Zaburi
Kwa Sababu Gani Ni Vizuri Kupiga Asante?
MAANDIKO Matakatifu yanatutia moyo mara nyingi tujithibitishe kuwa watu wenye shukrani. Roho ya kuthamini mambo inajenga watu wale wengine, inaendeleza amani na kutuongezea furaha sisi wenyewe. Lakini mambo ni tofauti sana kwa watu wasiopiga asante! Huenda wao wakawa na malalamiko kisha roho yao ya kichoyo inavunja watu moyo na kuwaumiza moyoni.
Roho ya kupiga asante tunayopaswa tujitahidi kuisitawisha imeonyeshwa katika Zaburi 92. Zaburi hiyo inafunua wazi sababu gani ni jambo linalofaa na lenye faida kusitawisha roho ya kuthamini mambo. Tunasoma hivi: “Ni neno jema kumshukuru [Yehova], na kuliimbia jina lako, Ee Uliye juu. Kuzitangaza rehema zako asubuhi, na uaminifu wako wakati wa usiku. Kwa chombo chenye nyuzi kumi, na kwa kinanda, na kwa mlio wa kinubi. Kwa kuwa umenifurahisha, [Yehova], kwa kazi yako; nitashangilia kwa ajili ya matendo ya mikono yako.”—Zaburi 92:1-4.
Maneno yale yale ya kwanza ya Zaburi 92 yanaonyesha sababu yenye nguvu ya kumpigia Yehova asante. Ni “neno jema” yaani, ni haki, inafaa, inastahili. Yule Aliye Juu Zaidi anastahili tumpe shukrani zetu, kwa maana yeye ndiye Mpaji-uzima wetu naye ametupa vitu vinavyohitajiwa kuendeleza uhai na vinavyoweza kutusaidia tupate furaha na afya ya milele. Pia, roho ya kuthamini mambo ina mafaa kwetu. Watu wasio na shukrani hawawi na furaha kamwe.
Zaidi ya kuonyesha shukrani tunaposali, tunaweza pia kuinua sauti zetu tukiimba kwa kufuatana na muziki. Hivyo tunaliimbia jina la Mungu, yaani, Yule anayesimamiwa na jina hilo.
Inafaa sana kuanza siku yetu kwa kumpa Yehova shukrani kwa ajili ya fadhili za upendo wake, kwa sababu ya kutuhangaikia kwa njia yenye huruma. Tunakuwa na siku nyingine mbele yetu ya kuishi, na katika siku hiyo tunaweza kumsifu Baba yetu wa kimbingu. Tunapoamka asubuhi tukiwa na roho hiyo ya kuthamini mambo, tunaweza kusaidika tuitumie siku hiyo kumsifu na kumtukuza Yehova. Hapo tutajitahidi kulitii onyo la upole la Biblia, linalosema: “Mlapo, au mnywapo, au mtendapo neno lo lote, fanyeni yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Katika vipindi vya usiku ambavyo tunakuwa macho na kabla ya kwenda kulala, inafaa tuukumbuke “uaminifu” wa Yehova, hali yake ya kusema kweli, kutegemeka kwake akiwa mtimizaji wa ahadi zake. Tunaweza kumpigia asante kwa ajili ya baraka za siku zinazohakikisha kwamba yeye ni Mungu wa uaminifu. Nia hiyo ya kuthamini mambo mwishoni mwa siku na wakati wa usiku inaweza kututuliza, kutuongezea furaha ya usingizi wenye amani. Pasipo shaka, si baraka za kila siku tu zinazotutolea nafasi ya kumsifu Yehova Mungu, bali utendaji wake wote au shughuli zake zinazohusu watu wake zinatupa sababu pia ya kufurahi. Kazi za Mungu za uumbaji na matendo yake ya kuokoa uhai zimo kati ya kazi ambazo tunapaswa kufurahia.
Akitoa maelezo juu ya kazi na mawazo ya Yehova, mtunga zaburi anaendelea kusema: “Ee [Yehova], jinsi yalivyo makuu matendo yako! Mawazo yako ni mafumbo makubwa.” (Zaburi 92:5) Kazi za uumbaji wa Yehova na matendo yake ya kuokoa uhai pia ni ajabu kubwa sana. Kwa sababu mawazo yake ni yenye kina kirefu (ni mafumbo), si vyepesi kuyafahamu. Ili kuyafahamu mtu anatakwa achunguze sana mambo, wala si kuyatazama kijuu-juu tu. Watu wasiotumia akili sawa na wanyama au wale walio na tabia chafu-chafu hawawezi kufahamu hata kidogo. Ni kama vile mtunga zaburi alivyosema: “Mtu mjinga hayatambui hayo, wala mpumbavu hayafahamu.”—Zaburi 92:6; Yuda 10.
Ingawa huenda wenye haki wakataabika kwa muda fulani, Mwenye Nguvu Zote anaendelea kuutayarisha utimizo wa kusudi lake kuu ili awabariki. Angalia namna jambo hili linavyotiwa mkazo katika mistari 7 mpaka 15 ya Zaburi 92, ambapo tunasoma hivi:
“Wasio haki wakichipuka kama majani, na wote watendao maovu wakisitawi. Ni kwa kusudi waangamizwe milele; bali Wewe, [Yehova], U Mtukufu hata milele. Maana hao adui zako, Ee [Yehova], hao adui zako watapotea, na watendao maovu watatawanyika wote pia. Bali pembe yangu umeiinua kama pembe ya nyati, nimepakwa mafuta mabichi. Na jicho langu limewatazama walioniotea, sikio langu limesikia habari za waovu walionishambulia. Mwenye haki atasitawi kama mtende, atakua kama mwerezi wa Lebanoni. Waliopandwa katika nyumba ya [Yehova] watasitawi katika nyua za Mungu wetu. Watazaa matunda hadi wakati wa uzee, watajaa utomvu, watakuwa na ubichi. Watangaze ya kuwa [Yehova] ni mwenye adili, Mwamba wangu, ndani yake hamna udhalimu.”
Hakuna jambo lo lote linalotendeka lisiloonwa na Yehova Mungu anayekaa katika mbingu zilizo juu ya mbingu zote. Wakati utafika ambapo watendao maovu ‘hawatasitawi’ tena, wavuvumke wala wafanikiwe, bali watafikia kikomo chao. Ni wazi kwamba mtunga zaburi anawasemea watumishi wa Mungu kwa ujumla anaposema kwamba “pembe” yake, uwezo wake, utainuliwa juu na Yehova na kwamba yeye angejipaka mafuta, huo ukiwa ni mfano wa burudiko na furaha. Wakati ambao waovu wangeangamia, watendao haki ya adili kwa kuthamini mambo wangesitawi sana kama mitende na mierezi mikubwa na mirefu ya Lebanoni. Ikiwa imepandwa katika nyumba ya Yehova, kwa usemi wa mfano, miti hiyo ndio waabudu wa Yehova waliojitolea utumishi wake. Wanapata nguvu za kuwaendeleza kutoka kwake, kama kwamba ni kutoka kwenye udongo mtakatifu wa pale patakatifu. Hata katika umri wa uzeeni watafanikiwa kama miti inayoishi muda mrefu. Watanenepa na kuwa wabichi, wawe wakifurahia kuwa na nguvu za uchangamfu na afya. Muda wa maisha yao watatoa ushuhuda juu ya unyofu wa Yehova, uaminifu wake wa kutimiza ahadi zake. Aliye Juu Zaidi ni “Mwamba” wenye kutegemeka, mahali pa imara, usalama na ulinzi. Yeye ni mwenye haki ya adili kabisa.
Basi, sisi na tujithibitishe wenyewe kuwa wenye shukrani kwa Yehova. Kufanya hivyo kutatuwezesha tufurahie maisha yenye kuridhisha sasa tukiwa na tazamio la kuishi milele.