Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w79 6/1 kur. 17-22
  • Kustahili Kuwa Waalimu Katika Kundi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kustahili Kuwa Waalimu Katika Kundi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “HUKUMU KUBWA ZAIDI”
  • “N’NANI ALIYE NA HEKIMA NA UFAHAMU?
  • SIFA ZA KUMFANYA MTU ASISTAHILI
  • SIFA ZINAZOSHIRIKISHWA NA HEKIMA ITOKAYO JUU
  • “Ni Nani Aliye na Hekima na Mwenye Uelewaji Kati Yenu?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?
    Mkaribie Yehova
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Ninaweza Kufanya Nini ili Nielewane na Mwalimu Wangu?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
w79 6/1 kur. 17-22

Kustahili Kuwa Waalimu Katika Kundi

“N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima.”​—Yak. 3:13.

1. Sababu gani ni jambo la maana sana kwamba wale wanaotumikia kama waalimu katika kundi la Kikristo wawe wanastahili?

MAONGOZI ya mwalimu yanaweza kuwa ama yenye faida au yenye kudhuru. Sana sana ndivyo ilivyo kwa habari ya ibada. Akiwataja Mafarisayo, Yesu Kristo alisema hivi: “Hao ni viongozi vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.” (Mt. 15:14) Wote waliofuata kwa ujinga mafundisho ya Mafarisayo yasiyopatana na Maandiko walikuwa wakielekea kwenye uharibifu wa kiroho na kifo, hali wale waliotii mafundisho yanayofaa ya Mwana wa Mungu walikuwa wakifuata njia iongozayo kwenye uzima. (Mt. 7:13-20, 24-27) Kwa kuwa maisha yanahusika ni jambo la maana kwamba wale wanaotumikia kama waalimu katika kundi la Kikristo wawe wanaume wanaostahili.

2. Sababu gani mtume Paulo angeweza kusema, “mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote”?

2 Yale ambayo mtume Paulo aliwaambia wazee wa kundi la Efeso kuhusu yeye mwenyewe yanaonyesha kwamba njia ambayo katika hiyo mwalimu Mkristo hushughulika na daraka lake yaweza kumfanya mtu awe au asiwe na hatia ya damu. Mtume huyo alisema hivi: “Nawashuhudia wote siku hii ya leo, ya kuwa mimi sina hatia kwa damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Wakati wo wote ambao wazee wa Efeso wangekuwa waasi na kuanza kupotoa Maandiko na kujiangamiza kiroho na kuwadhuru waamini wenzao, Paulo hangelaumiwa kwa sababu ya hilo. (Linganisha Matendo 20:29, 30.) Wao wenyewe ndio wangalikuwa na hatia ya damu. Mtume huyo alikuwa amefanya yote awezayo kuwahubiri habari ya “kusudi lote la Mungu.” Yeye hakuwa amekataa kuwajulisha jambo lo lote lililokuwa la lazima kwa ajili ya wokovu. Yeye hakuwa na tamaa ya kupendwa na watu wengi kwa kufurahisha wasikilizaji au kwa kuepuka kuzungumza habari zenye kufunua maoni mabaya, maneno na matendo.​—Linganisha 2 Timotheo 4:3, 4.

3. Kupatana na mfano wa Paulo, twaweza kutazamia nini kutoka kwa mwanamume anayestahili kuwa mwalimu katika kundi la Kikristo?

3 Kupatana na mfano wa mtume Paulo lazima mwanamume anayestahili kuwa mwalimu katika kundi la Kikristo ajue na kufahamu yote yaliyo ya muhimu kwa ajili ya wokovu ili kufundisha kwake kusiwe na kasoro kubwa. Vilevile lazima awe na nia ya kulihubiri “kusudi lote la Mungu,” bila kujari maoni ya kundi. Huenda kukawako nyakati ambazo kundi linaitikia vizuri karipio na sahihisho linalotolewa kutokana na Neno la Mungu. Walakini huenda vilevile kuwako nyakati ambazo wengi hawatataka kuguenza njia zao. Hata hivyo, mwalimu Mkristo lazima aendelee kushikamana na Neno la Mungu kwa uaminifu katika kutoa msaada wa kiroho. Ikiwa wengine wana maelekeo mabaya, lazima ajizuie mwenyewe asikose kuwasubiri bali aendelee kuitangaza kweli. Kwa habari hii, mtume Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho.”​—2 Tim. 4:2.

4. Shauri katika Yakobo 3:1 lilielekezwa kwa akina nani?

4 Kwa kuwa mafundisho sahihi yanahusiana na wokovu wa mtu, kufundisha ni daraka linalopaswa kukabidhiwa wanaume wale tu wanaostahili. Mwanafunzi Mkristo Yakobo aliandika hivi: “Ndugu zangu, wengi wenu msiwe walimu.” (Yak. 3:1, Habari Njema kwa Watu Wote) Onyo hili la upole lililoongozwa na Mungu halikutolewa kwa kusudi la kuwavunja moyo wanaume wanaostahili wasiwe waalimu, kwa kuwa vilevile Maandiko yanasema: “Ikiwa mwanaume ye yote anafikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi nzuri.” (1 Tim. 3:1, NW) Yakobo alikuwa akielekeza maneno yake kwa wanaume waliokuwa wakijifanya waalimu wa waamini wenzao ijapokuwa hawakuwekwa au hawakustahili kufundisha. Wanaume hawa walitaka ukuu na mamlaka yaliyoshirikishwa na kuwa mwalimu, pasipo kujari sifa. Lazima wawe walikuwa wanaume kama wale walioelezwa na mtume Paulo kuwa “wapenda kuwa waalimu wa sheria, ingawa hawayafahamu wasemayo wala mambo yale wayanenayo kwa uthabiti.”​—1 Tim. 1:7.

“HUKUMU KUBWA ZAIDI”

5. Sababu gani waalimu ‘wanapokea hukumu kubwa zaidi’?

5 Kwa sababu ya kutofahamu kabisa au kwa kutothamini “kusudi lote la Mungu,” wenye kujifanya waalimu walihitaji kujulishwa juu ya hali yenye hatari ya mwalimu. Yakobo alionyesha kwamba waalimu, kutia na yeye, ‘watapata hukumu kubwa zaidi.’ (Yak. 3:1) Kwa kuwa mwalimu husimama mbele ya wengine akiwafundisha au kuwaongoza, mengi zaidi yanahitajiwa kutoka kwake kuliko kutoka kwa wengine. Hii inapatana na kanuni hii ya Maandiko: “Naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi.” (Luka 12:48) Kwa hiyo, maneno na matendo ya mwalimu huchunguzwa zaidi ya yale ya Wakristo wengine. Zaidi ya hayo, mtu akikosea katika kufundisha kwake, nayo hiyo itokeze magumu kati ya washiriki wa kundi, au matendo yake yakitoa sababu halali ya kuchukizwa, yeye anahukumiwa vikali sana na Yehova Mungu kupitia kwa Bwana Yesu Kristo. Mwana wa Mungu alisema hivi: “Basi, nawaambia, Kila neno lisilo maana, watakalolinena wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu. Kwa kuwa kwa maneno yako utahesabiwa haki, na kwa maneno yako utahukumiwa.”​—Mt. 12:36, 37.

6. Kulingana na Yakobo 3:​2, ni hatari gani inayokamatana na kufundisha?

6 Mwanafunzi Yakobo anaendelea kutoa sababu: “Twajikwaa sisi sote katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yak. 3:2) Kwa kuwa hata waalimu walio mifano mizuri sana wanaelekea kukosea kwa maneno, hatari ya kufanya hivyo ni kubwa zaidi kwa habari ya wanaume wasiostahili. Na kadiri mwalimu ye yote anavyozidi kufanya makosa, ndivyo matokeo yanavyozidi kuwa yenye kudhuru kundi zaidi na ndivyo hukumu ya mtu huyo inavyozidi kuwa kubwa.

“N’NANI ALIYE NA HEKIMA NA UFAHAMU?

7. Ulizo linalopatikana katika Yakobo 3:13 jinafunua nini juu ya kustahili kwa mwanamume kuwa mwalimu?

7 Kwa sababu ya hatari inayohusiana na kuwafundisha wengine, inaweza kuulizwa kwa kufaa hivi: Kwa kweli ni nani anayestahili kufanya hivyo? Mwanafunzi Yakobo aliuliza ulizo linalofanana na hilo: “N’nani aliye na hekima na ufahamu?” (Yak. 3:13) Ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba Yakobo hakuuliza tu: N’nani aliye na uwezo mzuri wa kusema?’ Ili mtu awe mwalimu bora, anahitaji zaidi ya kuweza tu kusema vizuri. Hekima na ufahamu ni mambo ya lazima. Mtu mwenye hekima anamwogopa Yehova Mungu inavyofaa naye anajua namna ya kutumia maarifa katika njia itakayoleta matokeo mazuri. (Mit. 9:10) Mtu aliye na ufahamu anafahamu jambo, analielewa (analifahamu) na kuona namna sehemu mbalimbali za hali fulani zinavyohusiana. Mtu kama huyo anafahamu kabisa maana ya jambo analofikiria. Hii inamaanisha kwamba lazima awe Mkristo aliyekomaa ambaye “akili [zake], kwa kutumiwa, zimezowezwa kupambanua mema na mabaya.”​—Ebr. 5:14.

8. Ni jambo gani linaloweza kuonyesha kama mwanamume fulani anao ufahamu na hekima kumwezesha kufundisha waamini wenzake?

8 Inajulikanaje waziwazi kwamba mwanamume fulani anayo hekima na ufahamu wa kuwafundisha waamini wenzake? Maisha yake yanapaswa yaonyeshe kwamba anayo hekima na ufahamu unaoambatana na kumwogopa na kumheshimu sana Yehova Mungu. Mwanafunzi Yakobo anaendelea kusema hivi: “Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima.” (Yak. 3:13) Kwa hiyo, wengine wanapaswa kuona kwamba yeye anajiendesha katika njia inayopatana na utu wa Mungu pamoja na njia zake.

9. Mwanamume anaweza kuonyeshaje “upole wa hekima,” na sababu gani hili ni la maana ikiwa atatumikia kama mwalimu?

9 Mwenendo kama huo unaofaa unatia ndani kuonyesha “upole wa hekima.” Ili mtu astahili kuwa mwalimu, lazima awe mpole, mtulivu na mwenye amani, si mkali mwenye kupiga kelele na kushikilia kauli yake au mwenye kiburi. Wala hapaswi kuzoea kufanya madai .yenye nguvu pasipo sababu nzuri au ushuhuda wa kuyategemeza. Mtu ambaye si mpole anaweza kuona ugumu wa kutenda kupatana na shauri la Paulo kwa Timotheo: “Mtumishi wa Bwana asigombane. Anapaswa kuwa mpole kwa watu wote, mwalimu mwema na mvumilivu, ambaye ni mpole anapowaonya wapinzani wake.”​—2 Tim. 2:24, 25, Habari Njema kwa Watu Wote.

SIFA ZA KUMFANYA MTU ASISTAHILI

10. (a) Mtu kuwa na “wivu wenye uchungu” kunaweza kutia ndani mambo gani? (b) Ugomvi ni kitu gani?

10 Akielekeza maneno yake hasa kwa wanaume waliojidai kwamba walistahili kuwa waalimu kundini, mwanafunzi Yakobo aliendelea kuonyesha sifa za kuwafanya wasistahili. Tunasoma hivi: “Lakini, mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu, msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli.” (Yak. 3:14) Maneno haya yanamtaka mtu ajichunguze mwenyewe. Mtu anaweza kujiuliza hivi: ‘Je! mimi ninakuwa na wivu wenye uchungu? Je! mimi ninagombana?’ Kuwa na wivu wenye uchungu kungetia ndani mtu kuwa na tamaa yenye kupita kiasi ya kujitukuza yeye mwenyewe pamoja na maoni yake. Hii inaweza kujionyesha katika kuwa na juhudi ya kushikilia sana maoni yake huku akilaumu sana maoni yanayotofautiana na yake, au kwa kukataa kukubali kwamba wengine wana hekima na ufahamu unaolingana na wake au hata ulio mkubwa kuliko wake. Na kwa habari ya ugomvi hii inamaanisha mtu kuwa na roho ya mabishano. Huenda mtu akawa na maelekeo ya kutumia njia zenye kuudhi ili awavuruge wengine na kuendeleza njia zake mwenyewe. Ugomvi kama huo ungekuwa matokeo ya kuwa na kiburi na kujitafutia makuu kwa uchoyo.

11. Sababu gani Yakobo angeweza kuonyesha kwamba mwalimu wa kujifanya mwenye wivu wenye uchungu na mgomvi ‘anajisifu na kusema uongo juu ya kweli’?

11 Mwanamume mwenye wivu wenye uchungu na mgomvi, kwa kuvuta fikira kwenye sifa zake kama mwalimu, angekuwa kweli kweli akijisifu au kujidai. Walakini, kweli ya Kikristo, ambayo angekuwa akidai anafundisha, inalaumu hizo sifa mbaya anazoonyesha. Kwa hiyo, mwanamume mwenye roho yenye kuleta mgawanyiko ya mashindano na bado anajiona kuwa anastahili kuwa mwalimu Mkristo anasingizia au kusema uongo juu ya kweli kama ilivyoandikwa katika Maandiko. Zaidi ya hayo, kwa kuwa yeye anazo hizi sifa zisizotamanika, hangekuwa na sababu yo yote ya kujisifu juu ya sifa zake kama mwalimu. Kufanya hivyo kungekuwa uongo. Uhakika wa kwamba yeye anajitafutia makuu na ni mgomvi moyoni mwake ungemfanya asistahili kuwa mwalimu Mkristo.

12. Mwanamume mwenye wivu wenye uchungu na mgomvi ana hekima ya namna gani?

12 Hekima ambayo mwanamume kama huyo mwenye kujitafutia makuu na mgomvi angedai kuwa nayo haingekuwa hekima itokayo juu. Mwanafunzi Yakobo anaandika hivi: “Hekima ya namna hiyo haitoki juu mbinguni; hekima hiyo ni ya ulimwengu, na ya kidunia [ya kinyama, NW], tena ni ya Kishetani.” (Yak. 3:15, Habari Njema kwa Watu Wote) Hekima ya Kimungu inapinga wivu wenye uchungu na ugomvi.​—Mit. 6:16-19.

13-15. Hekima ya namna hii inakuwaje ya (a) “kilimwengu,’.’ (b) “kinyama” na (c) “kishetani”?

13 Hekima ya namna hiyo ambayo yule anayejifanya mwalimu anadai kuwa nayo inakuwa na sifa za walimwengu walio na uadui na Mungu. Yeye anakuwa sawa na watu wale wasio wa kiroho bali wanatumia nguvu na wakati wao wakitosheleza tamaa zao za anasa au wakijitafutia heshima na mali katika taratibu hii ya mambo isiyo imara na inayobadilika sikuzote. (Flp. 3:19; Kol. 3:2) Kusudi la kutaka kuwa mwalimu ni baya. Kwa kuwa ni mwenye kiburi, yeye anataka heshima na sifa ambayo akilini mwake ameishirikisha na cheo hicho.

14 Hekima ya mtu mwenye kiburi na mgomvi vilevile ni ya kinyama au ya kinafsi, yaani, kwa asili inatokana na uhakika wa kwamba mwanadamu ni kiumbe chenye kuvutwa na maono ya moyoni, ambacho ni nafsi. Kulingana na Maandiko, wanadamu na wanyama ni nafsi. (Mwa. 2:7; Hes. 31:28, NW) Wanadamu wakiwa viumbe (nafsi) vyenye kugutuka (kuitikia) wamepewa uwezo wa kupambanua mema na mabaya pamoja na uwezo wa kufikiri, walakini wanyama wakiwa viumbe wenye kugutuka hawana akili. (2 Pet. 2:12; Yuda 10) kwa hiyo, kwa kuitwa ya “kinyama” au ya ‘kinafsi,’ hekima ya namna hii inaonyeshwa kuwa si ya kiroho, inatokana na maono, tamaa na mapendo ya mwili.

15 Vilevile, Yakobo aliiita hekima ya kishetani. Sababu ni kwamba mashetani (roho wabaya) wanaonyesha nia iliyo kinyume cha hekima ya kimungu. Si wenye upole, bali ni wakali, kama inavyoweza kuonekana kutokana na hali yenye kusikitisha ya watu wale wanaopagawa nao. (Marko 5:2-5) Na kwa habari ya Shetani Ibilisi, aliye mtawala wa mashetani, Biblia inafunua kwamba kuanguka kwake kulisababishwa na kiburi chenye uchoyo na kujitafutia makuu.​—1 Tim. 3:6.

SIFA ZINAZOSHIRIKISHWA NA HEKIMA ITOKAYO JUU

16. Hekima itokayo juu ina sifa gani?

16 Ili mtu astahili kuwa mwalimu kwa waamini wenzake lazima awe huru na sifa zinazoshirikishwa na hekima ya kidunia, kinafsi na kishetani. Maisha yake yanapaswa yaonyeshe kwamba yeye anaongozwa na hekima itokayo juu. Mwanafunzi Yakobo alieleza hekima hii kama ifuatavyo: “Hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu [tayari kutii, NW], imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki.” (Yak. 3:17) Ebu fikiria hii maana yake ni nini.

17. Ni jambo gani linajomaanishwa na kuwa “safi” na “yenye amani”?

17 Wale wanaostahili kutumikia kama waalimu wanasemekana kuwa ni “safi,” wenye kutakata au wasiochafuliwa akili na moyo. Katika kuwa ‘wenye amani,’ wao ni watu wanaoendeleza amani. Si kwamba tu wanaepuka kuwa wachokozi au wenye kutaka vita, bali pia wanajitoa walete uhusiano mwema kati ya wengine. (Rum. 14:19; 1 Tim. 3:3) Wao hawajiungi au kukubaliana na lo lote linaloharibu amani.​—Linganisha Mithali 16:28; 17:9.

18. Mtu anaonyeshaje kwamba ni (a) ‘mwenye kiasi’? (b) ‘yuko tayari kutii’? (c) kwamba ‘anajaa rehema na matunda mema’?

18 Mtu ‘mpole’ au mwenye kiasi hukubaliana au huvumilia, si mwenye kushikilia sana juhudi yake. Yeye hatasisitiza sana njia yake au kushikilia sana sheria bali ataangalia jambo katika njia ya fadhili na kulifikiria kama linavyostahili. (Linganisha 1 Petro 2:18.) Mahali pa kuwa mwenye shingo ngumu, aliye na hekima itokayo juu huwa “tayari kutii.” Yeye huwa na roho ya ushirikiano, akiwa na nia ya kukubali maombi yanayofaa. Mtu wa namna hiyo atatii yanayosemwa na Maandiko, wala hatachukua msimamo fulani na kuushikilia, bila kujali kama ni sahihi au ni wenye makosa. Yeye atakuwa mwepesi katika kufanya marekebisho kukiwa na ushuhuda uliyo wazi kwamba amechukua msimamo wenye makosa au amefanya maamuzi yenye makosa. Vilevile mtu aliye na hekima itokayo juu ‘amejaa rehema na matunda mema.’ Katika kushughulika na wengine, ni mwenye huruma. Yeye huwahurumia wenye taabu, naye huwa na juhudi na nia ya kufanya lo lote awezalo ili awasaidie. “Matunda mema” yanatia ndani matendo yote yanayopatana na wema, haki na kweli.​—Efe. 5:9.

19. Mtu kutokuwa na ‘ubaguzi’ kunamaanisha nini?

19 Mtu anayeongozwa na hekima itokayo juu ‘hana fitina’ au hana ubaguzi. Yeye hapendelei watu mmoja mmoja kwa sababu ya kuonekana kwao kwa njenje, cheo, mali, ukubwa wao maishani au maongozi yao kundini. (Linganisha Yakobo 2:1-4.) Katika kushughulika na wanadamu wenzake, yeye anajitahidi kutopendelea.

20. (a) Mtu mnafiki ni mtu wa namna gani? (b) Mtu aliye na hekima itokayo juu anaonyeshaje kwamba yeye si mnafiki?

20 Hekima itokayo juu haimfanyi mtu ‘mnafiki’ hata kidogo. Mtu mnafiki anajisingizia kuwa vingine. Mtu anayeonyesha hekima itokayo juu hajifanyi vingine. Katika matendo yake yote, anakuwa mnyofu na mwenye kutumainika.​—Efe. 4:25.

21. Sisi tunaweza kutumiaje yale yanayosemwa na Biblia juu ya matakwa ya kutumikia kama mwalimu kundini?

21 Yale yanayotakiwa waalimu Wakristo wawe nayo yanapaswa yatufanye tujichunguze kwa uangalifu. Je! sisi tunaonyesha wazi kwamba tunataka kuishi kulingana na hekima itokayo juu? Ijapokuwa huenda tusiwe waalimu kundini, sisi sote tuna daraka la kufundisha wengine kweli tukiwa wanafunzi wa Kristo. Kwa hiyo, ni jambo la muhimu kwamba maoni yetu, maneno na matendo yapatane na vile tunavyodai kuwa. (Rum. 2:21, 22) Na tuendelee kujitahidi kuwa watumishi bora wa Baba yetu wa mbinguni na kufurahia baraka anazotumwagia.​—Linganisha 1 Timotheo 4:15, 16.

[Picha katika ukurasa wa 20]

“Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake . . . ”​—Mt. 15:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki