Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 4/15 uku. 3
  • Tumaini—Uwezo Kwa Ajili ya Kuvumilia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tumaini—Uwezo Kwa Ajili ya Kuvumilia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UHITAJI WA ‘KUSEMA KWA KUFARIJIANA’
  • TUMAINI AMBALO ‘HALIKATISHI TAMAA’
  • LAZIMA TUMAINI LIENDELEZWE NA KUTIWA NGUVU
  • MSAADA UNAOFAA
  • Furahia Tumaini Lisilokatisha Tamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Dumisha Tumaini Lako la Kikristo Likiwa Imara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Mtumaini Yehova na Uwe Hodari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kumfurahia “Mungu wa Tumaini”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 4/15 uku. 3

Tumaini—Uwezo Kwa Ajili ya Kuvumilia

LO! JINSI uvumilivu ulivyo jambo lenye thamani! Bila huo mcheza muziki anayejulikana sana hangepata kujulikana naye mwimbaji wa nyimbo mwenye sifa hangeweza kuwavutia wasikilizaji wake. Ndiyo, si kwamba tu uvumilivu unatamanika ili kutimiza mradi fulani bali ni wa lazima pia. Sana sana inakuwa hivyo kwa habari ya Mkristo ambaye yuko katika mashindano ya mbio akitazamia uzima wa milele. “[Na] tupige mbio kwa uvumilivu katika mashindano yaliyowekwa mbele yetu,” akahimiza mtume Mkristo Paulo. Pasipo uvumilivu mwisho hauwezi kufikiwa.​—Mt. 24:13; Ebr. 12:1.

Kwa kuona umuhimu wa uvumilivu, maulizo fulani yaweza kutokea. Je! mtu anayemwogopa Mungu aweza kuvumilia kwa nguvu zake mwenyewe? Sababu gani Wakristo wasaidiane kuvumilia? Wanawezaje kutoa msaada huo?

UHITAJI WA ‘KUSEMA KWA KUFARIJIANA’

Sisi twaishi katika “nyakati za hatari.” (2 Tim. 3:1) Mambo mengi sana yanafanya sasa iwe vigumu sana kwa Mkristo kuvumilia. Yeye aweza kufanya hivyo ikiwa tu atatii lile onyo la upole la Kimaandiko la kuzidi “kuwa hodari katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake.” Na zaidi ya yote, watu wenye kumwogopa Mungu lazima wapige vita “juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” mashetani walio chini ya uongozi wa Shetani. (Efe. 6:10, 12) Maongozi yao ni yenye nguvu hivi kwamba Mkristo aweza kupoteza uhakika wake juu ya uwezo wa Mungu na imani kudhoofika. Ndipo msaada wa haraka wa kiroho unapokuwa wa lazima. Lakini ni jambo gani linaloweza kufanywa?

Ebu fikiria namna mzee fulani Mkristo alivyotoa msaada wa kiroho katika pindi moja. Aliwatembelea mume na mke ambao walikuwa wamekuwa washiriki wa kundi wenye bidii sana. Kwa sababu ya ugonjwa katika jamaa hiyo na mikazo mingi katika mahali pa kazi pa mwanamume huyo, walikaribia sana kuacha mbio za Kikristo. Walakini mwishoni mwa ziara yake mzee huyo alifurahi sana kusikia maneno haya: “Ninafurahi sana kwamba ulikuja kuzungumza nasi. Mimi na mke wangu tumepata nguvu mpya kutuwezesha kuendelea kumtumikia Yehova.” Maneno yanayofanana na hayo yalipata kusikiwa kutoka kwa jamaa nyingine ya Kikristo, ambayo mikazo na matatizo yalikuwa yametokeza ugonjwa wa akili pamoja na hali mbaya sana ya kiroho. Ni jambo gani lililofanya jamaa hizi ziseme, ‘Tumepata nguvu mpya za kumtumikia Yehova’?

Wazee hao waliokuwa wakizuru walikuwa wamewatia moyo waamini wenzao waone mambo kama vile Yehova anavyoyaona. Mungu anajua kwamba watu wake wamefanyizwa kwa mavumbi, na ya kwamba, kwa sababu ya mikazo, magonjwa na mengine kama hayo, Mkristo anaweza kuhuzunika. (Zab. 103:14) Ndivyo Wakristo wengine wa kwanza walivyoona katika Thesalonike. Kwa hiyo, mtume Paulo alishauri hivi: “Mseme kwa kuzifariji nafsi zilizoshuka moyo.”​—1 The. 5:14, NW.

‘Kusema kwa kufariji’ kunamaanisha kusema kwa kutuliza, kuchangamsha, kutia moyo, kuburudisha roho ya mwingine kwa mahakikisho yenye kufurahisha. Ndiyo, kusema kwa kufariji kunamaanisha kuimarisha moyo wa msikilizaji hivi kwamba maoni yake yanaongezeka. Kwa habari ya zile jamaa mbili zenye kushuka moyo zilizotangulia kutajwa, ilikuwa kama kwamba mwangaza wa jua wenye kung’aa ulikuwa umeondoa ukungu wa asubuhi uliokuwa umetia giza hali yao ya kuona kiroho. Mioyo yao iliimarishwa kwa tumaini jipya. Tumaini hili ni nini?

TUMAINI AMBALO ‘HALIKATISHI TAMAA’

“Kutumaini” kunamaanisha kutamani ukiwa na taraja la kutimiziwa. Kwa hiyo, tumaini, lina uwezo wa kuendeleza, nguvu yenye kusukuma, kwa kuwa linatazamia mbele kwenye utimizo wake. Bila shaka, mtu anaweza kwa urahisi kuwa na tumaini la uongo, lisilo na msingi wa kweli. Mfano: Kwa muda wa miaka elfu nyingi wanadamu wamekuwa wakitumainia kupata serikali kamilifu ya kibinadamu. Walakini taraja hili halijatimizwa kwa sababu wanadamu si wakamilifu, ni wenye dhambi, wenye choyo na wenye kufa.​—Rum. 5:12; 7:14.

Tumaini lenye kutegemeka lazima limtegemee Mungu, aliye Chanzo cha vitu vyote vionekanavyo na visivyoonekana. (Ufu. 4:11) Kwa kweli tumaini la kweli lapata msingi wake katika kusudi lisiloshindwa la Mungu kwa wanadamu, na kwa hiyo, hili ‘tumaini halikatishi tamaa.’ (Rum. 5:5, NW) Kwa mfano, nabii Isaya alitaja kwamba Mungu aliumba dunia ikaliwe na wanadamu. (Isa. 45:18) Hili ndilo kusudi la Mungu, nalo litatimizwa. Mungu atafungua njia ili paradiso irudishwe katika dunia hii. (Luka 23:43, ZSB) Kurudishwa huko kutaletwa kwa njia ya ufalme wa Mungu, ambao ndio uliokuwa kichwa cha mahubiri ya Yesu na serikali ambayo alifundisha wafuasi wake kuiombea.​—Mt. 4:17, 6:9.

Yale ambayo ufalme huu wa Mungu utatimiza yanakaribia sana kutowazika. Utarudisha afya kamili na uzima wa milele. Ndiyo, mauti haitakuwapo tena na hiyo yamaanisha kwamba hata dhambi itaondolewa, kwa kuwa mauti huletwa na dhambi. (Rum. 6:23; Ufu. 21:4) Vilevile, matokeo mabaya ya dhambi ambayo yameletea wanadamu dhiki nyingi za mwilini na za akili hayatakuwapo. Faraja weee! Tumaini hili halikatishi tamaa kwa sababu msingi wake ni ahadi ya Mungu, na yeye hawezi kusema uongo. (Tito 1:1, 2) Ni kwa sababu gani, basi, Wakristo wengine wanashuka moyo sana hata kwamba wakati ujao unaelekea kutokuwa na tumaini?

LAZIMA TUMAINI LIENDELEZWE NA KUTIWA NGUVU

Mwanzo wa kupoteza tumaini huenda hata usionekane. Labda kutimizwa kwa tumaini kunaelekea kukawia na kuufanya moyo kukata tamaa. (Mit. 13:12) Au, hali maishani mwa mtu huenda zikamfanya ajifikirie sana mahali pa kufikiria uhusiano wake pamoja na Mungu. Huenda mtu huyo akashuka moyo kwa sababu ya ugonjwa, kutendwa vibaya au kwa sababu tu ya kuwa na mawazo yasiyofaa. Labda anaonea wivu ufanisi wa mambo ya kimwili na hali ya kiroho ya wengine. Akiendelea kupatwa na mambo haya polepole, huenda akaacha kumtupia Yehova mzigo wake. (Zab. 55:22) Upesi Mkristo huyo anajikuta akiwaza isivyofaa, hivi kwamba uhakika wa tumaini la Ufalme hufifia moyoni na akilini mwake. Ndiyo, tumaini laweza kupotezwa na ndipo watu huacha kuvumilia katika mbio za uzima.

Jinsi tumaini lilivyo inalifanya kuwa jambo linaloweza kutoweka kwa urahisi lisipowekwa akilini sikuzote. Kwa hiyo, lazima tupiganie sana kuliweka tumaini letu likiwa lenye nguvu, Sababu ni kwamba tunatumaini jambo lisiloonekana. (Linganisha Rom. 8:24, 25, HNWW.) Walakini, hii haimaanishi kwamba kwa lazima tumaini ni jambo dhaifu.

Tumaini lina nguvu sana hivi kwamba linalinganishwa na nanga ambayo yaweza kuimarisha merikebu na kuiwezesha kushinda upepo mkali sana wa dhoruba. Kwa kweli, tumaini linaitwa “nanga ya maisha.” (Ebr. 6:19, HNWW) Alipoandika maneno haya, Paulo alikuwa akizungumza juu ya ahadi ya Mungu ya kumbariki Ibrahimu. Ahadi hii ndiyo msingi wa kuwa na tumaini katika ufalme wa Mungu, kwa kuwa Yehova alimhakikishia huyo mzee wa ukoo mwaminifu hivi: “Na katika uzao wako mataifa yote ya dunia yatajibarikia.” (Mwa. 22:18) Yehova aliongeza kiapo chake juu ya ahadi hiyo ili kwamba “kwa vitu viwili visivyoweza kubadilika, ambavyo katika hivyo Mungu hawezi kusema uongo, tupate faraja iliyo imara, sisi tuliokimbilia kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu.” (Ebr. 6:18) Kuikumbuka ahadi hii ya Mungu iliyo juu ya kiapo kunalitia nguvu tumaini la Mkristo na kulifanya kweli kweli kuwa “nanga ya maisha.” Kunaimarisha, kutia nguvu, na kutoa uwezo wa kuvumilia.

Tumaini letu linatiwa nguvu siku baada ya siku tunaposema juu ya tumaini lililo ndani yetu. Tuzungumzapo juu yake zaidi na zaidi, tunaliona zaidi na zaidi kuwa hazina nalo linakuwa na nguvu zaidi na zaidi. Katika njia inayolingana na hiyo, maneno yaliyosemwa na yule msichana Mshulami kuhusu mpenzi wake kijana mchungaji, bila shaka yalitia nguvu upendo wake kwake. (Wim. 5:10-16) Kwa habari ya upendo kama huo, ingeweza kusemwa hivi: “Mwako wake ni mwako wa moto, na miali yake ni miali ya Yahu. Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, wala mito haiwezi kuuzamisha.”​—Wim. 8:6, 7.

Ndivyo ilivyo kwa habari ya maneno yanayosemwa kuhusu tumaini la Kikristo. Kwa hiyo Paulo aliwaonya kwa upole ndugu zake Waebrania ‘walishike sana ungamo la tumaini letu pasipo kugeuka.’ (Ebr. 10:23) Ungamo hili la hadharani la tumaini, kusema huku juu yake, kutalitia nguvu tumaini letu, na kulifanya kuwa halisi kabisa kwetu. Uhakika kama huo akilini ulio dhahiri unafanyiza viungo ambavyo hulifanya tumaini kuwa nanga yenye nguvu ya maisha.

MSAADA UNAOFAA

Ili kuamsha tena tumaini, msaada unaofaa unahitajiwa. Wakijua kwamba tumaini ni uwezo wenye kusukuma sana wa kuvumilia, wale wazee wenye kuzuru waliotangulia kutajwa, waligeuza mawazo ya jamaa hizo zilizokuwa zimeshuka moyo ziache kujifikiria zenyewe tu wakazungumza juu ya uhakika wa ufalme wa Mungu. Tumaini ni jambo lenye asili ya kiroho. Kwa hiyo lazima kujaza akili na moyo mambo ya kiroho ya Neno la Mungu, ahadi hakika za Mungu pamoja na maneno ya Yesu. Njia yenye nguvu ya kupashana habari na Yehova Mungu lazima irudishwe, nalo bila shaka hilo litaleta furaha. Je! hivyo si ndivyo Paulo anavyoonyesha kuwa ndiyo matokeo yenye kufaa ya sala? “Msijisumbue kwa neno lo lote,” akasema mtume, “bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, Itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”​—Flp. 4:6, 7.

Ili tupate kuvumilia tukiwa chini ya dhiki, lazima ‘tufurahi katika tumaini’ na ‘kudumu katika sala.’ (Rum 12:12) Na tutakuwa na furaha, hata wakati wa majaribu, tukitambua kwamba Yehova Mungu hajaribu kututafutia makosa naye ‘hasahau kazi yetu, na pendo tunaloonyesha katika jina lake.’​—Ebr. 6:10.

Vilevile, maneno haya ya Paulo ni yenye kutumainisha: “Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.” (Ebr. 6:11, 12) Uhakika huu wenye kutia nguvu wa kwamba Mungu yuko upande wetu na utusaidie kulifanya tumaini la Ufalme kuwa uweza wetu kwa ajili ya kuvumilia.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki