“Nifuateni, Nami Nitawafanya Kuwa Wavuvi Watu”
1-3. (a) Yesu aliwaalika watu wamfuate kwa ajili ya kazi gani? (b) Kuitikia kwa wale wa kwanza walioalikwa kwaonyeshaje kwamba walikuwa na imani?
YOHANA MBATIZAJI alikuwa amemaliza kazi yake, na sasa Yesu aliyetiwa mafuta alikuwa anaendeleza tangazo hilo lenye kusisimua: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 3:2; 4:12-17) Walakini Yesu Kristo asingekuwa peke yake katika kuzijulisha habari njema. Akitembea kando ya Bahari ya Galilaya, aliwaona Simoni Petro na Andrea wakitupa wavu wa kuvua samaki. Akawatolea mwaliko huu: “Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu.” Wao hawakusita-sita. ‘Mara moja’ wakaziacha nyavu zao na kumfuata Yesu. Kisha Yesu akawaona Yakobo na Yohana katika merikebu ya kuvulia samaki, na kuwaita. ‘Mara moja’ wakauacha mtumbwi huo na baba yao ili wamfuate Yesu.—Mt. 4:18-22.
2 Yesu aliwekea wanafunzi hawa wapya mfano mzuri, alipokuwa akiwazoeza wawe “wavuvi wa watu.” Wao walikuwa wenzi wake wa wakati wote alipokuwa “akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yote, na kuihubiri Habari Njema ya ufalme, na kuponya ugonjwa na udhaifu wa kila namna katika watu.”—Mt. 4:23.
3 Katika Kapernaumu, katika Galilaya, Yesu alimwona Mathayo (Lawi) ameketi kitako kwenye afisi ya kutoza ushuru na kumtolea mwaliko huu, “Nifuate.” Mara moja Mathayo akaacha kukusanya ushuru ili amfuate Yesu. (Mt. 9:9; Marko 2:14) Kwa mara nyingine, Yesu “alikuwa akizunguka katika miji yote na vijiji” apate kufundisha na kuhubiri habari njema za ufalme, huku pia akifanya maponyo. Ijapokuwa wafuasi wake walikuwa wakiongezeka katika hesabu, Yesu aliwaambia hivi: “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.”—Mt. 9:35-38.
4. (a) Sababu gani mitume walichaguliwa? (b) Yesu anatazamia nini kwa wale wanaomfuata?
4 Kutoka kwa wanafunzi hawa wa kwanza, sasa Yesu alichagua 12 wawe mitume wake, “wapate kuwa pamoja naye, na kwamba awatume kuhubiri.” (Marko 3:14) Baadaye, mitume wale waaminifu wangekuwa mawe ya msingi ya kundi la Kikristo. (Efe. 2:20; Ufu. 21:14) Walikuwa na nia, tayari kutumikia na wenye furaha kwa kushirikiana na Yesu katika kazi ya Ufalme. Yesu aliwashauri na kuwaagiza waende mijini na vijijini, na kutembelea nyumba za watu. Yeye aliwaambia hivi: “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Yesu aliwajulisha wanafunzi wake kwamba kazi hiyo isingekuwa rahisi na kwamba wengi wangekataa kusikiliza maneno yao. Hata hivyo, wangekuwa na lazima ya kutoa ushuhuda, hata mbele ya watawala na watu wa mataifa. Wangepaswa kuwa wenye kujinyima na hodari, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Wala mtu asiyechukua [mti wake wa mateso] akanifuata, hanistahili.”—Mt. 10:7-18, 38.
5. Sababu gani wengine hawakubaliki kama wafuasi wa Kristo?
5 Si kila mtu aliyekubali mwaliko wa Yesu wa kumfuata. Kwa mfano, kulikuwako yule tajiri aliyependelea mali kuliko hazina ya kiroho ambayo angeifurahia akihubiri habari njema za Ufalme. (Mt. 19:16-24) Wengine, pia, walitoa visababu, kama ambavyo masimulizi katika Luka 9:57-62 yanavyoonyesha:
“Nao walipokuwa wakienda njiani, mtu mmoja alimwambia [Yesu], Nitakufuata ko kote utakakokwenda. Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana vioto, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake. Akamwambia mwingine, Nifuate. Akasema, Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu. Akamwambia, Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu. Mtu mwingine pia akamwambia,. Bwana nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu. Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.”
6. Yesu aliwazoeza na kuwatia moyo wafuasi wake namna gani, kama inavyosimuliwa katika Luka 10:1-20?
6 Baada ya kutoa mifano hiyo isiyofaa, Luka anatoa mifano inayofaa. Yeye anasimulia namna Yesu alivyochagua 70 wa wafuasi wake na kuwatuma wawili wawili wakapainie eneo mbele yake. Walipaswa kuwajulisha watu kwamba “ufalme wa Mungu umewakaribia.” (Luka 10:1-16) Wale 70 walipata furaha nyingi sana katika utumishi wao. Walakini Yesu aliwaonyesha kwamba walikuwa na sababu kubwa hata zaidi ya kufurahi, akisema hivi: “Furahini kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”—Luka 10:17, 20.
YESU AWEKA KIELELEZO
7, 8. Taja faida fulani ambazo “wavuvi wa watu” wa kwanza walipata kwa kushirikiana kwa ukawaida na Yesu katika kazi hiyo?
7 Waandikaji wa Biblia walioongozwa kwa roho Mathayo, Marko, Luka na Yohana wanasimulia namna wanafunzi wa kwanza wa Yesu walivyoshirikiana naye katika kazi ya kuhubiri na kufundisha ambayo ilitokeza faida kubwa kwao na kwa wengine. Yesu aliwafundisha mambo mengi mazuri sana juu ya Ufalme, na kweli hizo waliweza kuzishiriki na watu waliosikiliza. Zaidi ya yote, Yesu aliwasaidia wanafunzi wake wathamini uhusiano wao wenye thamani sana kama watumwa, watumishi au mawakili wa Yehova Mungu na Kristo Yesu.—Mt. 6:24; linganisha Luka 12:37, 42, 43.
8 Kama vile Baba yake, Yesu alikuwa mfanya kazi. Yeye alitaka wanafunzi wake wawe wafanya kazi pia, katika kuujulisha ujumbe wa Ufalme. (Yohana 4:34; 5:17; 9:4) Kwa hiyo, kwa muda upatao kama miaka mitatu, Yesu aliwazoeza wanafunzi wake wawe “wavuvi wa watu.” Vilevile, aliwaonya kimbele kwamba wangetendwa jinsi ile ile ambayo yeye, Bwana wao, alivyotendwa. Waliona mfano wake na alivyotenda chini ya mateso, alipokuwa akiwapa kielelezo cha kufuata sana. (Mt. 10:22-26; 1 Pet. 2:21) Yesu aliwafundisha mambo mengi ambayo alikuwa ameyapata kutoka kwa Mungu, nao walimwona akitimiza unabii mbalimbali. Yote hayo yalitia nguvu imani yao.
9. Yesu aliwafunza nini wafuasi wake juu ya uhusiano wao na Mungu kama watumwa?
9 Vilevile Yesu aliwatia moyo kwa unyenyekevu wafuate kielelezo chake kama watumwa wa Mungu. Yeye alisema hivi:
“Ni nani kwenu mwenye mtumwa alimaye au achungaye [kundi], atakayemwambia mara arudipo kutoka shambani, Njoo upesi, keti, ule chakula? Je! hatamwambia, Nifanyie tayari chakula, nile; jifunge unitumikie, hata niishe kula na kunywa, ndipo nawe utakapokula na kunywa? Je! atampa asante yule mtumwa, kwa sababu ameyafanya aliyoagizwa? Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya.”—Luka 17:7-10; linganisha 1 Wakorintho 7:22, 23; Ufunuo 19:5.
10. Mfano wa Yesu ulikuwaje sehemu ya kuzoeza wafuasi wake wamtumikie Mungu?
10 Kazi ya Yesu duniani ilipokaribia mwisho wake, alikusanya mitume wake kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa, na hapo, faraghani, akawapa mashauri mengi na vitia moyo. Vilevile aliwasafisha miguu yao ili kukazia kwao uhitaji wa kutumikia wengine, akisema hivi: “Nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo. Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka. Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.”—Yohana 13:15-17.
11. (a) Maandishi ya mazungumzo ya kirafiki ya Yesu pamoja na wanafunzi wake kabla ya kukamatwa kwake yanapatikana wapi? (b) Katika pindi hiyo, Yesu alikaziaje uhusiano kati ya imani na matendo? (c) Ni katika njia gani wanafunzi wangefanya kazi kubwa zaidi kuliko zile za Yesu?
11 Baada ya kumruhusu msaliti Yuda, aondoke Yesu aliwaagiza mitume wake waaminifu 11 kuhusiana na mwadhimisho mpya—ukumbusho wa kifo chake. Yeye alizungumza nao kwa kirafiki sana, akiwatayarisha kwa ajili ya daraka ambalo wangelichukua baada ya kuondoka kwake. (Yohana 13:30–16:33) Ili kuonyesha imani yao katika Kristo, wanafunzi hao wangepaswa kufanya kazi kama zake. Kwa hiyo aliwatia moyo kwa maneno haya: “Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi yeye naye atazifanya; naam; na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Yesu alifanya kazi yake ya kuhubiri katika nchi ya Palestina peke yake walakini kazi ya Ufalme ingepaswa kupanuka baada ya kufa na kufufuliwa kwake. Wanafunzi wake wangepaswa kuiongoza kazi hiyo ya wakati ujao. Mwishowe, habari njema za Ufalme zingehubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kuwa ushuhuda kwa mataifa yote, kisha ule mwisho ungekuja.—Mt. 24:14.
12. Ni nini ulio uhusiano kati ya kumpenda Kristo na yale tunayofanya?
12 Katika pindi hii ya mwisho ya kuwa na wanafunzi wake, Yesu alikazia uhitaji wa upendo wa kujinyima, akisema hivi:
“Mkinipenda, mtazishika amri zangu. Yeye aliye na amri zangu, na kuzishika, yeye ndiye anipendaye; naye anipendaye atapendwa na Baba yangu nami nitampenda na kujidhihirisha kwake. . . . Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake. Mtu asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia siIo langu, ila ni lake Baba aliyenipeleka.” (Yohana 14:15, 21, 23, 24)
Ni jambo la lazima kama nini kuzitii amri za Yesu Kristo!
MSAIDIZI AAHIDIWA
13. Msaada ungewajiaje wanafunzi wa Yesu baada ya yeye kwenda zake, nao wangechochewa kufanya nini?
13 Mitume hao walikuwa wameshirikiana sana na Yesu. Wakati wo wote walipotaka kufahamu jambo fulani au wakati tatizo lo lote lilipotokea, wangeweza kuzungumza na Yesu juu ya jambo hilo. Walakini sasa Yesu alikuwa akienda zake kwa Babaye. Kwa hiyo alimwomba Babaye awape msaidizi mwingine, roho takatifu ya Mungu, ambayo ingewafundisha na kuwakumbusha mambo yote ambayo Yesu alikuwa amewaambia. (Yohana 14:16, 17, 25, 26) Hiyo maana yake ilikuwa kwamba wangekuwa na kazi nyingi ya kutoa ushuhuda, kwa kuwa Yesu alitoa usemi huu: ‘Lakini ajapo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, hiyo roho ya kweli itokayo kwa Baba, hiyo itanishuhudia. Nanyi pia mnashuhudia, kwa kuwa tangu mwanzo mmekuwapo pamoja nami.’—Yohana 15:26, 27.
14. Wanafunzi wangejifunzaje kweli nyingine nyingi zaidi baadaye?
14 Yesu hakuwaambia wanafunzi wake mambo yote katika wakati huo. Hata hivyo, kwa kufika kwa roho takatifu, wangepata ufahamu kamili zaidi, ambao ungewatayarisha kwa kazi iliyokuwa mbele. (Yohana 16:12-14) Inatia moyo kama nini! Wale wanaomfuata Yesu kama watumwa wa Mungu wanaweza kuwa na hakika kupata msaada wakati wote kutoka juu na uongozi katika kweli kupitia kwa roho takatifu.
15. (a) Sababu gani Wakristo wanapaswa kuendeleza uhusiano wa karibu pamoja na Yesu Kristo nyakati zote, kulingana na mfano wake wa mzabibu? (b) Upendo wa Kikristo una sehemu gani katika jambo hilo?
15 Ili wafaulu katika kazi yao, wafuasi wa Yesu wanapaswa kuendeleza umoja wa karibu sana pamoja naye na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wake. Yesu alionyesha jambo hilo kwa mfano wa mzabibu na matawi yake, akikazia kwao uhitaji wa kudumu katika mzabibu na kuzaa matunda ili kwamba Babaye atukuzwe. Walipaswa kuzaa matunda kwa kutoa ushuhuda juu ya Ufalme na kwa kuonyesha utu wa namna ya Kristo. Watu wangeona ya kuwa wao ni wanafunzi wake kwa sababu ya upendo wao wa kweli kati yao.—Mt. 21:43; Yohana 13:34, 35; 15:1-12; tazama pia Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 1979.
SI SEHEMU YA ULIMWENGU HUU
16. (a) Yesu aliwafunza wanafunzi wake nini katika Yohana 15:17-22 kwa habari ya msimamo wao katika ulimwengu? (b) Sababu gani alifunza juu ya jambo hilo?
16 Wale wanaokuwa “wavuvi wa watu” wanaonyesha upendo huo wenye nguvu, kwa mtu na mwenzake. Walakini, kwa sababu wao ni wafuasi wa Bwana wao, Kristo, Yesu, hawapendwi na ulimwengu. Yesu hakupendwa na ulimwengu, kwa kuwa yeye hakuwa sehemu yake. (Yohana 15:17-22; 16:1) Maarifa hayo yanasaidia Wakristo wote wa kweli katika kuendeleza ukamilifu wao chini ya majaribu—kama vile Yesu alivyoendeleza ukamilifu. Wale walio wa ulimwengu hawamjui Yesu Kristo. Wao wanachukia wafuasi wake, kwa kuwa wao wanafanya tamaa za Ibilisi.—Yohana 8:42-44; 14:30; 16:11.
17. Kwa sababu ya kutokuwa sehemu ya ulimwengu kama wafuasi wa Kristo, ni jambo gani ambalo lingewapata Wakristo wengine?
17 Kwa kuwa Wakristo wa kweli si ‘sehemu ya ulimwengu,’ hawapaswi kuiga roho ya ulimwengu yenye choyo, kiburi na yenye kugawanya. Jambo hilo linawawezesha kumtukuza Mungu na kuzaa matunda mengi kama uthibitisho wa uanafunzi wao. Lakini inamaanisha taabu kwao, kama vile Yesu alivyoonya:
“Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania kila mtu awauaye ya kuwa anamtolea Mungu ibada.”—Yohana 16:2-4; 15:8-10„
HAUKO PEKE YAKO KAMWE KATIKA UTUMISHI WA MUNGU
18, 19. (a) Wanafunzi wa Yesu wanahakikishiwa upendo wa nani, na kwa sababu ya nini? (b) Sababu gani ni jambo la maana kuthamini uhakika wa kwamba mtumishi wa Yehova hayuko peke yake kamwe, na kwa hiyo anapaswa kufanya nini?
18 Watumishi wa Yehova wanaweza kumtumainia kwa sababu ya upendo wake mwingi. Yesu alitoa uhakikisho huu: “Kwa maana Baba mwenyewe awapenda kwa kuwa ninyi mmenipenda mimi, na kusadiki ya kwamba mimi nalitoka kwa Baba.” (Yohana 16:27) Watumishi wa Yehova hawafanyi kazi peke yao. Ni kazi ya Mungu wanayofanya kama watumishi wake, na njia ya kutafuta msaada wa Yehova katika sala wakati wote imefunguliwa. Yesu alisema hivi: “Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu.” (Yohana 16:23, 24) Yesu akiisha kukamatwa, wakati wenye magumu ungewapata wafuasi wake, kama vile alivyoonya kimbele:
“Tazama, saa yaja, naam, imekwisha kuja, ambapo mtatawanyika kila mmoja kwao kwao, na kuniacha mimi peke yangu; walakini mimi si peke yangu, kwa kuwa Baba yupo pamoja nami. Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yohana 16:32, 33.
19 Ni jambo la maana kama nini kukumbuka kwamba hatuko peke yetu, kama vile tu Yesu asivyokuwa peke yake wakati alipokamatwa! Na lo! jinsi lilivyo jambo la lazima kumtegemea Yehova katika sala, sana sana katika nyakati za dhiki au taabu! Yesu aliomba kwa bidii mara nyingi katika wakati wake wa kujaribiwa. (Mt. 26:36-46; 27:46) Vivyo hivyo, wafuasi wake hawapaswi kukosa kutafuta msaada wa Yehova, bali wamwombe kwa uhakika na kwa imani.—Mt. 7:7, 8.
OMBI LA YESU KATIKA SALA
20. Ni baadhi ya mambo gani yanayotajwa na Yesu katika sala yake nzuri sana iliyoandikwa katika Yohana 17?
20 Baada ya Yesu kuwaagiza wanafunzi wake waaminifu katika usiku huo wa mwisho wa maisha yake ya kidunia, aliinua macho yake mbinguni na kumtolea Yehova sala nzuri sana kwa ajili yao. Sala yake ilitaja kwamba alikuwa amemaliza kazi yake mwenyewe duniani, walakini wafuasi wake walikuwa wangali ulimwenguni. Wanafunzi hawa wangeendelea kutangaza habari njema za Ufalme, wakilijulisha jina la Yehova, kama vile Yesu alivyokuwa amefanya. Kwa hiyo aliomba hivi:
“Baba mtakatifu, kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, . . . Mimi nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu. Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo naliwatuma hao ulimwenguni.”—Yohana 17:11, 14-18.
21. Yesu alionyeshaje uhakika wake katika mpanuko wa wakati ujao wa kundi la Kikristo?
21 Sala ya Yesu ilitia ndani zaidi ya wale mitume waaminifu 11. Yeye alikuwa akitazamia kundi lenye kupanuka ambalo lingeizunguka dunia yote, kukiwa na wanaume na wanawake zaidi wenye kumwamini Yesu kupitia kwa neno lenye kutangazwa na wafuasi wake. Yesu alisema hivi:
“Wala si hao tu ninaowaombea; lakini na wale watakaoniamini kwa sababu ya neno lao. Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo [na umoja nami] nami [na umoja nawe]; hao nao wawe [na umoja nasi]; ili ulimwengu upate kusadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma.’’—Yohana 17:20, 21.
22. Yesu aliimalizaje kazi yake duniani akiwa mmoja wa mashahidi wa Yehova?
22 Muda mfupi baada ya kuomba hivyo, Yesu alikamatwa. Alipoletwa mbele ya mtawala, Pilato, yeye alitoa ushuhuda kwamba, kwa kuwa ufalme wake haukuwa sehemu ya ulimwengu, watumishi wake—ambao vilevile hawakuwa sehemu ya ulimwengu—wasingepigana. Akiwa Shahidi mwenye kuongoza wa Yehova, yeye alitangaza hivi: “Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili ya haya, na kwa ajili ya haya mimi nalikuja ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu.” (Yohana 18:33-37) Hivyo Yesu aliwaachia Wakristo mfano mzuri wa kuiga katika miaka iliyofuata kuondoka kwake kutoka katika mambo ya duniani. Katika siku iyo hiyo aliuawa, akiwa amemaliza kwa uaminifu kazi ambayo Yehova alikuwa amempa afanye. (Yohana 17:4) Lo! namna alivyowapa wafuasi wake kielelezo kizuri sana, wakati wa huduma yake ya kidunia! Kweli kweli, wao wanatiwa moyo wamwige yeye kama mashahidi wa Yehova katika kazi yao kuu wakiwa “wavuvi wa watu”!
[Picha katika ukurasa wa 10]
Yesu aliwatuma wanafunzi wake kwenye nyumba za watu
[Picha katika ukurasa wa 11]
Chakula cha jioni cha mwisho cha Yesu duniani kilitutolea sisi leo ujumbe wenye nguvu nyingi