Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Je! inafaa kutofautisha ufalme wa Mungu na ufalme wa Kristo? Vilevile, kwa kuwa mtume Petro anautaja “ufalme wa milele wa Bwana wetu, Mwokozi wetu Yesu Kristo,” imekuwaje kwamba utawala wa Yesu utafikia mwisho wakati ‘atakapompa Mungu aliye Baba ufalme wake’?—2 Pet. 1:11; 1 Kor. 15:24?
Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali, “Ufalme wako [wa Baba] uje.” (Mt. 6:9, 10) Kwa hiyo ufalme ni wa Mungu, lakini Yehova, akiwa ndiye “Mfalme wa milele,” amempa Mwanawe mzaliwa wa pekee madaraka ya utawala kwa kipindi chenye kikomo na kwa kusudi lililo wazi. Wakati wa kipindi hicho kilichotajwa wazi Yesu atatumikia akiwa mtawala mdogo mwenye kutumwa kutoka mkono wa kuume wa Baba yake.—1 Tim. 1:17; Zab. 110:1, 2; Dan. 4:17.
Kwa sababu ya uasi wa yule mwana wa kiroho ambaye akawa Ibilisi, na vilevile uasi wa wanadamu wa kwanza duniani, Yehova alikusudia kuwe na wonyesho mpya wa utawala wake. Wonyesho huo ungetokea kupitia ule “uzao” wa ahadi. (Mwa. 3:15; Efe. 1:8-12) Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake siku ya kufa kwake: “Nami nawawekea ninyi [“nafanya pamoja nanyi agano” la, NW] ufalme, kama vile Baba yangu alivyoniwekea mimi; mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu.” Lakini Baba ndiye angewachagua wale ambao wangetawala pamoja naye na kuwapa migawo ya vyeo katika serikali ya Ufalme huo.—Mt. 20:23; Luka 12:32; 22:29, 30; Rum. 8:16, 17.
Kwa sababu Yesu amekabidhiwa (amepewa) mamlaka hiyo ya kutawala pamoja na wale wafalme wenzake 144,000, kwa kufaa inaweza kusemwa kwamba Yesu ana ufalme, ule ufalme wa Kimasihi. Danieli aliona njozi ya kutawazwa kwa Yesu na kwa “watakatifu” hao katika vyeo vyao, kutawazwa ambako wakati huo kulikuwa bado kutimizwa, akasema: “Akamkaribia huyo mzee wa siku [Yehova], wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie, mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa. Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu.”—Dan. 7:13, 14, 27.
Mamlaka hiyo waliyopewa kisheria inafanya kazi ikiwa ndani ya ufalme wa Yehova wa ulimwengu mzima wa juu na chini au ikiwa ndani ya mpango wa kiserikali, hivi kwamba wakati Yesu aanzapo kutawala akiwa ndiye mfalme wa Kimasihi, kwa kufaa sauti za kimbinguni zinaimba kwa sauti kubwa kusema; “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake [au, yule aliyetiwa mafuta na Mungu], naye [Yehova] atamiliki hata milele na milele.” Hivyo, ufalme wa Kimasihi unatoa uwezo na mamlaka yake kwa Yehova, ambaye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote aliye juu ya uumbaji wake.—Ufu. 11:15; 4:11; Yohana 5:19, 30.
Alipofufuliwa, Yesu Kristo aliyetukuzwa alingoja akiwa kwenye mkono wa kuume wa Baba yake mpaka ufike wakati wake wa kuanza kutawala akiwa kwenye mbingu juu ya wanadamu wote kwa ujumla. (Matendo 2:32-36; Ebr. 10:12, 13) Wakati huo unalingana na wakati ambao sauti kubwa yatoka mbinguni ikitangaza kwamba: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake.” (Ufu. 12:10; linganisha 11:17, 18.) Watu 144,000 waliochaguliwa kati ya wanadamu watatawala pamoja na Yesu wakiwa warithi wenzake, na juu yao inasemwa kwamba “watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.”—Ufu, 20:6; 14:1, 3.
Mwishoni mwa utawala wake wa mileani (miaka elfu moja), wanadamu wote duniani watakaokuwa wamejipatia faida za Ufalme watasimama wakiwa wakamilifu mbele za Mungu. Watakuwa mfano wa Adamu kabla ya yeye kutenda dhambi. Kwa kuwa sasa atakuwa amemaliza kufanya mambo aliyogawiwa na Baba yake, hapo ndipo Yesu ‘atakapompa Mungu aliye Baba ufalme wake, (1 Kor. 15:24-28) Wakati huo hakutakuwa tena na ufalme msaidizi kati ya Yehova na wanadamu watiifu. Mambo yaliyopasa kutimizwa na ufalme wa Kimasihi yatakuwa yamekwisha, lakini ufalme wa Yehova utaendelea kwa umilele. Utawala wa Kristo na warithi wenzake wa ufalme “hautaangamizwa milele’’ wala “watu wengine hawataachiwa enzi yake.” (Dan. 2:44) Ile mamlaka ya pekee waliyopewa kisheria itachukuliwa tena na Yehova. “Ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika yote [awe mambo yote kwa kila mtu, NW].”—1 Kor. 15:28.
Faida za Ufalme huo wenye kusimamiwa na Kristo zitakuwa ‘za milele,’ ingawa kwa kweli zitakuwa zimekuwa “zenye kudumu kwa kizazi” fulani tu, katika maana moja ya neno ai·oʹni·os la Kigiriki lililotumiwa kwenye 2 Petro 1:11. Kwa kulinganisha utawala wake na tawala nyingine, utawala wake wa miaka 1,000 ni wa milele. Tofauti na urefu wa utawala wa mfalme ye yote wa kibinadamu ambaye amepata kutawala duniani, ufalme wa Yesu juu ya Wanadamu utaendelea kwa muda wa karne nyingi. Utawala wake utaendelea kwa muda ulio mrefu kuliko urefu wa umri wa mwanadamu aliyeishi maisha na nyingi zaidi ya watu wote katika historia ya kibinadamu, yaani, Methusela, aliyeishi miaka mileani moja kasoro (kupungua) miaka 31. (Mwa. 5:27) Zaidi ya hilo, bado Yesu atakuwa na heshima ya kuitwa mfalme, kwa maana cheo chake cha kuwa mfalme hakitakwisha kwa sababu tu atakuwa amemrudishia Baba yake ule ufalme wa Kimasihi. Sikuzote yeye atapendezwa na wanadamu, kwa maana alipokuwa Stadi wa Kazi wa Yehova anatajwa kwamba alisema: “Furaha yangu ilikuwa pamoja na wanadamu.” (Mit. 8:31) Nayo mioyo ya wanadamu itamchangamkia kwa njia ya pekee wakipendezwa sana naye kwa sababu ya mambo yote aliyowafanyia. Jambo hilo linalingana na yanayosemwa na Waebrania 7:17 kwamba Yesu atakuwa “kuhani milele.”
Biblia haitaji hasa ni kazi gani ambazo Yesu na watawala wenzake watagawiwa baada ya utawala wa mileani. Inaposimulia hali za Yerusalemu Mpya ulio mfano wa mji katika mbingu, Ufunuo 22:5 unawataja wale ambao ‘watatawala hata milele na milele,” kwa wazi ukiwamaanisha watawala wenzi wa Yesu, wale 144,000 wanaokuwa bibi-arusi wake. Sisi tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba Yehova amewawekea akibani mapendeleo na nafasi nyingi nzuri za kutimiza migawo ya utumishi katika uumbaji wake wote.