Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 1/1 kur. 3-9
  • Wafufuliwa—“Kila Mmoja Mahali Pake”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wafufuliwa—“Kila Mmoja Mahali Pake”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIKU YA HUKUMU
  • ‘Tunajua Watainuka Katika Ufufuo’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Wakati Watu Waliokufa Watakapoishi Tena!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Suluhisho Pekee la Kifo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Zishikeni Sana “Habari Njema”!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 1/1 kur. 3-9

Wafufuliwa​—“Kila Mmoja Mahali Pake”

“Katika Kristo wote watarudishwa kwenye uzima; walakini kila mmoja katika mahali pake pafaapo.”​—1 Kor. 15:22, 23, The New English Bible.

1. Martha alionyeshaje kwamba aliamini kwamba Yesu angeweza kumponya ndugu yake Lazaro ugonjwa wake uliotokeza msiba?

YALIKUWA majira ya baridi kali yenye huzuni kule Bethania wakati jiwe lilipoviringishwa mlangoni pa kaburi la Lazaro aliyejulikana sana. Dada zake Waliobaki, Martha na Mariamu, na rafiki za jamaa hiyo walidhani kwamba hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya mwisho ya kumwona Lazaro wakati wa taratibu hii ya mambo. Rafiki yake mpendwa Yesu Kristo alifika siku ya nne ya kufa kwake Lazaro, ikaelekea kwamba amefika akiwa amechelewa mno. Martha aliondoka akaenda nje kumlaki Yesu, akamwambia hivi; “Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangelikufa.”

2, 3. (a) Martha alitazamia kufufuliwa kwa ndugu yake aliyekuwa ndani ya kaburi kutukie siku gani? (b) Kuhusiana na ufufuo huo, Martha alionyesha imani kama ya babu wake yupi?

2 Yesu akamwambia Martha: “Ndugu yako atafufuka.” Akionyesha imani yake katika ufufuo, Martha alimwambia Yesu: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”​—Yohana 11:1-24.

3 Martha alikuwa akifikiria ufufuo wa wanadamu wote waliokufa na kurudishwa kwenye uzima hapa duniani chini ya ufalme wa Mungu kupitia kwa Masihi wake, au Kristo. Yeye alimwamini Masihi huyu kuwa Yesu mwenyewe, ambaye alikuwa amefufua watu wengine kwenye uzima kama vile manabii Eliya na Elisha walikuwa wamefanya karne nyingi mapema. (Yohana 11:27) Imani yake katika ufufuo ilikuwa kama ile ya babu yake Ibrahimu, ambaye alikuja kuitwa “rafiki wa Mungu.” (Yak. 2:21-23) Ndugu wa Martha Lazaro alikuwa tayari amekwisha kufa na kuzikwa, walakini katika habari ya Ibrahimu mwana wake Isaka alikuwa yungali hai, akikaribia kutolewa kama dhabihu ya kibinadamu. Ilikuwa ni kama kwamba Isaka amekufa, kwa kuwa Ibrahimu alikuwa ameazimia kutii amri ya Yehova kwamba amtoe dhabihu. Kuhusu imani ya Ibrahimu wakati wa pindi hii yenye kujaribu, Paulo, mzao wa Ibrahimu, anaandika hivi:

4. Ibrahimu alimpataje mwana wake Isaka kutoka kwa wafu ‘katika njia ya mfano’?

4 “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee; naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka [kaburi]; akampata tena kutoka huko kwa mfano.”​—Ebr. 11:17-19; Mwa. 22:1-18; Isa. 41:8; 2 Nya. 20:7.

5, 6. (a) Ibrahimu alitazamia kufufuliwa kwa wanadamu wafu kuwe wakati gani? (b) Je! kufa kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo pasipo wao kupata mambo yaliyoahidiwa kuliiharibu imani yao katika serikali ya Mungu ya Kimasihi?

5 Kwa hiyo Ibrahimu aliuamini ufufuo unaokuja wa wanadamu waliokufa chini ya ufalme wa Kristo. Yesu Kristo, ambaye ufufuo wake mwenyewe ulifananishwa kimbele na ufufuo wa mfano wa Isaka, wakati mmoja aliwaambia wazao Wayahudi wa Ibrahimu hivi: ‘Ibrahimu, baba yenu alishangilia kwa taraja la kuiona siku yangu, naye aliiona, akafurahi.’ (Yohana 8:56) Kwa kupatana na maneno ya Yesu juu ya Ibrahimu, baba ya Isaka na babu ya Yakobo, twasoma hivi:

6 “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi, bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni, na wasafiri juu ya nchi. Maana hao wasemao maneno kama hayo waonyesha wazi kwamba wanatafuta nchi yao wenyewe. . . . Lakini sasa waitamani nchi iliyo bora, yaani, ya mbinguni [ufalme wa mbinguni ukiwa na Kristo aliyetawazwa]. Kwa hiyo Mungu haoni haya kuitwa Mungu wao; maana amewatengenezea mji.”​—Ebr. 11:13-16.

7, 8. (a) Maneno ya Yesu kwa Masadukayo kuhusiana na Ibrahimu, Isaka na Yakobo yanahakikishaje kwamba watafufuliwa? (b) Kupatana na Zaburi 45:16, Mtawala wa Kimasihi katika serikali ya kimbinguni atawafanyia nini Ibrahimu, Isaka na Yakobo?

7 Kwa kuwa Mungu amekwisha kufanya matayarisho kwa ajili ya Ibrahimu, Isaka na Yakobo waliokufa zamani, wanaume hao wa zamani wa imani wana hakika ya kupata ufufuo kutoka kwa wafu chini ya “mji,” au serikali, ambayo katika hiyo Masihi aliyetukuzwa, au Kristo, anatawala. Yesu mwenyewe alitaja uhakika huo katika mazungumzo na Masadukayo Wayahudi, ambao hawakuamini katika kufufuliwa kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Yeye alisema hivi: “Maana wafu watakapofufuliwa watakuwa kama malaika [siyo: ni malaika] mbinguni, hawataoa wala kuolewa. Lakini kuhusu swala la wafu kufufuliwa, hamjasoma yale aliyowaambieni Mungu? Alisema, “Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Isaka na Yakobo!” Basi, yeye si Mungu wa wafu, bali ni Mungu wa walio hai.”​—Mat. 22:30-32, HNWW.

8 Yehova alikuwa Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo kabla hawajafa. Yeye aweza kuwa Mungu wa Ibrahimu aliye hai, wa Isaka aliye hai, wa Yakobo aliye hai, kwa kuwafufua tu kutoka kwa wafu. Watakuwa watu wanaoishi duniani chini ya “mji,” au serikali ya kimbinguni, ambayo Yehova Mungu wao amewatayarishia. Hiyo itakuwa kwa utimizo wa Zaburi 45:16 kwa Masihi aliyetukuzwa, Yesu, akiwa mtawala katika “mji” huo, kuwaweka kama “wakuu katika nchi yote.” Masihi wa kimbinguni atawatimizia kila kimoja cha vyeo vyake kama vile imetabiriwa katika Isaya 9:6, hata na Baba wa milele.

9. Nabii Isaya aliandika nini kuhusiana na ufufuo wa wanadamu wafu, na baada ya “ghadhabu” ya Mungu juu ya nini?

9 Ibrahimu, Isaka na Yakobo na watu wengine wa kale wa imani watafufuliwa katika hiyo “siku ya mwisho” ambayo juu yake Martha alizungumza na Yesu muda mfupi tu kabla yeye hajamfufua ndugu yake Lazaro arudi kwenye uzima wa kidunia. (Yohana 11:24-44) Wanadamu watakaofufuliwa walikombolewa na dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, na kuhusu hawa nabii Isaya aliongozwa kwa roho aandike, akisema hivi: “Siku ile wimbo huu utaimbwa katika nchi ya Yuda; . . . ‘Wafu wako wataishi, maiti zangu zitafufuka; amkeni, kaimbeni, ninyi mnaokaa mavumbini, kwa maana umande wako ni kama umande wa mimea [tofauti na ukavu wa maiti], nayo ardhi itawatoa waliokufa.’” (Isa. 26:1, 19) Hivyo kutakuwako kuzaliwa tena, kuzaliwa mara nyingine kwa wafu wa dunia. Jambo hili litatukia baada ya Yehova kuonyesha hasira yake juu ya ulimwengu wenye hatia ya damu kwa ajili ya watu wote uliowaleta kwa kifo cha mapema kwenye Sheol, kaburi. Hiyo inamaanisha baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika hali ya ulimwengu ambayo Biblia huita Har–Magedoni.​—Ufu. 16:14, 16; 19:11-21.

10. Kwa hiyo, wakati wa hiyo “siku ya mwisho,”‏ ni kwa nini dunia haitakuwa tena kaburi la duniani pote?

10 Kwa hiyo, hiyo “siku ya mwisho” ambayo Martha aliitaja ndiyo ambayo katika hiyo wanadamu waliokufa warudishwe kwenye uzima tena mahali pa kulala wamefunikwa ndani ya ardhi. (Isa. 26:20, 21) Lo! namna hiyo “siku ya mwisho” itakavyoletea upya wanadamu wafu waliokombolewa uzima wa kibinadamu kwa mara nyingine! Dunia haitakuwa tena kaburi la duniani pote.

11 Hata watoto wachanga waliokufa na watoto walio chini ya ulinzi wa wazazi watapata kibali ya kurudishwa kwenye nafasi mpya za kukua kwenye ujana wa milele katika dunia ya paradiso. Katika njia hiyo kazi yenye kuleta kifo ya Mfalme Herode Mkuu itaondolewa. Yeye aliwatuma wanajimu wenye kuuliza habari waliotoka Mashariki waende Bethlehemu, ili wamtafutie “mfalme wa Wayahudi” aliyezaliwa karibuni. Alipanga hila ya kumwua Yesu, mwana wa bikira Mariamu Myahudi. Baada ya kushindwa katika jitihada zake zenye hila za kufahamu mahali alipokuwa “mfalme wa Wayahudi” mtarajiwa, Herode aliwatuma askari wake na kuwaamuru wawaue watoto wote wachanga waliokuwa na umri wa miaka miwili kurudi chini. Kuomboleza kwa akina mama waliofiwa katika Bethlehemu na kandokando yake kulikuwa kumetabiriwa katika unabii wa Biblia, pamoja na maneno yenye kufariji juu ya ufufuo.

11, 12. Mfalme Herode Mkuu alishindwaje katika jitihada zake zisizo na huruma za kumwua “mfalme wa Wayahudi” aliyezaliwa karibuni?

12 Mathayo mwandikaji wa Injili anatuambia hivi: “Ndipo lilipotimia neno lililonenwa na nabii Yeremia, akisema, Sauti ilisikiwa Rama, Kilio na maombolezo mengi, Raheli akiwalilia watoto wake, Asikubali kufarijiwa, kwa kuwa hawako.” (Mt. 2:1-18) Walakini Mariamu hakuwa kati ya wanawake wenye kulia na kuomboleza, kwani alikuwa ametoroka na mvulana Yesu na alikuwa amekwenda kule Misri kukaa huko mpaka Herode afe.

13. Kulingana na matumizi ya Mathayo ya unabii wa Yeremia, “nchi ya adui” ilikuwa nchi gani ambayo kutoka kwayo watoto hao waliochinjwa watatoka?

13 Hata hivyo, kwa mama hao waliofiwa mambo hayakuwa yasiyo na tumaini. Unabii wa Yeremia ambao kutokana nao Mathayo alitumia maneno yake uliendelea kusema hivi: “[Yehova] asema hivi, Zuia sauti yako, usilie, na macho yako yasitoke machozi; Maana kazi yako itapata thawabu, nao watakuja tena toka nchi ya adui; Ndivyo asemavyo [Yehova].” (Yer. 31:15, 16) Kulingana na njia ambayo unabii wa Yeremia ulivyotumiwa na Mathayo akiwa chini ya uongozi wa roho, “nchi ya adui” isingekuwa Babeli wa kale wa siku za Yeremia. Ilikuwa nchi ambayo adui, Herode Mkuu, alikuwa amewapeleka watoto wasio na hatia aliowaua kwa kifo cha mapema, nchi ya kifo. Vile-vile kifo kinatajwa kama “adui,” kwa kuwa 1 Wakorintho 15:26 lasema hivi: “Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.”

14. (a) Nchi ya Babeli ilipataje kuwa mahali pa kufia Waisraeli katika siku za Yeremia? (b) Watoto wachanga wasio na hatia wa Bethlehemu ‘watarudije,’ na katika siku gani?

14 Nchi ya kabla ya Ukristo Babeli ilipata kuwa nchi ambayo Wayahudi waliohamishwa ‘waliwekwa kwa kifo’ na watekaji wao. Wengi wa hao waliotekwa nyara walifia huko kama wageni. (Zab. 79:11; 102:20; Isa. 14:17) Wakati na baada ya mwaka 537 K.W.K. maelfu ya “wafungwa” Wayahudi ‘walirudi’ kutoka nchi ya adui Babeli. Kurudi kwa watoto wachanga wasio na hatia wa Bethlehemu ni kwa wakati ujao. Kutakuwa kwa njia ya kufufuliwa wakati wa “siku ya mwisho” iliyotajwa na Martha wa Bethania, “siku ya mwisho” hii itaanza baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni na baada ya kufungwa kwa Shetani Ibilisi na malaika zake walio mashetani.​—Ufu. 20:1-3, 11-15.

SIKU YA HUKUMU

15. Yesu alionyeshaje kwamba “siku ya mwisho” itakuwa ya kuhukumu wanadamu wafu waliofufuliwa?

15 “Siku ya mwisho” iyo hiyo itakuwa siku ya kuhukumiwa kwa wanadamu waliofufuliwa, kutia na wanadamu wale ambao hawakumsikia Yesu na hawakutii aliyosema. Yesu alionyesha jambo hilo aliposema: “Yeye anikataaye mimi, asiyeyakubali maneno yangu, anaye amhukumuye; neno hilo nililonena ndilo litakalomhukumu siku ya mwisho.” (Yohana 12:48) Yesu alishirikisha wakati wa kuhukumu ulimwengu wa wanadamu na ufufuo aliposema hivi: “[Mungu] akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.” (Yohana 5:27-29; tazama Mnara wa Mlinzi wa Februari 15, 1979, chini ya kichwa “Ufufuo wa Uzima na Mwingine wa Hukumu,” kur. 9-13.) Bila shaka hiyo “siku ya mwisho” haitakuwa siku ya saa ishirini na nne. Itakuwa kipindi cha wakati cha miaka 1,000 kwa urefu. Italingana na miaka 1,000 ya utawala wa Kristo.​—2 Pet. 3:8; Ufu. 20:4, 6.

16 “Siku” hiyo itakuwa yenye utukufu, kwa kuwa ndipo yatakapofutwa matokeo yote ya kifo tulichorithi kutoka kwa Adamu na Hawa kwa sababu ya hukumu ya kifo waliyopewa. Kwa hiyo utawala wa miaka 1,000 wa Kristo ni jambo ambalo sote twapaswa kutazamia, kwa sababu katika 1 Wakorintho 15:25, 26 ZSB, imeandikwa hivi: “Maana sharti atawale hata atakapoweka adui zote chini ya miguu yake. Adui ya mwisho ya kuondoshwa ni mauti [tuliyorithi kutoka kwa Adamu].”

17. Iwapo mtu ye yote atakufa baada ya “siku” hiyo ya hukumu, itakuwa kwa sababu gani, na kitakuwa kifo cha namna gani?

17 Kuuawa kwa kifo kilicholetwa na Adamu ambacho tulirithi kunafananishwa kwa ajili yetu na mambo ambayo Yesu alimtumia mtume Yohana aandike. Ukisimulia “siku ya mwisho” ya kufufuliwa kwa wanadamu, Ufunuo 20:13, 14 wasema hivi: “Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na [Hades] zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. Mauti na [Hades] zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto.” Kwa hiyo mtu ye yote duniani atakayekufa baada ya hapo hatakufa kwa sababu ya kurithi dhambi kutoka kwa Adamu. Atakufa kwa kuvunja sheria ya Mungu makusudi na kufanya dhambi. Kifo chake wakati huo kitakuwa “mauti ya pili,” ambayo kutoka kwayo hatafufuka tena.

18. Yesu anawakomboa wanadamu kutoka kwa kifo gani na matokeo gani, hivyo yeye ni nini kwao?

18 Yesu Kristo atawafungua wanadamu kutokana na kifo kilicholetwa na Adamu na kaburi letu la kawaida, Hades peke yake. Yeye alituhakikishia jambo hili aliposema hivi: “Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, . . . Nami ninazo funguo za mauti, na za [Hades].” (Ufu. 1:17, 18) Kwa hiyo, akiwa na sababu nzuri, Yesu alimwambia Martha hivi: “Mimi ndio huo ufufuo, na uzima.”​—Yohana 11:25.

19. Ni mtu gani mwenye kujulikana sana kwa ajili ya ustahimilivu wake atakayekuwa kati ya wale watakaofufuliwa, naye alitaka alale amezikwa katika Sheol mpaka lini?

19 Kati ya wale ambao Mfalme Yesu Kristo mwenye kutawala atatumia kwa ajili yake ufunguo wa Hades (au, Sheol, katika Kiebrania) ni mwanamume anayejulikana sana kwa ajili ya ustahimilivu wake. Huyu ni Ayubu wa nchi ya Uzi katika Mashariki ya Kati ya kale. Kwa sababu ya ole zinazoongezeka juu yetu leo, wengine wetu huenda wakaanza kuona moyoni kama Ayubu na kutamani kwamba tungekufa na kuzikwa katika Hades, au Sheol. Walakini twapaswa kuwa na kile alichokuwa nacho Ayubu, imani katika ufufuo. Alifahamu kwamba jambo hili litakapotukia wakati wa “siku ya mwisho,” angekombolewa kutokana na taabu zote za wanadamu za sasa. Iwapo angelala katika kifo na kuzikwa, angepumzika mpaka “mbingu” au majeshi yaliyo na nguvu zipatazo za kibinadamu ambayo sasa yanaongoza wanadamu yatoweke. Kutoweka kwao kutawezesha mwanzo wa badiliko la ajabu la hali za kidunia hapa chini. Kwa hiyo, Ayubu alimwomba Yehova Mungu hivi:

20. Kulingana na Ayubu 14:12-15, Ayubu alimwomba Mungu nini?

20 “Mwanadamu hulala chini, asiinuke; . . . hawataamka, Wala kuamshwa usingizini. Laiti ungenificha [katika Sheol], Ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, Na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka! Mtu akifa atakuwa hai tena? Mimi ningengoja siku zote za vita vyangu [kwa sababu ya Mungu kuruhusu uovu], Hata kufunguliwa kwangu kunifikilie. Wewe ungeita, nami ningekujibu; Ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.”​—Ayubu 14:12-15.

21. Ayubu alitaka kuona badiliko gani la uso, naye alitazamia “mkombozi” wake afanye nini kwa ajili yake?

21 Wakati wa mateso ya Ayubu, yeye hakuona uso wa Mungu ulimwelekea kwa kibali. Je! sisi leo wakati mwingine huona moyoni hivyo, kwa sababu ya taabu ambayo Mungu huachilia ije juu yetu, kwamba yeye hatukubali, na kwamba tungependa kuona badiliko la wonyesho wa uso wake kutuelekea? Wakati wa “siku ya mwisho” inayokuja kutakuwako ufufuo wa wanadamu waliokufa kutoka katika Sheol, au Hades, na uhakika huu utaonyesha kwamba Yehova Mungu huwatazama kwa kibali wanadamu waliokombolewa. Ayubu aliamini kwamba kungekuwako ufufuo kwake na kwa wanadamu wengine kwa sababu kulikuwa na “mkombozi,” mtu ambaye angetoa bei ya kumnunua amnunue kutoka kwa ‘vita vyake,’ au, ‘utumishi wa lazima,’ NW, ambao katika huo alikuwa ameuzwa.

22, 23. (a) Ayubu aliamini kwamba kungekuwako mtu wa kutoa msingi wa ufufuo wake kwa sababu alikuwa na uhakika katika nini? (b) Ayubu alimtazamia “mkombozi” huyu aje wakati gani, naye Ayubu alitazamia kuona uso wenye kibali wa nani?

22 Ayubu alikuwa na uhakika katika ukamilifu wake wa kibinafsi kwa Yehova wajapokuwa watu waliomshtaki kwa uongo. Hivyo, alikuwa na hakika kwamba kungekuwako “mkombozi” wake. “Mkombozi” huyo angetokea baada ya kufa kwa Ayubu, walakini Ayubu angeacha kumbukumbu zuri lipate kufikiriwa na “mkombozi” wake. Kwa uhakika wa kwamba “mkombozi” anayekuja angetoa msingi wa ufufuo, Ayubu alitamka hivi kwa mshangao:

23 “Lakini mimi najua ya kuwa [mkombozi] wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi. Na baada ya ngozi yangu kuharibiwa hivi, Lakini, pasipokuwa na [ngozi yangu kwa sababu ya kutoka ngozi] nitamwona Mungu; Nami nitamwona mimi nafsi yangu, Na macho yangu yatamtazama, wala si mwingine. [Figo z]angu [z]azimia ndani yangu!” kwa sababu ya matazamio makubwa sana.​—Ayubu 19:25-27.

24. Yule “mkombozi” ambaye Mungu alimtoa alipata kuhusianaje na wanadamu, naye huyu alitoa nini kama “fidia ya wengi”?

24 Hivyo, basi, acheni Shetani Ibilisi aendelee kuwashtaki wanadamu kuwa hawastahili kufufuliwa kwa sababu ya kutoweza kuzaa wanaume na wanawake ambao wangeendelea kuwa wakamilifu kwa Mungu. Ufufuo wa wanadamu waliokufa utatukia wakati wa “siku ya mwisho” iliyotajwa na Martha wa Bethania. Sababu gani hivyo? Kwa sababu Mungu, ambaye hakuna jambo lisilowezekana kwake, ametokeza “mkombozi,” Mwana wake wa pekee ambaye alipata kuwa na uhusiano na wanadamu kwa kuzaliwa kama mwanamume mkamilifu. Yeye alikuja duniani kwa muda, si kwamba atumikiwe, “bali kutumikia, na kutoa nafsi yake [ya kibinadamu] iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28; Marko 10:45) Hii ilimtolea Mungu njia ya kutoa ruhusa ya kufufuliwa kwa wengi waliotolewa fidia au kukombolewa na kifo cha dhabihu cha Yesu Kristo.

25. Ni kwa sababu gani “siku ya mwisho” haitakuwa ya mwisho kwa wanadamu kuwapo, na, katika “siku” hiyo, Mungu atafanya nini kwa ajili ya wanadamu?

25 Kama matokeo, “siku ya mwisho” haimaanishi siku ya mwisho ya kuwapo kwa wanadamu, kwa sababu kufufuliwa kwa wanadamu waliokombolewa kunatukia “siku” hiyo chini ya utawala wa Kristo wa miaka elfu moja. Hii itakuwa “siku ya mwisho” baada ya siku zote zilizotangulia wakati ambapo Mungu ameruhusu dhambi na mauti itawale juu ya wanadamu na mamilioni yasiyohesabika yakienda kwenye Sheol, au Hades. Hiyo ndiyo itakayokuwa “siku” ya Mungu kuhesabu wanadamu waliokombolewa kuwa wamesamehewa dhambi zote za kwanza na kuwafundisha matakwa yake ya haki ili wapate uzima wa milele katika paradiso iliyorudishwa duniani.​—Isa. 26:9; Rum. 6:7.

26. (a) “Mahali pake pafaapo” Kristo palikuwa wapi kuhusiana na ufufuo? (b) 1 Wathesalonike 4:16 linaonyeshaje kwamba kutakuwako ufufuo wa wengine kwa kufuatana na nafasi au mahali au ubora?

26 Kwa hiyo kulipaswa kuwako kifo na kufufuliwa kwa “mkombozi” kabla ya kuwezekana kuwapo ufufuo wa wanadamu waliohitaji kukombolewa. Kwa hiyo kufufuliwa kwa Mkombozi Yesu Kristo kulikuwa kwa nafasi ya kwanza. Yeye alifufuliwa “katika mahali pake pafaapo” kuhusiana na ubora wa mahali. Zaidi ya hayo, kutakuwako ufufuo wa wengine kwa kufuatana na nafasi au mahali au ubora, kabla ya kufufuliwa kwa Ayubu, watoto wachanga waliochinjwa wa Bethlehemu na wanadamu wengine waliokufa. Jambo hili linavutwa kwa fikira zetu na maneno yaliyoongozwa kwa roho yaliyoandikwa katika 1 Wathesalonike 4:16, ambapo pasema hivi: “Nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.” Ni nani hao watakaoshiriki kwanza katika ufufuo, na ni wakati gani na kwa namna gani?

16. Ni kwa sababu gani, kama inavyoonyeshwa katika 1 Wakorintho 15:25, 26, “Siku” ya hukumu inayokuja itakuwa yenye utukufu?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wasia furaha ya kuwakaribisha kutoka kwa wafu wanaume waaminifu wa kale, na furaha ya akina mama wakiwapokea tena Watoto wao waliouawa na Herode!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki