Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 12/1 kur. 7-12
  • Mwache Mungu Awe Katika Ndoa Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mwache Mungu Awe Katika Ndoa Yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KIPAWA CHENYE NEEMA CHA NDOA
  • KUMWACHA MUNGU AWE KATIKA NDOA YAKO
  • TAKWA LA FADHILI
  • KUONYESHANA UNYOFU
  • UPENDO USIO NA UCHOYO—“A.GA’PE”
  • Dumisha “Kamba Yenye Nyuzi Tatu” Katika Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Jinsi ya Kufanikiwa Katika Ndoa ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Jenga Ndoa Imara na Yenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 12/1 kur. 7-12

Mwache Mungu Awe Katika Ndoa Yako

“Kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi [haiwezi kuraruliwa vipande viwili kwa haraka, NW].”

1. Ni kanuni gani ya Maandiko inayotajwa kwenye Zaburi 127:1 inayoweza kutumika kuhusu ndoa?

UHITAJI wa Yehova Mungu wa kuwa katika kila shughuli yetu unakaziwa tena na tena katika Maandiko. Hivyo tunasoma hivi kwenye Zaburi 127:1: “[Yehova] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure. [Yehova] asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure.” Historia ndefu ya taifa la Israeli inaonyesha wazi kweli ya kanuni hiyo. Wakati Israeli walipomwacha Mungu awe katika mambo yao kwa kumpa ibada ya pekee, jitihada zao za kujilinda zilifanikiwa. Lakini wakati walipoiacha ibada safi yake wafuate miungu mingine, walinzi wao walilinda miji yao bure tu. Kanuni iyo hiyo inahusu kufanya ndoa ifanikiwe.

KIPAWA CHENYE NEEMA CHA NDOA

2. Kwa sababu gani ndoa inaweza kuonwa kuwa kipawa chenye neema?

2 Neno la Mungu linatuambia kwamba yeye ndiye Mpaji wa “kila kipawa chema na kila zawadi kamilifu.” (Yak. 1:17, NW) Kati ya vipawa hivyo vyema na zawadi kamilifu lazima kile kipawa cha ndoa, chenye neema na baraka, kitiwe ndani. Loo! jinsi kinavyoweza kuleta sana furaha! Kwa kweli hiyo ni moja ya baraka zilizo kubwa zaidi ambazo Muumba amewapa wanadamu. Si ajabu kwamba wakati mwishowe Hawa alipopokezwa kwa Adamu, Adamu alishangilia akisema: “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume”!—Mwa. 2:23.

3. Mwanasheria mmoja alisema nini juu ya kipawa cha Mungu cha ndoa?

3 Adamu angeweza kuifurahia baraka ya kuwa na mwenzi mwenye upendo, mtu wa aina yake mwenyewe ambaye angeweza kuzungumza, kufanya kazi, kupanga mambo naye—mwanamke huyo akawa kikamilishaji chake kitimilifu! Isitoshe, furaha zinazotokea kati ya mume na mke katika ndoa kweli zinashuhudia hekima na upendo wa Muumba wetu. Kwa uzuri mwanasheria I. Linton aliionyesha njia ambayo Mungu alitumia kuumba mwanamume na mwanamke kama uhakikisho wa kwamba mwanadamu hakutokea kwa mageuzi yenye kujitokeza yenyewe. Linton aliandika hivi:

“Zile fadhili na ufundi usio na mipaka wa Mungu aliyetangaza haikuwa vema mwanamume awe mseja, kwa kuingiza ndani ya moyo wa mwanamume upendo wa mwanamke na ndani ya moyo wa mwanamke upendo wa mwanamume, kwa kuwafanya kiakili, kimwili na kimoyoni wafanane sana ili waweze kuwa wenzi lakini wakiwa tofauti sana katika umbo lao ili wakamilishane na kuvutiana kwa mapenzi, zimechochea shukrani zangu na kunifanya nipendezwe sana na jambo hilo kama ushuhuda hakika wa ubuni malidadi wa uumbaji; tena ile amani na furaha inayositawi kutokana na uhusiano wa ndoa wakati Mungu yumo katika ndoa hiyo umeonyesha wazo fulani la uwezo wa ufundi wa Mungu wa kutokeza furaha.” (Kitabu cha Kiingereza kiitwacho Mwanasheria Aichunguza Biblia) Uangalie usemi huo, “wakati Mungu yumo katika ndoa hiyo.” Hiyo inaweza kuwa kweli tukimwacha Mungu awe katika ndoa yetu.

4. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba baraka ya ndoa ni ushuhuda unaoonyesha Mungu hana upendeleo?

4 Kipawa hicho na baraka ya ndoa ni ushuhuda pia wa kwamba Mungu hana upendeleo na anafanya hukumu za haki. Namna gani? Kwa sababu furaha hizi za ndoa, wakati Mungu anapokuwa katika ndoa hiyo, hazitegemei vitu vya kimwili kama vile utajiri, elimu ya juu, nguvu nyingi za kimwili wala urembo wa umbo la mwili na sura. Wala baraka za ndoa hazipatikani na mbari moja tu ya watu au taifa fulani, wala hazitegemei majira yo yote ya hali ya hewa. Si kitu hata watu wawili waliooana wawe wanaishi huko juu sana au chini sana kwenye ncha za dunia zilizo na baridi nyingi, au katika yale maeneo ya kati ya dunia yenye hali za joto la kadiri.

KUMWACHA MUNGU AWE KATIKA NDOA YAKO

5, 6. Ni mambo gani yanayotiwa ndani ya kumwacha Mungu awe katika ndoa ya mtu?

5 Solomoni aliandika hivi: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja; maana wapata ijara njema kwa kazi yao. . . . wala kamba ya nyuzi tatu haikatiki upesi.” (Mhu. 4:9, 12) Ndoa inaweza kufananishwa na kamba yenye kufunganisha watu wawili pamoja na, wakati sisi tunapomwacha Mungu awe katika ndoa hiyo, kwa kweli inakuwa ‘kamba ya nyuzi tatu isiyokatika upesi.’ Maana yake nini kumwacha Mungu awe katika ndoa yako? Ni wazi kwamba wenzi wa ndoa wanahangaikia kushiriki kufurahishana na kupeana raha, kutoshelezana mahitaji yao. Mume anahangaikia kumpendeza mkewe na kumfurahisha, kumpa starehe na usalama, naye mke anahangaikia kuhudumia mahitaji ya mumewe na kumpendeza sana kadiri awezavyo, kama vile mtume Paulo anavyoandika. (1 Kor. 7:33, 34) Kumwacha Mungu awe katika ndoa yako kunamaanisha kuhangaikia kutimiza matakwa yake kwa watu waliooana. Kusema kwa ufupi, matakwa hayo ni haya: “Ninyi wake, watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana. Ninyi waume, wapendeni wake zenu msiwe na uchungu nao.”​—Kol. 3:18, 19.

6 Zaidi ya hilo, kumwacha Mungu awe katika ndoa yetu kunamaanisha wenzi wote wawili wawe na uhusiano mchangamfu pamoja na Yehova Mungu, wasiachilie kamwe kusali pamoja. Shirikini naye furaha zenu, huzuni zenu, mambo yenu yenye kuwakatisha tamaa, majaribu yenu. Iweni na hangaiko la kumpa yeye kama Mtu furaha na raha ya moyoni. Kwenye Zaburi 147:11, ZSB, tunasoma hivi: “[Yehova] anapendezwa nao wanaomwogopa.” Naye Mungu anatuambia kwenye Mithali 27:11 kwamba kwa kuwa wenye hekima tunaweza kuufurahisha moyo wake. Kwa hiyo inatupasa tuhangaike, si kutimiza matakwa yake kwetu tu, bali pia tuhangaike tukifikiria jinsi yeye anavyojisikia kwa sababu ya njia yetu ya kuyatii matakwa hayo. Kumwacha Mungu awe katika ndoa yetu kutaitia nguvu ajabu na kutuhakikishia fanaka na furaha. Naam, hapo ndipo ndoa inapokuwa ‘kamba ya nyuzi tatu isiyokatika upesi.’​—Mhu. 4:12.

TAKWA LA FADHILI

7. Kwa sababu gani fadhili zinatakiwa ili tumwache Mungu awe katika ndoa yetu?

7 Kati ya mambo ambayo Mungu anataka viumbe vyote vya kidunia alivyoviumba viwe nalo, na ambalo lina maana ya pekee kwa wenzi wa ndoa, ni kwamba waonyeshane fadhili. Yehova Mungu mwenyewe hutuwekea sisi mfano, kama vile Neno lake linavyotuhakikishia kwamba “yeye ni mwenye fadhili [hata] kuelekea wasio na asante na waovu.” (Luka 6:35, NW) Kwa kweli, zaidi ya mara mia moja tunasoma katika Neno lake juu ya “fadhili zisizostahilika” zake (au neema, UV), na karibu mara mbili za hesabu hiyo juu ya “fadhili za upendo” wake. Ili tuwe na Mungu huyo mwenye fadhili katika ndoa yetu lazima tulitii shauri lililo kwenye Wakolosai 3:12: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.”

8. Ni nini moja ya njia zilizo rahisi zaidi na kubwa zaidi ambayo katika hiyo wenzi wa ndoa wanaweza kuonyeshana fadhili?

8 Tunaweza kuwaonyeshaje wenzi wetu wa ndoa fadhili na kwa njia hiyo tumwache Mungu awe katika ndoa yetu? Kuwa wenye fadhili kunamaanisha kuhudumia mahitaji ya mtu mwingine. Kunamaanisha tuwe watu wenye kuwaza, kila mmoja akifikiria kutaka mwenzake awe na hali njema. Kwa kuwa ni kawaida kutokutaka kuwa peke yetu, moja ya njia zilizo kubwa zaidi na rahisi zaidi za sisi tuliooana kufadhiliana ni kushirikiana kwa kuwa pamoja, kushirikiana urafiki wetu. Kwa kuwa pamoja tu, tunaweza kujengana, kumfanya kila mmoja ajisikie anahitajiwa na kuthaminiwa. Katika ndoa moja iliyovunjika baada ya miaka mingi mke alikuwa na maelekeo ya kawaida ya kuchukua malikizo marefu-marefu akiwa mbali na mumewe.

9, 10. (a) Ni kati ya mambo gani ambayo inawapasa waume na wake Wakristo watake kufanya pamoja? (b) Ni katika njia gani nyingine wenzi wa ndoa wanaweza kuonyeshana fadhili?

9 Kuwa pamoja tu kwenyewe ni kuzuri, lakini ni vizuri hata zaidi kufanya pamoja mambo mengi kadiri iwezekanavyo. Je! wewe hujisomea Biblia binafsi? Mbona usiisome kwa sauti ili muhebi wako asikie? Je! unajitayarishia mikutano ya Kikristo? Kwa kadiri ifaavyo, mbona msitayarishe masomo ya mikutano hiyo pamoja? Je! ewe mume, unakuwa na sehemu katika programu? Mbona usijizoeze mapema sehemu hiyo kwa sauti ukimfanya mkeo awe ndiye wasikilizaji wako? Ketini pamoja kwenye mikutano, na vilevile nyakati nyinginezo. Shirikini pamoja katika kazi ya Kikristo ya kuhubiri iliyopangwa kwa njia rasmi. Zote hizi ni njia za ziada ambazo katika hizo tunaweza kuonyesha fadhili, tuitie nguvu ndoa yetu na kumwacha Mungu awe katika ndoa yetu.

10 Vilevile ni jambo la fadhili wenzi wa ndoa wakisemezana, wakiacha kila mmoja wao ajue yaliyo katika moyo na akili ya mwenzake. Ah-ah, hiyo haimaanishi kupeana tu habari au mawazo bali pia kujisikia kama yule mwingine anavyojisikia kuhusu mambo. Fikirieni kutaja mambo ya kujengana katika mazungumzo yenu, kupatana na ile mithali inayosema: “Ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mit. 12:18) Si kwamba tu watu wawili waliooana ni mwili mmoja, bali pia wanapaswa kuwa wenye akili moja na moyo mmoja, sawa na vile Yesu alivyosali kwamba wafuasi wake wawe mtu mmoja. (Yohana 17:21) Ili umoja huo uwepo lazima kabisa kuwe na kupashana habari.

11. Inawapasa watu waliooana wafuate mashauri gani mazuri ya Maandiko kunapokuwa na hali za kuudhiana?

11 Hasa ni fadhili kurudia kuzungumza mambo wakati ambao kumekuwa hali za kutoelewana au kuudhiana. Yesu alitaja kanuni fulani inayohusu uhusiano wa kibinadamu ambayo mara nyingi watu waliooana husahau au huiachilia mbali kisha wanaumia. Je! wewe unajisikia kwamba umetendwa kwa njia isiyo na fadhili au ukakosewa kwa njia fulani? Basi kwa kuifuata roho ya Mathayo 18:15 uchochee ushujaa wako uweze kulitaja jambo lenyewe wakati ufaao, ukifanya hivyo kwa fadhili na busara. Unaweza hata kujifunza somo fulani kutokana na Malkia Esta, aliyetumia busara kumfanya mumewe awe tayari akilini kufikiria jambo zito kabla hajamweleza jambo lenyewe. (Esta 5:1-8; 7:1-10) Au, tukitumia usemi wa mfano wa Kiingereza, je! kiatu chenyewe kimevaliwa na mguu ule mwingine, yaani, inaelekea kuwa kwamba wewe ndiwe umemkosea mpenzi wako? Basi usilipuze jambo hilo, bali kwa unyenyekevu, fadhili na busara litaje jambo hilo kupatana na roho ya Mathayo 5:23, 24. Hivyo amani, mapatano na furaha yanaweza kurudishwa.

12. Inaweza kusemwa nini juu ya uhitaji wa mwenzi mmoja wa ndoa kusikiliza wakati yule mwingine anaposema?

12 Walakini, fadhili hazihusu kusema tu, kusemezana tu, bali pia kusikiliza kwa heshima. Hiyo maana yake ni kutega sikio lako mtego wakati mwenzi wako anaposema. Imesemwa kwa kufaa kwamba kusikiliza ni ufundi. Tunapaswa tusikilize si kwa kusudi la kuielewa maana tu ya maneno yanayosemwa bali pia kuona maneno hayo yanasemwa na mtu huyo akijisikia namna gani. Zaidi ya hilo, ili tuwe wasikilizaji wazuri lazima tuangalie ni mambo gani yasiyosemwa. Naam, inawapasa waume na wake wawe wasikilizaji wazuri. Ni jambo lisilo la fadhili kusikiliza kidogo-kidogo tu wakati mwenzi wako wa ndoa anaposema nawe. Ni kweli kwamba nyakati nyingine kunaweza kuwa na tatizo dogo kwa sababu mwenye kusema huenda akawa anayasema maneno akili zikiwa mbali na maneno anayoyasema, badala ya kujaribu kweli kweli kumpasha mwenzake habari. Ikiwa hilo linaelekea kuwa tatizo, basi jizoeze tabia ya kutolea maneno yako utangulizi wenye maneno ya moja kwa moja, kama vile “Ewe kipenzi,” “John,” “Maria.”

13. Ni nini moja ya njia zilizo nzuri zaidi ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kutumia kuonyeshana fadhili?

13 Tena, moja ya njia zilizo nzuri zaidi ambazo katika hizo wenzi wa ndoa wanaweza kuonyeshana fadhili, za huyu na huyu, ni kulitii agizo la mtume: “Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi.”(Efe. 4:32) Nawe unapoonyesha ile rehema ya kusamehe usifanye hivyo kwa kunung’unika, bali “mwenye kurehemu” afanye hivyo “kwa furaha.” (Rum. 12:8) Kufanya hivyo ni kumwacha Mungu awe katika ndoa yako, kwa maana tunasoma kwamba yeye ‘husamehe kwa njia kubwa.’ (Isa. 55:7, NW) Tukimsamehe mwenzi wetu anapofanya kosa, inakuwa vyepesi kutazamia msamaha sisi wenyewe tunapofanya kosa. Haikusemwa bila sababu nzuri kwamba ‘ndoa yenye furaha ni mwungano wa wasameheaji wawili.’

KUONYESHANA UNYOFU

14. Ni sifa gani nyingine ambayo lazima Wakristo waionyeshe ili kumwacha Mungu awe katika ndoa yao?

14 Neno la Mungu linaonyesha kwamba Mwandikaji walo mkuu ni Mungu mwenye haki ya hukumu na haki ya adili pia. Linasema hivi juu ya Yehova: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kum. 32:4) Ili tumwache Mungu awe katika ndoa yetu ni lazima sisi pia tuwe wenye haki ya hukumu, tuonyeshane unyofu. Hasa hiyo inamaanisha tutende mambo kulingana na ile Kanuni Bora ya Ufanisi: “Na kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”​—Luka 6:31.

15. Hasa ni katika jambo gani inawapasa waume na wake wahangaikie kuonyeshana unyofu, na ni hali gani zinazoelekea kufanya jambo hilo liwe gumu?

15 Unyofu unahusu mambo mengi. Ni wazi kwamba unahusu mambo ya pesa, ambayo huenda yakatatiza waume na wake pia. Walakini, unahusu mambo mengine ya maana zaidi, hasa hali ya kupendezwa na ngono. Ni jambo jepesi mume kuacha tamaa yake itange-tange, hasa kwa sababu ya vishawishi vyote vinavyomkabili kila siku, kutokana na watu wasio haki na vifaa (kama magazeti n.k.) vinavyotumiwa kutangaza habari chafu-chafu. Kama vile Yehova Mungu alivyotaka ibada ya pekee kwa upande wa watumishi wake (wajitolee yeye peke yake)—“ambaye jina lake ni mwenye wivu”​—vivyo hivyo waume na wake wana haki ya kujitolea wenzi wao peke yao wanapopendezwa na ngono, nao wana wajibu wa kuonyesha jambo hilo wao wenyewe. (Kut. 34:14) Mithali 5:15-20 ina mashauri yaliyo wazi sana, yenye mkazo na yenye kuwaeleza waume mambo bila kuwaficha lo lote katika habari hii. Kwa upande mwingine, wake wanahitaji kuwa waangalifu wayatii mashauri ya Paulo kwenye 1 Wakorintho 7:3-5 wala wasiitumie haki ya ndoa kama kitu cha kunyima wenzi wao ili wapewe mavazi wanayotaka, na kadhalika.

UPENDO USIO NA UCHOYO—“A.GA’PE”

16. Ni nani anayewekea watu waliooana mfano wa kuonyesha a·gaʹpe, na kwa sababu gani upendo huo unahitajiwa sana?

16 Yehova Mungu ndiye mfano mzuri ajabu wa upendo wenye kuongozwa na kanuni, usio na uchoyo, uitwao a·gaʹpe kwa Kigiriki. Hiyo ndiyo sababu tunasoma kwamba “Mungu ni upendo.” Kwa hiyo ili kumwacha Mungu awe katika ndoa yetu kuna uhitaji wa kuwa na upendo wa aina yenye kuongozwa na kanuni, usio na uchoyo, si kuwa tu na upendo wenye kutegemea mavutano ya mwili, wa tamaa ya kupendezwa na ngono (eʹros), na ule wa kuonyeshana shauku kwa sababu ya watu kuwa na hali zinazopatana za akili na roho (phi·liʹa). Upendo huo wenye kuongozwa na kanuni utaendeleza ndoa katika umoja, hata kama hizo aina nyingine mbili za upendo zitapungua.​—1 Yohana 4:8.

17. Maelezo ya Paulo juu ya ndoa yanatoa nuru gani juu ya wajibu mbalimbali wa ndoa?

17 Kwenye 1 Wakorintho 13:4-8 mtume Paulo anatoa maelezo mazuri juu ya jinsi upendo huu unavyojionyesha: “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu [si wenye wivu, NW]; upendo hautakabari [haujigambi, NW]; haujivuni [haujitutumui kwa kiburi, NW]; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote; huamini yote; hutumaini yote; hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wo wote [haushindwi kamwe, NW].”‏ Kulingana na maneno hayo ya Paulo, hatuwezi kuepuka kukata maneno kwamba kuwa Mkristo mwema kunamaanisha kuwa mwenzi mwema wa ndoa. Kinyume cha hilo, kushindwa kuendesha ndoa vizuri kunaleta sifa mbaya juu ya kuwa Mkristo. Matatizo katika ndoa yanapasa yaonwe kama nafasi zinazojitokeza ili kusitawisha matunda ya roho, na tunda lililo kubwa kati ya matunda hayo ni upendo. (Gal. 5:22, 23) Tena kumbuka, “UPENDO HAUSHINDWI KAMWE”!

18, 19. (a) Upendo wa a·gaʹpe unamtaka mke afanye nini? (b) Upendo wa a·gaʹpe utamfanya mume amtendee mke wake kwa njia gani?

18 Upendo wenye kuongozwa na kanuni, usio na uchoyo, unamtaka mke afanye nini? Unamtaka amtambue mumewe kuwa kichwa chake. (Efe. 5:22-24) Huenda kufanya hivyo kusiwe jambo jepesi nyakati zote, lakini upendo utamsaidia mke; utafanya iwe vyepesi zaidi kwake kutanguliza mapendezi ya mumewe mbele ya yake mwenyewe. Kwa mfano, kuna wake wenye upendo ambao, wakijua kwamba waume wao lazima wafuate kanuni fulani ya ulaji wa chakula, hawatayarishi vyakula vyo vyote tu ambavyo waume wao hawawezi kula pamoja nao. Wao wanajua kwamba kufanya hivyo hakuwaletei ugumu wo wote wao wenyewe, kwamba hata wanaweza kufaidika zaidi wao wenyewe.

19 Upendo usio na choyo unamtaka mume afanye nini? Unamtaka ayatii mashauri haya: “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake . . . Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Efe. 5:25, 28) Hapo mume anaombwa atimize mambo makubwa kweli kweli! Sawasawa na vile yeye anavyoutunza mwili wake mwenyewe kwa kuupa chakula, mavazi, makao, mapumziko, tafrija na mapendezi ya kiroho, vivyo hivyo ndivyo anavyopaswa kumtunza mkewe. Kama vile yeye asingetaka kujiaibisha mbele ya wengine, wala yeye hapaswi kumwaibisha mkewe mbele ya wengine. Kumpenda mkewe kama mwili wake mwenyewe kungetia ndani kukaa pamoja naye kulingana na maarifa, akiwa mwenye fadhili na kumhurumia juu ya yale mambo ya siri zaidi ya ndoa. Asiweze kushtakiwa kamwe kwamba alimchafua mke wake.​—1 Pet. 3:7.

20, 21. (a) Ni matumizi ya kanuni gani nyingine za Maandiko yatakayoonyesha kwamba Mungu yu katika ndoa ya mtu? (b) Habari ile nyingine itakayozungumzwa ni nini, na kwa sababu gani?

20 Loo! hali ya ndoa ina nafasi za kupata furaha namna gani! Yesu alisema “kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea,” na kanuni hiyo inatumika kwa watu waliooana pia. (Matendo 20:35, NW) Waume na wake wana nafasi nyingi sana za kutoa, kujitoa wenyewe, kutoa wakati wao, kusikiliza, kutoa mawazo yao, maoni yao ya ndani, kutoa vitu vya kimwili! Na katika uhusiano wao kanuni hii pia inatumika: “Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu.” Yatii mashauri yote hayo nawe utamwacha Mungu awe katika ndoa yako.​—2 Kor. 9:6.

21 Lakini hata watu wanaosema ni Wakristo waliooana walio wakf wanapungukiwa tena na tena katika mambo hayo. Kwa sababu hiyo kuna uhitaji mkubwa wa kutoboa wazi habari hii inayofuata: “Mungu wa Upendo Huchukia Kutaliki.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki