‘Afadhali Kuwa Wawili Kuliko Mmoja”
ILI TUWE wenye furaha, lazima tujione kuwa tunathaminiwa na tunatakiwa—ndiyo, tuone tunapendwa. Na ili tupendwe, lazima sisi wenyewe tuwe wenye kupenda. Twapaswa kuwa na nia ya kuingiza wengine katika utendaji wetu. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Afadhali wawili kuliko mmoja; maana wapata [thawabu] njema kwa kazi yao.”—Mhu. 4:9.
Thawabu hiyo ni nini? Sulemani anaendelea hivi: “Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake; lakini ole wake aliye peke yake aangukapo, wala hana mwingine wa kumwinua! Tena, wawili wakilala pamoja, hapo watapata moto; lakini mmoja aliye peke yake tu awezaje kuona moto? Hata ikiwa mtu aweza kumshinda yule aliye peke yake, wawili watampinga.” (Mhu. 4:10-12) Hivyo tukifanya kazi na mwenzi mzuri thawabu zinatokea kwa namna ya usaidizi, kutiwa moyo na ulinzi. Zaidi ya hayo, hujaona kwamba kufanya kazi pamoja na rafiki kunaifanya iwe rahisi zaidi, na kwamba wakati nao unaonekana ukipita haraka sana? Hata kukiwa na kazi isiyopendeza, hali ya kuona uchovu inapotea.
Mwenzi mwenye kutumainika si baraka tu kwa mambo ya kimwili. Kazi ya maana ya kuhubiri “habari njema” vilevile ni utendaji ambao “afadhali wawili kuliko mmoja.” Hiyo inahakikishwa na yale ambayo Yesu Kristo alifanya alipokuwa akiwapa mgawo wale 70 watangaze: “Ufalme wa Mungu umewakaribia.” Yeye ‘aliwatuma wawili wawili.’ Mpango huo ulikuwa mzuri kwa kujengana na kusaidiana. —Luka 10:1, 5-9.
WAKATI WA KUHUBIRI “HABARI NJEMA”
Baada ya kufufuliwa na kupaa kwa Yesu mbinguni, mara nyingi ilisaidia wanafunzi wake kufanya kazi pamoja na wenzi. Walipopata habari kwamba wengi katika Samaria walikuwa wamekubali kuhubiri kwa Filipo, mitume waliwatuma Petro na Yohana ili Wasamaria walioamini wapewe ‘roho takatifu.’ (Matendo 8:14, 15) Ijapokuwa Barnaba alitumwa peke yake kutoka Yerusalemu aende akasaidie kundi katika Antiokia, karibuni aliona uhitaji wa mwenzi wa kumsaidia kuendeleza “habari njema” huko. Kwa hiyo akaondoka aende Tarso akamchukue Sauli (Paulo). Baadaye wanaume hao wawili walifanya kazi pamoja katika kufanya na kufundisha wanafunzi katika Antiokia. Jitihada yao ya kushirikiana ilibarikiwa kukawa ongezeko. (Matendo 11:22-26) Baadaye, roho takatifu iliongoza kwamba Paulo na Barnaba washiriki katika kutangaza “habari njema” katika kisiwa cha Kipro na Asia Ndogo.—Matendo 13:2.
Angalia kwamba Barnaba alijitahidi sana kupata mwenzi ambaye aliona angekuwa msaada kwake. Iwapo alipitia njia ya nchi kavu, alisafiri zaidi ya maili 120 (kama kilomita 200) afike Tarso na kisha akajitahidi sana kumtafuta Paulo. Ingawa kumtafuta mwenzi wa kushiriki pamoja nawe katika kuhubiri “habari njema” kwa jirani zako huenda kusihitaji jitihada nyingi hivyo, je! wewe uko kama Barnaba katika kutaka mwenzi kweli kweli? Katika kundi unaloshiriki nalo, unapenda kufanya kazi hiyo pamoja na nani? Je! umekwisha kuchukua hatua ya kwanza kuuliza mtu huyo au watu hao?
USITAZAMIE MENGI MNO
Bila shaka, hatupaswi kutazamia mengi mno kutoka kwa wenzi wetu; wala hatupaswi kuacha mipango isipotimia vizuri kama tunavyotaka. Ingawa Paulo na Barnaba walifurahia miaka mingi pamoja wakiwa watoaji wa Injili, hawakuendelea kuwa wenzi. Baada ya kushiriki kuanzisha makundi mengi mapya, Paulo alipendekeza warudi wayatembelee. Barnaba alikubali lakini akataka kumchukua binamu yake Marko. Hata hivyo, Paulo hakutaka hivyo, maana Marko hakuwa ameandamana nao wakati wa safari yao ya kwanza ya umisionari. Kama matokeo, Barnaba akaamua kwenda na Marko Kipro, naye Paulo akachagua Sila awe mwenzi wake na wakasafiri kupitia Shamu na Kilikia, “wakatia nguvu makundi.”—Matendo 15:36-41, NW.
Kama ambavyo kitabu cha Biblia cha Matendo kinavyofunua, badiliko hilo halikuzuia kutangazwa kwa “habari njema.” Vivyo hivyo, ukimpoteza mwenzi ambaye umefurahia ushirika wake katika utendaji wa kutoa ushuhuda kwa wakati fulani, usivunjike moyo. Kuna washiriki wengine wa kundi wanaoweza kuchukua mahali pake iwapo una nia ya kuwatolea nafasi. Unaweza kushangaa namna inavyoweza kujenga kuhubiri nyumba kwa nyumba pamoja na wengine walio waamini wenzako. Bila shaka, hiyo haimaanishi kwamba sikuzote twahitaji kuwa pamoja na mtu mwingine. Mengi yanaweza kufanywa kwa kufanya kazi peke yetu, huku wenzi wetu wakitoa ushuhuda karibu nasi.
KUFAIDIKA KUTOKANA NA MIFANO YA KIBIBLIA
Mifano ya Kibiblia ya wale waliofanya kazi kwa uaminifu wakiwa na wengine katika kuendeleza “habari njema” yaweza kutusaidia leo katika kutafuta ‘thawabu njema kwa kazi yetu ya bidii.’ Barnaba alikuwa mtu mchangamfu, mwenye kusikitikia. Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu mitume walimpa jina la pili Barnaba, linalomaanisha “Mwana wa Faraja.” (Matendo 4:36) Ingawa alikuwa na sifa njema, mambo yanaonyesha kwamba Paulo alikuwa na zawadi bora zaidi bila shaka. Ilipokuwa ni kutoa “habari njema,” Paulo kwa wazi ‘aliongoza katika kusema.’ (Matendo 14:12, NW) Walakini hakuna dokezo kwamba mambo hayo yalitokeza wakati wo wote wivu au mashindano. Kwa hiyo, iwapo tutapata furaha katika kutumikia pamoja na wengine, twahitaji kuthamini kwamba Yehova Mungu anatumia washiriki wote wa kundi ili wafanye kazi yake. (1 Kor. 3:9) Twaweza kujifunza kwa mtu na mwenzake na kutiwa moyo na kujengwa na mtu na mwenzake. Mtume Paulo alikubali jambo hilo na, kwa hiyo, aliweza kuandika hivi kwa Waroma: “Kwa maana ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu.”—Rum. 1:11, 12.
Tunapothamini kweli kweli uwezo wa kufanya mambo na sifa njema za waamini wenzetu, tutachochewa tutumie vizuri zaidi karama zetu. Kwa mfano, huenda mtu akaona kwamba yeye ni mwenye urafiki na fadhili kwa watu anaokutana nao katika utendaji wake wa kutoa ushuhuda. Hata hivyo, baada ya kufanya kazi pamoja na babu au nyanya mwenye kuhurumia, huenda akapata kuona kwamba urafiki wake ni wa juu-juu tu. Kwa kwenda pamoja na mtu ambaye ni mwanafunzi wa Maandiko mwangalifu, ambaye maneno yanaonekana ni kama yanabubujika kutoka kinywani mwake, huenda mtu akapata kukubali kwamba anahitaji kufikiria zaidi anayosema. Licha ya kusaidiana kwa mfano, mara nyingi tukifanya kazi pamoja na mwenzi inamaanisha kwamba tutatumia wakati zaidi katika kutoa ushuhuda, maana hatutaki kumwacha mwenzi wetu peke yake.
Imependeza Yehova Mungu na Bwana Yesu Kristo kutumia watu wa kawaida kutimiza kazi ya maana zaidi duniani. Kazi hiyo ni kusaidia wengine wawe na waendelee kuwa watumishi waaminifu wa Aliye Juu Zaidi wakiwa wanafunzi washikamanifu wa Mwanawe. (Mt. 28:19, 20, NW; 1 Kor. 1:26, 27) Kwa sababu ni kazi ya Mungu, hatujui Yehova Mungu atatumia njia gani kufungua mioyo ya watu. Haihusu kusema peke yake. Jambo la maana sana sana ni roho ambayo kwayo ujumbe huo unatolewa. Watu wawili wanapofanya kazi pamoja, wote wanafanya sehemu yao kwa ajili ya roho hiyo. Miezi au miaka mingi baadaye huenda tukapata habari kwamba si mahubiri yetu ya ufasaha kutoka kwa Neno la Mungu yaliyomfanya mtu huyo atusikilize. Mahali pake, yaweza ikawa ni tabasamu (kicheko) nzuri ya mwenzi wetu ambaye alikuwa amejiunga nasi karibuni katika kutangaza “habari njema.”
Je! wakati huu unapata baraka zinazotokana na kutoa ushuhuda pamoja na mwenzi? Je! umeona kwamba hiyo imekusaidia utumie wakati zaidi katika kueneza “habari njema” na kwamba unafurahia jambo hilo zaidi? Kwa upande mwingine, iwapo unafanya sehemu kubwa ya kutoa ushuhuda ukiwa peke yako, mkumbuke Filipo mtoaji wa Injili. Kwa ajili ya mateso katika Yerusalemu alitoroka mpaka Samaria naye akabatiza Wasamaria wenye kuamini. Baadaye, malaika wa Yehova alimtuma aongoe na kubatiza towashi Mwethiopia. Baadaye, “[roho ya Yehova ikamnyakua] Filipo, . . . Filipo akaonekana katika Azoto, na alipokuwa akipita akahubiri Injili katika miji yote, hata akafika Kaisaria.” (Matendo 8:1-40) Vivyo hivyo, katika nyakati za kisasa, sehemu nyingi zimefunguliwa zitolewe ushuhuda wa Ufalme na Mashahidi wajasiri wenye kufanya kazi pamoja na usaidizi wa roho ya Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kama vile katika siku za Yesu, kuwa na mwenzi katika kuhubiri “habari njema” kunajenga