Zaburi
Ili Uwe Mwenye Furaha, Angalia Mashirika Yako
MASHIRIKA ya mtu yanaweza kuwa na uvutano kwake ama wa kutenda mema ama wa kutenda mabaya. Mara nyingi, watu wanakubali kwamba, kwa sababu ya rafiki zao, walianza kutumia dawa za kulevya na tumbako au wakaingilia maisha ya uasherati. Kwa kuazimia kufanya jitihada za kuvunja mashirika yasiyofaa, na, badala yake, kutafuta kushirikiana na watu wanaoongozwa na kanuni bora, wengine wamefaulu kushinda mazoea yenye kudhuru.
Basi, ikiwa kwa kweli unatamani kuwa na furaha ya kweli na usalama, lazima ujiepushe kushirikiana na watu wasiopenda mambo mema. Jambo hilo linaonyeshwa kwa nguvu sana katika Biblia. Katika kitabu cha Zaburi, kama mfano, twasoma hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la watu waovu, na katika njia ya wenye dhambi hakusimama, naye hakukaa katika kiti cha wenye dhihaka.”—Zab. 1:1, NW.
Furaha haiwezi kupatikana kamwe na wale wanaopuza njia za Mungu. Akiwa Baba mwenye upendo, Aliye Juu Zaidi ametoa sheria zile tu zinazoweza kuendeleza hali njema ya viumbe vyake vyenye akili. Hivyo, mtu mwenye furaha ni yule anayelikataa “shauri” la wale wasiomwogopa Mungu kama uongozi wa maisha. Kwa kuwa yeye anayakataa mawazo yao, kwa uthabiti, bila shaka yeye hatasimama ‘katika njia ya wenye dhambi.’ Hiyo maana yake ni kwamba yeye hatapatikana mahali walipo; yeye hataki ushirika wao. Kwa hiyo, yeye hajishushi chini na kushirikiana nao, akiketi nao na kudhihaki ibada ya Mungu.
Bila shaka, furaha ya mtu mwenye haki haipatikani tu kwa kuishi maisha ya kujizuia kufanya mambo yasiyofaa. Hapana, yeye anapata furaha ya kweli katika kufanya mambo yenye kujenga, akijaza akili na moyo wake mambo yanayofaa. Zaburi ya kwanza inaendelea kusema hivi: “Furaha yake i katika sheria ya Yehova, na sheria yake huisoma kwa sauti ndogo mchana na usiku.” (Zab. 1:2, NW) Furaha ya kweli ya mtu mwenye haki inatokana na kutosheleza tamaa yake ya kweli ya kuijua sheria ya Yehova na katika kuitumia. (Linganisha Yakobo 1:25.) Hakuna siku inayopita pasipo yeye kufikiria mambo ya kiroho.
Kama vile ilivyo kwa wanadamu wote, watu wenye haki wanapatwa na majaribu, lakini wanafaulu kuyavumilia kama vile mti ulio na nguvu unavyozishinda pepo zenye nguvu kwa kulinganisha. Kwa kufaa mtunga zaburi alimlinganisha mtu mwenye haki na mti wenye nguvu uliopandwa penye maji mengi, akisema hivi: “Naye atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.” (Zab. 1:3) Mti uliopandwa karibu na chemchemi ya maji isiyoshindwa hautakauka wakati wa ukavu au wa kiangazi, lakini utazaa matunda. Vivyo, nguvu za watu wenye haki hutoka kwa chanzo kisichoshindwa, yaani, Yehova Mungu. Kwa msaada wa roho ya Mungu, wanaweza kuvumilia wakiwa chini ya mikazo ya majaribu na magumu. Mwishowe, wanafanikiwa katika kila jambo, kwa kuwa kusudi lao kubwa ni kuendelea kuwa watumishi wenye kukubalika wa Mwenye Nguvu Zote. Joto au ukali wa upinzani hauwaondoshi kwenye azimio lao. Wao wanashinda na kuwa watu waliokubaliwa na Yehova Mungu.
Lo! namna hiyo ilivyo tofauti na hali ya wale walio waovu! Huenda wakaonekana kufanikiwa kwa kitambo, walakini hawana usalama wenye kuendelea. Huyo mtunga zaburi anaendelea kusema hivi: “Sivyo walivyo waovu, bali wako kama makapi ambayo hupeperushwa na upepo. Hiyo ndiyo sababu waovu hawatasimama wakati wa hukumu, wala wenye dhambi katika kusanyiko lao wenye haki. Kwa kuwa Yehova anajua njia ya wenye haki, bali njia yenyewe ya waovu itapotea.”—Zab. 1:4-6, NW.
Kwa hiyo, waovu hawana usalama, wanafanana na makapi wakati wa kupepeta nafaka. Makapi yanapeperushwa hali mbegu nzito zaidi za nafaka zinaanguka chini. Vivyo hivyo, wenye haki wanabaki lakini waovu wanapeperushwa kama makapi yasiyofaa kitu. Ukija wakati wa kuhukumiwa, waovu hawatasimama wakiwa wamekubalika bali watapewa hukumu ya laana. Wao hawatakuwa na sehemu yo yote kati ya wenye haki. Wenye kuzoea dhambi hawatafaulu katika singizio lao la kuwa katika kusanyiko la wenye haki.
Sababu kwa nini waovu hawatasimama wakiwa wanakubalika mbele za Yehova Mungu nao hawatahesabiwa pamoja na watu wanyofu ni kwamba Mwenye Nguvu Zote anajua “njia ya wenye haki.” Ndiyo, yeye anatambua mwendo wa maisha yao kuwa unakubalika naye anawathawabisha kulingana nayo. Kwa hiyo, njia ya wenye haki, inadumu wakati wote bali ile ya waovu inapotea. Kwa kuwa waovu wanapotea, njia au mwendo wa maisha unamalizika pamoja nao.
Kweli kweli, zaburi ya kwanza inatoa kitia-moyo chenye kuchangamsha kwamba sisi tupate furaha katika sheria ya Mungu huku tukijiepusha kuwa na urafiki wa karibu na wale wasiompenda kweli kweli Aliye Juu Zaidi. Mwendo huo utatutokezea furaha, si kwa miaka michache tu, bali kwa umilele tukiwa watumishi washikamanifu wa Yehova Mungu.