Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 11/15 kur. 3-25
  • Imani Katika Ufufuo—Je! Kuna Msingi wa Mambo ya Hakika?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Imani Katika Ufufuo—Je! Kuna Msingi wa Mambo ya Hakika?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TUMAINI KUBWA LA WANADAMU
  • USHUHUDA WA KIFO CHAKE YESU
  • USHUHUDA WA KUFUFUKA KWAKE KRISTO
  • USHUHUDA WA UNABII
  • MANENO YA YESU MWENYEWE
  • Ufufuo wa Yesu​—Kwa Nini Ni Muhimu Kwetu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Ufufuo wa Yesu—Je, Kweli Ulitukia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Tumaini la Ufufuo Ni Hakika!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • “Nina Tumaini kwa Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 11/15 kur. 3-25

Imani Katika Ufufuo​—Je! Kuna Msingi wa Mambo ya Hakika?

Je! wewe unaamini kwamba watu wanaweza kufufuliwa kutoka kwa wafu, waishi tena? Ikiwa ndivyo, kwa sababu gani? Ikiwa sivyo, kwa sababu gani? Ikiwa huamini ufufuo huenda ukasema hivi: ‘Mimi sijaona ye yote akifufuka kutoka kwa wafu.’ Lakini tukio fulani laweza kuwa halikutukia kwa sababu tu hatukuliona likitukia? Bila shaka, ili uamini lazima uwe na ushuhuda kwamba jambo hilo limetokea. (Ebr. 11:1) Je! ushuhuda kama huo unaweza kupatikana?

Ndiyo, unaweza kupatikana. Nao ni namna ya ushuhuda ambao ungetazamia kwa habari ya jambo la hakika au tukio​—ushuhuda wa watu waliolishuhudia wao wenyewe na wengine, pamoja na ushuhuda wa matokeo yake katika historia.

TUMAINI KUBWA LA WANADAMU

Tunao ushuhuda katika Biblia wa watu waliofufuliwa, kabla na baada ya kuonekana kwake Yesu duniani. (1 Fal. 17:21, 22; 2 Fal. 4:32-35; Yohana 11:43; Marko 5:41, 42) Lakini ushuhuda ulio wa maana zaidi​—ule unaotoa tumaini la ufufuo kwa wanadamu wote​—ni ufufuo wake Yesu Kristo. Kama ye yote kati yetu analo tumaini lo lote la uzima baada ya kufa, linategemea ufufuo wake Kristo kutoka kwa wafu. Sana sana fundisho hili ndilo lililowafanya mitume pamoja na Wakristo wa kwanza wadhihakiwe na kuteswa sana.​—Matendo 4:1-3; 7:32; 23:6, 10; 24:18-21.

Paulo alisema hivi mbele ya mkutano wa wanachuo na wanafilosofia katika Athene:

“[Mungu] ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.” Zaidi ya hayo, Paulo aliwaambia waamini Wakristo hivi: “Lakini kama hakuna [ufufuo] wa wafu, Kristo hakufufuka; tena kama Kristo hakufufuka, basi kuhubiri kwetu ni bure na imani yetu ni bure.”​—Matendo 17:31; 1 Kor. 15:13, 14.

USHUHUDA WA KIFO CHAKE YESU

Na tutoe na kuchunguza ushuhuda mwingine. Kwanza, tunazo habari za wale waliomwona Kristo akiuawa na kuzikwa. Hakuna shaka lo lote kwamba aliuawa na Warumi kwa amri ya viongozi wa Kiyahudi. Mapema kulikuwako jaribio la kumwua. (Luka 4:28, 29; Yohana 5:18; 8:59; 11:53) Walipokuwa wakitaka auawe, viongozi Wayahudi walipaza sauti mbele ya liwali wa Kirumi Pilato: “Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.” (Mt. 27:25) Vilevile walimtisha Pilato kwa tisho la kisiasa. (Yohana 19:12) Bila shaka wapinzani Wayahudi, sana sana adui wakubwa wa Kristo, makuhani wakuu pamoja na viongozi, hawangepatana wafanye mpango wa “kifo” chake cha uongo. Wangehakikisha kwamba amekufa. Kwa vyo vyote, mambo yalikuwa yamekwisha toka mikononi mwao naye alihukumiwa na kuuawa na Warumi. Tacitus (wa mwaka 110 W.K.) mwanahistoria Mrumi alisema juu ya Wakristo hivi: “Jina hilo linatokana na Kristo, aliyeuawa na liwali Pontio Pilato katika utawala wa Tiberio.”a Kitabu cha Wayahudi cha mafundisho vilevile kinayo habari ya kutundikwa kwa Yesu (juu ya mti). Habari hizi za kweli kutia na nyingine zisizo za Kikristo zinaunga mkono uhakika wa kwamba hata wapinzani wa Yesu hawakuwa na shaka lo lote juu ya ukweli wa kuwako kwake Yesu na wa kifo chake.

USHUHUDA WA KUFUFUKA KWAKE KRISTO

Kwa habari ya kufufuka kwake Kristo kuna watu wasiopungua wanne walioshuhudia waziwazi kwamba waliona Yesu baada ya kufufuka kwake, na mojawapo ya habari zao inatuambia kwamba alionwa na wanafunzi Wakristo zaidi ya 500. (Mt. 28:16, 17; Yohana 20:19; 21:1, 2; Matendo 1:15, 22; 1 Kor. 15:6-8) Walakini, huenda mtu akasema, ‘Ndiyo, lakini hizi zote ni habari za Biblia, zilizoandikwa na Wakristo. Tunajuaje kwamba ni za kweli?’

Kujibu ulizo hilo tunaweza kuuliza hivi: Ikiwa sivyo, unawezaje kueleza bidii ya watu wengi namna hiyo ya kuhubiri kufufuka huko? Hata adui zao walidai kwamba Wakristo walikuwa ‘wameupindua Yerusalemu na Uyahudi, ndiyo, ulimwengu wote’ kwa bidii yao ya kushuhudia kufufuka kwake Kristo. (Matendo 5:28; 17:6) Kuteswa kwao pamoja na mambo mengine yaliwafanya watawanyike na kulitangaza fundisho hili hivi kwamba ulimwengu wote uliotawaliwa na Warumi kutoka Rumi mpaka Mesopotamia, ulijua habari za bidii yao.

Kwa habari ya ukweli wa Wakristo hawa wa kwanza, angalia taarifa hii ya mwanafunzi wa Biblia A. J. Maas:b

“Kwa hiyo, kwa ufupi, uhakika wa Kufufuka kwake Kristo unashuhudiwa na zaidi ya mashahidi 500 waliomwona kwa macho yao wenyewe, ambao wepesi na unyofu wa maisha yao pamoja na mambo waliyoyaona yaliwafanya wasiweze kutunga hadithi ya uongo kama hiyo, [tena] waliishi wakati ambao kujaribu kudanganya kungalijulikana kwa vyepesi, [tena] ushuhuda wao haungewafaidi hata kidogo katika maisha haya, bali ungaliwafanya wapoteze vyote, [watu] ambao [sababu ya] ujasiri wao wa adili ulioonyeshwa na maisha yao ya kimtume unaweza kuwa ni kwa vile walivyohakikishwa na ukweli wa ujumbe wao. Vilevile uhakika wa Kufufuka kwake Kristo unashuhudiwa na unyamavu wa [viongozi Wayahudi] ambao walikuwa wamefanya yote wawezayo wazuie udanganyifu, ambao wangaliona udanganyifu wo wote kwa vyepesi, ikiwa ungekuwako, ambao walipinga tu mashahidi waliolala waliounga mkono ushuhuda wa Mitume, ambao hawakuwaadhibu walinzi wa serikali kwa kutojali kwao, na ambao hawakuweza kujibu ushuhuda wa Mitume Ila kwa kuwaogopesha tu ‘kwamba wasiseme na mtu ye yote katika jina hilo’ (Matendo, iv, 17). Mwishowe, maelfu na mamilioni, Wayahudi na Mataifa, walioamini ushuhuda wa Mitume hata kukiwako hasara yote iliyotokea kutokana na kufuata imani hiyo, kwa ufupi, mwanzo wa Kanisa, unahitaji sababu yake iwe uhakika wa Kufufuka kwa Kristo, kwa kuwa kutokea kwa Kanisa bila kuwako Ufufuo wa Kristo kungekuwa mwujiza mkubwa kuliko Ufufuo wenyewe.” linalopasa uzima na mauti, watu hawachukui.”

Kwa kutoa sababu kama hizo, tunaweza kukanusha uongo wa mashtaka ya adui za Yesu wanaosema kwamba ufufuo ulikuwa udanganyifu, kwamba mwili wake uliibiwa, au kwamba ilikuwa njozi ya wazimu, yalikuwa mapatano ya kufanya udanganyifu. Ni wazi kwamba mashahidi walioshuhudia ufufuo huo bila shaka hawakuwa watu wenye mamlaka au uwezo, ili waweze kuwashinda au kuwahonga walinzi waliokuwa wamewekwa kaburini. Kulikuwako uwezekano mdogo sana wa watu wengi hivyo kufanya mapatano ya kufanya udanganyifu, sana sana juu ya jambo ambalo halingaliwaletea faida zo zote za kibinafsi. Kushuhudia kwao ufufuo hakukufanywa kwa makusudi ya kichoyo; kuliwaletea mateso na kifo. Walitoa ushuhuda wao mahali pale pale adui zao wakubwa walipokuwa, ambapo udanganyifu wo wote ungefunuliwa. Tena hawakungojea, bali walitoa ushuhuda wao wakati uo huo, hasira ya Wayahudi ilipokuwa imefikia kilele chake. Sasa, basi, kama ingalikuwa njozi tu ya uongo au jambo tu la kuwazia, lingekuwa jambo walilolitazamia; walakini kuonekana kwa Yesu baada ya kufufuka kwake ni jambo lililowashangaza sana katika hali waliyokuwa nayo ya kukosa tumaini na kushuka moyo​—⁠jambo lisilotazamiwa. Kwa kweli, jambo hilo ndilo lililowapa ujasiri wa kutoa ushuhuda ambao haungevunjwa hata chini ya mateso yenye jeuri nyingi sana.

Katika jambo hili lenye maana kubwa sana, ni jambo lenye faida kuangalia sababu yenye nguvu sana ya mwanachuo mwingine na mchimbuzi wa mambo ya kale anayejulikana sana, George Rawlinson, aliyeandika hivi.c

“Wale walioanza kuongoka walijua kwamba wangehitajiwa wakati wo wote kufia dini yao. Walihubiri na kufundisha wakitazama upanga, msalaba, wanyama-mwitu, pamoja na mti wa mateso. . . . na kila mwandikaji wa kwanza aliyeunga mkono Ukristo, alikuwa akishindana na mamlaka ya serikali, na kwa sababu ya kuuunga mkono, alijitia katika hali ya kupana adhabu iyo hiyo. Imani inapokuwa jambo linalopasa uzima na mauti, watu hawachukui imani yo yote tu inayowapendeza vivi hivi: wala hawajitambulishi waziwazi na madhehebu inayoteswa, isipokuwa wawe wamechunguza sana madai ya dini hiyo, wakajihakikishia wenyewe kwamba ndiyo kweli. Ni wazi kwamba wale walioanza kuongoka walikuwa na mambo mengi ya kuwasaidia wajue usahihi wa kweli wa habari ya Kikristo kuliko tuliyo nayo; wangeweza kuwachunguza mashahidi na kuwauliza-uliza maulizo​—walinganishe habari zao​—waulize namna adui zao walivyoitikia habari zao​—wachunguze habari za Wapagani za wakati huo​—wachunguze ushuhuda kabisa na kwa ukamilifu. Ni lazima ikumbukwe kwamba ushuhuda unaongezeka na hayo yote yanafanyiza ushuhuda ambao mara nyingi haupatikani kwa habari ya matukio ya nyakati za zamani; nayo yanathibitisha bila shaka lo lote ukweli wa Habari ya Kikristo. Habari hiyo . . . haina uongo wo wote.”

USHUHUDA WA UNABII

Zaidi ya hayo, kuna mambo mengine yanayotoa ushuhuda. Ikiwa ufufuo wa Kristo ulitabiriwa hata kabla haujatokea, je! huo haungekuwa ushuhuda wenye kutokeza sana wa kuhakikisha kwamba ulitokea kweli kweli? Kwa sababu ushuhuda kama huo ungewezaje kutungwa, sana sana unapoeleza juu ya kifo cha Masihi mikononi mwa watu wake mwenyewe, ambao tangu siku za Ibrahimu, karibu miaka 2,000 mbele, walikuwa wakimtazamia? Katika Maandiko ya Kiebrania, yaliyotunzwa na Wayahudi kwa karne nyingi yakiwa kama kitabu chao cha sheria na vilevile kama habari ya historia ya taifa lao, tunaona ushuhuda uliotolewa mbele. Katika karne ya nane K.W.K., nabii Isaya alitoa maelezo juu ya kifo cha Yesu kwa amri ya watu wake mwenyewe, Wayahudi:

“Alidharauliwa na kukataliwa na watu. . . . Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. . . . Kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, . . . amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai. . . . Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; na pamoja na matajiri katika kufa kwake.”​—Isa. 53:3-9.

Kwa habari ya uhakika wa kwamba Mungu angalimfufua aishi tena, nabii huyo aliendelea kusema hivi: “Utakapofanya nafsi yake kuwa dhabihu kwa dhambi, ataona uzao wake, [akifufuliwa] ataishi siku nyingi, na mapenzi ya [Yehova] yatafanikiwa mkononi mwake; . . . mtumishi wangu mwenye haki atawafanya wengi kuwa wenye haki; naye atayachukua maovu yao.”​—Isa. 53:10, 11.

Danieli nabii wa baadaye alitabiri juu ya kifo chake cha dhabihu:

“Na baada ya yale majuma sitini na mawili [katika 33 W.K.], Masihi atakatiliwa mbali, naye atakuwa hana kitu; . . . ataikomesha sadaka na dhabihu [zilizotolewa katika hekalu la Wayahudi, mahali pake atoe dhabihu iliyo ya kweli ya uhai wake].”​—Dan. 9:26, 27.

Mfalme Daudi alitabiri kufufuliwa kutoka kaburi, naye mtume Petro anatumia unabii huo kwa Yesu Kristo. Siku 50 baada ya kufufuka kwake Kristo alisema na Wayahudi 3,000 waliokubali kwamba unabii huo ulikuwa ukimtaja Yesu wakakubali maelezo ya Petro. Petro alisema hivi:

“Mungu alimfufua [Yesu], akifungua uchungu wa mauti, kwa sababu haikuwezekana ashikwe nao. Maana ataja habari zake, Nalimwona [Yehova] mbele yangu sikuzote, kwa kuwa yuko upande wa mkono wangu wa kuume, nisitikisike. . . . Tena mwili wangu nao utakaa katika matumaini. Kwa maana hakuiacha [nafsi] yangu katika [kaburi]; wala hutamtoa Mtakatifu wako aone uharibifu. . . . Basi kwa kuwa [Daudi] ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi; yeye mwenyewe akitangulia kuyaona haya, alitaja habari za kufufuka kwake Kristo, ya kwamba [nafsi] yake haikuachwa [kaburini], wala mwili wake haukuona uharibifu. Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake.”​—Matendo 2:24-32; linganisha Zaburi 16:10.

Vilevile mtume Paulo alitaja kwamba Zaburi ya 40 ilipasa dhabihu ya Yesu Kristo. Paulo anaonyesha Yesu akisema hivi wakati wa ubatizo wake: “Mwili uliniwekea tayari . . . Tazama, nimekuja kufanya mapenzi yako.” Paulo anaongeza hivi: “Katika mapenzi hayo tumepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu.”​—Ebr. 10:5, 7, 10; Zab. 40:6-8.

Bila shaka kuna upatano mkubwa sana kati ya unabii huu uliotolewa karne nyingi mbele na kifo cha Yesu na ufufuo wake. Haingewezekana mambo haya yote ya hakika yanayohusika yaongozwe na Yesu kwa werevu, au mitume wake watunge hadithi yake.

MANENO YA YESU MWENYEWE

Zaidi ya hayo, wakati wa Sikukuu ya Kupitwa baada ya ubatizo wake, Yesu alianza kusema juu ya kifo chake na ufufuo wake uliokuwa unakuja, ingawa wanafunzi wake walifahamu maana ya mambo ambayo alikuwa akisema baada tu ya kuyashuhudia matukio hayo. Mtume Yohana anaandika juu ya mwanzo huo wakati huu wa mapema wa Yesu kushirikiana nao, Yesu aliposema kwa Wayahudi: “Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu nitalisimamisha.” Yohana anaongeza hivi: “Yeye alinena habari za hekalu la mwili wake. Basi alipofufuka katika wafu, wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa alisema hivi, wakaliamini lile andiko na lile neno alilolinena Yesu.”​—Yohana 2:19, 21, 22; linganisha Mathayo 12:40; 16:21-23; Marko 8:31; 10:33, 34.

Kwa kuwa ukweli wa ufufuo unalipasa tumaini peke yake kwa waliokufa pamoja na wanadamu wote wanaotazamia kufa, inapaswa kuwa habari ya kufikiriwa sana na wanadamu wote kila mahali, wala si wale tu wanaouamini Ukristo.

Watu wengi wanapenda uzima nao wangependa kuona ukiendelea milele pamoja na afya na uradhi. Wanatazama magazeti kila siku, wakitumaini kusikia habari njema za amani, maendeleo katika kumaliza magonjwa, na hali bora za uchumi. Wanasikia ushuhuda wa mashahidi juu ya matukio ya kila siku, na kukubali habari za kweli zilizoandikwa na watu, hata kutumia historia kama msingi wa kupangia mambo ya wakati ujao. Hivyo, basi, namna lilivyo jambo la maana zaidi na la akili, kuchunguza kwa unyofu ushuhuda mwingi uliopo wa kufufuka kwake Kristo, ambao ndio msingi wa tumaini na ahadi ya uzima katika furaha kwa wanadamu!

[Maelezo ya Chini]

a Annals (XV, 44).

b The Catholic Encyclopedia (Chapa ya 1913), Kitabu cha XII, uku. 790.

c The Historical Evidences of the Truth of the Scripture Records, kur. 225-227.

[Picha katika ukurasa wa 25]

“Kufufuka kwake Kristo kunashuhudiwa na zaidi ya mashahidi 500 waliomwona kwa macho yao wenyewe . . . [tena] waliishi wakati ambao kujaribu kudanganya kungalijulikana kwa vyepesi”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki