Ushuhuda Mkubwa wa Utukufu wa Mungu na wa Kwamba Yeye Ndiye Muumba
Watu wengi wanaotilia shaka kuwako kwa Mungu wanajipofusha wasione ushuhuda wa kuwako kwake. Kwa sababu mambo fulani yanatukia kila siku, hata watu wanaoamini kuwako kwa Mungu huenda wasione matukio hayo ya kawaida kuwa ushuhuda wa utukufu wa Mungu wa kwamba yeye ndiye Muumba. Walakini, mtunga zaburi aliyeongozwa kwa roho, anatofautiana sana na watu hao. Yeye aliona katika mambo ya kawaida yenye kutukia kwa kurudia-rudia ushuhuda wenye kuongezeka uliotangaza bila kukosea utukufu wa Yeye Aliye Juu Zaidi.
USHUHUDA WA MBINGU ZIONEKANAZO
Mtunga zaburi aliandika hivi: ’‘Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake. Mchana husemezana na mchana, usiku hutolea usiku maarifa. Hakuna lugha wala maneno, sauti yao haisikilikani. Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu. Katika hizo ameliwekea jua hema, kama bwana arusi akitoka chumbani mwake, lafurahi kama mtu aliye hodari kwenda mbio katika njia yake. Kutoka kwake lautoka mwisho wa mbingu, na kuzunguka kwake hata miisho yake, wala kwa hari yake hakuna kitu kilichositirika.”—Zab. 19:1-6.
Katika njia hiyo ya kimashairi, mtunga zaburi Daudi alionyesha kwamba mbingu zionekanazo—jua, mwezi na nyota—zinautangaza utukufu wa Mungu. Hesabu kubwa mno ya vitu vilivyomo katika mbingu, utaratibu wavyo, kutegemeka kwa mwendo wavyo na kusudi lenye kufaidi vinalotimiza hutoa ushuhuda mkubwa kwamba yuko Mungu mwenye hekima, uweza, na mwenye kufadhili. Mungu ambaye ameupanga vizuri sana hivyo ulimwengu wote mkubwa mno unaoonekana lazima awe mwenye hekima sana na mwenye uweza sana. Tunapofikiria, kwa mfano, namna uhai duniani unavyotegemea sana jua, lazima tukate maneno kwamba Mfanyiza jua anahangaikia sana vitu vyenye uhai. Katika kufunua sifa fulani za Yehova Mungu zenye kutamanika, mbingu zenye kuonekana huwa kweli kweli zinautangaza utukufu wake.
Ushuhuda juu ya utukufu wa Mungu na wa kwamba yeye ndiye Muumba hautolewi tu na vitu vinavyoweza kuonekana katika mbingu katika wakati wa mchana au usiku mmoja. Mchana mmoja baada ya mwingine na usiku mmoja baada ya mwingine hutoa ushuhuda ule ule. Wonyesho mmoja tu wa saa 24 wa jua, mwezi na nyota waweza kutoa ushuhuda mwingi sana juu ya Muumba. Walakini kila siku ushuhuda huo waweza kuonekana katika mbingu zilizo juu. Kwa hiyo inakuwa kama kwamba ushuhuda huo unatolewa mchana na usiku, vitu katika mbingu vinavyoonekana vivyo hivyo hutoa maarifa kuhusu utukufu wa Yehova na wa kwamba yeye ndiye Muumba.
Bila shaka, ushuhuda unaotolewa hausikilikani. Walakini hakuna sehemu hata moja ya dunia isiyopata ushuhuda huo. Unaijaza dunia, kana kwamba kwa kamba ya kupimia ambayo imetandazwa katika kila sehemu ya sayari hii.
Mtunga zaburi anataja kwamba jua lina hema katika mbingu zionekanazo. Katika njia inayolingana na hiyo, Ayubu 22:14 husema juu ya mbingu zikiizunguka dunia kama “kuba.” Vilevile, Isaya 40:22 husema juu ya Mungu kuwa “yeye ndiye azitandazaye mbingu kama pazia; na kuzikunjua kama hema ya kukaliwa.” Katika “hema” hii ya mfano, jua linatembea kila siku kama mtu mwenye kuhama-hama. Na kwa sababu ya uangavu wake, kwa kufaa jua linalinganishwa na bwana-arusi akitoka chumbani mwake akiwa amejivika kipekee kwa ajili ya pindi hiyo, na, kama mtu hodari anayepiga mbio, linafuata “mzunguko” wake kupitia katika mbingu. Kwa kuwa jua linaangaza mwangaza wake katika kila sehemu ya dunia kutoka mahali linapotokea mpaka mahali linapochwea, kila kitu kilichomo duniani kinafaidika kutokana na joto au hari yake. Hakuna sehemu isiyofaidika hivyo.
SHERIA YA MUNGU HUTOA USHUHUDA
Ushuhuda kuhusu utukufu wa Mungu na wa kwamba yeye ndiye Muumba hautolewi tu na vitu vinavyoweza kuonekana katika mbingu zionekanazo. Kulingana na Mwanzo 1:14, sababu mojayapo ya kuwako kwa mianga katika mbingu ni kwamba “iwe ndiyo dalili na majira na siku na miaka.” Kwa hiyo imetoa njia ya kuhesabu siku na miaka, imeongoza watu baharini nayo imekuwa ndiyo njia ya kuamua juu ya wakati unaofaa kwa mipango fulani ya ukulima. Walakini mianga ya mbinguni si ndiyo njia ambayo Mungu ametoa ili kuwaongoza watu katika kufanya maamuzi ya maana ya kiadili. Aliye Juu Zaidi ametoa amri, nazo hizo, pia, zinashuhudia utukufu wake.
Mtunga zaburi Daudi aliendelea kusema hivi: “Sheria ya [Yehova] ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya [Yehova] ni ya akili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru. Kicho cha [Yehova] ni kitakatifu, kinadumu milele. Hukumu za [Yehova] ni kweli, zina haki kabisa. Ni za kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, kuliko sega la asali. Tena mtumishi wako huonywa kwazo, katika kuzishika kuna thawabu nyingi.”—Zab. 19:7-11.
Hapa Daudi alikuwa akitaja sheria ya Mungu aliyotoa kupitia kwa Musa. Ilikuwa kamilifu, bila kasoro, ikifaa kabisa kusudi la kutolewa kwayo. Sheria hiyo ingeweza kuiburudisha au (‘kuirudisha,’ NW) nafsi au mtu huyo katika maana kwamba kuitii kuliihuisha nafsi yake na kuendeleza hali yake njema.
Shuhuda au kumbukumbu zote zilizotiwa ndani ya sheria ya Mungu zilikuwa zenye kutegemeka. Zingaliweza kufuatwa kwa usalama zikiwa uongozi maishani. Ijapokuwa awe hana hekima au awe hajiamini sana, mtu ambaye angalitii kumbukumbu za Yehova angalitenda kwa hekima, na kujiepusha na mwendo ambao ungeongoza kwenye uharibifu.
Amri au kanuni zilizoonyeshwa waziwazi katika sheria ya Musa zilikuwa adilifu, yaani, zilipatana kabisa na kanuni za haki na haki ya hukumu. Kwa kujiongoza mwenyewe kupatana na sadikisho la kwamba amri za Mungu ni adilifu, mtu angepata furaha ya ndani, kushangilia moyoni.
Zikiwa safi, bila kuwa na sifa yo yote isiyotakikana, amri za Yehova hufanya macho yaangaze kwa kuona waziwazi. Zinamsaidia mtu ajiepushe na kosa la kiadili na kufuata mwendo wa unyofu.
Hofu inayofaa au heshima kubwa anayopewa Muumba inaonyeshwa kwa kutii amri zake. Hofu ya namna hiyo ni safi. Haimshushi mtu kama vile ulivyofanya woga wa kuogopa miungu ya uongo, iliyoonwa na wenye kuiabudu kuwa yenye kukasirika ikitaka kutulizwa kwa dhabihu za kibinadamu. Sheria hiyo ilifundisha kwamba watu wawe na hofu inayofaa juu ya Mungu. Hofu ya namna hiyo itaendelea kuonyeshwa na watumishi wa Yehova waliojitoa. Kwa hiyo, ni hofu inayodumu milele.
Sehemu ya sheria ya Mungu ilikuwa maamuzi ya hukumu. Hayo yalikuwa ya kweli, yenye kutegemeka, thabiti, msingi wake imara ukiwa utaratibu wa haki ya hukumu ya kimungu. Maamuzi hayo ya hukumu yalikuwa ya haki katika sehemu zake zote. Kwa kuwa maamuzi hayo ya haki ya hukumu yalitoka kwa Mungu nayo yalikuwa yenye kufaidi kabisa, ni jambo linalotamanika sana kuwa nayo katika akili na moyo wa mtu. Ni yenye thamani zaidi kuliko utajiri wa mambo ya kimwili—dhahabu. Kwa watu wanaojiruhusu waongozwe nayo, ni matamu kuliko asali. Maamuzi hayo ya hukumu yanamwonya mtu juu ya kuchukua mwendo wenye makosa, yakitia nguvu azimio lake la kupinga vishawishi. Kushikamana nayo kunathawabisha kwa kuwa kutii kwa namna hiyo kunaendeleza hali njema kabisa ya mtu huyo. Yeye anajiepusha na mwendo wa maisha unaoweza kudhuru kimoyoni, kimwili na kiakili.
Kweli kweli sheria yenye kusaidia na kufaidi namna hiyo kama ile waliyopewa Waisraeli inatoa ushuhuda mwingi kuhusu Mungu mwenye hekima, haki ya hukumu na mwenye upendo.
WATUMISHI WA MUNGU WAPEWA MSAADA
Ushuhuda zaidi juu ya Muumba unapatikana katika msaada anaotoa kwa watumishi wake wasiokamilika. Kama vile inavyoonekana waziwazi kutokana na Zaburi ya 19, Daudi alithamini sana sheria ya Mungu. Hata hivyo yeye alitambua kwamba akiwa mwanadamu asiyekamilika alihitaji msaada kutoka kwa Muumba wake ili aweze kujiongoza ifaavyo. Hiyo inaonekana wazi kutokana na sehemu ya kumalizia ya Zaburi ya 19. Twasoma hivi: “Ni nani awezaye kuyatambua makosa yake? Unitakase na mambo ya siri. Umzuie mtumishi wako asitende mambo ya kiburi, yasinitawale mimi. Ndipo nitakapokuwa kamili, nami nitakuwa safi, sina kosa lililo kubwa. Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee [Yehova], Mwamba wangu, na mwokozi wangu.”—Zab. 19:12-14.
Daudi alitambua kwamba akiwa mwanadamu asiyekamilika angeweza kufanya dhambi na hata asijue. Kwa hiyo yeye aliomba kwamba asamehewe makosa ambayo huenda yakawa yamefichika asiyatambue. Kisha, wakati ambapo huenda mwili wake wenye dhambi ukamsukuma achukue mwendo wenye makosa, alitamani sana apate msaada wa Mungu. Alitamani kwamba Yehova amzuie asitende matendo ya kiburi na ya kujitanguliza. Alitaka azuiwe ili matendo ya kujitanguliza yasimtawale na kuwa mwendo wake wa kawaida. Kama angekuwa amejifurahisha sana tamaa za mwili wake wenye dhambi, angetawalwa na dhambi. Badala yake, yeye alitaka ajitoe kabisa kwa Aliye Juu Zaidi. Kwa kadiri iwezekanayo, yeye alitaka aonekane akiwa ‘safi, hana kosa lililo kubwa.’ Kwa hiyo, yeye aliomba kwamba kusihi kwake kwa kutaka msaada, kukitokana na “mawazo ya moyo” wake, kukubalike mbele za Mungu. Katika nyakati za hatari na dhiki Daudi alimtegemea Yehova kana kwamba alikuwa mwamba ulio imara. Vilevile alimwona Yehova kuwa Mwokozi wake, Yeye ambaye angeweza kumwokoa na mikono ya waovu pamoja na kuangukia dhambi.
Hivyo, Zaburi ya 19, inaelekeza kwa nguvu sana kwenye ushuhuda wa mwungano wa kuumba, sheria iliyoandikwa inayopatikana katika Biblia pamoja na msaada wa kimungu wanaopewa wanyofu kuwa jambo linalofunua kuwako kwa yeye Aliye Juu Zaidi. Ushuhuda huo wapaswa utusukume tutake kupatikana tumekubalika kwake. Ndiyo, “mawazo ya moyo” wetu na yapate kibali yake tuendeleapo kumtegemea Yehova Mungu aongoze hatua zetu ifaavyo.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Kuumba, uongozi ulioandikwa kwa uongozi wa roho na msaada wa kimungu hushuhudia kuwako kwa Mungu mwenye upendo.