Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 11/15 kur. 6-12
  • Imani Inafaa!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Imani Inafaa!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WENGI WALIPOTEZA IMANI
  • IMANI KATI YA WANAWAKE
  • CHINI YA WAKUU WAWILI WENYE KUTUMIA UKATILI
  • Kuendeleza Imani Pamoja na Mume Wangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Chuki Yangu Iligeuka Kuwa Upendo
    Amkeni!—1995
  • Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 11/15 kur. 6-12

Imani Inafaa!

Ushuhuda Kutoka Kambi za Mateso

KAMBI za mateso​—Unakumbuka nini juu yazo?

Huenda ukakumbuka picha za watu wenye kuogopa wakitolewa kwenye motokaa zilizofunikwa kila mahali wakiongozwa waende wakafe. Au, wafungwa wenye kufanyishwa kazi kupita kiasi, na wenye kufa njaa wakilazimishwa waishi pamoja na mavi yao na mateso yao yenye kutokana na maradhi. Au, huenda ikawa ni majaribio ya kitiba ya ukatili au meko yaliyochoma miili ya kibinadamu isiyohesabika.

Mambo hayo ni sehemu ya matukio katika kambi hizo zilizo mbovu sana.

Hata hivyo kuna jambo jingine la kuchunguza. Ingawa kambi hizo za Nazi zilikuwa mbaya sana, mamia ya maelfu ya wanawake walikuwa wanajaribu kuishi. Walikuwa wanang’ang’ana siku baada ya siku waendelee kuishi yajapokuwapo magonjwa, kupigwa, kuishiwa nguvu na kuuawa ovyo ovyo. Walijaribu kula, kujipasha joto na kuepuka maradhi. Walilazimika kufanya kazi, kulala na kushughulika na wale waliokuwa kando yao.

Hivyo, yajapokuwapo mateso yao​—au kwa sababu yayo—kambi za mateso za Nazi ni mahali tunapopaswa kuangalia tuone namna imani inavyofaa. Ingawa huenda sisi binafsi tusiishi katika kambi za namna hiyo, twaweza kujifaidi na masomo yanayohusiana nazo.

WENGI WALIPOTEZA IMANI

Jambo moja lenye kutokeza sana la kambi hizo lilikuwa kupoteza imani. Mwandikaji Philip Yancy anaeleza hivi: “Waokokaji wengine waliacha kumwamini Mungu. Sana-sana, ilikuwa hivyo kwa Wayahudi: ambao walilelewa wakisadiki kwamba wao ni watu wateule, ghafula wakagundua kwamba, kama Myahudi mmoja alivyosema kwa uchungu, ‘Hitler peke yake ndiye aliyetimiza ahadi zake.’”

Elie Wiesel anaeleza matokeo ya kuona kivulana akinyongwa. Askari wa SS walikusanya wafungwa mbele ya jukwaa la kunyongea watu. Kivulana huyo alipokuwa akifa polepole, mfungwa mmoja akalia hivi, “Mungu yu wapi sasa?” Wiesel anasema hivi, “Nami nikasikia sauti ndani yangu ikimjibu ‘Wauliza Yu wapi? Yu hapa—Yeye ananing’inia hapa juu ya jukwaa la kunyongea. . . . ’”

Vilevile wengi waliodai kuwa Wakristo walipoteza imani yao. Katika kitabu The Christian Century, Harry J. Cargas alisema kwa maneno haya namna wengi waliokuwa waenda-kanisani hapo kwanza walivyoona: “Kulingana na maoni yangu, mauaji hayo makubwa ndio msiba mkuu zaidi kwa Wakristo tangu kutundikwa [kwa Yesu]. Kwa pindi ya kwanza, Yesu alikufa; katika pindi iliyofuata, twaweza kusema Ukristo ulikufa. . . . Je! mtu anaweza kuwa Mkristo leo, zikiwapo kambi hizo za kifo, ambazo kwa sehemu kubwa, zilikusudiwa, zikajengwa na zikaendeshwa na watu waliojiita Wakristo . . . ?”

Hata hivyo, kulikuwako kikundi ambacho imani yacho haikuharibiwa. Mashahidi wa Yehova walifahamu kutoka katika Biblia kwamba Mungu hakuwa akitokeza maovu ya kambi hizo wala mateso ambayo yamewapata wanadamu kwa miaka mingi. Tofauti yake, mambo hayo yanamhuzunisha Yeye nayo yanathibitisha kwamba wanadamu hawawezi kuongoza hatua zao bila kumtegemea yeye. (Yer. 10:23; Mhu. 8:9) Yeye ameahidi katika Neno lake kwamba katika wakati alioweka ataondoa uovu duniani. Vilevile ataondoa umizo ambalo limepata wale wenye imani, hata ataweza kuwafufua waishi tena.—Ufu. 21:4; tazama pia sura “Uovu—Sababu Gani Mungu Ameruhusu?” katika kitabu Happines​—How to Find it.a

IMANI KATI YA WANAWAKE

Kwa mfano, ebu tuchunguze matokeo ya kambi za mateso juu ya wanawake.

Katika kitabu cha maisha yake kiitwacho Commandant of Auschwitz, Rudolf Hoess anasema hivi: “Kambi ya wanawake, ikiwa imesongamana tangu mwanzo kabisa, ilikuwa inamaanisha kuharibiwa akili kwa wafungwa wengi wanawake, nalo jambo hilo liliwafanya wapate umizo la mwili upesi au baadaye. Kulingana na maoni yote, na nyakati zote, hali mbaya zaidi zilikuwa katika kambi ya wanawake.”

Bila shaka, hali zilitofautiana kidogo katika kambi moja na nyingine na zilitofautiana nyakati mbalimbali wakati wa vita kuu. Hata hivyo Hoess alisema hivi: “Wanawake walipofika mwisho wa kuvumilia, walijiacha washindwe kabisa. Walikuwa wakijilikokota kama mazimwi, . . . mpaka siku ifike walipokufa kwa utulivu.” Jambo mojalapo lililotokeza mambo hayo ni mwenendo wa wafungwa wengine waliopewa mamlaka. Kulingana na Hoess, “walikuwa wamewapita sana wanaume waliokuwa na cheo kimoja nao kwa ukali, ukaidi, kulipiza kisasi, na kwa ufisadi.”

Walakini Hoess anaongeza hivi: “Tofauti yenye kupendeza ilikuwa Mashahidi wa Yehova wanawake, ambao walikuwa wamepewa jina ‘nyuki wa Biblia’ au ‘funza walaji wa Biblia.’ Kwa kusikitisha walikuwa wachache sana.”

Mashahidi wa Yehova hao waliokuwa wanawake walivumilia jinsi gani yajapokuwapo maovu ya kambi za mateso za Nazi? Imani yao ilipatwa na nini? Habari yenye kutoka moja kwa moja kwa mtu aliyeshuhudia matukio ya huko ilichapishwa katika kitabu Under Two Dictators (Chini ya Wakuu Wakatili Wawili) (1949), cha Margarete Buber.

Yeye na mume wake walikuwa washiriki maarufu wa chama cha Kikomunisti cha Ujeremani katika miaka ya mapema ya kuanza na wa 1930. Baada ya kuamriwa waende Moscow, walikamatwa kwa ajili ya “usaliti wa kisiasa.” Ingawa alikuwa angali anasadiki wazo la Ukomunisti, Margarete Buber alipelekwa kwenye kambi moja ya Siberia. Baadaye aliwekwa katika mikono ya Wanazi na kwa miaka mitano akatumika katika kambi ya mateso ya wanawake yenye kujulikana sana ya Ravensbrueck.

Katika sehemu ya wakati huo, yeye alikuwa Mkuu wa Jengo, yaani, mfungwa anayekuwa na mamlaka juu ya jengo au nyumba za wafungwa wengine. Wengi wa wale waliokuwa katika jengo lake walikuwa Mashahidi wa Yehova (Wanafunzi wa Biblia). Masimulizi ya Margarete Buber ni habari ya mfungwa wa kisiasa aliyeshuhudia matukio hayo ambaye hakuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Masimulizi yake yanathibitishwa na Gertrude Poetzinger, mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye alikuwa mfungwa katika Ravensbrueck kwa miaka zaidi ya minne na ambaye leo anatumika pamoja na mumewe kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York. Vifuatavyo ni visehemu vilivyofupishwa vya kitabu hicho, kulingana na maneno ya Margarete Buber mwenyewe, navyo vimetumiwa kwa ruhusu yake.

CHINI YA WAKUU WAWILI WENYE KUTUMIA UKATILI

Kila mwanamke mpya anayekuja katika kambi ya mateso anapitia kipindi kibaya sana ambacho katika hicho anatetemeshwa kabisa, hata awe ni mwenye mwili wenye nguvu kama nini, hata awe ni thabiti kama nini. Nayo mateso ya wapya waliokuja yalipata kuwa mabaya zaidi na zaidi kila mwaka katika Ravensbrueck, na hivyo hesabu ya vifo ilikuwa juu zaidi kati yao. Kwa kulingana na utu wa mtu, ingechukua juma nyingi, miezi mingi, au hata miaka mingi, kabla ya mfungwa kukubali hali iliyompata na kukubali yumo katika kambi ya namna hiyo. Ni wakati wa kipindi hicho utu wa mtu unapobadilika. Polepole kupendezwa na ulimwengu ulio nje [ya kambi] na wafungwa wengine kunapunguka.

Nadhani hakuna kitu chenye kukosesha adili kama mateso, kuteseka sana pamoja na kushushiwa heshima wanakopatwa nako wanaume na wanawake katika kambi za mateso. [Askari wa] SS walipokupiga, hungethubutu kujipigia. [Askari wa] SS walipokuchokoza na kukutusi, ulipaswa kunyamaza kimya wala usiwajibu. Ulikuwa huna haki zo zote za kibinadamu—bila zote kabisa. Ulikuwa mwanadamu tu mwenye kuishi mwenye namba ya kukutofautisha na wengine kando yako wenye hali mbaya hiyo.

Hapa sisemi juu ya wafungwa wale waliokuwa na vyeo fulani na ambao waliweza kuwatenda vibaya wale waliokuwa chini ya usimamizi wao. Ninamaanisha wanawake wafungwa wa kawaida tu. Ikiwa mmoja alipata chakula kingi zaidi kidogo, kipande cha mkate kikubwa zaidi kidogo, kipande kikubwa zaidi kidogo cha siagi au nyama ya sausage, mara moja zilitokea tamasha za hasira na chuki.

Tangu wakati tulipotoka vitandani mwetu mpaka wakati tulipojipanga kwenye mstari nje ili tuitwe majina zilikuwa dakika arobaini na tano za kunawa, kuvaa nguo, kupanga kabati ndogo na kula “kiamsha-kinywa” chetu. Hilo halingekuwa jambo rahisi hata hali zikiwa nzuri kabisa, basi waza namna ilivyokuwa katika kanyumba kenye wanawake wengine 100 wote wakifanya harara wakiwa na kusudi la kufanya jambo ilo hilo! Hali ilikuwa imejaa matukano na matusi.

[Hiyo ni sehemu ya masimulizi ya namna maisha yake yalivyokuwa katika Ravensbrueck. Walakini ndipo mwandikaji huyo alipowekwa awe Mkuu wa Jengo katika Jengo 3, ambamo ndani yake walikaa Wanafunzi wa Biblia.]

Nilianza kazi yangu alasiri hiyo kwenye Jengo 3. Hapa hali ilikuwa tofauti kabisa. Mahali hapo palikuwa pamenyamaa napo palinukia unga-unga wa kusafishia, dawa za kuua viini na mchuzi wa kabichi (cabbage). Wanawake mia mbili na sabini waliketi kuzizunguka meza. Mara tu nilipoingia chumbani humo, mwanamke mmoja mrefu, mwenye nywele ya rangi nyeupe-nyeupe akasimama, akaniketisha naye akanipa bilauri lenye mchuzi wa kabichi. Sikujua la kufanya kabisa.

Ko kote nilikotazama kuzunguka meza hiyo nyuso zile zile zenye kutabasamu kwa kiasi zilikuwako. Nywele za wote zilikuwa zimefungamanishwa nyuma na kuwa kifundo, nao waliketi chini kwa utaratibu mzuri kabisa na kula chakula chao kama kwamba wote walikuwa kitu kile kile kimoja. Wengi wao walionekana kuwa wanawake wa mashambani, nazo nyuso zao nyembamba zilikuwa zenye rangi ya kahawa na zenye makunyanzi kwa sababu ya jua na upepo. Wanawake wengi kati ya hawa walikuwa wamekuwa kifungoni na kwenye kambi za mateso kwa miaka mingi.

Kulikuwako wafungwa 275—wote Wanafunzi wa Biblia. Wote walikuwa wafungwa wenye mfano mzuri na wote walikuwa wanajua kabisa amri na maagizo ya kambi hiyo na walizitii kabisa kabisa. Kabati zile ndogo zilifanana, na zote zilikuwa mfano mzuri wa kuwa safi na nadhifu. Taulo zote zilikuwa zinaning’inia kwenye milango ya kabati hizo ndogo kwa mtindo ule ule ulioagizwa; kila bilauri, sahani, kikombe, na kadhalika, vyote vilikuwa safi na vilipigwa sulu na kung’aa kabisa. Vibago (viti) vilikuwa vimesuguliwa na kuwa safi kabisa na sikuzote visipotumiwa vilikuwa vimewekwa vikiwa nadhifu mahali pamoja. Vumbi lilitolewa kila mahali, hata kutoka kwa mbao zilizopita juu ya kanyumba hako, kwa maana kanyumba ketu hakakuwa na kifuniko cha upande wa chini cha dari na tulikuwa tunaliona paa lenyewe. Niliambiwa kwamba baadhi ya wasimamizi wa SS walizunguka-zunguka wakiwa wamevaa glovu nyeupe (vifuko vya mikononi), na kupitisha vidole vyao ju ya mbao zilizoungwa ukutani na juu ya vikabati na hata kupanda juu ya meza ili waone kama mbao zilizopita juu ya [kanyumba hako] zilikuwa bila vumbi.

Vyoo na vyumba vya kunawa vilikuwa safi vivyo hivyo. Walakini zilizokuwa nadhifu na safi zaidi ni zile bweni, kila moja ikiwa na vitanda 140. Vitanda vilivyotengenezwa hapa vilikuwa tukio lenye kustaajabisha. Magunia na mito ya nyasi ilikuwa kama visanduku. Blanketi zote zilikunjwa kwa uangalifu na kwa njia ile ile na ukubwa ule ule, na zote ziliwekwa juu ya kitanda kwa njia ile ile. Juu ya kila kitanda palikuwa karatasi yenye majina na namba za wafungwa waliolala juu yacho, na juu ya mlango palikuwa ramani iliyochorwa kwa uangalifu ya bweni hiyo yenye kuonyesha kila kitanda na ni nani hasa aliyelala juu yacho, ili kwamba ye yote mwenye kukagua aweze kujua mara moja mahali kila mtu alipokuwa.

Nilipokuwa Mkuu wa Kanyumba kati ya Wakatili,b siku nzima ilikuwa ya kazi fulani-fulani nami niliona mambo mbalimbali yenye kuniogopesha-ogopesha. Nikiwa na Wanafunzi wa Biblia maisha yangu yalikuwa mepesi sana. Kila kitu kilitendeka kwa utaratibu. Asubuhi, wakati kila mtu alipokuwa na kusudi la kumaliza kazi zake kabla ya kuitwa majina, hakuna mtu aliyesema neno lo lote kwa sauti kubwa. Katika majengo mengine Wakuu wa jengo na Wakuu wa Kanyumba walilazimika kupiga kelele ndipo waliokuwa chini ya usimamizi wao watoke nje na kupanga mstari, walakini hapa utaratibu wote ulifanywa kwa unyamavu na bila mimi kusema lo lote, na ndivyo ilivyokuwa kwa mambo mengine yote—ugawaji wa chakula, kuzimwa kwa taa, na sehemu nyingine ya siku nzima ya wafungwa hao.

Kazi yangu kubwa nikiwa na Wanafunzi wa Biblia ilikuwa kufanya maisha yao yawe rahisi kwa kadiri ilivyowezekana, kuzuia hila za Kiongozi wa Jengo wa SS.

Hakuna cho chote kilichopata kuibwa katika Jengo 3. Hakukuwako kusema uongo wala kutoa hadithi za uongo. Kila mwanamke alikuwa mwaminifu sana, pia alijiona kuwa mwenye daraka la kufanya kikundi chote kiwe chenye hali njema. Baada ya mimi kuwa hapo muda mfupi wakajua kwamba nilikuwa rafiki yao.

Mara tu uhusiano huo ulipokwisha kuimarishwa nami nikawa na uhakika kwamba hakuna ye yote wao angenisaliti, kulikuwako mambo mengi ambayo ningeweza kuwafanyia; kwa mfano, nilizuia wazee-wazee na walio dhaifu mwili wasisimame saa nyingi wakati wa kuitwa majina kwa kutoa visababu vya namna zote na ujanja wote. Nisingeweza kufanya hivyo nikiwa na Wakatili, maana wale ambao wangeweza kuvumilia zaidi mkazo huo wangenisaliti kwa [askari wa] SS kwa sababu ya kuchukizwa na wazo la kwamba mtu mwingine alikuwa anapendelewa.

Wanafunzi wa Biblia tu ndio waliokuwa watu wenye umoja wenye kuishi katika jengo moja kati ya wafungwa katika Ravensbrueck. Nilipokwenda kwenye Jengo 3 nilikuwa na wazo dogo tu juu ya masadikisho yao ya kidini na sababu gani Hitler hakuwapenda. Kutowapenda ni neno lisilo na uzito wa kusimulia maoni yake kuwaelekea; alitangaza kuwa wao ni adui wa Serikali naye akawatesa kikatili.

Baada ya muda mfupi wakajua kwamba ni vigumu kwangu kuwa mfuasi, walakini wakaendelea kunihurumia nao hawakuacha kutumaini kwamba siku moja huenda “nikaona nuru.” Kwa kadiri nilivyojua wao waliamini kwamba wanadamu wote, isipokuwa Mashahidi wa Yehova, karibuni wangetupwa kwenye giza la milele wakati ulimwengu ungefikia mwisho wake. Wema ungeshinda Uovu. Taifa halingeinua upanga juu ya taifa jingine, chui angelala pamoja na mwana-mbuzi; na ndama na mwana-simba na kinono wangelala pamoja, na hakuna mtu ye yote angedhuru wala kuharibu kitu katika mlima mtakatifu Wake wote. Wala hakungekuwako kufa tena na kila mtu, yaani, waokokaji, angeishi kwa furaha milele baada ya hapo na uradhi wao haungekuwako na mwisho.

Sadikisho hilo jepesi na lenye kuridhisha liliwapa nguvu na likawawezesha kuvumilia miaka mingi ya maisha ya kambi ya mateso na ya kuvunjiwa heshima na kudharauliwa na bado wakaendelea kujiheshimu kama wanadamu. Walikuwa na jambo la kuthibitisha, nao walilithibitisha, kwamba kifo hakikuwatisha. Wangeweza kufa kwa ajili ya masadikisho yao bila kuacha.

Waliichukua Amri ya Sita kwa uzito na hivyo walikuwa wameazimia kupinga vita vyote na utumishi wote wa kijeshi. Kushikamana na jambo hilo kulipotezea Mashahidi wengi wanaume maisha zao. Wanawake wa madhehebu hiyo vilevile walikataa kufanya kazi yo yote ambayo kulingana na maoni yao ilikusudiwa kuendeleza jitihada ya vita.

Hali yao ya kuona wajibu wao na daraka lao isingeweza kutikiswa; walikuwa watenda kazi wenye bidii, wanyofu na watiifu. Twaweza kusema Mashahidi walikuwa “wafungwa kwa hiari,” maana jambo peke yalo walilopaswa kufanya ili waachiliwe mara moja ni kutia sahihi karatasi ya pekee ya Wanafunzi wa Biblia iliyosema hivi: “Natangaza hapa kwamba tangu leo na kuendelea sijioni mwenyewe kuwa Mwanafunzi wa Biblia na kwamba sitafanya jambo lo lote lenye kuendeleza faida za Shirika la Mataifa Yote la Wanafunzi wa Biblia.”

Kabla sijawa Mkuu wa Jengo lao, waliteseka sana kwa sababu Kaethe Knoll [Mkuu wa Jengo aliyetangulia ambaye alikuwa mbaya sana] alifanya yote aliyoweza ili awazuie wasishiriki katika mazungumzo yao ya kidini wao kwa wao. Kuwazuia wasiseme juu ya hayo yote na wasilinganishe maandishi yao, yaani, kwa ufupi “kujifunza Biblia,” kulikuwa namna ya mateso ya kuumiza pole-pole, naye Kaethe Knoll alikuwa amefanya hivyo kwa bidii yenye chuki.

Nilikuwa nimekuwa Mkuu wa Jengo lao kwa muda fulani kabla sijagundua kwamba “Funza Walaji wa Biblia” niliokuwa nikitunza, kama walivyoitwa kambini, walikuwa na Biblia na vitabu vya Wanafunzi wa Biblia. Wakaanza kuviingiza, vikiwa vimefichwa ndani ya ndoo na vitambaa vya kusafisha sakafu, na kadhalika, walipotoka kazini. Nilipogundua hivyo nikapendekeza kwamba ingepunguza hatari kama wangevificha mahali fulani katika jengo, nalo pendekezo hilo likafuatwa kwa shauku. Baada ya hapo funzo la Biblia lilifanywa waziwazi katika jengo nyakati za jioni na siku ya Jumapili. Na wakiwa vitandani usiku, kabla wanawake wa SS hawajafika pamoja na mbwa zao, waliimba kwa sauti ndogo nyimbo zao za kidini. Kazi yangu ilikuwa kuhakikisha kwamba walikuwa na onyo la kutosha juu ya hatari na nafasi ya kuficha vitabu vyao vilivyokatazwa.

Nilikuwa najihatirisha sana. Nilikuwa Mkuu wa Jengo nami nilikuwa na daraka la yote yaliyokuwa yakiendelea. Kilikuwa “Kipindi Chenye Ufanisi” cha maisha yangu katika kambi ya mateso—baada ya Har–Magedoni kwa usemi wa mfano—walakini namna nilivyoweza kuponyoka ukaguzi baada ya ukaguzi uliokuwa ukiongozwa na mkatili yule Koegel bila kupelekwa kwenye Jengo la Adhabu sijui kufika siku hii.

Lakini kulikuwako jambo hatari zaidi nililofanya. Mfungwa alipokuwa mgonjwa alipaswa kupiga ripoti kwa idara ya utibabu kupitia kwangu. Jaribu kali la jambo hilo lilikuwa kipimaji-joto la mwili. Kulingana na kilivyoonyesha, mwanamke yule mgonjwa angepelekwa kwenye chumba cha wagonjwa, na aruhusiwe kufanya “kazi ya ndani,” au apelekwe nje bila huruma akafanye kazi zake za kawaida. Basi, kati ya “Mashahidi” walikuwapo wanawake wengi wazee ambao, ingawa hawakuwa na joto jingi, walikuwa dhaifu sana hata kwamba kazi iliwaweza kabisa. Njia pekee ya kuwaepusha na kuwapa siku ya kupumzika pindi kwa pindi ilikuwa kwamba nitoe ripoti za uongo za hesabu ya vikundi, nami nilifanya hivyo. Sitaki kuwaza yalo ambayo yangalinipata kama jambo hilo lingaligunduliwa. Ilikuwa vigumu zaidi kwa kuwa sisi ndio tuliokuwa Jengo la Kukaguliwa [nyumba ambazo wakuu wa Nazi wenye kuzuru waliletwa ndani yazo. Mwandikaji huyo anasimulia ziara kama hiyo ya ghafula:]

Nilikuwa nikiripoti kwa sauti ya unyenyekevu aliostahili kuonyeshwa mkubwa:

“Mkuu wa Jengo Margarete Buber, Na. 4,208. Tafadhali sana fika kwenye Jengo Na. 3 linalokaliwa na Wanafunzi wa Biblia 275 na Wanasiasa watatu, ambao 260 kati yao wako kazini, wanane wanafanya kazi katika kanyumba na saba wana vibali vya kufanya kazi ndani.”

Koegel alikuwa akinikodolea macho yake ya samawati, na kidevu chake kilichonyolewa kabisa kilitikisika, na kisha akawa akikoroma jambo fulani. Kisha ningeendelea na ukaguzi wa kawaida, nikifungua mlango mmoja baada ya mwingine, na vikabati vitatu vya kwanza. Tulipowakaribia wafungwa waliokuwapo kama ilivyotakiwa kwa ukawaida, nilikuwa ninaamrisha “Achtung!” kisha wote wangeruka kama mpira. Wageni wote, wanaume na wanawake, SA, SS, au wengineo, sikuzote walivutiwa na vyuma vyenye kung’aa. Wakati wote Koegel ndiye aliyewauliza wafungwa maulizo. “Sababu gani ulikamatwa?” na sikuzote jibu lilikuwa: “Kwa sababu mimi ni Shahidi wa Yehova.” Hilo ndilo lililokuwa ulizo peke yake, kwa maana Koegel alijua kutokana na yaliyompata kwamba hawa Wanafunzi wa Biblia wasiobadilika wageni walikuwa wakitazama bweni, na sikuzote kulikuwako sauti za mshangao kwa ajili ya utaratibu usio na doa walioona hapo.

Ingawa Msimamizi Mkuu wa SS Frau Langefeld alipendelea na kulinda “Mashahidi,” mmoja wa waangalizi wenye kuongoza, mwanamke ambaye jina lake lilikuwa Zimmer, aliwachukia kama matapiko. Frau Zimmer hakutoshelezwa na jambo lo lote; hata kitanda kilicho mfano mzuri zaidi hakikuvutia macho yake, naye hakukosa kutumia nafasi ya kutusi na kuchokoza Mashahidi.

[Ili kuharibu amani ya Mashahidi na umoja wa Kikristo, wenye mamlaka waliweka Wakatili wapatao 100 katika jengo hilo.]

Ilikuwa kama kwamba mbwa-mwitu walikuwa wameingia ndani ya zizi hilo. Hasira, wizi na ugomvi vikawa sehemu na jambo la kukabili kila siku ya maisha yetu. Upesi Wakatili wakaanza kuwasemea vibaya “Mashahidi” kwa ajili ya mafunzo yao ya Biblia na mazungumzo ya kidini; waliiba kila kitu ambacho wangeweza kukifikia kwa mikono yao; na, wakiwa wanajiona wenyewe kuwa wawakilishi wa mamlaka, kwa ujumla wakajiendesha kwa ukali mwingi na uchokozi mwingi. Nalo hilo lilinisikitisha kama nini! Kwa kufaa “Mashahidi” wangu walinitegemeza wakati wa matatizo yangu nao wakaniunga mkono katika kila njia iliyowezekana. Shukrani ziwaendee, tuliweza kung’ang’ana tukavumilia kwa miezi sita—muda wote ambao tatizo hilo lilikuwapo—bila taabu kubwa.

Nilifanya yote niliyoweza kutenga wenye kuleta matata. Niliwaweka “Mashahidi” kwenye meza tofauti ili wazungumze mambo yao wakati wa kula bila hatari ya kukasirikiwa, na wakati wa usiku niliwaweka Wakatili katika vitanda vya juu na “Mashahidi” chini. Hata hivyo, kama ilivyopata kuwa, wenye mamlaka—hasa mwenye kutokeza mpango huo alikuwa Frau Zimmer—lazima wawe walituletea watu wote wenye kukojoa vitandani sana katika kambi hiyo, na usiku baada ya usiku kukanya mvua ya mkojo juu ya wasiokuwa na hatia katika vitanda vya chini.

Siku moja adui yetu wa zamani, Frau Zimmer, akaja kuchunguza kazi yake. Mara moja akaona nilivyotenganisha kondoo kutoka kwa mbuzi naye akanigeukia kwa hasira.

“Usifikiri mimi ni kipofu,” akasema. “Najua kabisa unakinga na kulinda waendeshaji-Biblia hapa. Usithubutu kutenganisha Funza Walaji wa Biblia na Wakatili, umesikia?”

Basi, huo ndio uliokuwa mwisho; nililazimika kuwachanganya wote na kutumainia mazuri. Ni wakati huu Yehova alipoingilia mambo. Wanafunzi wa Biblia wakawakubali Wakatili kama dada waliopotea kwa muda mrefu: Je! walikuwa na njaa? Walikuwa nayo! Je! wangetaka kipande cha ziada cha mkate? Wangetaka! Na ikaendelea hivyo. Nikatazama huruma hiyo ya Kikristo ikitenda kazi nikiwa na maoni mbalimbali, walakini ikawa na matokeo. Wakatili walilainishwa na fadhili na urafiki, na kisha shughuli fulani ikaanza kuwaonyesha nuru. Baada ya muda mfupi hesabu fulani ya Wakatili—Mgipsi mmoja, Mpolandi mmoja, Myahudi mmoja na Mwanasiasa mmoja—walikwenda kwenye afisi ya SS, wakitangaza kwamba tangu wakati huo na kuendelea walitaka waonwe kuwa Mashahidi wa Yehova na wakataka alama ya pembe tatu yenye rangi ya zambarau-samawati iwekwe juu ya nguo zao. Mambo yalipoharibika sana hivyo, [askari wa] SS waliwarukia wakisema kiwazimu na wakawatupa nje. Mwishowe SS walichoka wakahamisha Wakatili kutoka jengo letu na amani ikarudi tena, Nilishusha pumzi ya kufarijika, nao “Mashahidi” wakafanya mkutano wa kutoa sala ili kumrudishia Yehova shukrani.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. (1980)

b Wakatili walikuwa malaya, watanga-tanga, wevi wa mifukoni, walewaji na wengine “wasiotulia.”

[Picha katika ukurasa wa 8]

Gertrude Poetzinger mwaka 1944. Alikuwa kati Mashahidi wa Yehova 275 waliofungwa Ravensbrueck.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Gertrude Poetzinger leo. Anatumika kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki