Baraka za Umoja wa Kidugu
BILA shaka umoja ni baraka. Kupitia kwa jitihada ya umoja ya wengi, mengi zaidi yanaweza kutimizwa kuliko anavyoweza kufanya mtu mmoja. Wakati watu wanaposikizana, wanapata furaha nyingi katika kufanya kazi pamoja.
Akiongozwa na Mungu, Daudi aliandika juu ya baraka ya umoja wa kidugu. Kwa kuwa Waisraeli wote walikuwa wazao wa mwanamume mmoja Yakobo, maneno ya Daudi katika Zaburi 133 kweli kweli yalilipasa taifa lote. Leo Wakristo waliojitoa ni washiriki wa udugu wa ulimwenguni pote na kwa hiyo wapaswa kujitahidi kuendeleza umoja wenye kupendeza unaosimuliwa na mtunga zaburi hiyo. “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja. Ni kama mafuta mazuri kichwani, yashukayo ndevuni, ndevu za Haruni, yashukayo mpaka upindo wa mavazi yake. Kama umande wa Hermoni ushukao milimani pa Sayuni. Maana ndiko [Yehova] alikoamuru baraka, naam, uzima hata milele.”—Zab. 133:1-3.
Wakati makabila yote ya Israeli walipokuja Yerusalemu kwa zile sikukuu tatu za kila mwaka, walikuwa na nafasi ya kukaa pamoja kwa umoja. Ingawa walikuwa wametoka katika mataifa mbalimbali, walikuwa jamaa moja ya ndugu. Kuwa kwao pamoja kulikuwa na uvutano unaopendeza na kujenga. Matokeo ya kukaa pamoja hivyo kwa umoja yalikuwa kama mafuta mazuri ya kupaka—kitu chenye kuburudisha chenye harufu nzuri inayodumu na kupendeza. Mafuta yaliyomwagwa kichwani mwa Haruni yalitiririka kwenye ndevu zake ndefu na kumwagika kwenye upindo wa vazi lake. Vivyo hivyo, matokeo yenye kujenga ya kukaa pamoja kwa Waisraeli yalikuwa na uvutano wenye kuenea, ukienea kati ya watu waliokusanyika. Jambo hilo liliwezesha kutokuelewana na kupendelea kuondolewe. Ilikuwa kana kwamba mafuta mazuri yalikuwa yameenea pote. Bila shaka, wa kusifiwa kwa ajili ya jambo hilo, alikuwa Yehova Mungu ambaye baraka zote hutoka kwake.
Vivyo hivyo, wakati umoja huo wa kidugu unaosimuliwa na mtunga zaburi unapokuwa kati ya Wakristo, hakuwi kugombana, kutafutia wengine makosa au kulalamika wakati wote. Walakini kushirikiana kwao ni kwema, kwenye kujenga na kufaidi. Wakiwa wameunganishwa katika kifungo cha upendo, kwa vitendo wanahangaikiana na kufurahia kuwa pamoja. Umoja wao unawaletea furaha kwa sababu ya kutiana moyo na kujengana kunakofuata. Kutokuelewana au matatizo yo yote yanaweza kuondolewa wakati wote wanapomkaribia Yehova Mungu kwa umoja katika unyenyekevu, wakitaka uongozi, msaada na msamaha wake kwa ajili ya dhambi zao.
Kukaa kwa Israeli pamoja katika umoja kulikuwa kama umande wa Mlima Hermoni pia. Mlima huo, ulioinuka zaidi ya futi 9,000 (metre 2,700) juu ya bahari, vilele vyake vinafunikwa kwa theluji karibu mwaka wote. Kilele cha Hermoni chenye Theluji kinagandisha mivuke ya usiku na katika njia hiyo unatokeza umande mwingi unaohifadhi mimea wakati wa majira marefu ya ukame. Mikondo ya hewa yenye baridi kutoka vilima vya Hermoni vilevile yaweza kuchukua mivuke hiyo hata kufika Mlima Sayuni kule-e-e kusini, ipate kuganda kuwa umande. Kwa hiyo mtunga zaburi hiyo alisema kwa usahihi juu ya ‘umande wa Hermoni ukishuka milimani pa Sayuni.’ Maana yake ni uvutano wenye kushuka, uvutano wenye kuburudisha, unaohifadhi (unaotunza) mimea.
Umoja wa ndugu Wakristo ni wenye kupendeza vivyo hivyo. Una uwezo wa kuhifadhi uhai pia. Ndivyo ilivyo kwa sababu, wanapoona upendo uliopo kati ya watumishi wa kweli wa Mungu leo, watu wengi wanaanza kutaka kujua juu ya chanzo cha umoja huo. Ndiposa uchunguzi wao unapowaingiza katika njia inayoongoza kwenye uzima.
Kabla ya kuanzishwa kwa kundi la Kikristo, Sayuni, au Yerusalemu, ulikuwa ndio makao makuu ya ibada ya kweli. Kwa hiyo, kwa kuwa Yehova Mungu alikuwa amechagua mahali hapo, ndipo ambapo Aliye Juu Zaidi alipoamuru baraka iwe. Yeye, Chanzo cha baraka zote, kwa kuwakilishwa alikuwa anakaa hekaluni Yerusalemu; kwa hiyo ingeweza kusemwa kuwa baraka zilikuwa zikitoka huko. Kwa maana hiyo, uzima wote wa taifa la Israeli ulishikamanishwa na Yerusalemu, au Sayuni.
Kwa sababu ibada ya kweli haitegemei tena sehemu yo yote ya mahali fulani, upendo kati ya watumishi wa Mungu unapaswa kuonekana kila mahali. (Yohana 4:21, 23, 24) Upendo huo ndio unaotofautisha kweli kweli wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. Mwana wa Mungu alisema hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:35) Hakika twapaswa kufanya kazi kwa bidii ili tuuonyeshe upendo huo ili kwamba umoja wetu na waamini wenzetu ufananishwe na mafuta ya kupaka yenye kunukia na umande wenye kuburudisha wa Mlima Hermoni.