Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 12/15 kur. 12-17
  • Je! Unaweza Kuvumilia Majaribu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Unaweza Kuvumilia Majaribu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSUDI LA MAJARIBU NA UVUMILIVU
  • HEKIMA YA KUWEZESHA KUKABILI MAJARIBU
  • MATOKEO YENYE KUHARIBU YA MASHAKA
  • SHAURI KWA TAJIRI NA MASKINI
  • THAWABU YA UVUMILIVU
  • Yajapokuwa Majaribu, Shikeni Imani Yenu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Jinsi ya Kudumisha Shangwe Tunapovumilia Majaribu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Uvumilivu Unathawabishwa
    Huduma Yetu ya Ufalme—2004
  • Shikamana na Tengenezo la Yehova
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 12/15 kur. 12-17

Je! Unaweza Kuvumilia Majaribu?

“Mwione kuwa furaha yote, ndugu zangu, mnapopatwa na majaribu ya namna nyingi, mkijua kwamba sifa hii iliyojaribiwa ya imani yenu inatokeza uvumilivu.”​—Yak. 1:2, 3, NW.

1. Tunaposoma juu ya majaribu ambayo Wakristo walipata na wanayopata, ni maulizo gani huenda yakatokea akilini mwetu?

TUMESIKIA watu wakisema, “Sijui kama mimi ningalivumilia,” wanaposoma habari za mateso yaliyowapata Wakristo wa karne ya kwanza, pamoja na wale waliokuwako katika nchi za Nazi wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu, na katika nyakati za karibuni, katika nchi zote kuizunguka dunia. Walakini, hata katika maisha ya kila siku ya Wakristo wote, magumu yanatokea ambayo si kwamba tu yanakuwa vigumu kuyavumilia bali pia mara nyingi inakuwa vigumu kushughulika nayo. Je! mtu anayemwamini Kristo na ambaye ni mtumishi wa Mungu anaweza kuvumilia? Je! yeye anaweza kukabili (kukutana na) majaribu na magumu akiwa na hakika kabisa kwamba atayashinda?

2, 3. Ni kwa sababu gani barua ya Yakobo iliandikwa katika wakati uliofaa na ikawa yenye kufaa?

2 Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu Kristo, aliwaandikia watu waliokuwa wakipatwa na majaribu na waliokuwa wakikabili (wakikutana na) maulizo kama hayo. Maneno yake yanafariji sana, kwa kuwa aliandika si wakati tu Wakristo walipokuwa wakipatwa na mateso makali sana, bali pia walikuwa wakikaribia wakati ambao mambo ya taifa la Kirumi yangekuwa yenye msukosuko zaidi kwa Wakristo.

3 Muda mfupi tu baada ya Yakobo kuandika, Wakristo waliokuwamo Rumi wangelaumiwa bure na Mfalme Nero Mrumi kwa sababu ya moto mkubwa ambao ungeharibu sehemu kubwa ya mji huo. Bila shaka, hiyo ingefanya Wakristo wote walioko katika milki hiyo wateswe. Kisha, baadaye kidogo, katika mwaka wa 70, Yerusalemu pamoja na nchi ya Uyahudi ingeharibiwa na majeshi ya Warumi. Wakristo katika Yerusalemu, wakitii onyo la Kristo, wangekimbia wavuke Yordani kabla ya mji huo kuharibiwa, wakiokoa maisha zao, lakini wakipoteza mali zao na kupatwa na magumu mengi.

4. Barua ya Yakobo inawasaidiaje Wakristo wasipatwe na maoni mabaya yanayoonyeshwa katika Zaburi 73:2, 3, 5, 11-13?

4 Kwa hiyo barua ya Yakobo iliandikwa katika wakati unaofaa. Walakini Wakristo wanauhitaji uvumilivu wawe katika mateso makali au hapana. Kwa kuwa inawalazimu kuishi katika ulimwengu unaodharau kanuni za Kikristo, na zaidi ya hayo, wanapatwa na magonjwa na magumu mengine. Zaburi ya 73 inazungumza juu ya magumu yanayowapata watumishi wa Mungu ambayo hayawapati wale wasio Wakristo. Kwa sababu gani? Kwa sababu mara nyingi wale wasio Wakristo hawajali. Wao hawana tumaini na imani waliyo nayo Wakristo katika Mungu, nao hawasukumwi na moyo wao wampendeze. Barua ya Yakobo inawasaidia Wakristo wasiwe na maoni ambayo Asafu, mwandikaji wa zaburi hiyo, alikuwa nayo kwa muda. Asafu alisema:

“Nami miguu yangu ilikuwa karibu na kupotoka, hatua zangu zilikuwa karibu na kuteleza. Maana naliwaonea wivu wenye kujivuna, nilipoiona hali ya amani ya wasio haki. Katika taabu ya watu hawamo, wala hawapati mapigo pamoja na wanadamu [wengine]. Nao husema, Mungu ajuaje? Yako maarifa kwake aliye juu? Fahamu, ndivyo walivyo wasio haki, na kwa kustarehe sikuzote wamepata mali nyingi. Hakika nimejisafisha moyo wangu bure, nimenawa mikono yangu kwa kutokukosa.”​—Zab. 73:2, 3, 5, 11-13.

5. Yakobo aliandika barua yake kwa “kabila kumi na mbili waliotawanyika.” Alikuwa akiwaandikia nani?

5 Yakobo anaanza barua yake katika njia ya unyenyekevu, si kwa kuonyesha uhusiano wo wote wa kijamaa na Yesu Kristo, bali kwa kujiita “mtumwa wa Mungu, na wa Bwana Yesu Kristo.” Anaanza kuwaandikia “kabila kumi na mbili waliotawanyika” kwa “Salamu”! (Yak. 1:1) Hawa si wale kabila kumi na mbili wa Israeli wa asili. Yaliyomo katika barua hii yanaonyesha hivyo. Yakobo hangeandika namna alivyoandika ikiwa wasomaji wa barua yake wangekuwa Wayahudi tu. Zaidi ya hayo, kusalimiana katika njia hii lilikuwa jambo la kawaida kati ya Wakristo, sana sana wale waliokuwa Wayahudi, kama alivyokuwa Yakobo. Paulo analiita kundi la Kikristo “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16; linganisha Warumi 2:28, 29.) Wakati huo walikuwa wametawanyika katika kila sehemu ya Milki ya Kirumi. Jitihada za Paulo katika upande wa magharibi wa ulimwengu huo ulioendelea, pamoja na jitihada za Petro katika eneo la Babeli katika upande wa mashariki, zilisaidia sana kuleta ongezeko lililokuwa likifurahiwa na Wakristo. Petro aliandika barua yake ya kwanza kwa “utawanyiko, wakaao hali ya ugeni” katika sehemu za Asia Ndogo.​—1 Pet. 1:1.

KUSUDI LA MAJARIBU NA UVUMILIVU

6. Kwa sababu gani inampasa Mkristo ‘aione yote kuwa furaha’ anapopatwa na majaribu, nayo majaribu yana faida gani kwake?

6 Yakobo anaendelea hivi: “Mwione kuwa furaha yote, ndugu zangu, mnapopatwa na majaribu ya namna nyingi.” (Yak. 1:2, NW) Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alikuwa amesema hivi: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mt. 5:11, 12) Si kwamba tu kuna thawabu ya kimbinguni, bali pia kuna faida ya sasa, kama anavyoongeza Yakobo: “mkijua kwamba sifa hii iliyojaribiwa ya imani yenu inatokeza uvumilivu.” (Yak. 1:3, NW) Imani inayostahimili majaribu ni bora zaidi​—ni imani iliyojaribiwa. Imani ya namna hii inatokeza uvumilivu wenye nguvu zaidi kwa ajili ya jaribu litakalofuata.

7. Ni kwa sababu gani Mkristo hapaswi kujaribu kuepuka majaribu au achoke anapojaribiwa?

7 Mkristo hapaswi kujaribu kuepuka majaribu au aone kwamba amevumilia vya kutosha. Yakobo anasema hivi: “Lakini acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake, mpate kuwa wakamilifu na timamu katika mambo yote, bila kasoro yo yote.” (Yak. 1:4, NW) Kazi inayokamilishwa na uvumilivu katika Wakristo haipaswi kuzuiwa kwa kunung’unika, kulalamika au kuasi. Akivumilia kwa uaminifu bila kulalamikia Mungu au ndugu zake, na pasipo kuacha kuwaambia wengine makusudi ya Mungu kupitia kwa ufalme Wake, kwa sababu ya woga au kwa sababu ya kuchoka, atakuja kuwa mkamilifu na timamu katika mambo yote. Uvumilivu wa namna hiyo utamsaidia abadili utu wake. Atakuja kuwa mtu anayeweza kusaidia wengine, kwa akili nzuri, huruma na rehema. Pasipo kupatwa na majaribu na kuyavumilia, mtu hawezi kustahili katika njia hii. Yeye hawezi kuwa Mkristo anayekamilika.​—Linganisha Mathayo 5:48; 24:13.

HEKIMA YA KUWEZESHA KUKABILI MAJARIBU

8, 9. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tutapata hekima ya kutuwezesha kukabili (kukutana na) jaribu fulani na kulivumilia?

8 Tunawezaje kuwa na hakika kwamba tutakuwa na nguvu na hekima ya kukabili (kukutana na) tatizo (gumu) fulani​—jaribu lo lote​—⁠na kulivumilia? Yakobo anasema hivi: “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.” (Yak. 1:5) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tukiomba tupewe hekima ya kushughulika na (kumaliza) tatizo lo lote au jaribu tunalokabili, tutapewa.

9 Hii haina maana kwamba sikuzote tatizo hilo litatoweka au kwamba litatatuliwa mara hiyo, bali kwamba tutaweza kuchukua mwendo utakaofanya mema, kiroho, kwetu sisi na kwa wale wengine wanaohusika. Tutavumilia jaribu hilo mpaka mwisho na kulimaliza tukiwa Wakristo bora zaidi kuliko tulivyokuwa tulipolianza. Na wengine wanaotutazama, ambao wana mioyo mizuri, watasaidiwa.

10. (a) Tunapata jibu la namna gani tunapoomba mambo fulani? (b) Kwa habari ya sala tunayoomba tupate hekima ya kukabili jaribu, tunaweza kupata jibu katika njia gani?

10 Kuna mambo mengi ambayo huenda tukaomba na ambayo huenda yasijibiwe katika njia tunayotamani. Tutapata jibu, ambalo huenda likawa tofauti na lile tulilotazamia; litakuwa lile ambalo Mungu anajua kwamba linatufaa zaidi. Kwa kweli, mambo mengine ambayo tunaomba huenda yasitufaidi tukipewa kama tunavyoomba au tunavyotamani. Walakini, hekima ya kutuwezesha kukabili (kukutana na) jaribu tumehakikishiwa na Mungu. Tuna hakika ya kupata hekima inayohitajiwa tukiiomba katika njia inayofaa. Tutapewa hekima hiyo katika mojawapo au zaidi ya njia hizi tatu: (1) Maandiko fulani ambayo yatatupa jibu tunalohitaji yataelekezwa kwetu, ama kwa kujifunza sisi wenyewe au kupitia kwa ndugu zetu. (2) Hali au matukio yanayoongozwa na Mungu yatatusaidia tuone katika njia iliyo wazi jambo la kufanya. Vipingamizi fulani huenda vikaondolewa. (3) Malaika wa Mungu wanaweza kuongoza roho zetu katika mwendo unaofaa.

11. Mungu ‘anatoaje kwa ukarimu, pasipo kukemea’?

11 Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, yaani, katika roho ya wepesi, ya nafsi yote. (Efe. 3:20; 1 Yohana 5:14, 15) Yeye anafanya hivyo pasipo kukemea. Hali, ukimwomba mwanadamu, huenda akajibu, ‘Hilo ni ombi la upumbavu.’ Hata huenda akakudharau. Au, baada ya kumwomba mara kadha, huenda akakosa subira amalize maneno yako mara moja kwa kukataa. Walakini sivyo Mungu. Yeye hasemi hata kidogo, ‘Ombi la upumbavu namna gani!’ Wala hamfanyi mtu ajione kuwa mtu wa chini. Yeye hakukemei kwa sababu ya mwenendo wako wa zamani, kama wanavyofanya wanadamu mara nyingi. Yeye anathamini sana mtu ambaye ana imani na anayehangaikia sana jambo fulani analotaka hivi kwamba analiomba mara nyingi.​—Linganisha Luka 18:1-14.

12. Tunahakikishiwa nini na maneno ya Yakobo, “naye atapewa”?

12 “Naye atapewa.” Hekima tunayopata chini ya uongozi wa roho ya Mungu, ni mojawapo ya mambo ambayo Mungu hutamani sana kuwapa watumishi wake. Anafurahi sana tunapomwomba hekima. Tunapata mema na kusaidiwa tunapoomba tulifahamu Neno la Mungu kama linavyotumika katika hali yetu. (1 Kor. 2:9, 10) Yesu alisema hivi: “Ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa [roho takatifu] hao wamwombao?”​—Luka 11:13; Marko 11:24.

MATOKEO YENYE KUHARIBU YA MASHAKA

13. Mtu anapaswa kuomba hekima akiwa na maoni gani, na kwa sababu gani?

13 “Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku.” (Yak. 1:6) Mwenye kuomba lazima awe na imani katika Mungu na Mwanawe, na aamini utayari wao wa kutoa kinachohitajiwa, naye hapaswi kuwa na wazo jingine ila faida za imani ya Kikristo na makusudi ya Mungu. Yeye hapaswi kuwa akiomba kitu fulani huku akitaka kitu kingine. Ombi lake lapaswa litoke ndani kabisa moyoni mwake. Ama sivyo yeye ni kama wimbi la bahari, linalopeperushwa huku na huku. Akibadilishwa na kila upepo​—⁠kila namna ya uvutano wa nje, kila namna ya woga.

14. Yakobo anasema nini zaidi kwa habari ya mtu mwenye mashaka?

14 Kwa habari ya mtu kama huyo, Yakobo anafikia uamuzi huu: “Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa [Yehova]. [Ni] mtu wa nia mbili [Kigiriki, “nafsi mbili”] husita-sita katika njia zake zote.” (Yak. 1:7, 8) Yeye ana nia mbili, akijaribu kufuata njia mbili wakati ule ule, akigawanyika katika mambo mawili ya Mungu; au akivutwa na mambo mengine zaidi ya Neno la Mungu, akiwa na wazo moja kisha na jingine. (Linganisha Mathayo 6:24.) Hata huenda akasita kumpelekea Mungu jambo hilo. Yeye ana shauku katika wakati mmoja na kuvunjika moyo wakati mwingine. Yeye yuko hivyo si kwa habari ya sala (maombi) tu bali pia katika mambo mengine yanayohusiana na imani. Yeye si Shahidi wa Yehova aliye imara, anayeweza kutumainiwa. Kinyume chake, Maandiko yanasema hivi: “Pasipo imani haiwezekani kumpendeza [Mungu]; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao [kwa bidii].”​—⁠Ebr. 11:6.

SHAURI KWA TAJIRI NA MASKINI

15. Ndugu maskini anawezaje kufurahi “kwa kuwa ametukuzwa”?

15 Akiendelea kufikiria majaribu, Yakobo anazungumza juu ya hili linalofuata ambalo ni la kawaida: “Ndugu asiye na cheo na afurahi kwa kuwa ametukuzwa.” (Yak. 1:9) Wakristo wengi walikuwa hivyo, na leo ni watu wa hali ya chini katika kuzaliwa kwao. (1 Kor. 1:26) Wakiwa katika hali ya chini, hali yao ya uchumi inaweza kuwaletea magumu zaidi wakati wa mateso. Pia, wengine waliokuwa matajiri walifanywa kuwa maskini na mateso. Hata hivyo, wangeweza kufurahi kwa sababu, katika kundi la Kikristo, hali yao ya chini haiwanyimi faida. Wao ni watoto wa Mungu, ‘wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu.’ (Efe. 2:19) Mtu aliye maskini anaweza kusahau umaskini wake wa kidunia kwa sababu ya utajiri ulio mkuu zaidi wa uhusiano alio nao na Mungu na Kristo pamoja na upendo wa ndugu zake Wakristo. Naye anaweza kufurahi kwamba anaweza kusaidia wengine kwa kuwagawia “habari njema.” Yeye anaweza kujisifia mambo haya.

16. Ndugu aliye tajiri anawezaje kufurahi “kwa kuwa ameshushwa”?

16 Kwa habari ya tajiri ambaye amekuwa Mkristo, anaweza kufurahi “kwa kuwa ameshushwa.” Sasa jambo ambalo ni la maana si utajiri wake. Mahali pa majivuno ambayo yanaletwa na utajiri mara nyingi, roho ya Kristo ni ile ya upole wa akili pamoja na unyenyekevu. (Flp. 2:3-8) Yeye anaweza kufurahia ufahamu wa kwamba sasa, kupitia kwa fadhili zisizostahilika za Mungu, anaweza kuuona “udanganyifu wa mali” na kwamba mali si vitu vya kutumainiwa. (Mt. 13:22) Anajua vilevile kwamba kutumia wakati na jitihada ajiwekee lundo kubwa la mali za ulimwengu ni kupoteza wakati na kunaelekea kuharibu hali ya kiroho ya mtu pamoja na afya yake. Yakobo anatoa sababu ya hili: “Kwa maana kama ua la majani atatoweka.” Anajua kwamba mali zake haziwezi kuendeleza maisha yake. “Maana jua huchomoza kwa hari, huyakausha majani; ua lake huanguka, uzuri wa umbo lake hupotea; vivyo hivyo naye tajiri atanyauka katika njia zake [za maisha].”​—Yak: 1:10, 11.

17. Toa maelezo juu ya masimulizi ya Yakobo ya yale yanayompata tajiri na “uzuri” wake.

17 Majani yananyaushwa na jua nao uzuri wake unapotea. Vivyo hivyo, tajiri anapozeeka na kufa, fahari ya mali iliomzunguka na ‘kumfanya kuwa mzuri’ inatoweka. Bila shaka, maskini anakufa vilevile, walakini yeye hakutokeza hata kidogo uzuri wenye kuchanua kama ule wa tajiri. Walakini “uzuri” huu wa tajiri unachukuliwa na warithi wake pamoja na wengine, na mara nyingi ile “milki” aliyokuwa akijenga inavunjwa au miradi aliyokuwa akifuata inaachwa. Anapokuwa “katika njia zake [za maisha,]” labda akiwa katika safari yenye shughuli (kazi) ya biashara au anapoendeleza mpango fulani ili apate mali zaidi, anakufa. Mara nyingi tajiri anakufa kabla ya kupata nafasi ya kujifurahisha mali zake. Kwa upande mwingine tajiri anayekuwa Mkristo anaweza kufurahia mali zake kwa kuzitumia katika kuendeleza faida za ufalme wa Mungu. Mara nyingi anaweza kupanga atumie wakati mwingi zaidi katika kutangaza “habari njema” na anaweza kutoa michango ya kuendeleza mahali pa mikutano na ya kuendeleza kazi ya Ufalme kama inavyofanywa ulimwenguni pote.

THAWABU YA UVUMILIVU

18. Yakobo anaeleza juu ya thawabu gani kwa habari ya mtu anayevumilia jaribu kwa uaminifu?

18 Ijapokuwa Yakobo anaonyesha faida zinazofuata mara moja baada ya kuonyesha uvumilivu katika mstari wa 3 na 4, katika mstari wa 12, anatilia mkazo matokeo yake ya mwisho​—⁠thawabu inayotokana na kusimama imara wakati wa majaribu. Anaandika hivi: “Mtu mwenye furaha ni yule anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu atakapokubaliwa atapokea taji ya uzima, ambayo Yehova aliiahadi kwa wale wanaoendelea kumpenda.” (Yak. 1:12, NW) “Taji ya uzima” ni zawadi ya uzima ambayo Mungu anawapa “wale wanaoendelea kumpenda” wanapopitia katika majaribu mengi ambayo Mungu anataka yafanye kazi pamoja kuwakamilisha watumishi wake, ikiwa watayavumilia wakiwa imara, pasipo kunung’unika, na kuyashinda, kwa msaada wake. (Rum. 8:28) Hii haimaanishi kwamba yeye anajipatia haki ya kuwa na uzima kwa sababu ya kazi zake au uvumilivu wake, kwa kuwa uzima ni zawadi inayotolewa bure kwa kumwamini Yesu Kristo. Walakini, Mkristo anayevumilia ameonyesha kwamba ana imani hiyo. Sifa yake imejaribiwa ikaonekana kuwa yenye nguvu na kamilifu.

19. Kwa hiyo, basi, maoni yanayofaa ya Kikristo juu ya majaribu ni maoni gani?

19 Kwa hiyo, Mkristo ANAWEZA kuvumilia majaribu yo yote yanayompata, hata yale makali zaidi. Yeye hapaswi kuingia katika majaribu hayo akitumainia nguvu zake mwenyewe. Hekima pamoja na nguvu za Mungu zapaswa kutafutwa kupitia kwa sala katika jina la Yesu Kristo, ambaye, alipokuwa duniani, aliweka mfano mkamilifu wa uvumilivu. Mkristo anaweza kuwa na tumaini kabisa na uhakikisho huu wa mtume Petro wenye kufariji: “Baada ya kuteswa kwa muda, Mungu wa fadhili zote zisizostahilika, aliyewaitia utukufu wake wa milele katika umoja na Kristo, yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu.”​—1 Pet. 5:10, NW; Rum. 8:35-39.​—

Kutoka The Watchtower July 15, 1978.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki