imani ya Mashahidi wa Yehova, lakini wanaonwa kuwa ndugu walio sawa na wengine na wenye wajibu wa uwakili.—1 Kor. 4:1, 2; 2 Kor. 1:24; 1 Pet. 4:10.
WAZEE KATIKA MAKUNDI
Halafu kila kundi la mahali lina baraza ya “wazee,” au “waangalizi” (Kigiriki, episkopoi). Wazee hao si watu wakubwa kwa njia yo yote, bali wao ni watumishi wa “kundi” la Mungu. Nia na kazi yao inasimuliwa na mtume Petro katika 1 Petro 5:1-4, mahali wanapoitwa wachungaji. Inawapasa walisaidie “kundi” wanalosimamia. Maneno yanayotumiwa kuwataja wanaume hao si majina ya heshima, bali yanaonyesha kwamba wao ni “wazee” ambao ni wanaume Wakristo waliokomaa na kuwekwa wafanye kazi ya kuchunga na kuangalia mambo ya kiroho. Mashahidi wa Yehova hawatumii majina ya pekee na ya heshima yanayotenganisha “makasisi” (mapadre) na wale wasio makasisi, “watu wa kawaida.”—Ayubu 32:21, 22.
Wanaume wanaopendekezwa na kila kundi wajulikane kama wazee au waangalizi wanachaguliwa na sifa za Maandiko zilizoandikwa katika 1 Timotheo 3:1-7, Tito 1:5-9 na maandiko mengine yanayosimulia sifa na kazi ya waangalizi wa kweli. Kwa njia hiyo “roho takatifu” inaonyesha baraza kuu ya wazee watu ambao imewapasa wawaweke ‘walichunge kundi la Mungu.’—Matendo 20:28, NW.
Kusimamia kundi la Mungu ni kazi ya ‘kuchunga.’ Anaposema habari ya kazi yao ya ‘kuliangalia kundi la Mungu,’ mtume Paulo anatumia neno la Kigiriki epimeléomai, ambalo maana yake ni “kuangalia,” kukitia ndani busara na kutoa msaada, epi likiwa linaonyesha ‘kuelekeza akili kwenye kitu kinachoangaliwa.’ (1 Tim. 3:5; NW) Katika Luka 10:34, 35 neno hilo linatumiwa kwa habari ya yule Msamaria mwema aliyemwangalia mtu aliyekuwa ameumizwa.
Kwa hiyo, kazi kubwa ya wazee ni kuangalia vizuri hali ya kiroho ya kundi, kufundisha, kusaidia, kukaripia, kuonya na kutia moyo. Wazee hawapendezwi na kundi kama jumla ya watu, bali wanapendezwa na hali ya kiroho ya kila mshiriki mmoja mmoja wa kundi. ‘Kustahili kwa wazee kufundisha’ kunatia ndani uwezo wa kuwapa watu mmoja mmoja, watu waliooana na jamaa shauri la msaada juu ya kutumia Maandiko ili wanyoshe maisha na kumaliza magumu yao.—1 Tim. 3:2, NW; 2 Tim. 4:2; 2:24, 25.
Wazee wa kundi wanakutana wanapotakiwa ili wasikilize mashauri ya mabishano yanayokuwa kati ya washiriki wa kundi, au yakiwako mashtaka ya kufanya makosa. Walakini, wanapofanya hivyo hawapaswi kuona kama mahakimu wakali, bali wanapaswa waonwe kama ndugu wenye upendo wanaotaka sana kumsaidia mkosaji. Kusudi lao ni kusaidia wale walio na ugumu waondoe ugumu wao kama Neno la Mungu linavyoagiza na kutunza mwenendo safi wa kundi kupatana na Maandiko. Hii inaendeleza kibali ya Mungu na vilevile kuzuia kundi la Mungu lisipate lawama. (1 Pet. 2:15, 16) Kwa hiyo, mambo yanayofikiriwa kwanza ni rehema na hali njema ya kiroho ya kundi. Bidii yote inatumiwa ili ‘kumpata’ mkosaji, kumsaidia atengenezeke, anyoshe njia yake na kurudia hali nzuri ya kiroho. (Mt. 18:5) Walakini, ikiwa watu wanafanya makosa mazito ya kuvunja kanuni za Maandiko nao hawaonyeshi toba ya kweli au nia ya kuacha mazoea mabaya, labda baraza ya wazee inaweza ‘kumtenga mkosaji na ushirika.’ Hatua hii ni kuvunja ushirika na urafiki wa kiroho pamoja na mtu huyo.—1 Kor. 5:9-13.
Zaidi ya kuliondolea kundi mashtaka ya kwamba linaachilia makosa, kumtenga mkosaji na ushirika kunaweza kumsaidia apate fahamu zake. (1 Tim. 1:20) Wakati ujao mtu huyo akigeuka na kuacha mwendo wake mbaya kisha anaomba arudishwe katika kundi, anaweza kupokewa baraza ya wazee ikiisha kuchunguza mwenendo na nia yake na kuona kwamba imekuwa nzuri zaidi. (2 Kor. 2:5-8) Anapokuwa ametengwa na ushirika, mtu huyo hatendwi mabaya, lakini anaonwa “kama mtu wa mataifa” kama Yesu alivyoshauri, yaani, kama mtu wa ulimwengu nje ya kundi, si kama mshiriki wa kundi la Kikristo.—Mt. 18:17.
WATUMISHI WA HUDUMA
“Watumishi wa huduma” (Kigiriki, diakonoi, watumishi au wahudumu) wanachaguliwa kufuatana na sifa zilizoandikwa katika 1 Timotheo 3:8-13. Wanaume hawa wanafanya kazi kwa kusimamiwa na wazee ili wasaidie kuangalia mambo mengi ya kundi yanayotakiwa. Wanafanya hivyo kwa kutunza maandishi ya kundi, kuangalia usafi wa mahali pa kukutania na vifaa vinavyotakiwa hapo, kuona kwamba watu wa mtaa huo wanafikiwa kwa njia ya utaratibu kwa “habari njema,” jambo linalotia kutayarisha ramani za eneo, kugawia watu mmoja mmoja au wengi eneo la kuhubiri, wakihakikisha kwamba washiriki wote wa kundi wanapatiwa vitabu vya kujifunzia Biblia ili vitumiwe katika kazi ya kuhubiri na kufundisha, wakasaidia wapya wazitangaze “habari njema,” kutembelea watu wanaopendezwa, na vivyo hivyo. Wanatumikia pamoja na wazee kupatana na “karama” ambazo Mungu ameona yafaa awape. (Rum. 12:6-8) Hakuna ye yote kati ya wazee wala watumishi wa huduma anayepokea mshahara kwa kutoa utumishi huo. Utumishi wao wanautoa bila kulipwa. Ijapokuwa wanawake wanafanya kazi ya kutangaza “habari njema” na kuwafundisha watu kama walivyofanya wanawake wa kundi la karne ya kwanza, hakuna ye yote kati yao anayewekwa kuwa mzee. Hii inapatana na maneno ya mtume Paulo katika 1 Timotheo 2:12 na 1 Wakorintho 14:34.
Mara kwa mara masomo yanatolewa mahali panapofaa ili kuwapa wazee mafundisho ya pekee. Wazee wote wa makundi wanaitwa wahudhurie shule hizo, zinazoitwa “Shule za Huduma ya Ufalme,” ambako wanapewa vitabu vya masomo vilivyotayarishwa kutimiza mahitaji yao. Waalimu wanaostahili wanaongoza shule hizo. Labda makundi yaliyo karibu na mahali ambapo masomo hayo yanatolewa wanaweza kuwapatia wageni chakula na mahali pa kulala. Masomo kama hayo yanatolewa kwa Mashahidi ambao ni “mapainia” wale wanaohubiri habari njema kwa kawaida saa 90 au zaidi kila mwezi.
WAANGALIZI WA MIZUNGUKO NA WILAYA WANAOSAFIRI
Wazee wanaoweza kutumia wakati wao wote au sehemu kubwa ya wakati wao ili wafanye kazi ya kuwa waangalizi wa mizunguko wanawekwa watembelee kwa kawaida makundi kama 20 hivi yaliyo katika eneo linalopewa. Kazi ya mwangalizi wa mzunguko ni kushirikiana na wazee walio katika makundi anayotembelea, akizungumza pamoja nao magumu yanayotokea na kutia moyo kundi kwa kushirikiana na kwa kufanya kazi ya kutangaza “habari njema” pamoja na washiriki wengi wa kundi. Vilevile anatoa hotuba za kutia wote moyo waendelee katika imani.—Rum. 1:11, 12.
Kazi ya mwangalizi wa wilaya inafanana na ile ya mwangalizi wa mzunguko. Kwa kawaida wilaya moja ina mizunguko kama 20 hivi au kisehemu kidogo. Mwangalizi wa wilaya anatembelea mizunguko hii na wakati huo “makusanyiko ya mizunguko” yanafanywa katika miji ambapo ni mahali pa kati panapofaa kufanyia makusanyiko hayo. Yeye anatumika kama mwenyekiti wa makusanyiko hayo. Kwa kawaida makusanyiko hayo yanafanywa siku mbili. Hotuba na mazungumzo ya Maandiko yenye kujenga, yanayotolewa na waangalizi wa mizunguko na wilaya na wazee wengine wa mizunguko hiyo, yanakuwa juu ya maisha ya Mkristo, kazi yake na magumu yanayompata. Ile baraza kuu ya wazee inasimamia utayarishaji wa vipindi na mazungumzo ya makusanyiko hayo yanayofanywa mara mbili kwa mwaka. Kipindi cha ubatizo kinaongozwa katika makusanyiko hayo.
MIKUTANO
Wakiwa kundi, Mashahidi wa Yehova wanayo mikutano hii kila juma, mikutano inayopangwa katika nyakati zinazofaa watu wa mahali hapo.
Funzo la kundi la kitabu. Mashahidi wa Yehova pamoja na watu ambao wanajifunza Biblia nao wanakutana kila juma katika nyumba katika mitaa mbalimbali ili wajifunze muda wa saa moja, wakitumia Biblia na kitabu cha masomo ya Biblia kilichotolewa kwa uongozi wa Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova. Hapa ndipo mtu anaweza kujuana sana na wengine wanaomtumikia Mungu katika mahali pake. Udogo wa kikundi hiki unatia mtu moyo aseme bila kusita na kujizoeza kutangaza imani yake mbele ya wengine. (Ebr. 13:15) Vilevile anayo nafasi ya kuuliza maulizo na kupokea majibu, pamoja na mazungumzo ya maandiko ya kutegemeza majibu hayo. Jambo hili linamwongezea mtu maarifa ya Biblia.—Mit. 27:17.
Nyakati nyingine, nyumba ambamo funzo la kundi la kitabu linamofanyiwa inatumika kama mahali pa kukutania kikundi hicho ili waende kutembelea nyumba za watu mtaa huo kwa kuhubiri “habari njema.” Mpango huu wa kikundi unawapa watu wanaofanya maendeleo mazuri katika kujifunza kwao Biblia nafasi ya kupokea msaada wa kushiriki kuzitangaza “habari njema.”
Mkutano wa watu wote. Kwa kawaida siku ya Jumapili, kila kundi linakutana ili wasikie hotuba ya Biblia. Habari zenye mazungumzo mbalimbali juu ya Biblia zinatayarishwa, na wasemaji waliostahili ambao kwa kawaida ni wazee, wanatoa hotuba hizo. Mtu akija kwenye mkutano huu akiwa na Biblia, anapata nafasi ya kumfuata msemaji anapotumia maneno au kutaja habari za Maandiko na kwa njia hiyo anawezeshwa afahamu mambo ambayo Biblia inafundisha juu jambo hilo.
Funzo la “Mnara wa Mlinzi.” Kwa kawaida mkutano huu unafuata mkutano wa watu wote. Ni funzo la Biblia linalotolewa kwa msaada wa gazeti Mnara wa Mlinzi. Utaratibu unaofuatwa kuongoza mkutano huu pamoja na kundi zima, unafanana na ule katika kuongoza funzo la kundi la kitabu pamoja na watu wachache. Mwenyekiti anauliza maulizo na wasikilizaji wanajitolea kutoa maelezo.
Shule ya Kitheokrasi. Kila kundi linaongoza shule hii ili lisaidie washiriki wote walioandikwa wajitayarishe zaidi sana kusema kweli kwa wengine kwa njia yenye matokeo. Inatayarisha wengi wawe “kielelezo kwao waaminio, katika usemi” wanapotoa hotuba za watu wote, na kutia moyo na kufundisha kundi jukwaani. Wote waliojiandikisha katika shule hiyo wanagawiwa watoe hotuba juu ya mazungumzo ya Biblia, nao wanasaidiwa wafanye maendeleo kwa kupewa shauri la upole na la faraghani na mzee anayeongoza shule hiyo. (1 Tim. 4:12, 13, 15; 2 Tim. 2:15) Mtu ye yote anayeshirikiana na kundi anaruhusiwa ajiandikishe katika shule hiyo. Kwa njia hiyo wanakuwa watu wanaofaa zaidi kusema na kufundisha katika nyumba za watu wanaopendezwa.
Mkutano wa utumishi. Mkutano huo ambao kwa kawaida unafuata Shule ya Kitheokrasi jioni ile ile, unaitwa hivyo kwa sababu unakazia utumishi ambao Mkristo anamtolea Yehova Mungu. Mkutano huo unatia mambo ya maisha ya kila siku na vilevile kutangazwa kwa “habari njema” kwa watu na kuwafundisha. Yanayozungumzwa vilevile ni namna ya kutolea wengine kweli ya Biblia, kulea na kutia watoto adabu, mwenendo, mambo yanayoonwa na Mashahidi wanapozitangaza “habari njema,” wanaposhindana kwa kufaa na magumu ya maisha, na mengine. Kipindi hicho kinatia ndani hotuba na mazungumzo ya watu wengi. Vilevile maonyesho yanatolewa katika mkutano huu juu ya kuzungumza habari za Biblia pamoja na wengine wanaotaka kusikia, na kuongozwa kwa mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu wanaopendezwa.
MAJUMBA YA UFALME NA FEDHA ZA KUENDESHEA KAZI
Mashahidi wa Yehova wanaita mahali wanapokutana “Majumba ya Ufalme.” Nyakati nyingine majumba ya kukodishwa yanatumiwa, lakini mara nyingi Mashahidi wanajenga majumba mazuri yasiyo ya gharama sana na yanayofaa kutumiwa. Kwa kawaida kazi yote ya kujenga inafanywa na Mashahidi wenyewe. Gharama za kujenga na kutunza Majumba ya Ufalme na gharama nyingine zote za kundi zinalipwa kwa michango ya kupenda kwa moyo inayotokana na washiriki wa kundi. Hakuna sahani za sadaka au kuchangiza fedha zinazopitishwa katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova, na hawaombi-ombi fedha kwa watu hata kidogo. Kisanduku cha michango kinawekwa katika jumba, na ye yote anayetaka kusaidia kulipia gharama anaweza kufanya hivyo akiona inafaa.—Mt. 6:3, 4.
Vivyo hivyo, kazi ya Mashahidi wa Yehova inayofanywa ulimwenguni pote inaendeshwa kwa michango inayotokana na wale wanaotaka kuona “habari njema ya ufalme” ikihubiriwa. (Mt. 24:14) Michango inayopokewa kutoka kwa watu wanaopendezwa kwa vitabu vya kusaidia kujifunza Biblia, inasaidia kidogo kulipia gharama ya kuchapwa na kuenezwa kwa vitabu hivyo.
Wakifahamu kwamba “kundi la Mungu aliye hai” ni “nguzo na tegemeo la kweli” duniani, Mashahidi wa Yehova wanaifuata Biblia sana ili wapate kujua mwundo na utendaji wake. Kusudi lao ni kwamba kundi hilo lipate kusaidia watu wengi wajifunze habari za mipango ya Mungu na kuizoea kweli, wamtukuze Mungu wa kweli.—1 Tim. 3:15, NW.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Baraza ya wazee Amerika
[Picha katika ukurasa wa 23]
Jamaa inaingia katika Jumba la Ufalme Australia
Kuhubiri Brazil
. . . katika Ivory Coast