Kumwendea Daktari wa Moyo Aliye Hodari Kupita Wote Nyakati Zetu
“Umechunguza moyo wangu, umefanya ukaguzi.”—Zab. 17:3, NW.
1. Kwa sababu gani ni jambo la kusisimua kumsikia daktari hodari akisema moyo wako umo katika hali barabara?
LO! MTU anasisimkaje anapochunguzwa na daktari hodari na kuambiwa kwamba moyo wake umo katika hali barabara! Mtu huyo anakuwa na hakika kwamba si vyepesi sana moyo wake kupatwa na hatari ya kuacha kufanya kazi, tena anakuwa na mataraja mazuri sana ya kuishi siku nyingi. Jambo hilo linaleta faraja nyingi hasa katika nyakati kama zetu ambapo ugonjwa wa moyo ndio Namba 1 kwa kuua watu kati ya magonjwa yote yanayojulikana.
2. Kwa sababu gani leo wanadamu wana deni ya madaktari hodari wa moyo?
2 Leo kuna madaktari wengi wa moyo wenye sifa, nao wanaendewa na watu wengi sana. Wanaganga magonjwa ya moyo ya namna nyingi. Wao wanapasua moyo. Hata wanaingiza katika moyo vidude vinavyoitwa valves vinavyotengenezwa na wanadamu ili kuelekeza damu upande mmoja tu. Wanafanya yote hayo ili kumsaidia mtu mwenye ugonjwa au kasoro ya moyo aendelee kuishi kwa muda fulani. Sisi tuna deni kubwa sana ya madaktari hao wa moyo walio hodari kwa sababu ya utumishi mzuri sana wanaowapa wanadamu.
3. Moyo wa kibinadamu una uwezo gani, na ni jambo gani ambalo madaktari wa moyo wameshindwa kufanya?
3 Moyo wa kibinadamu una uwezo au uwezekano wa kupiga-piga damu milele. Madaktari wanakubali hivyo. Loo! madaktari wa moyo wangestahili kupata zawadi iliyoje kama wangejua njia ya kufanyiza mioyo yetu kazi kwa ukamilifu hata tuweze kuishi milele tukiwa na afya kamili! Wao wamekwisha pata maarifa na ujuzi mwingi, lakini wameshindwa kufanya tendo hilo hodari lisilo na kifani. Kwa hiyo, tunapata kufahamu kwamba ni kazi bure kutegemea madaktari wa moyo ambao ni wanadamu wasiokamilika watutimizie jambo hilo.
4. Ni moyo wa nani ulioweka sifa ya kufanya kazi muda mrefu zaidi, na ni muda gani wa maisha uliotajwa na Musa ambao watu wanatazamiwa kuishi hata leo?
4 Lakini, Mfanyi wa moyo si kama madaktari hao. Yeye aliumba moyo ukiwa na uwezo wa kuzungusha-zungusha milele damu inayoendeleza uhai katika miili yetu. Yeye ana sifa isiyopata kifani ya kutendesha moyo wa kibinadamu kazi muda wa miaka mia tisa sitini na tisa. Moyo uliofanya kazi muda huo ni wa Methusela mwana wa Henoko, kwa maana yeye ndiye aliyeishi muda huo. Yeye ndiye aliyekuwa mtu wa nane katika ukoo wa mwanadamu wa kwanza duniani, yaani, Adamu. Moyo wa Methusela ndio unaopita mioyo yote kwa kuonyesha muda mrefu zaidi jinsi moyo wa kibinadamu unavyoweza kufanya kazi. Kulingana na maneno ya Musa mwanahistoria wa kale, aliyekuwa mwana wa Amramu, Methusela huyo mwenye maisha marefu alikufa mwaka 2370 kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Tangu wakati huo nguvu na utendaji wa mioyo ya kibinadamu zimepungua sana. Katika nchi zilizo na maendeleo mengi zaidi leo, kwa wastani wanaume wanatazamiwa waishi miaka 70. Kwa hiyo hakujawa na maendeleo ya kuupita muda uliotajwa na mwanahistoria Musa katika siku zake: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”—Zab. 90:10.
5. Kwa sababu gani tuyatii maagizo ya Mfanyi wa moyo, na ni nani anayeshiriki kuamua muda ambao moyo utaendelea kufanya kazi?
5 Kama vile mtengenezajl anavyojua habari zote kuhusu kitu alichotengeneza na kuweza kutoa maagizo juu ya jinsi ya kukitumia na kukitunza, ndivyo Mfanyi wa moyo wa kibinadamu anavyojua habari zote juu ya jinsi ulivyoumbwa na mambo yanayoupata—tena anajua habari hizo kuliko daktari ye yote anayechunguza mwili au kuupasua. Basi, inatupasa tuyatii maagizo Yake juu ya kuutumia musuli huo wa mwili unaohitajiwa kabisa. Sisi tulio na mioyo ndisi tunaoweza kuonyesha sana kama tunataka mioyo yetu iendelee kufanya kazi milele. Sasa kuna uwezekano wa kufanya mioyo yetu iendelee kutenda kazi milele. Kwa kuwa moyo ndio ulio katikati ya miili yetu, Biblia inataja maneno kama “moyo wa bahari” na “moyo wa nchi.”—Kut. 15:8; Mt. 12:40.
6, 7. (a) Kwa sababu gani ulizo linatokea juu ya moyo kushindwa kufanya kazi? (b) Ni nani anayefaa zaidi kuendewa ili atupashe habari hizo, na kwa sababu gani?
6 Muumba wa mwanamume na mwanamke anajua kilichomo katika “moyo” wa tatizo lililoko leo. Yeye aliifanya mishipa ili izungushe damu milele katika mwili wa kiumbe cha kwanza cha kibinadamu. Aliipa mishipa hiyo uwezekano wa kufanya hivyo. Mbona haijafanya hivyo? Ili tujue sababu, tunahitaji kumwendea Yeye, maana ndiye daktari wa moyo aliye hodari kupita wote leo.
7 Katika Neno Lake lililoandikwa, Biblia Takatifu, alieleza sababu hasa inayotufanya tufe. Tangu mwanzo mpaka mwisho Biblia inasema mengi juu ya moyo, nayo inautaja zaidi ya mara mia nane. Kwa kuwa daktari huyo amesomea sana moyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba anaijua kazi yake. Anaweza kutushauri vizuri kuliko daktari ye yote wa kibinadamu juu ya mambo tunayohitaji hasa ili tuifanye mioyo yetu iweze kututumikia milele. Hata Mfalme Daudi wa Yerusalemu, mheshimiwa mkubwa zaidi wa taifa la kale, alimwomba amchunguze mara nyingi. Ndiyo sababu Daudi aliweza kumwambia hivi: “Umechunguza moyo wangu, umefanya ukaguzi.”—Zab. 17:3, NW.
8. Tunaweza kuwa na uhakikisho gani tunapomjia Mungu atuchunguze na kutukagua mioyo yetu?
8 Tunaweza kumjia huyo daktari wa moyo aliye hodari kupita wote tukiwa na uhakikisho wa kwamba anaijua kabisa hali yetu hata tusipoweza kuieleza vizuri sana kwa maneno yetu wenyewe. Kuhakikisha hilo, tunasoma yafuatayo katika Biblia Takatifu, katika Warumi 8:27: “Yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya [roho] ilivyo.” Naam, anaelewa maana ya mambo tunayotaka kumwambia tunapomjia atuchunguze na kutukagua. Ikiwa mtu amekuwa akiishi maisha safi yanayolingana na Biblia, hana cha kuogopa. Ndiyo sababu mtunga zaburi wa kale aliweza kumwomba sana amchunguze, akisema: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu.”—Zab. 139:23.
“MAWAZO YA MOYO WA MWANADAMU”
9. Ni maelezo gani yaliyotolewa katika karne ya kumi na sita ya kuwako kwa mwanadamu juu ya jinsi moyo ulivyo, na ni mioyo ya nani iliyoendelea kupiga-piga mpaka Gharika ikapita?
9 Mwanzoni sana katika historia ya mwanadamu daktari wa moyo aliye hodari zaidi alieleza jinsi moyo wa mwanadamu ulivyo. Katika kitabu cha kwanza cha Biblia, katika sura yake ya sita, tunasoma habari za tabia iliyokuwako katika karne ya kumi na sita ya kuwako kwa mwanadamu. Maandishi yanasema: “[Yehova] akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. [Yehova] akaghairi kwa kuwa amemfanya mwanadamu duniani, akahuzunika moyo.” (Mwa. 6:5, 6) Hapo moyo wa mwanadamu na wa Mungu pia umetajwa. Kwa sababu ya kuhuzunika sana moyoni Yehova alinyesha gharika duniani pote katika mwaka ambao Methusela alikufa. Aliokoa jamaa moja tu ya kibinadamu, yaani, Nuhu na mkewe na wana wao watatu na mabinti-wakweze watatu, jumla ya nafsi nane za kibinadamu. Basi mioyo minane ya kibinadamu iliendelea kupiga-piga. Upesi baada ya kutoka katika safina isiyopenywa na maji walimwabudu Mhifadhi wao wa mbinguni. Upinde ulitokea angani ukawatakia mema huku wakiwa wameungana kumtolea Yehova Mungu dhabihu. Yehova alilionaje tendo hilo?
10, 11. (a) Wakati huo Yehova alisema nini juu ya moyo wa mwanadamu? (b) Alionyesha kwamba mioyo ya kibinadamu ingeendelea kupiga-piga muda gani, na wapi?
10 “[Yehova] akasikia harufu ya kumridhisha; [Yehova] akasema moyoni, Sitailaani nchi tena baada ya hayo kwa sababu ya wanadamu, maana mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake; wala sitapiga tena baada ya hayo kila kilicho hai kama nilivyofanya.”—Mwa. 8:21.
11 Ndipo Yehova alipoonyesha kwamba dunia yetu halisi itadumu milele. Mioyo ya kibinadamu itaendelea kupiga-piga hapa duniani ikiwa pamoja daima dawamu.
12. Wakati huo, kwa sababu gani moyo wa wanadamu ulikuwa na maelekeo mabaya tangu ujana wao?
12 Katika mwaka huo wa 2369 K.W.K. uliofuata gharika, kwa sababu gani Yehova alisema kwamba “mawazo [au “maelekeo,” NW] ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake”? Ni kwa sababu jamaa ya kibinadamu ilikuwa imerithi maelekeo hayo mabaya ya moyoni kwa mwanadamu aliyekuwa wa kwanza duniani, Adamu mumewe Hawa. Yehova alikuwa amempa Adamu amri hii: ‘Fanya mapenzi yangu uishi. Kosa kutii mapenzi yangu ufe.’ (Mwa. 2:15-17) Wakati Adamu alipojaribiwa baadaye juu ya kama alimpenda sana Muumba wake, yeye alichagua kumpendeza mkewe kwa kuelekeza moyo wake mwenyewe kwenye ubaya, asimtii Yehova Mungu Mpaji-Uzima wake.
13. Moyo wa Adamu uliacha kazi wakati gani, naye aliturithisha nini?
13 Mwanadamu hajaondoa kamwe maelekeo hayo mabaya ya moyo. Ilikuwa lazima Adamu apate adhabu ya dhambi aliyomtenda Muumba wake kwa makusudi. Katika umri wa miaka mia tisa na thelathini, moyo wa Adamu uliokuwa umeumbwa ukiwa na uwezo wa kufanya kazi milele bila tatizo ulikoma. Uliacha kupiga damu na kuieneza mwilini mwake. Basi Adamu akafa. Lakini kabla hajafa alizaa wana na mabinti wengi, kisha wakaoana wao kwa wao na kuzaa jamaa nyingi. (Mwa. 5:1-5) Adamu aliwarithisha wazao wake wote maelekeo mabaya ya moyo. Sisi sote tunayo leo. Ndiyo sababu maelekeo ya moyo wa wanadamu ni mabaya tangu ujana wao.—Rum. 5:12.
14. Usemi “kila kusudi analowaza moyoni mwake” unatokeza maulizo gani?
14 Bila shaka sisi sote tunakumbuka kwamba Mwanzo 6:5 inatumia maneno “kila kusudi analowaza moyoni mwake,” inapotaja hali yenye dhambi ya wanadamu. Je! tuelewe kutokana na maneno hayo kwamba Biblia inafundisha ya kuwa moyo wa mwanadamu unafikiri au kwamba wakati inapoutaja inakuwa ikimaanisha akili? Je! Mithali 16:9 na 19:21 zinaonyesha hivyo? Mithali hizo zinasema: “Moyo wa mtu huifikiri njia yake; bali [Yehova] huziongoza hatua zake.” “Mna hila nyingi [mipango mingi, NW] moyoni mwa mtu; lakini shauri la [Yehova] ndilo litakalosimama.” Vilevile, 1 Wakorintho 2:9 inasema: “Wala hayakuingia [hayakuwazika, NW] katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.” (Angalia Isaya 64:4 pia.) Kwa kuangalia juujuu inaonekana kama kwamba neno “moyo” linatumiwa likiwa na maana ya “akili,” uwezo wetu wa kufikiri.
15. Ni maandiko gani yanayoweza kutumiwa kuonyesha kwamba Biblia inaonyesha tofauti kati ya “moyo na “akili”?
15 Lakini, Biblia inaonyesha tofauti iliyo wazi kati ya “moyo” na “akili.” Kwa mfano mtume Paulo anatumia maneno ya Isaya 40:13 (Septuagint Version ya Kigiriki) na kusema: “Kwa maana ‘ni nani amepata kuijua akili ya Yehova, hata amfundishe yeye?’ Lakini sisi tunayo akili ya Kristo.” (1 Kor. 2:16, NW) Vilevile, katika Wafilipi 4:7 Paulo anasema: “Amani ya Mungu, ipitayo akili zote [Kigiriki: nous] itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” Na katika Mathayo 22:37 (NW) Yesu anatajwa kama akisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili zako zote.” Nayo Marko 12:30 inaongezea maneno haya: “Na kwa nguvu zako zote.” (Angalia Luka 10:27 pia.) Tusionyeshe tofauti ya maneno hayo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo tu. Ili usemi wetu upatane inatupasa tuionyeshe katika Maandiko yote yaliyoongozwa na Mungu, kuanza Mwanzo na kuendelea.
16. Kwa njia halisi moyo ni nini nao unachukuliwa kuwa nini kwa njia ya mfano?
16 Bila shaka akili ndio Ule uwezo wa ubongo tunaotumia kukusanya habari, kuzigawanya na kuchagua zinazotakiwa, kuzijumlisha na kukata maneno. Moyo nao ndio ule musuli wa mwili unaopiga-piga damu inayouingia na kuendelea kuieneza katika mwili mzima, hata katika ubongo. Moyo hauguswi na vitu vionekanavyo tu vinavyoupata mwili, bali unaguswa na misisimko pia na maoni ya ndani. Kwa sababu moyo unaweza kusukuma mtu afanye mambo, unachukuliwa kuwa ndiyo makao yanayoongoza matendo yake, nayo yanaweza kuwa ya upendo au chuki, woga au choyo.
17. Tuna mifano gani ya kuonyesha kwamba moyo una uwezo wa kuongoza watu watende mambo?
17 Ikitoa mfano wa kazi hiyo ya moyo ya kuongoza matendo ya watu, Kutoka 35:21, 26 inasema: “Wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza, na kila mtu ambaye roho yake ilimfanya kuwa apenda, nao wakaleta sadaka za kumpa [Yehova], kwa kazi . . . Na wanawake wote ambao mioyo yao iliwahimiza katika hekima wakasokota hizo singa za mbuzi.” (Vilevile Kutoka 36:2) Yehova alimwambia Musa hivi: “Kila mtu ambaye moyo wake wampa kupenda mtatwaa kwake sadaka yangu.” (Kut. 25:2) Moyo uliojazwa mambo unamwongoza mwenyewe kunena: “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake [nao moyo huwa unatunza sana mambo].”—Mt. 12:34.
18. Moyo unahusianaje na maneno yanayotokea kinywani, nao unafanyaje kazi pamoja na akili?
18 Ingawa moyo hauwezi kufikiri, unaweza kuamsha mawazo. Hivyo ndivyo Yesu alivyokuwa akimaanisha alipowaambia maneno yafuatayo watu wenye kushikilia desturi ya kunawa mikono: “Vitokavyo kinywani vyatoka moyoni; navyo ndivyo vimtiavyo mtu unajisi. Kwa maana moyoni hutoka mawazo mabaya, uuaji, uzinzi, uasherati, wivi, ushuhuda wa uongo, na matukano.” (Mt. 15:18, 19) Hakika mashuhuda ya uongo na makufuru (matukano) yanatoka kinywani, nayo mawazo maovu ya akili yanayotokea kinywani yanachochewa na maelekeo mabaya ya moyo. Naam, moyo ndio unaoelekeza mawazo, kwa maana unapenda mawazo hayo yaelekee katika njia fulani. Basi, Mwanzo 6:5 inasema vizuri inapotaja kwamba “kila kusudi analowaza [mwanadamu] moyoni mwake” lina maelekeo mabaya. Mawazo yanasaidiwa na moyo kufanya kazi.
19. Moyo unafananishaje hali ya kuthamini mambo?
19 Moyo unasitawisha upendo, tamaa nyingi na shauku nyingi juu ya kitu. Basi baadaye unakuja kuthamini sana mtu au kitu. Katika maana hiyo moyo unafananisha hali ya kuthamini hata mambo yanayohusika katika jambo fulani.
‘KUPUNGUKIWA NA MOYO’
20, 21. ‘Kupungukiwa na moyo’ kuna maana gani, nao watu wenye hali hiyo hawaepuki nini?
20 Basi Biblia inasema kwamba mtu anaweza kujipatia moyo au ‘kupungukiwa na moyo.’ ‘Kupungukiwa na moyo’ kunaonyesha kwamba mtu hana akili au hajali vile matokeo yanavyoweza kuwa. Mtu asiye na akili au asiyejali matokeo ya jambo anaweza kuwa na kusudi baya, lakini pia anaonyesha hathamini mambo. Hata ikiwa hajali hataepuka adhabu au matokeo mabaya. Kwa mfano, tunasoma hivi:
21 “Mtu ye yote [kama mwanamume aliyeoa] anayefanya uzinzi na mwanamke amepungukiwa na moyo; anayeufanya anaileta nafsi yake mwenyewe kwenye uharibifu.” (Mit. 6:32, NW) Vilevile: “Nilitazama chini, nipate kuwachungulia watu wasio na akili. Nilitaka kuona kati ya wana kijana mwanamume mwenye kupungukiwa na moyo, akipitia barabarani karibu na pembe aliko mwanamke huyo. . . . Na, tazama! alitokea mwanamke kumlaki, akiwa na vazi la malaya na werevu wa moyo.” (Mit. 7:6-10, NW) “Fimbo inaufaa mgongo wa mtu aliyepungukiwa na moyo.” (Mit. 10:13, NW) “Kwa sababu ya kupungukiwa na moyo wapumbavu ndio wanaoendelea kufa.” (Mit. 10:21, NW) “Mtu anayefuatia vitu visivyo na thamani amepungukiwa na moyo.” (Mit. 12:11) “Upumbavu ni furaha kwa mtu aliyepungukiwa na moyo, lakini mtu mwenye ufahamu ni yule anayesonga mbele moja kwa moja.”—Mit. 15:21, NW; vilevile 12:8, NW; angalia 28:16.
22. “Hekima ya kweli” inafananishwa na nini, nasi napata nini kwa kukubali ukaribishaji wake?
22 Hekima ya kweli inafananishwa na mwanamke safi mwenye adili, aliye tofauti na “mwanamke mwenye upumbavu.” Mwanamke huyo safi anakaribisha mtu ‘aliyepungukiwa na moyo’ aingie katika kao lake na kumfaidi sana mtu huyo kwa kula karamu pamoja naye. (Mit. 9:1-9, NW) Kwa hiyo inatupasa sisi leo tumsikilize “hekima ya kweli” na kuukubali ukaribishaji wake. Ndipo tutakapokuja kupata uzima wa milele tukiwa na upendeleo wa Mungu. Kwa kufanya hivyo tutakuwa ‘tukijipatia moyo,’ nayo Mithali 19:8, (NW) inatuhakikishia hivi: “Yeye anayejipatia moyo anaipenda nafsi yake mwenyewe. Yeye anayeulinda ufahamu atapata mema.”—Itofautishe na Mithali 9:13-18.
KUUELEKEZA MOYO
23. Tumerithi maelekeo gani ya moyo, kwa hiyo ni sala gani zilizomo katika Zaburi zinazopasa tumtolee Mungu?
23 Kulingana na mambo hayo yote ambayo tumeangalia, je! tunahitaji kumwendea daktari wa moyo aliye hodari kupita wote nyakati zetu? Kabisa! Kwa kuliangalia Neno lake lililoandikwa, lililo na maagizo yenye thamani nyingi, tunajifunza kwamba tumerithi maelekeo ya moyo yanayoelekea ubaya, hata tangu gharika ya siku za Nuhu. (Mwa, 8:21) Basi ni jambo la hekima tujifunze maagizo ya Neno la Mungu yenye kuwapa watu afya na uzima kisha tumpelekee sala kwa unyofu kama mtunga zaburi: “Uelekeze moyo wangu kwenye makumbusho yako, wala si kwenye faida [za kimwili].” (Zab. 119:36, NW) “Ee [Yehova], nimekuita, unijie hima . . . Usiuelekeze moyo wangu kunako jambo baya, nisiyazoelee matendo yasiyofaa, pamoja na watu watendao maovu; wala nisile vyakula vyao vya anasa.”—Zab. 141:1, 4; angalia Danieli 11:27.
24. (a) Ili tuzifurahie njia za Mungu tunaweza kutendaje kulingana na ukaribishaji huu: “Mwanangu, nipe moyo wako”? (b) Tunataka Mungu aikute mioyo yetu katika hali gani wakati aipimapo?
24 Mwendo ambao Muumba wetu mwenye upendo anatutaka tufuate ndio wenye hekima. Yeye anasema: “Mwanangu, nipe moyo wako; macho yako yapendezwe na njia zangu.” (Mit. 23:26) Anataka tumthamini jinsi anavyostahili kuthaminiwa, ili tumfurahie pamoja na sifa zake na njia zake kamilifu. Halafu tutajisikia tukitaka kuziiga njia hizo na kutembea katika zile zinazopendekezwa na Neno lake. Kufanya hivyo kutatuongoza tuyatii yanayosemwa katika Mithali 2:2: “Utege sikio lako kusikia hekima, ukauelekeze moyo wako upate kufahamu.’ Inafaa kufanya hivyo, kwa sababu Yehova ndiye “Mungu anayetupima mioyo yetu.” (1 The. 2:4) Atupimapo, tunataka akute kwamba tunampenda na kumwonea shauku nyingi, maana Ndiye tunayeabudu kwa unyofu, wala si miungu ya uongo. (Yos, 24:23; 1 Fal. 8:57, 58; 11:3, 4, 9) Ili jambo hilo liwe hivyo kwa upande wetu, lazima tuweze kusema mwishowe kama vile mtunga zaburi alivyomwambia Yehova Mungu: “Nimeuelekeza moyo wangu nizitende amri zako, daima, naam, hata milele.”—Zab. 119:112.
25. Kwa sababu gani tutake kuwa na afya ya kiroho kati ya ulimwengu mgonjwa, na inatupasa tufuate agizo gani la kimungu?
25 Leo, wakati ambao magonjwa yamewazidia sana wanadamu yajapokuwako maendeleo ya udaktari na utabibu wa kuponya akili, magonjwa ya kiroho ndiyo hatari zaidi. Magonjwa hayo yanaweza kuharibu maisha yetu ya sasa na vilevile mataraja yetu ya kupata uzima wa milele katika makao makamilifu yenye haki. Je! tunataka kuwa na hali njema ya kiroho sasa katikati ya ulimwengu mgonjwa? Ni hekima kutaka kuwa hivyo, kwa maana tunapata ahadi ya kuwa na uzima usiokwisha katika ushirika na Mungu na tengenezo lake la ulimwengu wote. Mioyo yetu ikitaka tuwe hivyo, tutafuata sana agizo hili lenye kuaminika lililotolewa na daktari wa moyo aliye hodari kupita wote nyakati zetu: “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”—Mit. 4:23.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kwa moyo tunamshukuru Mungu kwa sababu ya upendo wake kisha tunajisikia tukitaka kumtumikia