Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Yesu alisema, “kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapopita.” Hiki ni kizazi kipi, nacho kina muda wa urefu gani?
Mitume wa Yesu walipomwomba “ishara” ya kuwapo kwake na ya mwisho wa taratibu ya mambo, alitoa unabii wake unaojulikana sana juu ya vita, njaa, matetemeko ya nchi ambayo yangetukia pamoja na kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme kabla ya mwisho kuja. Mt. (24, NW, 25; Marko 13; Luka 21) Vilevile alisema hivi: “Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.”‘—Mt. 24:23.
Kulingana na Biblia na utimizo wa matukio ya historia, Mashahidi wa Yehova wamesema mara nyingi kwamba unabii wa Kristo ungekuwa na utimizo wa mara mbili: Kwanza, kuanzia mwaka 33 W.K. mpaka uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka 70 W.K.; wa pili, utimizo ulio mkubwa zaidi katika huu “wakati wa mwisho” tangu 1914 W.K.
Hata hivyo, wengine wanaotoa maelezo ya Biblia wameshindwa kujua namna hizi mbili za unabii huu. Kwa hiyo wameshikilia kwamba kwa neno “kizazi” Yesu alimaanisha jamii au watu, kama vile watu Wayahudi au jamii ya wanadamu waovu ambao wamekuwapo karne zote zilizopita. Hata huenda wakataja andiko la 1 Petro 2:9, ambalo, katika Authorized Version, huliita kundi la Kikristo lililotiwa mafuta “kizazi kilichoteuliwa.” Walakini, wanachuo wa Biblia sasa wamefahamu kwamba neno hilo la Kigiriki katika 1 Petro 2:9 linapaswa kutafsiriwa “jamii” nalo ni tofauti na neno lililotafsiriwa “kizazi” katika Mathayo 24:34.
Yesu hakuwa akimaanisha jamii fulani ya watu ambao wangekuwako katika muda wa karne nyingi au hata Wakristo tu. Kwanza yeye alikuwa akimaanisha wasikilizaji wake pamoja na Wayahudi wengine wa wakati huo. Jambo linaloonyesha hivyo ni uhakika wa kwamba mapema siku iyo hiyo, alipokuwa akiwalaumu viongozi wa kidini, Yesu alisema juu ya namna walivyowaua manabii akaongeza hivi: “Mambo hayo yote yatakuja juu ya kizazi hiki.” (Mt. 23:36) Mambo hayo yote yalikipata kizazi hicho wakati Wayahudi waliokuwa katika Yerusalemu walipopatwa na uharibifu mkali katika mwaka 70 W.K. (Luka 3:16, 17) Vilevile huo ulikuwa ndio ‘mwisho wa taratibu ya mambo ya Kiyahudi’ katika utimizo wa kwanza wa unabii wa Kristo.
Hii inatusaidia kufahamu “kizazi” katika Mathayo 24:34. Neno hili “kizazi” linaweza kutumiwa kumaanisha (1) watu wote waliozaliwa na kuishi wakati ule ule, au (2) muda wa maisha kwa wastani tangu kuzaliwa kwa wazazi na kule kwa watoto wao, mara nyingi miaka kati ya 20 na 30. Yesu alimaanisha kizazi kipi? Kwa wazi si kile cha pili, kwa kuwa katika matumizi yake ya kwanza “kizazi” kiliendelea kuanzia mwaka 33 W.K. mpaka 70 W.K., au miaka isiyopungua 37.
Vilevile, ni wazi kwamba alipotumia neno “kizazi” Yesu hakumaanisha vitoto vya Kiyahudi tu vilivyozaliwa katika mwaka wa 33 W.K. Luka anaeleza kwamba baada ya Yesu kuulizwa na Mafarisayo wakati ufalme ungekuja, aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kwanza, [Mwana wa Adamu] hana budi kupata mateso mengi, na kukataliwa na kizazi hiki.” (Luka 17:20-25) Bila shaka yeye hakukataliwa hivyo na vitoto vichanga vilivyozaliwa karibuni. Vivyo hivyo, namna mambo yalivyotukia inaonyesha kwamba “kizazi” alichomaanisha katika Mathayo 24:34 kilitia ndani wasikilizaji wake na wengine ambao wangefahamu utimizo wa maneno yake kuanzia mwaka wa 33 W.K. mpaka Yerusalemu ulipoharibiwa.
Kwa hiyo, tunapoutumia katika wakati wetu, kulingana na akili nzuri neno “kizazi” haliwezi kutumiwa kuhusu vitoto vilivyozaliwa wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Linahusu wafuasi wa Kristo pamoja na wengine walioona vita hiyo pamoja na mambo mengine ambayo yametukia katika utimizo wa “ishara” ya Yesu yenye mambo mengi. Wengine wa watu hawa ‘hawatapita, hata’ mambo yote yaliyotabiriwa na Yesu yatakapotukia, kutia na mwisho wa taratibu hii mbovu iliyopo.
Yesu hakuwatia moyo wafuasi wake wajaribu kuhesabu urefu barabara wa “kizazi” hiki. (Zab. 90:10) Mahali pa kujaribu kuhesabu ni miaka mingapi inayobaki, tukiweka kadiri iliyo kubwa zaidi, kabla ya mwisho kuja, Wakristo wanapaswa kukumbuka onyo la Yesu: “Kesheni . . . kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”—Mt. 24:42-44.
Tuna ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba Mathayo sura ya 24 inatimizwa sasa, wakati huu wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” Ushuhuda mmoja ni kuhubiriwa duniani pote kwa habari njema za ufalme wa Kimasihi uliosimamishwa, ambazo Yesu alisema kwamba lazima zihubiriwe kabla ya mwisho kuja. (Mt. 24:14) Kwa hiyo, mahali pa kuvutwa katika kukisia-kisia juu ya tarehe tusiyoweza kujua, Wakristo wa kweli na washiriki kwa bidii katika kazi hii ya maana ya kuhubiri, wanapotazamia mbele kwa uhakika kwenye utimizo wa maneno ya Yesu juu ya “kizazi hiki” yaliyo katika Mathayo 24:34.