Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! ubatizo ni wa lazima kwa mtu anayetaka kuzamishwa walakini hali mbaya ya afya yake au umri mkubwa ungefanya kufanya hivyo kuwe hatari?
Biblia inaonyesha kwamba kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa ni jambo la maana sana. Kwa hiyo hata inapokuwa lazima hatua fulani zisizo za kawaida zichukuliwe kwa sababu ya hali ya mtu, inampasa abatizwe ikiwezekana.
Yesu aliyefufuliwa aliwaambia wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza . . , kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:1, 20, NW) Ndiyo, wale ambao wangejifunza mapenzi ya Mungu na kujiweka wakf wamtumikie iliwapasa wazamishwe kabisa katika maji, kama vile Yesu mwenyewe alivyobatizwa. (Neno la Kigiriki baptizein lamaanisha “kuchovya, kutumbukiza, kuzamisha.”) Kwa habari ya Kornelio mkuu wa jeshi na jamaa yake, twasoma hivi: “[Petro] akaamuru wabatizwe kwa Jina lake Yesu Kristo.”—Matendo 10:48.
Katika nyakati za kisasa Mashahidi wa Yehova wamefanya mipango ya ubatizo katika makusanyiko yao. Ubatizo wenyewe waweza kufanyiwa katika kidimbwi kilicho karibu, ziwa au mto mahali penye maji mengi kutosha kuzamisha mtu kabisa. (Linganisha Matendo 8:38.) Walakini watu wengine, wajapokuwa wanataka kubatizwa hivyo, wameshindwa kufika kusanyikoni kwa sababu ya hali fulani ya mwilini. Kwa hiyo, ubatizo ulio halali kabisa umefanyiwa katika birika la kuogea nyumbani. Huo umekuwa msaada kwa wale wenye ugonjwa wa moyo, walio na umri mkubwa au wenye hali mbaya sana ya afya. Maji katika birika ya kuogea yaweza kupashwa moto na hivyo yasimdhuru mtu. Naye anayebatizwa anaweza kuingizwa majini polepole na kwa utulivu. Akiisha zoeana nayo, ubatizo wenyewe waweza kufanywa.
Namna gani juu ya watu wenye hali zisizo za kawaida kabisa? Hata katika nyingi za hali kama hizo uzamisho umewezekana. Watu walio na vidonda vilivyo wazi au matundu yenye kudumu kooni wamepata kubatizwa. Kidonda hicho kilifunikwa kwa kipande cha plastiki kikafungwa pembeni kwa muda mfupi kwa utepe. Vilevile watu wenye kutumia mashine ya kuwasaidia kuvuta pumzi wamepata kubatizwa. Mipango ilifanywa daktari au mwuguzi wa kike mwenye ujuzi asaidie. Mtu huyo aliyepooza aliingizwa majini huku akivuta hewa kwa kutumia mrija pamoja na kidude cha kutiwa mdomoni. Kisha, wakati wa kubatizwa, kidude hicho cha kutiwa mdomoni kiliondolewa, nao mwili ukazamishwa, na kisha mara tu baada ya kuinuliwa kutoka majini kile kidude cha mdomoni kikarudishwa mdomoni. Hali kama hizo zaonyesha kwamba, ijapokuwa uangalifu mwingi sana huenda ukahitajiwa, karibu katika hali zote ubatizo waweza kufanywa.
Bila shaka, huenda ikawa kwamba katika hali fulani zenye kupita kiasi ubatizo ungeonekana usiowezekana hata kidogo kwa wakati huo. Basi twatumaini kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye rehema atafahamu na kumkubali mtu huyo mwenye moyo wa kupenda ambaye amejiweka wakf moyoni mwake. (Zab. 103:13, 14; Omb. 3:22) “[Yehova] humjaribu mwenye haki. . . . Wanyofu wa moyo watamwona uso wake.” (Zab. 11:5, 7) Hivyo twaweza kuwa na hakika kwamba, inapokuwa haiwezekani hata kidogo kumbatiza mtu aliyejiweka wakf karibuni kwa sababu ya hali fulani ya mwili, Yehova ataangalia jambo hilo kwa rehema.