Kuondoa Doa la Dhambi
BAADA ya Yehova Mungu kumaliza utendaji wake wa kuumba, alichunguza vyote alivyoumba na kuvitangaza kuwa ‘vyema sana.’ (Mwa. 1:31) Kila kitu alichokuwa ameumba kilikuwa kikamilifu. (Kum. 32:4) Wakati dhambi ilipoingilia mpango huo wa haki, ilikuwa kama donda baya lisilotakiwa lenye kuvamia mwili wenye afya.
Kwa kweli, si wanadamu peke yao ambao wamemwasi Mungu na kufanya dhambi. Biblia huzungumza juu ya “malaika waliofanya dhambi.” (2 Pet. 2:4, NW) Ni kiumbe wa kiroho, Shetani Ibilisi, aliyeongoza hapo kwanza Adamu na Hawa kwenye mwendo mbaya. (Yohana 8:43, 44) Hata hivyo, hakuna jambo lo lote linaloweza kufanywa kwa ajili ya roho hao wabaya. Walikuwa wakamilifu nao walifanya uchaguzi wa kukusudia. Hivyo, dhambi yao ilikuwa isiyoweza kusamehewa. Doa la dhambi yao litaondolewa toka ulimwenguni wote kwa kuharibiwa kwao kwa mwisho katika wakati wake Mungu.—Mt. 25:41.
Vivyo hivyo, Adamu na Hawa walichagua kufanya dhambi. Ingawa waliumbwa wakiwa wakamilifu, walifanya kosa kwa kukusudia. Kwa hivyo, kwa kupenda wakawa watumwa wa dhambi, kwa kuwa Yesu mwenyewe alieleza hivi: “Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:24) Hatimaye waliondolewa, Mungu alipowaruhusu wafe kama matokeo ya kutokamilika kwao kulikoletwa na dhambi.—Mwa. 3:19; 5:5.
Hata hivyo, kwetu ni tofauti. Sisi, pia, tu watumwa wa dhambi, walakini si kwa kuchagua. Sisi tu wafanya dhambi kwa sababu tulizaliwa hivyo, kana kwamba tulikuwa tumeuzwa kama watumwa hata kabla ya kuzaliwa kwetu. (Rum. 5:12; 7:14) Hivyo, Yehova Mungu, katika upendo wake na hekima pia, amefanya mpango ili tutoke katika utumwa wa dhambi, iwapo twataka kweli kweli.
Kutatua Tatizo Hilo
Katika kushughulika kwake na taifa la Israeli, Yehova alionyesha kwamba anakubali kanuni ya ukombozi. Kwa mfano, iwapo Mwisraeli alikuwa maskini naye akalazimika kujiuza kama mtumwa kwa mtu asiye Mwisraeli, mtu wa ukoo wa karibu angeweza kumkomboa, iwapo angeweza kufanya hivyo. (Law. 25:47-49) Bei yenyewe ilikuwa imewekwa, hata kwamba ukombozi ulikuwa wa haki kabisa.
Vilevile Yehova aliweka kanuni ya ulinganifu katika kushughulika na hatia ya dhambi. Kwa mfano, iwapo mtu angemwumiza Mwisraeli mwenzake kwa kukusudia, kulingana na haki angepaswa kuumizwa vivyo hivyo. Sheria ilitaja kwamba “utatoza uhai kwa uhai, jicho kwa jicho, jino kwa jino, mkono kwa mkono, mguu kwa mguu, kuteketeza kwa kuteketeza, jeraha kwa jeraha.”—Kut. 21:23-25.
Kwa kulinganisha, Mungu angeruhusu wanadamu wakombolewe kutoka utumwa wa dhambi, walakini hiyo ingefanywa kwa kupatana na haki ya hukumu. Bei ya kulipwa ingepaswa kuwa sahihi, si ndogo, kana kwamba kile kilichokuwa kikikombolewa hakikuwa chenye thamani. Bei hiyo ilikuwa nini? Ebu fikiri. Adamu alikuwa amepoteza uhai mkamilifu wa kibinadamu, usio na dhambi wenye uwezo wa kuishi milele. Ulikuwa wenye thamani sana.
Hakuna cho chote walicho nacho wanadamu kinacholingana na thamani hiyo. Hata watu tajiri zaidi ulimwenguni wanakufa. Fedha na dhahabu yao yote haiwezi hata kurefusha uzima huu usiokamilika, achana na kununua uzima wa milele. Mtunga zaburi aliyeongozwa kwa roho alisema hivi: “Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu [ukombozi] kwa ajili yake . . . ili aishi sikuzote asilione kaburi.” (Zab. 49:7-9) Kwa hiyo, msaada ulipaswa kuja kutoka nje ya jamii ya kibinadamu.
Kwa mara ya kwanza Mungu alifunua kusudi lake la kutoa msaada huo mara tu baada ya Adamu na Hawa kuchagua dhambi mahali pa utii. Alitabiri juu ya kuja kwa “uzao” ambaye angepinga uongozi wa kiumbe mwovu wa kiroho aliyekuwa ameongoza wanadamu kwenye dhambi. (Mwa. 3:15) Kwa mafunuo yaliyofuatana, alijulisha jamaa ambayo ingezaa uzao huo. Hatimaye, mafunuo hayo yalielekeza kwenye wenzi wawili walioposana, yaani, Yusufu na Mariamu, waliokuwa wakiishi katika Palestina siku za Milki ya Roma.—Mwa. 22:15-18; 49:10; Luka 1:26-35.
Wenzi hao walipata kujua kwamba Mariamu angepata mwana ambaye angefanya sehemu kubwa katika kuondoa doa la dhambi kutoka kwa uumbaji wa Mungu. Malaika wa Yehova alimwarifu hivi Yusufu katika ndoto: “Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa [roho takatifu]. Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao.” (Mt. 1:20, 21) Sasa kulikuwako mmoja ambaye angeweza “kumkomboa ndugu.”
Yesu alizaliwa akiwa mwana wa Mariamu, na, kwa hiyo, kweli kweli alikuwa Myahudi wa jamaa ya Daudi. Hata hivyo, kama ilivyofunuliwa baadaye, alikuwapo mbinguni kabla ya kuwa mwanadamu. Uhai wake ulihamishwa kwa nguvu ya kimwujiza ya Yehova kwenye tumbo la uzazi la Mariamu, ili Mwana wa Mungu azaliwe kama mwanadamu. (Yohana 1:1-3, 14) Kwa njia hiyo, Yesu hakurithi hali ya dhambi ambayo ilikuwa imelemaza wanadamu wote kufikia wakati wake. Kama vile Adamu, yeye alikuwa mkamilifu. Tofauti na Adamu, aliendelea kuwa mtii. Kwa hiyo, akiwa ndiye wa pekee katika historia ya kibinadamu, Yesu alikuwa mwanadamu ambaye hakufanya dhambi wakati wo wote. Mtume Petro alisema hivi: “Yeye hakufanya dhambi, wala udanganyifu haukupatikana katika kinywa chake.” Paulo alieleza kwamba Yesu alikuwa ‘mshikamanifu, mnyofu, asiye na unajisi, aliyetengwa na watenda dhambi.’—1 Pet. 2:22, NW; Ebr. 7:16, NW.
Hivyo Yesu alikuwa na kitu pekee kinacholingana katika thamani yake na uhai mkamilifu wa kibinadamu: uhai mwingine mkamilifu wa kibinadamu. Alipokufa, kifo chake hakikuwa “mshahara wa dhambi.” (Rum. 6:23) Yesu hakustahili kufa. Hivyo, wakati wa kufa kwake alitoa dhabihu kitu kilicholingana kabisa na uhai mkamilifu aliopoteza Adamu.—1 Tim. 2:6.
Dhabihu ya Yesu ilikuwa na matokeo tofauti kabisa na dhambi ya Adamu. Mtume Paulo alisema hivi: “Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.” (1 Kor. 15:22) Yesu aliweza kutumia uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa bei ya kununua wanadamu kutoka kwa dhambi. “Yeye alijitoa mwenyewe kwa ajili ya dhambi zetu ili apate kutuokoa sisi na taratibu mbovu ya sasa ya mambo na kulingana na mapenzi ya Mungu wetu na Baba.”—Gal. 1:4, NW.
Kukombolewa katika Dhambi
Kwa hiyo sasa kuna njia ya wanadamu kutokea! Bei ya ukombozi imekwisha lipwa. Je! hiyo inamaanisha kwamba kila mtu sasa atawekwa huru kutoka kwa utumwa wa dhambi naye arudishwe kwenye ukamilifu bila jitihada yo yote? Sivyo kabisa. Namna ambavyo mpango huo unavyofanya kazi ilielezwa na Yesu mwenyewe, aliyesema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Ndiyo, wale wanaomwamini Yesu Kristo, ambaye kupitia kwake Mungu alifanya mpango wa ukombozi, watafurahia uzima wa milele ambao walikosa kwa sababu ya kutokutii kwa Adamu kwa kukusudia.
Hata sasa, wale wanaokubali kweli kweli dhabihu ya Yesu wanapata faida. Wakati wa Mungu wa kurudisha wanadamu kwenye ukamilifu wa kibinadamu kwa njia halisi haujafika bado. Walakini iwapo, kwa sababu ya kutokamilika wanafanya dhambi, hiyo haivunji uhusiano wao na Baba yao wa kimbinguni usiweze kutengenezeka. Mtume Yohana aliandika hivi: “Nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki.” (1 Yohana 2:1, 2) Ndiyo, iwapo kwa sababu ya kutokamilika tunafanya dhambi, twaweza kumwomba Mungu kwa msingi wa dhabihu ya Yesu, tukiwa na hakika kwamba Yehova atatusamehe.—1 Yohana 1:7-9.
Basi, hiyo inamaanisha kwamba dhambi haina ubaya? Kwa sababu ya mpango huo wa upendo, sasa twaweza kufanya dhambi yo yote tunayotaka, na tuwe na hakika kwamba tutasamehewa kwa sababu ya dhabihu ya Yesu? Hapana, sivyo ilivyo. Tukitaka kufaidika na mpango huo, lazima tuonyeshe maoni yale yale kuelekea dhambi kama alivyofanya Yesu. Yeye ‘anapenda haki na kuchukia uasi,’ ndivyo inavyopaswa kuwa kwetu (Ebr. 1:9) Kama Paulo, twapaswa ‘kupiga-piga miili yetu na kuiongoza kama watumwa’ ili tushinde maelekeo ya dhambi. (1 Kor. 9:27, NW) Hiyo inahitaji kufahamu wazi dhambi ni nini na kupigana ili kuizuia. Mungu atatusaidia katika jambo hilo, nalo hilo laweza kutugeuza kabisa kama watu.—Rum. 12:2.
Walakini, tusipopigana na maelekeo yetu ya dhambi, huenda maneno yaliyofuata ya mtume Paulo yakatuhusu: “Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; bali kuna kuitazamia hukumu kwenye kutisha.”—Ebr. 10:26, 27.
Nao, wanaoonyesha kwamba, ujapokuwa wa mwili wao usiokamilika, wanataka kweli kweli kutoka kwenye utumwa wa dhambi wana taraja zuri ajabu. Wanaahidiwa nafasi ya kuishi katika taratibu mpya ambapo dhambi itakuwa jambo la wakati uliopita. Itakuwa imekwisha ondolewa kabisa katika uumbaji wa Mungu. Wakati huo, “hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isa. 11:9) Mtunga zaburi aliyeongozwa kwa roho anatuahidi kwamba “asiye haki [au, anayefanya dhambi kwa kukusudia] hatakuwapo.” Tofauti yake, “wenye upole watairithi [dunia], watajifurahisha kwa wingi wa amani.’—Zab. 37:10, 11.
Matokeo yote mabaya ya dhambi—magonjwa, kifo, na kutenganishwa na Mungu—yatakuwa mambo ya wakati uliopita. (Ufu. 21:3, 4) Mahali pake, kusudi la Mungu kuelekea dunia hii litatimizwa kabisa.—Mt. 6:9, 10.
Ndiyo, shukrani kwa dhabihu ya Yesu, kwa kuwa wanadamu wenye kuamini wana nafasi nzuri ajabu ya kutoka katika utumwa wa dhambi mwishowe. Kwa hiyo, kitia-moyo cha mtunga zaburi ni chenye kufaa kabisa: “Jiepue na uovu, utende mema, na kukaa hata milele. Kwa kuwa [Yehova] hupenda haki, wala hawaachi [washikamanifu] wake. Wao hulindwa milele.”—Zab. 37:27, 28.